Kenya

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Jamhuri ya Kenya)
Jamhuri ya Kenya (Kiswahili)
Bendera ya Kenya Nembo ya Kenya
(Bendera ya Kenya) (Nembo ya Kenya)
Lugha rasmi Kiswahili, Kiingereza
Mji Mkuu Nairobi
Mji Mkubwa Nairobi
Miji mingine Mombasa, Kisumu na Nakuru
Serikali Jamhuri
Rais William Ruto
Eneo km² 580,367
Idadi ya wakazi 47,564,296 (2019)
Wakazi kwa km² 82
Jumla la pato la taifa kinaganaga Bilioni $114.68[1]
Jumla la pato la taifa kwa kila mtu $2,252[1]
Pesa Shilingi ya Kenya
Kaulimbiu "Harambee"
Wimbo wa Taifa Ee Mungu Nguvu Yetu
Kenya katika Afrika
Saa za Eneo UTC +3 (Wakati wa Afrika Mashariki)
Mtandao .ke
Kodi ya Simu +254

Jamhuri ya Kenya ni nchi iliyoko Afrika Mashariki katika ikweta, kando ya Bahari ya Hindi.

Kenya imepakana na Ethiopia (kaskazini), Somalia (kaskazini mashariki), Tanzania (kusini), Uganda na Ziwa Victoria (magharibi), kisha Sudan Kusini (kaskazini magharibi).

Kenya ni nchi mwanachama wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki na wa miundo mingine mbalimbali ya kimataifa.

Mji mkuu ni Nairobi.

Idadi ya watu imeongezeka sana katika miaka ya karibuni na kufikia milioni 49.

Kenya ina mbuga mbalimbali wanamoishi aina elfu kadhaa za wanyama pori.

Jina la nchi limetokana na mlima Kenya[2], ulio wa pili kwa urefu barani Afrika.[3][4]

Jiografia

Makala kuu: Jiografia ya Kenya
Mlima Kenya ni kilele cha juu kabisa nchini. Kenya imepata jina lake kutoka mlima huo.

Kenya ni nchi ya 47 kwa ukubwa duniani ikifuata mara Madagaska 580,367 km2 (224,081 sq mi) [5] ikiwa na eneo la kilomita mraba 580,367 (maili mraba 224,081).

Kutoka pwani ya Bahari ya Hindi, nyanda za chini zimeinuka hadi milima ya kati. Milima hii imetenganishwa na eneo la Bonde la Ufa; sehemu tambarare yenye rutuba upande wa mashariki. Milima ya Kenya ni kati ya iliyofaulu kwa kilimo barani Afrika.

Eneo hili la milima ndilo la juu zaidi nchini Kenya (na la pili kwa urefu barani Afrika): Mlima Kenya, unaofikia urefu wa mita 5,199 (futi 17,0570) 5,199 m (17,057 ft)na ni eneo lenye mito ya barafu.

Kusini mashariki milima ya Taita ndiyo mwanzo wa tao la Mashariki, safu za milima zenye miaka zaidi ya milioni 100 ambazo zinaenea hasa nchini Tanzania.

Upande huohuo wa kusini Mlima Kilimanjaro (5,895 m (19,341 ft)*) huweza kuonekana ukiwa ng'ambo ya mpaka wa Kenya na Tanzania.[6]

Halihewa

Kenya ni nchi yenye jua kali na nguo za majira ya joto huvaliwa mwaka mzima. Hata hivyo, huwa na baridi usiku na pia asubuhi na mapema.

Hali ya hewa ina joto na unyevu sehemu za pwani, joto kiasi sehemu za bara na ni kame katika sehemu za kaskazini na kaskazini-mashariki mwa nchi. Hata hivyo kuna mvua nyingi kati ya Machi na Aprili, na mvua ya kadiri kati ya Oktoba na Novemba. Halijoto huwa juu zaidi miezi hii yote.

Mvua ya masika hunyesha kuanzia Aprili hadi Juni. Mvua ya vuli nayo hunyesha kuanzia Oktoba hadi Desemba. Wakati mwingine mvua hii huwa nyingi na aghalabu hunyesha wakati wa alasiri na jioni. Majira ya joto jingi ni kuanzia Februari hadi Machi nayo ya baridi ni Julai hadi Agosti.

Wastani wa halijoto
Mji Mwinuko (mita) Upeo wa juu (°C) Upeo wa chini(°C)
Mombasa (Mji wa Pwani)    17 30.3 22.4
Nairobi(Mji Mkuu) 1,661 25.2 13.6
Eldoret align = "center" 3,085 23.6 9.5
Lodwar (Sehemu kame nyanda za juu) 506 34.8 23.7
Mandera (Sehemu kame nyanda za juu) 506 34.8 25.7

Mazingira

Twiga katika Mbuga ya wanyama ya Kitaifa ya Nairobi, na upeo wa macho wa Nairobi nyuma yake.

Kenya ina maeneo makubwa wanapoishi wanyamapori likiwemo Masai Mara, ambapo nyumbu na wanyama wengi walanyasi hushiriki katika uhamaji kila mwaka. Uhamaji huo, hasa uhamaji wa nyumbu, hutokea Juni hadi Septemba na hushirikisha mamilioni ya wanyama. Tukio hili huwavutia sana wapigaji picha za sinema. Takribani nyumbu 250,000 huangamia kila mwaka katika uhamaji huu wa kutafuta lishe wakati wa kiangazi.

Wale wanyama wakubwa watano wa Afrika wanapatikana Kenya: simba, chui, nyati, kifaru na ndovu. Wanyama wengine wengi wa pori na ndege hupatikana katika mbuga za taifa na hifadhi za wanyama hawa nchini.

Mazingira ya Kenya yanahatarishwa na ongezeko kubwa la idadi ya watu na athari zake.

Njia katika Hifadhi ya Taifa ya Tsavo Mashariki.

Historia

Makala kuu: Historia ya Kenya

Historia ya awali

Mabaki ya mamba mkubwa ajabu wa zamani za Mesozoic Era, ambayo ni miaka milioni 200 iliyopita, yaligunduliwa nchini Kenya katika chimbo zilizochimbwa na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Utah na Makavazi ya Kitaifa nchini Kenya miezi ya Julai hadi Agosti 2004 katika bonde la Lokitaung, karibu na Ziwa Turkana.[7]

Mabaki yaliyopatikana Afrika Mashariki yaonyesha kuwa miaka milioni 20 iliyopita viumbehai mfano wa sokwe waliishi eneo hili. Uchunguzi wa juzijuzi karibu na Ziwa Turkana waonyesha kuwa viumbe aina ya Homo habilis (walioishi miaka milioni 1.8 na 2.5 iliyopita) na Homo erectus (walioishi miaka milioni 1.8 na miaka 350,000 iliyopita) huenda ndio wazazi wa watu wa kisasa homo sapiens walioishi Kenya enzi za barafu kuu kuisha barani.

Katika mwaka wa 1984, uvumbuzi uliofanywa na mtafiti maarufu Richard Leakey na Kamoya Kimeu huko Ziwa Turkana ulikuwa wa mifupa ya mvulana iliyohusishwa na Homo erectus wa miaka milioni 1.6 iliyopita. Utafiti wa awali wa viumbe hawa unahusishwa na Mary Leakey na Louis Leakey, ambao ndio waliofanya uchunguzi wa mwanzo wa kiakiolojia huko Olorgesailie na Hyrax Hill. Baadaye utafiti wa Olorgesailie uliendelezwa na Glynn Isaac.

Historia kabla ya ukoloni

Msikiti mkuu wa Gedi ambao ni wa kutoka karne ya 13.

Wakazi wa kwanza wa eneo linaloitwa Kenya walikuwa wa jamii ya Wakhoisan: hadi leo kuna makabila matatu madogo yenye asili hiyo, ingawa yanatumia lugha za Kikushi: Waata, Waawer na Wadahalo.

Wakushi kutoka kaskazini waliingia Kenya kati ya miaka ya 3200 KK na 1300 KK[8]. Mwaka 500 KK hivi wazungumzaji wa lugha za Kinilo-Sahara na katika milenia ya kwanza KK wale wa lugha za Kibantu waliingia katika eneo hili, na sasa Waniloti ni 30% ya Wakenya wote.

Wafanyabiashara Waarabu walianza kufika pwani ya Kenya karne ya 1 BK. Ukaribu wa Kenya na Uarabuni ulirahisisha ukoloni, hivyo Waarabu na Waajemi walianza kuishi eneo la pwani karne ya 8. Hata hivyo, baadhi ya walioitwa "Waarabu" katika eneo la Afrika Mashariki walikuwa machotara, Waafrika-Waarabu.

Pwani ya Kenya imekuwa makao ya jamii ya wahunzi na jamii ya wakulima wadogowadogo, wawindaji na wavuvi ambao walikuwa mhimili wa uchumi kwa kushiriki katika kilimo, uvuvi, utengenezaji chuma, na biashara na nchi za kigeni.[8]

Kuanzia karne ya 6 au karne ya 9, Kenya ilijihusisha na shughuli za ubaharia kukuza uchumi ikaanza kutengeneza meli za kuabiria kusini hadi miji mingine yenye bandari kama Kilwa na Shanga iliyo katika pwani ya Afrika Mashariki.

Mombasa ulikuwa mji wenye bandari wa nchi ya Kenya katika karne za kati. Bandari hiyo ilitumika kuendeleza biashara na miji mingine yenye bandari Afrika, Uajemi, na wafanyabiashara Waarabu, Yemeni na hata Bara Hindi.[9]

Baharia Mreno Duarte Barbosa wa karne ya 15 alidai kuwa "[Mombasa] ni bandari nzuri na yenye shughuli nyingi, mashua nyingi na hata meli kubwa ajabu, ambazo zote hutoka Sofala na nyingine kutoka Cambay, Melinde na nyingine zinazoabiri hadi kisiwani Unguja."[10]

Karne kadhaa kabla ya ukoloni, upwa wa Kenya wanakoishi Waswahili ulikuwa sehemu ya eneo la mashariki mwa Afrika lililofanya biashara, hasa ya watumwa na pembe za ndovu na Waarabu na Wahindi. Inasemekana kwamba kabila la Wameru lilitokana na watumwa waliotoroka utumwa Uarabuni miaka ya 1700. Mwanzoni wafanyabiashara wengi walitokea milki za Uarabuni lakini baadaye wengine wakatokea Unguja (kama Tippu Tip).[11]

Kiswahili, ambacho ni lugha ya Kibantu iliyokopa misamiati ya Kiarabu, Kiajemi na mingine kutoka Mashariki ya Kati na Asia Kusini, baadaye ilikua ikawa lingua franca ya biashara kwa jamii mbalimbali.[8]

Kwa karne nyingi, upwa wa Kenya umekuwa mwenyeji wa wafanyabiashara na wasafiri. Kati ya miji iliyopo kwenye upwa wa Kenya , mji wa Malindi umebakia kuwa makazi muhimu ya Waswahili tangu karne ya 14 na wakati mmoja ulishindana na Mombasa kwa ukuu pande hizi za Afrika Mashariki. Kwa kawaida, Malindi umekuwa mji na bandari ya kirafiki kwa serikali nyingine. Mwaka wa 1414, Sultani Mwarabu wa Malindi alianzisha uhusiano wa kidiplomasia na utawala wa Uchina wa Ming, wakati wa safari za mchunguzi Zheng He.[12] Katika mwaka wa 1498, utawala wa Malindi ulimkaribisha msafiri na mvumbuzi maarufu kutoka Ureno, Vasco da Gama.

Chini ya ukoloni

Seaport Mombasa, chini ya Malindi, ina reli ya Nairobi (kituo), kusini ya Naivasha & Nyeri. (bonyeza ramani ilu kuipanua)

Wareno walikuwa Wazungu wa kwanza kuzuru eneo la Kenya ya sasa: Vasco da Gama alikuwa amezuru Mombasa mwaka wa 1498. Safari ya Vasco da Gama ilifaulu alipofikia huko India, na jambo hilo liliwawezesha Wareno kufanya biashara moja kwa moja na Mashariki ya Mbali kupitia bahari na hivyo kutatiza mitandao ya kibiashara ya awali ya nchi kavu na baharini kama njia za biashara ya viungo zilizotumia Ghuba la Uajemi, Bahari Nyekundu na misafara iliyofika hadi eneo la mashariki ya Mediterranea.

Jamhuri ya Venisi ndiyo iliyotawala maeneo ya biashara kati ta Uropa na Asia. Baada ya njia za kawaida za nchi kavu hadi India kufungwa na Waturuki wa Ottoman, Ureno ulitarajiwa kutumia njia ya baharini iliyotumiwa kwanza na Vasco da Ghama ili kuvunja ukiritimba wa Venice.

Utawala wa Wareno huko Afrika Mashariki ulijihusisha hasa na pwani iliyokaribia Mombasa. Kuwepo kwa Wareno Afrika Mashariki kulianza rasmi baada ya mwaka wa 1505, wakati manowari za Wareno, zikiongozwa na Don Francisco de Almeida, zilipokishinda Kilwa, kisiwa kilicho katika eneo ambalo sasa ni Tanzania kusini.

Kuwepo kwa Wareno Afrika Mashariki kuliwawezesha kudhibiti biashara katika Bahari ya Hindi, na kulinda njia za baharini zinazounganisha Uropa na Asia. Manowari zao za kivita zilikwamisha biashara za maadui wao magharibi mwa Bahari ya Hindi na walitoza kodi juu ya bidhaa zilizosafirishwa kupitia eneo hilo kwani walitawala bandari zote na njia kuu za meli.

Kujengwa kwa ngome iliyoitwa Fort Jesus Mombasa mwaka wa 1593 kulikusudiwa kuimarisha utawala wao katika eneo hilo, lakini ushawishi wao ulikatizwa na kuja kwa Waingereza, Waholanzi na Waarabu wa Omani katika eneo hilo karne ya 17.

Waarabu kutoka Omani ndio waliokuwa tishio kuu la utawala wa Wareno Afrika Mashariki na waliizingira ngome ya Wareno, wakazishambulia meli zao za kivita, kisha kuwafukuza Wareno waliobaki kutoka pwani ya Kenya na Tanzania mwaka wa 1730. Kufikia wakati huo, ufalme wa Ureno haukuwa na haja na njia ya bahari ya biashara ya viungo kwani faida yake ilikuwa imepungua sana. Utawala wa Wareno ulibakia tu katika bandari na maeneo ya kusini mwa Msumbiji hadi mwaka wa 1975.

Kutawaliwa kwa pwani ya Kenya na Tanzania na Waarabu kutoka Omani kuliifanya miji hii iliyojitawala hapo awali iwe chini ya uangalifu mkali wa wageni kuliko ilivyokuwa katika enzi za utawala wa Wareno. Waarabu wa Omani, kama Wareno waliowatangulia, waliweza kutawala eneo la pwani tu, si eneo la bara. Hata hivyo, kuanzishwa kwa mashamba makubwa ya mikarafuu, kuongezeka kwa biashara ya utumwa na kuhamishwa kwa makao makuu ya Waomani hadi Zanzibar mwaka wa 1839 na Seyyid Said kulisababisha Waomani kuimarisha utawala wao katika eneo hilo.

Utawala wa Waarabu katika bandari kuu zote za pwani ya Afrika Mashariki uliendelea hadi Uingereza ilipoamua kumaliza biashara ya utumwa na uanzishaji wa utaratibu wa kufanya kazi kwa malipo ukaanza kushinikiza utawala wa Waomani.

Kufikia mwisho wa karne ya 19, biashara ya watumwa katika bahari zote kuu ilikuwa imeharamishwa na Waingereza: Waarabu wa Omani hawakuwa na uwezo wa kupingana na jeshi la wanamaji la Uingereza lililokuwa likitekeleza amri hiyo. Waomani waliendelea kuwepo visiwani Unguja na Pemba hadi mapinduzi ya mwaka wa 1964, lakini kuwepo kwa Waarabu wa Omani nchini Kenya rasmi kulisitishwa wakati Wajerumani na Waingereza walipozidhibiti bandari zote kuu na kuanzisha mahusiano ya kibiashara na viongozi mashuhuri waliokuwa wenyeji miaka ya 1880. Hata hivyo, urithi waliouacha Afrika Mashariki ungali unaonekana kupitia kwa vizazi vyao vipatikanavyo pwani ya Kenya na ambavyo vinaona kuwa asili yao ni Oman. Vizazi hivi hata leo humiliki utajiri mwingi na ndio wenye ushawishi mkubwa wa kisiasa katika jamii za pwani ya Kenya.

Reli ya Kenya-Uganda karibu na Mombasa, 1899 hivi

Hata hivyo, wanahistoria wengi hushikilia kuwa historia ya ukoloni nchini Kenya ilianza wakati Wajerumani walipoanza kutawala mali ya Sultani wa Unguja iliyo pwani mwaka wa 1885, ikifuatwa na kuja kwa kampuni ya Imperial British East Africa Company mwaka wa 1888.

Uhasama wa kwanza baina ya mabepari ulikatizwa wakati Ujerumani ulipouachia Uingereza sehemu ya pwani iliyomiliki. Hii ilifuatia kujengwa kwa reli iliyounganisha Kenya na Uganda. Baadhi ya makabila ya Kenya yalipinga ujenzi huo, hasa Wanandi wakiongozwa na Orkoiyot Koitalel Arap Samoei kwa miaka kumi, kuanzia 1895 hadi 1905 – lakini hatimaye Waingereza waliijenga reli hii.

Inaaminika kuwa Wanandi walikuwa kabila la kwanza kuwekwa kwenye maeneo yaliyotengewa Waafrika ili kuwazuia kutatiza ujenzi wa reli. Wakati huo Wahindi wengi wenye ujuzi waliingia nchini ili kuchangia ujenzi. Wakati wa ujenzi wa reli kupitia Hifadhi ya Taifa ya Tsavo Magharibi, Wahindi wengi na wenyeji Waafrika walivamiwa na simba wawili waliojulikana kama “wala watu wa Tsavo”. Wahindi hao na vizazi vyao baadaye walibakia nchini Kenya na kuunda kitovu cha jamii za Wahindi zijulikanayo kama Ismaili Muslim na Sikh.[13][14]

Mnamo Agosti 1914, Vita vya Kwanza vya Dunia vilipoanza, magavana wa British East Africa (kama eneo hilo lilivyojulikana) na German East Africa walifikia makubaliano ili kuepusha makoloni yao machanga na uhasama. Hata hivyo, Luteni Kanali Paul von Lettow-Vorbeck alichukua mamlaka ya majeshi ya Ujerumani, akiwa na kusudi la kutwaa raslimali nyingi iwezekanavyo za Uingereza. Jeshi la Uingereza likiwa limemtenga na Ujerumani, von Lettow aliendesha kampeni iliyofaulu ya vita vya kuvizia, wakila walichopata, wakiteka bidhaa za matumizi za Uingereza, na kuepuka kushindwa. Mwishowe alisalimu amri na akajisalimisha nchini Zambia siku kumi na moja baada ya mapatano ya kusimamisha vita kutiwa sahihi mwaka wa 1918. Waingereza walitumia jeshi la Wahindi kumfukuza Lettow na walihitaji wachukuzi wengi ili kubeba vifaa vya matumizi hadi bara kwa miguu na hivyo kutatua shida kuu ya uchukuzi. Kundi la wanajeshi wachukuzi liliundwa na kuwajumuisha Waafrika 400,000, na kuchangia katika uhamasishaji wao wa muda mrefu kisiasa.

Hadi mwaka wa 1920, eneo linaloitwa Kenya lilijulikana kama Himaya ya Uingereza ya Afrika Mashariki.[15] Mwaka huo, koloni la Kenya liliundwa na kupatiwa jina linalotokana na Mlima Kenya[16]Waingereza walilitamka jina hilo kama pronounced /ˈkiːnjə/[17] ingawa matamshi ya wenyeji na yaliyokusudiwa katika maendelezo asili, Kenia yalikuwa ˈkɛnja.[18] Enzi ya Jomo Kenyatta kuwa rais wa Kenya miaka ya 1960-1969, matamshi ya Kiingereza, yaani /ˈkɛnjə/ yalikubalika na kutumiwa sana kwa sababu jina lake lilidumisha matamshi asilia ya wenyeji.[19] Kumbe saa ya uhuru, mwaka 1963, Jomo Kenyatta alichaguliwa kama rais wa kwanza.[20] Awali alikuwa alishika jina hili kutafakari ahadi yake ya kuikomboa nchi yake na matamshi yake ya jina lake ulisababisha katika matamshi ya Kenya katika Kiingereza kubadilisha nyuma ya makadirio ya awali uliotokea matamshi, pronounced /ˈkɛnjə/

Mwanzoni mwa karne ya 20, wakulima Waingereza na Wazungu wengine walituama katika nyanda za juu katika eneo la kati walikoondokea kuwa matajiri kwa kulima kahawa na chai.[21] Kufikia mwaka 1930, takribani walowezi 30,000 waliishi katika maeneo hayo na walikuwa na ushawishi mkubwa wa kisiasa kwa sababu ya uwezo wao wa kiuchumi.

Maeneo hayo yalikuwa makao ya watu milioni moja wa kabila la Wakikuyu, na wengi wao hawakuwa na ithibati ya kumiliki mashamba kwa mujibu wa Waingereza (ingawa mashamba hayo yalimilikiwa na kabila hilo kabla ya Wazungu kufika), na waliishi kama wakulima wanaohamahama. Ili kuendeleza matakwa yao, walowezi waliwakataza kilimo cha kahawa na kuwalazimisha kulipa kodi ya nyumba, na maskwota walipewa mashamba madogo baada ya kuwafanyia kazi. Wakikuyu wengi walihamia mijini kwani mashamba yao hayangeweza kutosheleza mahitaji yao.

Mwaka wa 1951, Horace Hector Hearne akawa mkuu wa sheria nchini Kenya (alitoka Ceylon alikoshikilia wadhifa huohuo) na alifanya kazi katika Mahakama Kuu mjini Nairobi. Alihudumu katika wadhifa huo hadi mwaka 1954 alipoteuliwa kama Hakimu wa Rufaa katika Mahakama ya Rufaa ya Afrika Magharibi. Usiku wa tarehe 5 Februari 1952, wakati Mfalme George VI alipoaga dunia, Hearne alimsindikiza Malkia Elizabeth II na mumewe Filipo mwanamfalme wa Edinburgh, kwa dhifa ya kitaifa hotelini Treetops, ambayo sasa ni kivutio maarufu cha watalii. Hapa ndipo alipouanzia umalkia.[22] Alirudi Uingereza mara moja akiandamana na Hearne.

Kuanzia Oktoba 1952 mpaka Desemba 1959, Kenya ilikuwa katika hali ya hatari kufuatia uasi wa Mau Mau dhidi ya utawala wa Uingereza. Gavana aliomba na kupata msaada wa wanajeshi Waingereza na Waafrika, pamoja na King's African Rifles. Mnamo Januari 1953, Meja Jenerali Hinde aliteuliwa kuwa mkuu wa oparesheni ya kuzima uasi. Hali hii haikuimarika kwa kukosa uchunguzi, kwa hivyo Jenerali George Erskine aliteuliwa kuwa kamanda msimamizi wa majeshi ya kikoloni mnamo Mei 1953, akiungwa mkono hasa na Winston Churchill.

Kutiwa mbaroni kwa Warũhiũ Itote (aka General China) tarehe 15 Januari 1954, na kuhojiwa kwake kulipelekea Waingereza kuuelewa vyema usimamizi wa Mau Mau. Oparesheni Anvil iliyoanzishwa tarehe 24 Aprili 1954 ilipangwa na jeshi kwa wiki kadhaa baada ya kukubaliwa na kamati kuu ya vita. Wakati wa oparesheni hiyo, mji wa Nairobi ulidhibitiwa na wanajeshi na wakazi wake walihojiwa huku wafuasi wa Mau Mau wakikamatwa na kupelekwa vizuizini.

Mnamo Mei 1953, walinzi wa nyumbani walitambulika rasmi kama askari wa usalama. Askari hao wa nyumbani ndio waliounda kikosi cha kupambana na mikakati ya Mau Mau kwani walikuwa Waafrika waaminifu, na si majeshi ya kigeni kama Jeshi la Uingereza na King's African Rifles. Kufikia mwisho wa hali ya hatari, askari hao walikuwa wamewaua Mau Mau 4886, ambao ni asilimia 42% ya waasi wote. Kukamatwa kwa Dedan Kimathi huko Nyeri tarehe 21 Oktoba 1956 kuliashiria kushindwa kwa Mau Mau kukamaliza vita.

Baada ya uhuru

Sanamu ya Jomo Kenyatta mjini Nairobi.

Utawala wa Kenyatta

Waafrika walichaguliwa moja kwa moja katika bunge la uwakilishi kwa mara ya kwanza mwaka wa 1957. Licha ya Waingereza kutamani kuwakabidhi mamlaka wapinzani wasio na siasa kali ya Kiafrika, ni chama cha Kenya African National Union (KANU) kilichoongozwa na Jomo Kenyatta kilichounda serikali punde tu kabla ya Kenya kupata uhuru tarehe 12 Desemba 1963. Tarehe 12 Desemba 1964, Kenya ilipotangazwa kuwa jamhuri, Kenyatta akawa rais wa kwanza.

Mwaka huohuo, jeshi la Kenya lilipigana na Vita vya Shifta dhidi ya kabila la Wasomali waliokusudia kuiona NFD imejiunga na Jamhuri ya Somalia. Mashifta walililemea jeshi la Kenya lakini baadaye walishindwa mwaka wa 1967.

Kenya ilitia saini mkataba na nchi ya Ethiopia mwaka wa 1969 unaodumu mpaka leo kwa kuhofia mashambulizi kutoka kwa jeshi la Somalia lililokuwa na nguvu zaidi.[23] Eneo la NFD nchini Kenya halijaendelea kutokana na kiangazi na mafuriko. Hata hivyo, wakimbizi wafanyabiashara wa Kisomali waliotajirika wamebadilisha mtaa wa Eastleigh uliokuwa wa mabanda na kuufanya kuwa ngome ya kibiashara katika sehemu kubwa ya mashariki mwa mji wa Nairobi.[24]

Utawala wa Moi

Mwaka wa 1978, Kenyatta alifariki na Daniel Arap Moi akawa rais. Moi alidumisha urais kwa kuchaguliwa bila kupingwa katika chaguzi za mwaka wa 1979, 1983 (uchaguzi wa dharura) na 1988, zote zikiwa zilifanyika chini ya katiba ya chama kimoja. Uchaguzi wa 1983 ulifanyika mwaka mmoja kabla ya wakati kutokana na njama ya kupindua serikali iliyokosa kufaulu tarehe 1 Agosti 1982.

Mapinduzi hayo yaliyotibuka yalipangwa na askari mwanahewa wa cheo cha chini, Bwana Hezekiah Ochuka na kuendelezwa hasa na wanahewa. Jaribio hilo lilizimwa kwa haraka na wanajeshi waaminifu wakiongozwa na Jeshi la Nchi Kavu, General Service Unit (GSU) - kikosi cha polisi wenye hadhi ya kijeshi - na baadaye polisi wa kawaida. Hata hivyo raia kadhaa walijeruhiwa na wengine kuuawa. Tukio hilo lilisababisha kuvunjwa kwa kikosi chote cha wanahewa, huku wengine wakiachishwa kazi na wengine wakishtakiwa kwenye mahakama ya kijeshi.

Katika uchaguzi wa 1988 kura za mlolongo zilianzishwa, ambapo wapigakura walitakiwa kupiga foleni nyuma ya wagombea wanaowapenda, badala ya kutumia kura ya siri[25] Jambo hilo lilionekana kama kilele cha enzi ya ukiukaji mkubwa wa demokrasia likasababisha msukumo mkuu wa mageuzi ya kikatiba. Vipengele vilivyokuwa na utata, kikiwemo kile kilichoruhusu chama kimoja pekee cha kisiasa, vilibadilishwa miaka iliyofuata.[26]

Katika uchaguzi wa kidemokrasia wa vyama vingi wa miaka ya 1992 na 1997, Daniel Arap Moi alichaguliwa tena.

Utawala wa Kibaki

Kulingana na katiba, mwaka 2002 Moi hakuruhusiwa kuwania urais tena, na Mwai Kibaki wa chama cha upinzani cha "National Rainbow Coalition" — NARC akachaguliwa kuwa rais. Uchaguzi huo ulitambulikana kuwa wa kidemokrasia na wachunguzi wa humu nchini na wa kimataifa na hivyo kuwa chanzo cha mageuzi makubwa ya kidemokrasia nchini Kenya.

Mnamo Desemba 2002, Wakenya walifanya uchaguzi uliokuwa wa kidemokrasia na uwazi ambao kwa kiasi kikubwa uliamuliwa kuwa huru na wa haki na wachunguzi wa kimataifa. Uchaguzi wa mwaka huo ulikuwa mwanzo mpya na uliiletea Kenya mabadiliko makuu ya kisiasa yaliyowezesha chama cha Kenya African National Union (KANU), kilichokuwa kimeitawala nchi tangu uhuru, kukabidhi kwa amani mamlaka kwa chama cha National Rainbow Coalition (NARK), uliokuwa muungano wa vyama vingi.

Chini ya uongozi wa Rais Mwai Kibaki, muungano wa vyama tawala ulihahidi kushughulikia ukuaji wa kiuchumi, kumaliza ufisadi, kuimarisha elimu na kuandika katiba mpya. Baadhi ya ahadi hizi zimeshatimizwa. Kuna elimu ya msingi ya bure. Mwaka wa 2007 serikali ilitangaza kuwa, kuanzia mwaka 2008 gharama ya masomo ya shule za upili itapunguzwa huku serikali ikilipia gharama zote za mafundisho.

Uchaguzi wa 2007

Katika uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 27 Desemba 2007, Rais Kibaki wa chama cha Party of National Unity (PNU) aliwania uchaguzi dhidi ya chama kikuu cha upinzani Orange Democratic Movement (ODM). Kulingana na wachunguzi wa kimataifa, uchaguzi huo ulikumbwa na udanganyifu na hivyo kutofikia kiwango kinachokubalika kimataifa. Chama cha ODM kilisambaratika na kupoteza 8 % ya kura zake kwa chama kipya cha Orange Democratic Movement-Kenya (ODM) - kikiongozwa na Kalonzo Musyoka. Kinyang’anyiro kilikuwa kikali kati ya mgombea wa ODM, Raila Odinga na Kibaki wa PNU. Kuhesabiwa kwa kura na Tume ya Uchaguzi ya Kenya kulionyesha Raila akiongoza kwa kura chache na baadaye kwa kura nyingi. Hata hivyo, kura zilipoendelea kuhesabiwa na Tume ya Uchaguzi, Kibaki alimkaribia mpinzani wake kwa kura, kisha akamshinda. Matokeo hayo yalisababisha maandamano na kulaumiwa kwa Tume ya Uchaguzi ya Kenya kwa kumpendelea Kibaki, hivyo Oginga akajitangaza “rais wa watu” na kutaka kura zihesabiwe tena.[27]

Maandamano hayo yalibadilika kuwa ghasia zilizosababisha kuharibiwa kwa mali.[28].[29] Viongozi mashuhuri wa Afrika, wakiongozwa na aliyekuwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan walisuluhisha mzozo huo wa kisiasa. Kundi la Annan liliungwa mkono na Umoja wa Mataifa, Jumuia ya Ulaya, Muungano wa Nchi za Afrika, Serikali ya Marekani na nchi nyingine maarufu ulimwenguni kote. Kwa habari zaidi rejelea Ghasia nchini Kenya (2007-2008).

Annan aliomba usaidizi kwa kamati yake ya upatanishi kutoka kwa shirika la kushughulikia mizozo la Uswisi lijulikanalo kama Kituo cha Mazungumzo ya Kihisani yaani Centre for Humanitarian Dialogue.

Serikali ya muungano

Tarehe 12 Februari 2008 Kibaki na Odinga walitia sahihi mkataba wa kuunda serikali ya muungano ambapo Odinga angekuwa waziri mkuu wa pili nchini Kenya. Kulingana na mkataba huo, rais angeteua baraza la mawaziri kutoka pande zote mbili za PNU na ODM kulingana na wingi wa wabunge wa kila chama bungeni. Mkataba huo ulieleza kuwa baraza la mawaziri litajumuisha Makamu wa Rais na manaibu wawili wa Waziri Mkuu. Baada ya majadiliano bungeni ilipitishwa kuwa muungano huo utadumu hadi mwisho wa kipindi cha bunge, ama chama kimoja kikijitoa kwenye muungano kabla ya kipindi cha bunge kuisha.

Wadhifa huo mpya wa waziri mkuu utakuwa na nguvu na mamlaka kuratibu na kusimamia shughuli za serikali. Vilevile itaongozwa na mbunge aliyechaguliwa ambaye pia atakuwa kiongozi wa chama au muungano wa vyama wenye idadi kubwa ya wabunge bungeni. Ulimwengu ulimshuhudia Annan na kamati yake iliyoungwa mkono na Umoja wa Mataifa na mwenye kiti wa muungano wa nchi za Afrika Jakaya Kikwete, walipowaleta pamoja wapinzani hawa sugu kwenye sherehe za kutia sahihi mkataba huu. Sherehe hizi zilionyeshwa moja kwa moja kwenya televisheni ya kitaifa kutoka kiingilio cha Jumba la Harambee mjini Nairobi. Wawakilishi wa PNU na ODM walianza majadiliano ya kina kuhusu ugavi wa mamlaka tarehe 29 Februari 2008.[30] Wabunge wa Kenya, kwa pamoja, waliidhinisha mkataba wa ugawaji mamlaka tarehe 18 mwezi wa Machi 2008 ili kuiokoa Kenya iliyoaminika kama mojawapo ya nchi thabiti na iliyoendelea barani Afrika. Mkataba huu uliunganisha PNU iliyoongozwa na Kibaki na ODM ya Odinga kisha kupelekea kuundwa kwa serikali ya muungano, vyama vyote viwili vikiwa na mamlaka sawa.[31]

Tarehe 13 Aprili 2008, Rais Kibaki aliitangaza baraza la mawaziri 41 wa serikali hii ya muungano ikijumuisha waziri mkuu na makamu wake wawili. Baraza hili lilijumuisha pia manaibu wa mawaziri 50 na lilitawazwa katika Ikulu ya Nairobi tarehe 17 Aprili 2008 huku Kofi Annan na viongozi wengine mashuhuri wakishuhudia.

Tarehe 4 Novemba 2008 ilitangazwa kuwa sikukuu ya kitaifa kusherehekea ushindi wa Barack Obama, ambaye baba yake alikuwa Mkenya, kama rais wa Marekani.

Katika sehemu za mashambani, kama wilayani Kisii, visa vya kuchoma watu wakidaiwa kuwa wachawi vinaongezeka.[32] Waathiriwa hasa ni wanawake wakongwe. Mnamo Mei 2008, watu 11 waliuwa na nyumba 30 kuchomwa.[33]

Siasa

Tazama pia: Orodha ya vyama vya kisiasa nchini Kenya

Kwa sasa Kenya ni jamhuri ya kidemokrasia ya kiuwakilishi inayoongozwa na rais, ambaye ndiye mkuu wa taifa na kiongozi wa serikali, na yenye mfumo wa vyama vingi. Serikali ndiyo yenye mamlaka ya juu.

Utungaji wa sheria ni jukumu la serikali na la bunge la taifa. Idara ya Mahakama ni huru, na imejitenga na serikali kuu na bunge. Hata hivyo, kulikuwa na kutoridhika kwingi, hasa katika enzi ya rais mstaafu Daniel Arap Moi, kuwa serikali iliingilia sana shughuli za mahakama.

Kenya imedumisha uthabiti wa kutosha licha ya mabadiliko katika mifumo yake ya kisiasa na michafuko katika nchi kadhaa jirani. Bunge la mseto wa vyama vingi la 1997 lilianzisha mageuzi yaliyobadilisha sheria za kikoloni zenye dhuluma zilizotumika kuuzuia uhuru wa kuongea na kutangamana. Jambo hilo liliimarisha uhuru wa umma na kuchangia kiasi kuaminika kwa uchaguzi wa Desemba 1997.

Kaunti na tarafa

Kaunti za Kenya.

Kenya ina kaunti 47, kila moja ikiongozwa na Mkuu wa Kaunti anayechaguliwa na watu ambao wanaishi kwenye hiyo kaunti.

Serikali za mitaa huendelezwa kupitia mabaraza ya miji. Maeneo mengi ya mijini huwa ni mji, manisipaa au baraza la mji. Serikali za mitaa katika maeneo ya mashambani huitwa serikali za wilaya. Madiwani wa mitaa hii huchaguliwa katika uchaguzi wa madiwani unaofanywa wakati mmoja na uchaguzi mkuu.

Maeneo ya uwakilishi bungeni yamegawanywa kwa sababu ya upigaji kura. Kuna maeneobunge 210 nchini Kenya.[34]

Idadi ya watu katika miji muhimu

Mji Idadi ya Watu
Nairobi 4 397 073
Mombasa 1 208 333
Nakuru 570 674
Ruiru 490 120
Eldoret 475 716
Kisumu 397 957
Kikuyu 323 881
Thika 251 407
Naivasha 198 444
Karuri 194 342

Watu

Kenya ni nchi yenye makabila mengi tofautitofauti, hasa ya Kibantu (67%) na ya Kiniloti. Wakenya wengi huzungumza lugha mbili, Kiingereza na Kiswahili, na asilimia kubwa pia huzungumza lugha mama ya kabila lao.

Makundi ya makabila ni kama ifuatavyo: Wakikuyu 22%, Waluyia 14%, Wajaluo 13%, Wakalenjin 12%, Wakamba 11%, Wakisii 6%, Wameru 6%, makabila mengine ya Kiafrika 15%, wasio Waafrika (Wahindi, Waingereza na Waarabu) 1% [5] Kila kundi au kabila lina lugha yake na Kiswahili hutumika kama chombo cha kuwasiliana miongoni mwa makabila tofauti.

Dini

Dini nchini Kenya mwaka 2009
Ukristo
  
82.5%
Uislamu
  
11.1%
Dini za jadi
  
1.6%
Kupunguza: CIA World Factbook (2009)[35]
Kanisa Katoliki huko Mombasa.

Upande wa dini, idadi kubwa ya Wakenya ni Wakristo: kulingana na sensa ya mwaka 2019, asilimia 85.5 ya wakazi wa Kenya walikuwa Wakristo (asilimia 53.9 ni Waprotestanti, asilimia 20.6 ni Wakatoliki, asilimia 11.8 ni Wakristo wa madhehebu mengine mbalimbali, wakiwemo Waorthodoksi 621,200), asilimia 10.9 ni Waislamu, asilimia 0.7 ni wafuasi wa dini asilia za Kiafrika, asilimia 1.7 ni wa makundi mengine ya dini (kuna Wahindu takribani 60,000, ambao wameingiliana vyema na Wakenya wengine na huchangia pakubwa uchumi wa nchi), na asilimia 1.6 wanadai hawana uhusiano na dini yoyote ile.[35]

Asilimia 60 ya idadi ya Waislamu huishi katika Mkoa wa Pwani, wakiwa asilimia 50 ya jumla ya wakazi wa pale. Wengi wa wanaoishi sehemu ya magharibi mkoani Pwani ni Wakristo. Eneo la kaskazini la Mkoa wa Mashariki ni makazi ya asilimia 10 ya jumla ya Waislamu nchini; hii ndiyo dini ya wakazi wengi wa hapa, na mbali na idadi ndogo ya Wasomali wanaoishi Nairobi, idadi kubwa ya Wakenya wengine ni Wakristo.[36]

Utamaduni

Askari Wamasai
Mmasai katika mapambo ya jadi

Kenya ni nchi yenye tamaduni anuwai. Tamaduni zinazotambulika ni pamoja na Waswahili walio katika eneo la pwani, jamii za wafugaji katika eneo la kaskazini na jamii nyingine mbalimbali katika maeneo ya kati na magharibi.

Wajaluo wa Kenya ni wazawa wa jamii za wakulima na wafugaji walioishi magharibi mwa Kenya kabla ya ukoloni. Inafahamika kwamba asili ya Wajaluo na makabila mengine ya Waniloti ni kaskazini mwa Kenya, pengine maeneo ya Sudan Kusini ya sasa. Waniloti, kama wanavyoitwa, ni kikundi cha kianthropolojia kilichotoka maeneo ya kaskazini mashariki mwa Afrika. Pengine walihamia kusini kutokana na vita vilivyosababishwa na ukuaji wa Kush na Misri. Waniloti nchini Kenya ni Wajaluo, Waturkana, Wakalenjin na Wamasai. Hili linadhihirika kutokana na kuwepo kwa lahaja zinazofanana kati ya makabila fulani nchini Sudan Kusini leo. Makabila haya ni pamoja na Akoli na Lwo (si sawa na Luo) wanaoishi katika eneo la Darfur.

Kuna makabila mengine ya Waniloti yanayoishi nchini Uganda na Tanzania. Hii hasa ni kwa sababu ya Wajaluo kuvutiwa na Ziwa Victoria, ambako wanapatikana katika nchi hizi tatu (Uganda, Tanzania na Kenya). Nchini Uganda, wanajulikana kwa kuanzisha himaya ya Waganda na ya himaya ya Watoro. Wajaluo nchini Kenya walipigana vita na majirani wao, hasa Wakalenjin, ili kulidhibiti ziwa hilo.

Leo hii, utamaduni wa Wamaasai unajulikana sana kwa kuangaziwa vilivyo na utalii, hata hivyo Wamaasai ni asilimia ndogo ya idadi ya Wakenya kwa jumla. Wamaasai wanatambulika kwa kujipamba sehemu ya juu ya mwili na kwa vito.

Kenya ina utajiri mwingi wa muziki, vituo vya runinga na maonyesho ya sanaa.

Elimu

Makala kuu: Elimu nchini Kenya

Mfumo wa elimu nchini Kenya unajumuisha elimu ya chekechea, ya msingi, ya sekondari na ya vyuo. Elimu ya watoto wadogo aghalabu huchukua miaka mitatu, ya msingi miaka minane, sekondari minne na chuo kikuu miaka minne au sita kwa kutegemea kozi.

Shule za chekechea, ambazo ni za watoto wa umri wa miaka mitatu hadi mitano, ni sehemu muhimu ya mfumo huu wa elimu na ni kigezo muhimu kabla ya kusajiliwa katika darasa la kwanza (Gredi ya Kwanza).

Mwishoni mwa elimu ya msingi wanafunzi hufanya mtihani wa Cheti cha Kuhitimu Masomo ya Msingi Kenya (KCPE), ambao huamua watakaojiunga na shule ya sekondari au vyuo vya ufundi. Umri wa shule ya msingi ni miaka 6/7 hadi 13/14.

Wale wanaojiunga na shule ya upili hufanya mtihani wa taifa mwishoni mwa kidato cha nne - Mtihani wa Cheti cha Kuhitimu Masomo ya Shule ya Upili Kenya (KCSE), ambao huamua watakaojiunga na vyuo vikuu, vyuo vya taatuma nyinginezo au kuajiriwa. Baraza Kuu la Usajili (JAB) ndilo lenye jukumu la kuwachagua wanafunzi watakaojiunga na vyuo vikuu vya umma. Mbali na shule za umma, kuna shule nyingi za binafsi nchini, hasa katika sehemu za miji. Vilevile, kuna shule kadhaa za kimataifa zinazofundisha mifumo mbalimbali ya elimu ya ng'ambo.

Historia ya elimu

Mfumo wa kwanza wa elimu nchini Kenya baada ya uhuru uliletwa na wakoloni Waingereza. Baada ya nchi kupata uhuru tarehe 12 Desemba 1963, Tume ya Ominde iliundwa ili kuleta mabadiliko ambayo yaakisi matarajio ya taifa huru la Kenya. Tume hii ilimulika masuala ya usawa na umoja, ambayo yalikuwa muhimu hasa wakati huo. Mabadiliko ya kilichofundishwa katika historia na jiografia yalifanywa ili kuakisi umoja wa kitaifa. Kati ya miaka 1964 na 1985, mfumo wa 7-4-2-3 ulifuatwa (miaka saba masomo ya msingi, miaka minne sekondari ya daraja la chini, miaka miwili sekondari ya daraja la juu, na miaka mitatu masomo ya chuo kikuu). Shule zote zilifuata mtaala mmoja.

Mwaka wa 1981, kamati iliyoteuliwa na rais kuratibu namna ya kuanzisha chuo kikuu cha pili nchini Kenya, na pia kuubadilisha mfumo wa elimu kwa jumla, ilianza kazi yake. Kamati hii ilipendekeza kuwa mfumo ule wa 7-4-2-3 ubadilishwe kuwa mfumo wa 8-4-4 (miaka minane shule ya msingi, miaka minne shule ya upili, miaka minne elimu ya chuo kikuu). Jedwali lililo katika Elimu ya Sasa Nchini Kenya linaonyesha muundo wa mfumo wa 8-4-4. Ingawa mfumo wa 7-4-2-3 kinadharia ulifikia kikomo mfumo wa 8-4-4 ulipoanzishwa mwaka wa 1985, kundi la mwisho la mfumo huo wa awali lilihitimu kutoka vyuo vikuu vya Kenya mwaka wa 1992.

Elimu nchini Kenya sasa

Mfumo wa sasa wa 8-4-4 ilizinduliwa Januari 1985. Ulitilia mkazo masomo ya kiufundi kwa matarajio kuwa, muundo huu mpya utawawezesha wanaoacha shule katika viwango mbalimbali aidha kujiajiri wenyewe au kupata ajira katika sekta ya juakali.

Mnamo Januari 2003, Serikali ya Kenya ilitangaza kuanzishwa kwa masomo ya shule za msingi bila malipo. Hili lilipelekea kuongezeka kwa wanafunzi waliojiunga na shule za msingi kwa asilimia 70. Hata hivyo, idadi ya waliojiunga na shule za upili na vyuo haikuongezeka sana kwa sababu malipo bado yalihitajika ili kuhudhuria masomo.

Mtihani wa kuhitimu cheti cha masomo ya msingi nchini Kenya (KCPE) hufanywa katika darasa la nane. Matokeo ya mtihani huu huhitajika ili kusajiliwa katika shule ya upili. Mtihani wa kuhitimu cheti cha masomo ya shule ya upili nchini Kenya (K.C.S.E.) hufanywa katika kidato cha nne. Wanafunzi hufanya mtihani katika masomo nane.

Ukosoaji

Mfumo wa elimu wa Kenya 8-4-4 umepitia mengi magumu katika kipindi kirefu ulichodumu. Punde tu baada ya kufuzu kwa kundi la kwanza la wanafunzi wa mfumo huu mwaka wa 1989, wananchi wengi walijitokeza kuilaumu na kuihukumu serikali kwa kuuanzisha mfumo huu. Wakosoaji hao walidai kuwa waliohitimu hawajaandaliwa vyema na hawangeweza kushindana na wenzao kutoka sehemu nyingine za ulimwengu. Wengine walihoji kuwa waliofuzu kupitia mfumo huu walikuwa aidha wachanga sana au hawajaandaliwa vyema kwa nafasi za kazi zilizokuweko. Serikali haikusikiliza hayo yote pengine kwa sababu uwezekano wa kuubadilisha na kuuunda upya kungeigharimu pesa nyingi.

Hata hivyo, kwa miaka mingi waliofuzu kupitia mfumo huu wamewaaibisha walioupinga kwa kufualu katika vyuo vya nchini na ng’ambo. Pia wasomi na wafanyakazi wa afya kuhamia nchi zilizoendelea ni dhihirisho tosha la hali hii.

Mkazo uliotiliwa masomo ya ufundi umefifia na mabadiliko ya hivi juzi katika mtaala yanasisitiza teknolojia ya upashanaji habari, sayansi, hesabu na lugha. Kwa vyovyote vile, kazi ya kiakademia na kusisitizwa kwa kupita mitihani iliyoandikwa hakujaacha nafasi kwa useremala, uashi, upishi na mafunzo mengine ya ufundi.

Michezo

Makala kuu: Michezo ya Kenya

Kenya hushiriki katika michezo mbalimbali ikiwemo kriketi, mbio za magari, soka, raga na ngumi.

Lakini nchi hii inajulikana hasa kwa kutawala katika mbio za masafa ya kadiri na mbio za masafa marefu. Kenya, kwa muda mrefu, imetoa mabingwa wa Olimpiki na michezo ya Jumuia ya Madola katika nyanja mbalimbali, hasa katika mbio za mita 800, mita 1,500, mita 3,000 kuruka viunzi na maji, mita 5,000, mita 10,000 na mbio za masafa marefu. Wanariadha wa Kenya (hasa wa kabila la Wakalenjin) wanaendelea kutawala mbio za masafa ulimwenguni, ingawa ushindani kutoka nchi ya Moroko na Ethiopia umepunguza umaarufu huu.

Wanariadha wa Kenya wanaosifika sana ni pamoja na mshindi mara nne wa mbio za masafa marefu za Boston kwa wanawake na mshindi mara mbili wa mbio za dunia Catherine Ndereba, aliyeshikilia rekodi ya awali ya mbio za dunia Paul Tergat, na John Ngugi.

Wakati wa michezo ya Olimpiki ya Beijing Kenya ilishinda medali 6 za dhahabu, 4 za fedha, 4 za shaba na kulifanya taifa lililofaulu sana barani Afrika katika michezo ya Olimpiki ya mwaka 2008. Wanariadha wapya walitambulikana, kama Pamela Jelimo, mshindi wa medali ya dhahabu katika mbio za mita 800 kwa wanawake aliyejitahidi na kushinda tuzo la Golden League, na Samuel Wajiru aliyeshinda mbio za masafa marefu kwa wanaume.

Bingwa mstaafu wa mbio za Olimpiki na za Jumuia ya Madola, Kipchoge Keino, alisaidia kuanza ubingwa wa mbio za masafa marefu miaka ya 1970 akafuatwa na bingwa wa michezo ya Jumuia ya Madola, Henry Rono, aliyeshikilia rekodi kadhaa za dunia.

Hivi majuzi, kumekuwa na mzozo wa wanariadha wa Kenya waliosaliti nchi yao na kuwakilisha nchi nyingine, hasa Bahrain na Qatar.[37] Wizara ya michezo ya Kenya imejaribu kuzuia usaliti huu, lakini umeendelea tu, Bernard Lagat akiwa wa mwisho, akichagua kuiwakilisha Marekani.[37] Usaliti huu, kwingi unatokana na sababu za kiuchumi au kifedha ingawa pia wanariadha wazuri wasioweza kufaulu katika timu nzuri ya taifa huona ni rahisi kufaulu kwa kukimbilia nchi nyingine.

Kenya pia imetawala voliboli ya wanawake barani Afrika, huku vilabu na timu ya taifa vikishinda mashindano kadhaa barani Afrika katika mwongo uliopita. Timu ya wanawake pia imeshiriki katika michezo ya Olimpiki na Mashindano ya Ulimwengu ingawa haijafaulu vilivyo.

Mchezo wa kriketi ni maarufu na pia ni mchezo wa timu ambao umefaulu sana. Kenya imeshiriki katika Kombe la Dunia la Kriketi tangu mwaka 1996. Timu hii ilishinda baadhi ya timu maarufu ulimwenguni na kufikia semifainali katika mchuano wa mwaka 2003. Walishinda ligi ya kriketi ya dunia daraja la 1 iliyofanyika Nairobi kwa mara ya kwanza, kisha wakashiriki katika mchuano wa ulimwengu wa T20. Nahodha wa sasa wa timu ni Collins Obuya.

Kenya imejiundia jina katika muungano wa raga. Mchezo huo ni maarufu nchini hasa kwa sababu ya mchuano wa kila mwaka wa Safari Sevens. Timu ya Kenya ya raga ya wachezaji saba kila upande ilikuwa nambari ya 9 katika michezo ya dunia ya wachezaji saba IRB katika msimu wa mwaka 2006.

Kenya ilikuwa bingwa wa soka katika eneo hili lakini ubingwa huu umefifia kutokana na kutoelewana kwa maafisa wa Kamati ya Soka Nchini.[38] Mizozo hii ilipelekea Kenya kupigwa marufuku na FIFA, lakini marufuku hii iliondolewa mnamo Machi 2007.

Kwa upande wa mbio za magari, Kenya ndio waandalizi wa mbio za magari maarufu za Safari Rally zinazotambulika kuwa ngumu zaidi ulimwenguni,[39] na ambazo ni sehemu ya Bingwa wa Mbio za Magari kwa miaka mingi hadi kuondolewa kwake baada ya mbio za 2002 kwa sababu ya matatizo ya kifedha. Baadhi ya madereva maarufu wa mbio za magari ulimwenguni walioshiriki na kushinda mbio hizi ni Bjorn Waldegard, Hannu Mokkola, Tommi Makinen, Shekhar Mehta, Carlos Sainz na Colin McRae. Ingawa mbio hizi bado huendelea kila mwaka kama sehemu ya kutafuta Bingwa wa Mbio za Magari Afrika, waandalizi wanatarajia kuruhusiwa kujiunga tena na Ubingwa wa Magari Ulimwenguni katika miaka michache ijayo.

Fasihi

Makala kuu: Fasihi ya Kenya

Ngugi wa Thiong'o ni mmoja wa waandishi maarufu wa Kenya. Kitabu chake en:Weep Not, Child ni ufafanuzi wa maisha yalivyokuwa Waingereza walipoitwaa Kenya. Hii ni hadithi kuhusu athari za Mau Mau katika maisha ya Wakenya asili. Kinavyochanganya maudhui - ukoloni, elimu, na mapenzi - kunakifanya kuwa kimojawapo kati ya vitabu bora vya hadithi barani Afrika.

Kitabu cha hadithi cha M. G. Vassanji The In-Between World of Vikram Lall kilishinda tuzo la Giller Prize mwaka 2003. Hii ni hadithi ya kubuni ya Mkenya mwenye asili ya Kihindi na familia yake wavyojizatiti na mabadiliko ya kisiasa wakati wa ukoloni na baada ya ukoloni nchini Kenya.

Kuanzia mwaka wa 2003, jarida la fasihi Kwani? limekuwa likichapisha fasihi ya kisasa ya Kenya.

Uchumi

Noti ya shilingi 20 ya mwaka 1994, ikimuonyesha Rais Daniel Arap Moi.

Baada ya uhuru, Kenya iliendeleza ukuaji wa kiuchumi haraka kupitia kwa uwekezaji wa umma, kuhimiza uzalishaji wa kilimo, na kushawishi uwekezaji wa watu binafsi na wageni katika viwanda. Pato la taifa lilikua kwa asilimia 6.6 kuanzia 1963 hadi 1973. Uzalishaji wa kilimo ulikua kwa asilimia 4.7 kila mwaka kwa kipindi hicho ukiwa umechochewa na ugawaji upya wa mashamba, kuanzishwa kwa kilimo cha mimea iliyoimarishwa, na kuanzisha mashamba mapya.

Hata hivyo, kati ya 1974 na 1993 ukuaji wa uchumi wa Kenya ulipungua. Kupungua kwa kilimo kulisababishwa na sera za kilimo zisizofaa, mikopo isiyotosha na vikwazo visiyofaa vya biashara ya kimataifa.

Mnamo mwaka wa 1993, Serikali ya Kenya ilianzisha mpango mkuu wa kuimarisha uchumi na kuufanya huru. Waziri mpya wa fedha na gavana mpya wa Benki Kuu ya Kenya walianza mikakati iliyofuatana kuimarisha uchumi kwa usaidizi wa Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa). Kama sehemu ya mpango huu, serikali iliondoa usimamizi wa bei za bidhaa, leseni za uagizaji na uthibiti wa ubadilishaji fedha, kubinafsisha kampuni nyingi zilizomilikiwa na umma, kupunguza idadi ya wafanyi kazi wa serikali na kuanzisha sera madhubuti za kulinda fedha. Kuanzia mwaka wa 1994 hadi 1996 ukuaji halisi wa uchumi wa Kenya ulikadiriwa juu kidogo ya asilimia 4 kwa mwaka.

Hata hivyo, kati ya 1997 na 2000, uchumi uliingia kipindi cha kupungua au kutoimarika, kwa sababu ya hali mbaya ya anga na kupungua kwa shughuli za kiuchumi. Mwaka wa 2001 pato la taifa liliimarika kiasi kwani mvua ilirejea kunyesha karibu na viwango vya awali. Ukuaji wa kiuchumi uliendelea kuimarika kiasi mwaka wa 2002 na kufikia asilimia 1.4 mwaka wa 2003, asilimia 4.3 mwaka wa 2004, kisha asilimia 5.8 mwaka wa 2005.

Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta, ambao ndio mkubwa zaidi na wenye shughuli nyingi zaidi katika eneo la Afrika Mashariki.

Mnamo Julai 1997, Serikali ya Kenya ilikataa kutimiza makubaliano ya awali na IMF kuhusu mabadiliko ya utawala wake. Jambo hili lilisababisha kukatizwa kwa misaada kwa miaka 3, nayo Benki ya Dunia ikaubana mkopo wa dola milioni 90 za mpango wa kuufufua uchumi. Ingawa mabadiliko mengi ya kiuchumi yaliyofanywa kati ya 1993-94 yalibakia, wataalamu wa maswala ya kiuchumi wasiopendelea mabadiliko waliamini kuwa Kenya iliitaji mabadiliko zaidi, hasa ya kiutawala ili kuongeza ukuaji wa pato la taifa (GDP).

Serikali ya Kenya ilichukua hatua yakini za mabadiliko, pamoja na kuunda Tume ya Kupambana na Ufisadi (KACA), kuanzisha hatua za kuimarisha uwazi wa katika mikakati ya serikali kupata bidhaa na kupunguza fedha inayotumiwa na serikali kulipia mishahara. Mnamo Julai 2000, shirika la IMF lilitia saini dola milioni 150 za Poverty Reduction and Growth Facility (PRGF), nayo Benki ya Dunia ilifuatia na mkopo wa dola milioni 157 kuimarisha uchumi na kuibadilisha sekta ya umma. Mwezi wa Desemba 2000, iliamuliwa kuwa tume ya kupambana na ufisadi haikuwa ya kikatiba na sehemu za juhudi za mabadiliko kukatizwa mwaka 2001. Shirika la IMF na Benki ya Dunia zilikatiza mipango yao. Juhudi zilizofanywa kuanzisha upya mipango hii katikati ya mwaka wa 2002 hazikufaulu.

Chini ya uongozi wa Rais Kibaki, aliyechukua hatamu za uongozi tarehe 30 mwezi wa Desemba 2002, serikali ya Kenya ilianzisha mipango mipya na kabambe ya uimarishaji uchumi na imerejelea ushirikiano wake na Benki ya Dunia na IMF. Serikali mpya ya National Rainbow Coalition (NARC) iliidhinisha Sheria dhidi ya Ufisadi na Uhalifu wa Kiuchumi pamoja na Sheria ya Maadili ya Watumishi wa Umma mnamo Mei 2003 iliyolenga kupiga vita ufisadi katika ofisi za umma. Mabadiliko mengine, hasa katika idara ya sheria, kuagiza bidhaa za umma na kadhalika yamepelekea kurejelewa kwa misaada na matumaini ya kuimarisha uchumi. Kufuatia kupitishwa kwa sheria muhimu za kupambana na ufisadi na serikali mpya, wafadhili walirejelea ufadhili mwezi wa Novemba 2003 na IMF ikaidhinisha msaada wa miaka mitatu wa dola milion 250 ili kupunguza umaskini na kuimarisha uchumi. Wafadhili wakatoa dola bilioni 4.2 kama msaada wa miaka minnne. Kurejelewa kwa ufadhili na kujihusizisha upya kwao kumevutia imani ya wawekezaji.

Mswada wa ubinafsishaji umeidhinishwa ingawa kuanzishwa kwa tume ya ubinafsishaji hakujakamilika, mabadiliko katika utendakazi wa umma yametekelezwa na mwaka wa 2007 Kenya ilishinda tuzo la Umoja wa Kimataifa la Utendakazi wa Umma.[40][41] Hata hivyo, kazi nyingi zinahitajika kufanywa ili kuiwezesha nchi hii kuyafikia mataifa yaliyoendelea sana kiuchumi, hasa yale ya Mashariki ya Mbali. Changamoto kuu ni pamoja na kuchukua hatua thabiti dhidi ya ufisadi, kupitisha sheria zinazoshughulikia ugaidi na biashara haramu, kutatua upungufu wa ufadhili wa bajeti kisha kurekebisha na kuunda miundo msingi. Inaaminika haya yatasaidia kudumisha sera za kimsingi za kiuchumi, na kuhakikisha ukuaji wa kasi wa kiuchumi uliofikia asilimia 7.2 mwaka wa 2007.

Mwaka wa 2007, serikali ya Kenya ilizindua Ruwaza 2030, ambao ni mpango wa kiuchumi wenye matumaini makuu na ambao ikiwa utatekelezwa kikamilifu, una uwezo wa kuifanya nchi hii kuwa katika kiwango sawa na mataifa yaliyoendelea kiuchumi ya Asia.

Nairobi inaendelea kuwa kituo muhimu na cha kimsingi kwa mawasiliano na biashara cha Afrika Mashariki. Kinajivuna kuwa na miundo msingi ya uchukuzi na mawasiliano bora zaidi katika eneo hili, na wafanyi kazi wenye ujuzi. Makampuni mengi ya kigeni hudumisha matawi yao katika eneo hili ama ofisi za kuyawakilisha mjini Nairobi. Mnamo Machi 1996, Marais wa Kenya, Tanzania na Uganda waliifufua Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC). Shabaha za EAC ni pamoja na kusawazisha kodi na ada zinazotozwa bidhaa, utembeaji huru wa watu na kuimarisha miundo msingi katika eneo hili. Nchi hizi tatu za Afrika Mashariki zilitia saini mkataba wa Customs Union Agreement mwezi wa Machi 2004.

Mji wa Nairobi
Muhtasari wa uchumi wa nchi
Pato la taifa Dola bilioni 41.84 (2012) kwa bei ya sasa. Dola bilioni 76.07 (Uwezo wa kununua bidhaa usio sawa, 2012) Kuna pia uchumi mkubwa usio rasmi ambao haujawahi kujumuishwa kama sehemu ya pato la taifa.
Ukuaji wa kiuchumi kwa mwaka 5.1% (2012)
Pato la kila mtu kwa mwaka Pato la kila mtu kwa mwaka (PPP)= $1,800
Malighafi ya kiasili Wanyama wa pori, Ardhi (5% inayolimika)
Bidhaa za kilimo Chai, kahawa, mahindi, ngano, miwa, mboga na matunda, pareto, bidhaa za maziwa, nyama na bidhaa za wanyama
Viwanda Bidhaa za petroli, usagaji wa nafaka na miwa, saruji, pombe, vinywaji, nguo, uunganishaji magari, makaratasi, utengenezaji wa bidhaa za kimsingi, utalii
Biashara ya mwaka 2012
Biasharanje Dola bilioni 5.942 chai, kahawa, bidhaa za mboga na matunda, bidhaa za petroli, saruji, samaki
Masoko muhimu (2012) [5] Uganda, Tanzania, Uholanzi, Uingereza, Marekani, Misri, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
Maduhuli Dola bilioni 14.39 mashine, magari, bidhaa za petroli, vyuma, resini na bidhaa za plastiki
Mataifa muhimu yaletayo bidhaa Kenya    China, Uhindi, Muungano wa Falme za Kiarabu, Saudi Arabia, Afrika Kusini, Ujapani

Utafutaji wa mafuta

Mwanzoni mwa mwaka wa 2006 Rais wa Uchina, Hu Jintao, alitia saini kandarasi ya utafutaji wa mafuta na Kenya. Haya ndiyo makubaliano ya hivi punde kati ya mfululizo wa mapatano yaliyopagwa kuelekeza maliasili ya Afrika huko Uchina ambako uchumi wake waendelea kukua kwa haraka.

Kandarasi hii iliwezesha kampuni inayoongozwa na taifa la Uchina “offshore oil and gas company” CNOOC Ltd kutafuta mafuta Kenya, ambayo ilianza kuchimba visima vya kwanza mpakani mwa Sudan na Somalia na katika maji ya upwa wake.[42]

Tazama pia

Marejeo

  1. 1.0 1.1 World Economic Outlook database: April 2022.
  2. Kabla ya mwaka wa 1920, eneo linaloitwa Kenya liliitwa Himaya ya Uingereza Afrika Mashariki, kwa hiyo hapakuwa na haja ya kutaja neno mlima uliporejelea mlima huo.
  3. The Times|articlename=British East Africa Annexed--"Kenya Colony" |author=Reuter|section=News|day_of_week=Thursday|date=8 Julai 1920|page_number=13|issue=42457|column=C
  4. "East Africa: Kenya: History: Kenya Colony". Encyclopedia Britannica. 17 (15 ed.). 2002. pp. 801, 1b. ISBN 0-85229-787-4.
  5. 5.0 5.1 5.2 Hitilafu ya kutaja: Invalid <ref> tag; no text was provided for refs named CIA World factbook Kenya
  6. Rough Guide (2006). Rough Guide Map Kenya [map], 9 edition, 1:900,000, Rough Guide Map. Cartography by World Mapping Project. ISBN 1-84353-359-6.
  7. [1], ABC News Online, 2005/03/10
  8. 8.0 8.1 8.2 Wonders wa Afrika World - PBS
  9. Hybrid Urbanism By Nezar Al-Sayyad
  10. Dispersal Afrika katika Deccan By Shanti Sadiq Ali
  11. Kiswahili Coast. Archived 30 Desemba 2007 at the Wayback Machine. Nationalgeographic.com.
  12. Sultani wa Malinda, PBS
  13. Ismaili muslim. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-01-03. Iliwekwa mnamo 2021-01-16.
  14. Sikh
  15. The Times|articlename=British East Africa Annexed--"Kenya Colony"|author=Reuter|section=News|day_of_week=Thursday |date=8 Julai 1920|page_number=13|issue=42457|column=C
  16. Foottit, Claire (2006) [2004]. Kenya. The Brade Travel Guide. Bradt Travel Guides Ltd. ISBN 1-84162-066-1. 
  17. "Kenya". Oxford English Dictionary. Oxford University Press. 2nd ed. 1989.
  18. The Spelling ya Kenya. BJ Ratcliffe. Journal ya Royal African Society, Vol. 42, Namba 166 (Januari 1943), uk. 42-44
  19. Foottit, Claire (2006) [2004]. Kenya. The Brade Travel Guide. Bradt Travel Guides Ltd. ISBN 1-84162-066-1. 
  20. Castro, Alfonso Peter (1995). Facing Kirinyaga. London: Intermediat Technology Publications Ltd. ISBN 1-85339-253-7. 
  21. "Tunataka nchi yetu" Archived 23 Julai 2013 at the Wayback Machine.. Wakati. 5 Novemba 1965.
  22. Kenya, AfricaGenWeb
  23. Post-Uhuru Low intensiteten Conflict Nchini Kenya
  24. E. H., Campbell (2006). "Urban Refugees in Nairobi: Problems of Protection, Mechanisms of Survival, and Possibilities for Integration". Journal of Refugee Studies (full text) 19 (3): 396. doi:10.1093/jrs (inactive 2009-04-25). 
  25. Wapiga kura wengi kukaa nyumbani kama Kenya Drops Secret Ballot katika Uchaguzi Parliamentary http://www.highbeam.com/doc/1P2-1241691.html Archived 15 Februari 2011 at the Wayback Machine.: The Washington Post Kifungu tarehe: 25 Februari 1988 Author: Blaine Harden
  26. religiousfreedom.lib.virginia.edu / rihand / Kenya.html
  27. ghasia za uchaguzi Kenya unatishia mafanikio yake ya kiuchumi http://www.chinadaily.com.cn/language_tips/auvideo/2008-01/07/content_6375707.htm
  28. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-07-15. Iliwekwa mnamo 2009-12-07.
  29. http://www.iol.co.za/index.php?set_id=1&click_id=68&art_id=nw20080113081804606C678503[dead link]
  30. 'Hope is back' kwa Kenya - CNN.com Archived 5 Machi 2008 at the Wayback Machine. saa edition.cnn.com
  31. wabunge Kenya kupitisha sheria ya kugawana madaraka-english.aljazeera.net/NR/exeres/111A3F40-0FD9-4DCB-ACB0-822D1E3A09EA.htm Al Jazeera Kiingereza 18 Machi
  32. Horror ya Kenya's 'Witch' lynchings
  33. Mob nzito kifo 11 Kenya 'witches'
  34. Kenya Roads Board Constituency ufadhili chini ya RMLF Archived 13 Januari 2008 at the Wayback Machine.
  35. 35.0 35.1 The World Fact Book: Kenya. Jalada kutoka ya awali juu ya 2020-08-31. Iliwekwa mnamo 21 Juni 2014.
  36. US Department of State
  37. 37.0 37.1 IAAF: Mabadiliko ya utii 1998-2005[dead link]
  38. New Vision, 3 Juni 2004: Wrangles ardhi Kenya utan fastställd FIFA marufuku Archived 10 Januari 2008 at the Wayback Machine.
  39. The Auto Channel, 21 Julai 2001: FIA Rally: Delecour inachukua pointi kumaliza tarehe Safari Rally kwanza
  40. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-02-15. Iliwekwa mnamo 2009-12-07.
  41. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-03-24. Iliwekwa mnamo 2009-12-07.
  42. Barber, Lionel; Andrew England. "China's scramble for Africa finds a welcome in Kenya", Financial Times, 10 Agosti 2006. Retrieved on 2008-06-27. 

Viungo vya nje

Serikali
Jumla
Vyombo vya habari
Utalii
Historia
Nyingine


Nchi za Afrika Bara la Afrika
Afrika ya Kati (Jamhuri ya) | Afrika Kusini | Algeria | Angola | Benin | Botswana | Burkina Faso | Burundi | Cabo Verde | Chad | Cote d'Ivoire | Eritrea | Eswatini | Ethiopia | Gabon | Gambia | Ghana | Guinea | Guinea Bisau | Guinea ya Ikweta | Jibuti | Kamerun | Kenya | Komori | Kongo (Jamhuri ya) | Kongo (Jamhuri ya Kidemokrasia ya) | Lesotho | Liberia | Libya | Madagaska | Malawi | Mali | Misri | Morisi (Visiwa vya) | Mauritania | Moroko | Msumbiji | Namibia | Niger | Nigeria | Rwanda | Sahara ya Magharibi | Sao Tome na Principe | Senegal | Shelisheli | Sierra Leone | Somalia | Sudan | Sudan Kusini | Tanzania | Togo | Tunisia | Uganda | Zambia | Zimbabwe
Maeneo ya Afrika ambayo ni sehemu za nchi nje ya Afrika
Hispania: Kanari · Ceuta · Melilla | Italia: Pantelleria · Pelagie | Ufaransa: Mayotte · Réunion | Uingereza: · St. Helena · Diego Garcia | Ureno: Madeira
Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Kenya kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.