Karafuu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Karafuu kadhaa
Karafuu ikiangaliwa kwa karibu
Maua kwenye mkarafuu
Karafuu tayari kukauka

Karafuu (kutoka Kiarabu قَرَنْفُل qaranful[1]) ni matumba (macho ya maua) makavu ya mikarafuu ambayo ni miti ya familia ya Myrtaceae.

Karafuu hutumiwa kama kiungo cha chakula na chanzo cha mafuta yenye harufu inayopendwa na watu wengi.

Asili ya mti na pia matumizi ya matumba ni visiwa vya Indonesia. Katika karne ya 19 mikarafuu ilipelekwa Unguja na Pemba hasa na mtawala wa Omani na kuanzisha uzalishaji mkubwa saa wa karafuu kwenye visiwa hivi.

Matumizi[hariri | hariri chanzo]

Karafuu hutumiwa katika upishi wa nchi nyingi za Asia, Afrika, Ulaya na hata Amerika. Hutumiwa katika kupika nyama, curry na michuzi mbalimbali pamoja na kupika matunda pamoja na vinywaji. Ni kiungo cha lazima kwenye pilau.

Hutafunwa pia mdomoni kuboresha harufu ya pumzi.

Kutafuna karafuu ni dawa ya kupunguza maumivu ya meno.

Nchini Indonesia sigara huungwa na mafuta ya karafuu.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Karafuu zilifanyiwa biashara tangu kale. Kuna ushuhuda wa karafuu katika chombo kilichopatikana nchini Syria kilichogunduliwa kuachwa huko mnamo mwaka 1721 KK[2].

Kuna taarifa ya kwamba mtawala nchini China alitaka watu wanaotaka kuongea naye watafune karafuu ili wawe na pumzi ya kupendeza.[3]

Katika karne ya 17 karafuu ilikuwa kati ya vivutio vya kiuchumi vilivyoleta Uholanzi kuanzisha makoloni yake kwenye visiwa vya Indonesia.

Katika karne ya 18 Mfaransa Pierre Poivre alifaulu kuiba miche ya mikarafuu na kuipeleka Morisi ambako Wafaransa walianzisha kilimo hicho.

Soko la karafuu lilikua duniani na hii ilikuwa changamoto ya Sultani wa Omani kupeleka miti hiyo Unguja na Pemba iliyoendelea kuwa nchi ya kuzalisha karafuu nyingi zaidi duniani na kuunda utajiri wa Zanzibar ilhali kilimo hicho kilichochangia pia katika biashara ya watumwa waliotumiwa kuzalisha zao hili katika karne ya 19. [4]

Mapato ya karafuu yalimsababisha Said bin Sultani kuhamisha makao makuu yake Unguja na baada ya kifo chake Usultani wa Zanzibar ulianzishwa kama nchi ya pekee na Omani.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Waarabu walipokea jina kutoka Kigiriki καρυὁφυλλον karyofilon , tazama kamusi ya Sacleux, "Karafuu".
  2. Turner, Jack (2004). Spice: The History of a Temptation. Vintage Books. pp. xxvii–xxviii. ISBN 0-375-70705-0.
  3. Andaya, Leonard Y. (1993). "1: Cultural State Formation in Eastern Indonesia". In Reid, Anthony. Southeast Asia in the early modern era: trade, power, and belief. Cornell University Press. ISBN 978-0-8014-8093-5. 
  4. The world's oldest clove tree, BBC, 23 June 2012

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons