Ukristo

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Wakristo)
Sanamu ya Kristo mkombozi huko Rio de Janeiro (Brazil) ni sanamu ya Yesu kubwa kuliko zote zilizopata kutengenezwa.


Ukristo (kutoka neno la Kigiriki Χριστός, Khristos, ambalo linatafsiri lile la Kiebrania מָשִׁיחַ, Māšîăḥ, linalomaanisha "Mpakwamafuta" [1]) ni dini inayomwamini Mungu pekee[2] kama alivyofunuliwa kwa Waisraeli katika historia ya wokovu ya Agano la Kale na hasa Yesu Kristo katika Agano Jipya ambaye ni mwanzilishi wake katika karne ya 1.

Dini hiyo, iliyotokana na ile ya Wayahudi, inalenga kuenea kwa binadamu wote, na kwa sasa ni kubwa kuliko zote duniani,[3][4][5] ikiwa na wafuasi 2,400,000,000 (33% kati ya watu 7.274 bilioni)[6][7][8][9], ambao nusu ni waamini wa Kanisa Katoliki na nusu ya pili wamegawanyika kati ya Waorthodoksi (11.9%) na Waprotestanti (38%) wa madhehebu mengi sana.

Karibu wote wanakubali Utatu Mtakatifu, yaani kwamba milele yote Mungu ni nafsi tatu zenye umoja kamili: Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Ni kwa jina lao kwamba mataifa yote wanahimizwa kubatizwa kwa maji, ili kuzaliwa upya, kadiri ya agizo la Yesu ili kuingizwa katika fumbo la Mungu pekee kupitia fumbo la kifo na ufufuko wake mwenyewe.

Kitabu kitakatifu cha Ukristo kinajulikana kama Biblia. Ndani yake inategemea hasa Injili na vitabu vingine vya Agano Jipya.

Wakati wa Mababu wa Kanisa misingi ya imani ya Ukristo ilifafanuliwa na Mitaguso ya kiekumeni namna inayokubaliwa na wengi kabisa kati ya Wakristo wa leo. Maungamo yao yanakiri kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu aliyefanyika mtu ili kuwaokoa binadamu. Baada ya kuteswa na kuuawa msalabani alizikwa ila akafufuka, siku ya tatu akapaa kwa Mungu akishiriki mamlaka ya Baba hadi atakaporudi kuhukumu waadilifu na wasiotubu, akiwapa tuzo au adhabu ya milele kadiri ya imani na matendo yao.

Hivyo, kati ya madhehebu ya Ukristo, karibu yote yanamkiri Yesu kuwa kwa pamoja Mungu kweli na mtu kweli: katika umoja na nafsi yake ya Kimungu zinapatikana sasa hali hizo zote mbili.

Yote yanamkiri kuwa Mwokozi wa watu wote, na kuwa ndiye atakayerudi mwishoni mwa dunia kwa hukumu ya wote, ingawa maelezo kuhusu jambo hilo yanatofautiana.

Vilevile yote yanamchukua kama kielelezo cha utakatifu ambacho - kwa msaada wa Roho Mtakatifu na wa sakramenti zilizowekwa na Yesu mwenyewe, kuanzia ile ya ubatizo - kiwaongoze ndani ya Kanisa katika maadili yao maalumu, kuanzia unyenyekevu na upole hadi upendo unaowaenea wote, bila kumbagua yeyote, hata adui.

Asili

Chimbuko la Ukristo ni mtu huyo aliyezaliwa takriban miaka 2000 iliyopita huko Mashariki ya Kati, katika kijiji cha Bethlehemu kilichopo hadi hivi leo kwenye mipaka ya Palestina; alikuwa akiitwa Yesu wa Nazareti (kijiji alikokulia) au mwana wa Yosefu mchonga samani,mama yake akifahamika kwa jina la Bikira Maria.

Kwa kumuita pia Kristo, wafuasi wake walikiri kwamba ndiye aliyetimiza utabiri wa manabii wa kale, kama unavyopatikana katika vitabu vya Biblia ya Kiebrania na Deuterokanoni.

Habari za maisha na mafundisho yake zinapatikana kirefu zaidi katika Injili nne zilizokubalika, katika Agano Jipya kwa jumla, lakini pia ziliandaliwa na kutabiriwa na Agano la Kale.

Yesu kama Masiya aliyetarajiwa

Ukristo ni matokeo ya utume wa Yesu, uliopokewa na waliomwamini kuwa ndiye Masiya, yaani mkombozi aliyetimiliza ahadi za Mungu kwa binadamu.

Katika kitabu cha Mwanzo tunasoma utabiri wa kuja kwake ulianzia katika bustani ya Edeni pale Mungu alipomwambia nyoka, yaani shetani, kuhusu mwanamke kwamba "uzao wake utakuponda kichwa" (Mwa 3:15).

Baadaye Abrahamu, babu wa taifa la Israeli, kwa imani na utiifu wake kwa Mungu, aliahidiwa kwamba katika uzao wake mataifa yote yatabarikiwa.

Musa, mwanaharakati aliyewakomboa watu wa Israeli kutoka utumwani Misri takribani miaka 1250 KK (kabla ya kuzaliwa kwa Yesu), ndiye nabii wa kwanza kutabiri wazi kwa niaba ya Mungu ujio wa Masiya au Kristo (Kumb 18:15-22, hususan mstari 18: "Nitawainulia nabii kama wewe kutoka miongoni mwa ndugu zenu; na nitatia neno langu kinywani mwake na atasema nao yote niliyomwamuru."

Kuja kwake kulitimia katika Agano Jipya, ambalo ni ukamilifu wa yote yaliyotabiriwa katika Agano la Kale. Kwani Musa alitumwa kuanzisha Agano la Kale kama maandalizi ya Agano Jipya, akikabidhi mifumo mingi ya nje na ndani kwa watawala na waamuzi waliomfuatia watakaoshikilia Agano la kusubiri Masiya wakishirikiana na manabii na makuhani.

Yesu alizaliwa miaka kama 1800 baada ya Abrahamu. Vitabu vya Injili vinaeleza matukio na mafundisho ya Yesu ambayo ndiyo mwongozo wa imani hiyo. Maisha na kazi ya Yesu vimeibua mambo mengi katika historia. Ndiyo sababu kalenda iliyoenea duniani huhesabu miaka kutoka ujio wake; huu ni mchango mmojawapo wa Ukristo katika ustaarabu.

Mafundisho ya msingi ya Yesu

Hotuba ya Mlimani kadiri ya Carl Heinrich Bloch. Hotuba ya Mlimani inachukuliwa na Wakristo kuwa utimilifu wa Torati iliyotolewa na Musa katika Mlima Sinai.

Yesu alifanya ishara za kustaajabisha, au miujiza. Matokeo ni kwamba, watu wengi wakamwamini.

Nikodemu, mshiriki mmojawapo wa baraza la Sanhedrini, ambalo lilikuwa pia mahakama kuu ya Wayahudi, alivutiwa na kutaka kujua zaidi kuhusu siri ya miujiza hiyo na ujumbe kutoka kwa Mungu; kwani yeye alihamasika kuona ishara zile kutoka kwa Mungu.

Yesu akamjibu kwamba hakika mtu hawezi kuingia ufalme wa Mungu asipozaliwa mara ya pili kwa maji na Roho Mtakatifu.

Pia akajieleza kuwa mpatanishi wa ulimwengu wa dhambi na Mungu na kwamba kila anayemgeukia kwa imani hatapotea, bali atarithi uzima wa milele: alisema mwenyewe ni mfano wa nyoka wa shaba aliyetengenezwa na Musa. (Yoh 2:23-3:21; Hes 21:9).

Akiwa kando ya Ziwa la Galilaya, Yesu alikuta umati wa watu umekusanyika. Basi akapanda mashuani na kuenda mbali kidogo na ufuoni, akaanza kuwafundisha kuhusu Ufalme wa mbinguni kupitia mfululizo wa mifano.

Mmojawapo ni huu ufuatao: "Ufalme wa mbinguni ni kama punje ya haradali ambayo mtu anaipanda. Ingawa ni mbegu ndogo sana inakua na kuwa mti wa mboga mkubwa kuliko yote. Inakuwa mti ambao ndege wanauendea, wakipata makao katika matawi yake". (Math 13:1-52; Mk 4:1-34; Lk 8:4-18; Zab 78:2; Isa 6:9,10).

Kanisa siku za mwanzo

Umoja wa waamini na Kristo ndio lengo la Ukristo.

Jumuia ya Wakristo inaitwa Kanisa, yaani "mkusanyiko" kama lilivyotajwa na Yesu mwenyewe hasa katika Injili ya Mathayo 16:18: "Wewe ndiwe Petro na juu ya mwamba huu, nitalijenga kanisa langu. Wala milango ya kuzimu haitalishinda".

Yesu aliita wengine 11 pamoja na Petro kuunda kundi la mitume wake. Idadi yao ilipangwa kwa kusudi la kudokeza kwamba ndiyo mwanzo mpya wa taifa la Mungu, kama vile watoto 12 wa Yakobo Israeli walivyokuwa mwanzo wa taifa lake la kale.

Yesu aliwapa hao Thenashara mamlaka ile aliyopewa na Mungu Baba ili kuokoa watu.

Yesu na wanafunzi wake wa kwanza walikuwa Wayahudi. Yaani walizaliwa katika uzazi wa Abrahamu wakiwa watoto wa Agano lililofanywa kati ya Mungu na taifa lake la Israeli zamani za Musa.

Wakati wa Yesu Waisraeli hao waliitwa "Wayahudi". Walio wengi waliishi nje ya nchi ya Israeli/Palestina, kutokana na vita vingi vya zamani vilivyosababisha wakimbizi kuhamia nchi zenye usalama zaidi. Jumuiya za Wayahudi zilipatikana katika miji yote mikubwa ya Afrika Kaskazini (hasa Misri na Libia), Ulaya Kusini na Asia Magharibi mpaka Uajemi.

Kwa upande mmoja Wayahudi walitoka katika ukoo wa Ibrahimu, hasa waliokaa Israeli/Palestina. Lakini watu wengine wenye asili ya mataifa tofauti waliwahi kujiunga na imani ya Wayahudi na kuchukua hatua ya kuongoka na kutahiriwa.

Katika mazingira yao Wayahudi walikuwa watu wa pekee waliomshuhudia Mungu mmoja tu. Walikuwa tofauti na wengine kwani hawakushiriki katika ibada ya miungu ya serikali, tena walitunza utaratibu wa sabato yaani kutotenda kazi siku ya saba.

Mitume wa Yesu walizunguka awali hasa katika jumuiya za Wayahudi kila mahali walipokwenda. Mwanzoni Kanisa lilionekana kama dhehebu la Kiyahudi tu. Baada ya kupokea watu kutoka mataifa bila kuwatahiri hali ilibadilika: Kanisa likawa taifa la Mungu kutoka kwa Wayahudi na kwa Mataifa.

Ujio wa Roho Mtakatifu

Mara baada ya Yesu kwenda zake katika tukio linalotajwa kupaa kwake mbinguni, wafuasi wake wakarudi Yerusalemu, yapata mwendo wa sabato, na walipoingia huko, wakapanda ghorofani walipokuwa wakikaa Mtume Petro na wenzake.

Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwapo wote mahali pamoja. Ukaja upepo toka juu kama upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukatokea na ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa na Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia. (Mdo 1:12-14, 2:1-4).

Hii ilifuatiwa na Petro na wenzake kuanza kuhubiri ufufuko wa Bwana Yesu na hatimaye kugusa watu 3,000 waliokubali kubatizwa siku hiyo. (Mdo 2: 37-40).

Ustawi wa jumuia ya kwanza ya wafuasi wa Kristo

Watu walipokuwa wakidumu katika fundisho la mitume, sala, kumega mkate na katika ushirika, wengi wakaona ishara zao nyingi basi nao wakauza mali zao, na vitu walivyokuwanavyo, na kugawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja.

Basi, siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakila pamoja na kushiriki kwa moyo mweupe.

Hivyo ndivyo jumuia ilivyozaliwa na kufahamika kama Kanisa. (Mdo 2:42-47).

Kukutanika na kushiriki mafumbo makuu, kushukuru na kusifu, pamoja na uwepo wa vipaji na karama za Roho Mtakatifu, hufanya Kanisa liwe hai.

Uenezi wa awali wa Kanisa

Ujumbe wa Yesu ulienea haraka toka Yerusalemu hata Lida, Yafa, Kaisaria, Samaria, Damasko n.k. na kuanzisha jumuia nyingi.

Nazo jumuia kwa bidii za waamini wa mwanzo zikafika Foinike, Kipro, Antiokia, ambako waliitwa Wakristo kwa mara ya kwanza, kutokana na waamini wa mataifa mengine kuwazidi wale wenye asili ya Kiyahudi (Mdo 11:1-23).

Imani na desturi za mikusanyiko hiyo zenye asili ya Kiyahudi zilitapakaa na hivyo kuanza kusuguana na mapokeo ya jamii mbalimbali zilipopenya. Hii inatokana na ukweli kwamba watu wengi wa siku zile tayari walikuwa na imani zao walizokuwa wakizitunza.

Basi ukaja wakati ambao Wakristo wakaanza kukosoana kuhusu dhamiri zao na huduma. Ndiyo asili ya nyaraka mbalimbali ambazo zinaunda sehemu muhimu wa Agano Jipya.

Uongozi wa Kanisa

Kila jumuiya inatumia mbinu zake za uongozi. Mkuu wa jumuiya ya wanafunzi tangu mwanzo ni Bwana Yesu. Lakini kama kundi ni kubwa kazi ya uongozi ni tofauti. Haiwezekani kufanya kila kitu pamoja watu wakiwa wengi. Ipo lazima ya kugawana kazi na madaraka.

Suala hili limekuwa muhimu sana katika historia ya Ukristo. Njia mbalimbali za uongozi ambazo zilitafutwa na kujaribiwa zinaonyesha tofauti muhimu kati ya madhehebu mbalimbali. Kwa jumla njia hizo zote zinajaribu kuiga mifano ya ushirika wa kwanza inayopatikana katika Biblia. Vyeo na shughuli maalumu zilizopo katika Ukristo leo, vina asili na mwanzo katika ugawaji wa madaraka ulivyokuwa wakati wa mitume.

Katika nyaraka za Paulo (ambazo ni maandiko ya kwanza katika Agano Jipya) tunaona hali ya Ukristo mwanzoni kabisa. Paulo anataja mitume, manabii, walimu, wenye vipawa mbalimbali (1Kor 12,28 n.k.), au maaskofu na mashemasi, pia wazee. Kwa jumla hakuna picha kamili ya utaratibu mmoja uliokuwepo kila mahali.

Katika ushirika wa kwanza kule Yerusalemu Mitume, yaani marafiki wa Yesu wa karibu waliotumwa naye na kupewa kazi ya kueneza Habari Njema, ndio waliokuwa viongozi. Lakini baada ya muda mfupi kazi zilikuwa nyingi, hivyo wakaongeza "Wasaidizi saba". Hao saba walishughulikia hasa huduma za upendo, yaani kuwagawia wajane na wazee misaada.

Baada ya Mtume Petro kuhama Yerusalemu, Yakobo Mdogo ndiye aliyeongoza ushirika huo.

Mwishoni mwa karne ya 1 cheo cha "Askofu" kiliimarika sana, lakini pia vikundi vya Wakristo wenye vyeo maalumu vya utumishi vilianza kutokea. Pamoja na Askofu vyeo vya Kasisi na Shemasi vilikuwa kawaida. Mashemasi wa kike walipatikana pia mwanzoni, lakini walipotea baadaye, kutokana na utamaduni uliokazia kipaumbele cha wanaume.

Kuanzia mwaka 100 hivi Kanisa likaitwa "katoliki" maana yake Kanisa moja kwa ajili ya nchi zote na watu wote, tofauti na vikundi vilivyojitenga nalo. Kila mji ulikuwa na askofu wake aliyeongoza kanisa. Maaskofu wa eneo au mkoa mmoja walikuwa chini ya Askofu Mkuu. Maaskofu wa Roma (Ulaya hadi Afrika Kaskazini-Magharibi), Aleksandria (Afrika) na Antiokia (Asia), waliheshimiwa kuliko maaskofu wengine wote wakaitwa "Papa" na "Patriarki". Cheo cha Patriarki kilipatikana pia kwa Askofu wa Bizanti (leo nchini Uturuki) baada ya makaisari wa Roma kuhamia kule, na vilevile kwa Askofu wa Yerusalemu.

Katika karne za baadaye vikundi mbalimbali vilianza kupinga kuwapo kwa vyeo maalumu vya utumishi. Walisisitiza zaidi "ukuhani wa Wakristo wote" maana yake kila Mkristo hushiriki utumishi ulio mmoja tu katika Kanisa. Madhehebu mengine ya Kiprotestanti, yakikumbuka sana matatizo ya utaratibu wa kiaskofu wakati wa karne za kati, yaliona afadhali kuendelea bila cheo hicho. Wakatoliki, Waorthodoksi, Waorthodoksi wa Mashariki pamoja na Wamoravian na Waanglikana wamehifadhi ngazi za kale yaani Uaskofu, Ukasisi na Ushemasi. Nchini Tanzania Walutheri pia Wabatisti wa aina ya A.I.C. wanaheshimu cheo cha Uaskofu. Lakini kimataifa sehemu kubwa ya Walutheri, na hasa Wapresbiteriani (Reformed) na Wabatisti hawana Askofu, wakisisitiza zaidi uwezo na haki ya kila Mkristo kushiriki katika shughuli zote za utumishi akichaguliwa.

Imani ya Ukristo ni juu ya Yesu. Alikuja kwelikweli hapa duniani. Alichagua kuja katika nchi ile ya Israeli miaka 2000 iliyopita. Akawachagua wanafunzi wake ambao tunawaita "mitume". Hakika alikuwa na maana kufanya hivyo. Mitume ndio waliotekeleza maagizo ya Yesu, "Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyoamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dhahari" (Math 28:19-20). Biblia inatupa habari za aina hii: wale Mitume ni mifano ya Ukristo wetu katika nguvu au karama zao, lakini pia katika udhaifu wao.

Petro

Petro ni jina lenye maana ya "mwamba". Alikutana na Yesu akiwa mvuvi, akaendelea kuwa rafiki yake wa karibu sana. Yesu alipokamatwa, Petro alitaka kutumia upanga wake ili amtetee. Lakini alipoulizwa baadaye kama yeye ni rafiki wa Yesu aliogopa akasema hamjui.

Katika ushirika wa Yerusalemu alikuwa kiongozi muhimu. Alikuwa Mtume wa kwanza kumpokea katika Kanisa watu wasio Wayahudi bila kudai watahiriwe kwanza. Baadaye akawa katika mji mkubwa wa Antiokia. Katika taarifa ya Luka tunamwona tena Yerusalemu alipokutana na Paulo na kushauriana juu ya kupokea Wapagani katika Ukristo.

Agano Jipya ina nyaraka mbili zilizoandikwa kwa jina lake. Kumbukumbu ya kale inasema alifika mpaka Roma. Hapo aliuawa pamoja na Paulo katika mateso ya kwanza ya Wakristo chini ya serikali.

Petro ni mfano mzuri wa nguvu na udhaifu katika maisha ya Kikristo. Alikuwa na moyo mkuu kumtetea Yesu kwa upanga asikamatwe - lakini mpaka siku ile hakuelewa kwamba njia ya Yesu si njia ya silaha. Alitaka kuwa karibu na Yesu - lakini kwa hofu akamkana. Alimwingiza katika Kanisa jemadari Mpagani - lakini baadaye akawaogopa waliosema kwamba Mpagani asiingie katika ushirika mpaka awe ametahiriwa na kuwa Myahudi kwanza. Mwishoni mwa maisha yake Petro akawa shahidi wa damu kwa Bwana wake kule Roma akafa msalabani kama Yesu.

Kanisa la Roma linamkumbuka kama askofu wake wa kwanza. Kila Papa wa Kanisa Katoliki huitwa "mwandamizi wa Petro" kwani anashika cheo cha Askofu wa Roma kinachoaminika kuwa cha kwanza kati ya maaskofu wote duniani.

Paulo

Nyumba ya Mt. Anania, Damascus, Syria, ni kati ya zile za kwanza kutumika kwa ibada katika karne ya 1.

Paulo hakuwa mfuasi wa Yesu alipokuwa duniani. Alikuwa Myahudi Farisayo mzaliwa wa Tarso (mji wa Kilikia, leo nchini Uturuki). Alikwenda Palestina kwa masomo ya kidini. Tunasikia habari zake alivyohusika na kifodini cha Stefano (Mdo 6).

Baadaye akatumwa na Baraza Kuu la Kiyahudi kuwatafuta Wayahudi waliojiunga na Ukristo na kuwakamata kama wakosaji. Aliposafiri hadi Dameski (mji mkuu wa Siria) kwa ajili hiyo, Yesu alimtokea katika ono akaongoka kuwa Mkristo. Hivyo mtesaji wa Wakristo akawa mhubiri mkuu wa Injili.

Hakuna mwingine kati ya mitume wote aliyesafiri, kuhubiri na kuanzisha shirika kama Paulo. Katika safari kubwa tatu alizunguka Asia Magharibi na Ulaya Kusini. Akaendelea kufundisha shirika alipoondoka kwa njia ya barua (au nyaraka). Nyaraka zake mbalimbali zimehifadhiwa katika Agano Jipya. Katika nyaraka hizo Paulo anaonekana kuwa mtaalamu wa Sheria ya Kiyahudi ilivyo katika Agano la Kale. Akatetea kupokea Wapagani katika Kanisa akafundisha jinsi gani uhuru katika Kristo unavyopita masharti ya sheria ya kale.

Mwishoni akakamatwa kule Yerusalemu akashtakiwa ya kuwa amehatarisha amani. Kama mzaliwa wa Tarso alikuwa na uraia wa Roma akadai haki yake ya kukata rufaa kule, mbele ya Kaisari. Akapelekwa Roma (Mdo 28). Hatuna hakika juu ya kesi yake. Labda alipata nafasi ya kusafiri tena na kuhubiri Injili mpaka Hispania. Lakini kumbukumbu ya kale inatuambia kwamba aliuawa baada ya Petro kwa kukatwa kichwa katika mateso ya kwanza ya Wakristo (64-68 BK).

Paulo ni mfano mzuri jinsi gani mtu aliyepinga Injili vikali aliongozwa kuihubiri. Nyaraka zake zinatuonyesha jinsi gani Mkristo anaweza kutumia akili yake pamoja na imani. Katika maandishi yake tunapata mtu aliyebebwa na imani katika matatizo na mateso makubwa. Anatufundisha kutoangalia Ukristo kama sheria au amri tu (Fanya! Acha!) bali kama jibu la upendo la mtu aliyeelewa upendo wa Mungu kwanza.

Thoma

Mtume anayekumbukwa sana kule India ni Thoma (au: Tomaso) aliyefika mpaka Bara Hindi. Kaburi lake huonyeshwa katika mji wa Madras. Mpaka leo wako "Wakristo wa Thoma" kusini-magharibi mwa Bara Hindi. Kwa muda mrefu walikosa mawasiliano na Wakristo wengine waliokuwa mbali, lakini siku hizi wanashiriki katika umoja wa Kanisa duniani.

Muhtasari wa historia ya Kanisa

Makala kuu: Historia ya Kanisa
Samaki ilipata kuwa ishara ya Ukristo, kutokana na jina lake la Kigiriki lililoandikwa hivi huko Efeso, Uturuki.

Ukristo ulianza Mashariki ya Kati kama madhehebu ya Uyahudi ukaenea haraka kwa watu wa mataifa mengine mengi ya Asia, Afrika na Ulaya hivi kwamba waamini wenye asili ya Kiyahudi walizidi kuwa asilimia ndogo hasa kufikia mwisho wa karne ya 1.

Kwa juhudi za Mitume waliowahi kuchaguliwa na Yesu na za wengineo, hasa Mtume Paulo. Ukristo ulienea hasa ndani ya mipaka ya Dola la Roma na kupokea yaliyo mema kutoka umataduni hasa wa Wagiriki (mashariki) na Walatini (magharibi), bila kukwamishwa na dhuluma za serikali zilizodumu kwa kwikwi miaka karibu 250 (64-313). Hata nje ya dola hilo, Ukristo ulikabiliana na dhuluma, kama vile Mesopotamia na Uajemi, ambapo ulidumisha zaidi sura asili ya Kisemiti.

Wakati wa maisha ya Mitume, dhuluma zilizotabiriwa na Yesu zilianza kutoka kwa Wayahudi wasiomuamini na kutoka kwa watu wengine. Wa kwanza kuuawa alikuwa Stefano, na kati ya Mitume Yakobo Mkubwa. Kabla ya kufa, wengi kwa kuuawa, mitume waliweka waandamizi wao, ambao kati yao maaskofu mwanzoni mwa karne ya 2 walikuwa wameshika uongozi wa makanisa wakisaidiwa na mapadri na mashemasi.

Wakati huohuo vitabu vingi vya Kikristo vilivyotungwa katika nusu ya pili ya karne ya 1 vilizidi kuenea na kukusanywa hadi vikaunda Agano Jipya.

Baada ya hapo vitabu viliendelea kuandikwa kwa kutetea, kutangaza na kufafanua imani sahihi: ndiyo mwanzo wa teolojia kama fani maalumu. Tofauti za ufafanuzi huo, kama zile kati ya shule ya Aleksandria na shule ya Antiokia, ndizo chanzo cha mabishano yaliyochangia mafarakano makubwa yaliyotokea hasa katika karne ya 5, ingawa kuanzia mwaka 325 mitaguso mikuu ilikusanya maaskofu wengi kutoka sehemu mbalimbali ili kumaliza migogoro. Tofauti za lugha na utamaduni, pamoja na utaifa, zilichangia sana mafarakano.

Monasteri ya Khor Virap (karne ya 7) ikiwa na Mlima Ararat nyuma yake, Armenia.[10]

Maendeleo mengine muhimu yalipatikana katika maisha ya Kiroho kwa uanzishaji wa umonaki wa Kikristo, kwanza katika majangwa ya Misri, halafu sehemu nyingine zote. Juhudi za watu hao zilichochea waumini wenzao pia kuwa waaminifu katika ulimwengu uliozidi kuwashawishi badala ya kuwatesa.

Ni kwamba kufikia mwisho wa karne ya 4 Ukristo ulikuwa dini rasmi ya Dola la Roma ambalo kabla ya hapo kwa miaka karibu 250 (64-313) lilikuwa limeukataza kikatili. Kabla yake Armenia ilikuwa nchi ya kwanza kupokea Ukristo kama dini ya taifa (301). Ushindi huo ulifanya wengi watamani vyeo ndani ya Kanisa, kwa kuwa viliendana sasa na heshima na mali: hivyo ubora ulipungua.

Dola la Roma Magharibi lilipozidi kudhoofiwa na uvamizi wa Wagermanik na makabila mengine yasiyostaarabika, askofu wa Roma kama mchungaji mkuu alilazimika kuwajibika ili kuokoa jahazi. Ndivyo walivyofanya hasa Papa Leo I na Papa Gregori I. Kwa juhudi za wamonaki Wabenedikto na wengineo, ustaarabu wa kale uliokolewa katika vitabu vyake na uinjilishaji uliendelea katika Ulaya ya Kati.

Picha kadhaa zikionyesha Wakristo maarufu na athari ya Ukristo katika utamaduni.

Kumbe, uenezi wa Uislamu kuanzia karne ya 7 ulidhoofisha na pengine kukomesha kabisa Ukristo katika nchi nyingi, ukirudisha nyuma ustawi wa Kanisa lote. Hata hivyo, mwanzoni mwa karne ya 8, Uislamu ulizuiwa na Wafaranki kuenea zaidi Ulaya bara. Kabila hilo kubwa la Kigermanik liliwahi kujiunga na Kanisa Katoliki likawa msaada mkubwa kwa Mapapa. Isipokuwa kwa kuwaachia watawale Italia ya Kati, walisababisha Papa aanze kuwa kama mfalme wa dunia hii, jambo lililoathiri sana majukumu yake ya kiroho hadi mwaka 1870.

Katika Karne za Kati Ulaya yote ilikwisha kuwa ya Kikristo. Kutoka huko ulienea, pamoja na ustaarabu wa magharibi ulioathiriwa sana na Ukristo, katika Amerika yote na sehemu nyingine za dunia.

Mafarakano makuu kati ya Wakristo

Matawi ya Ukristo yalivyotokea katika historia ya Kanisa. Upande wa juu ndio Kanisa la Magharibi, upande wa chini Makanisa ya Mashariki. Unene wa mistari haulingani na ukubwa wa madhehebu husika.
Ibada ya pamoja katika monasteri ya kiekumeni Taizé, Ufaransa.

Katika historia ndefu ya Ukristo, yalitokea mafarakano mengi, waamini wa Yesu wakizidi kutofautiana. Makundi makubwa zaidi ni: Kanisa Katoliki, Makanisa ya Waorthodoksi na ya Waorthodoksi wa Mashariki na madhehebu ya Uprotestanti. Hasa tangu mwaka 1910 madhehebu mengi yanashiriki juhudi za ekumeni kwa ajili ya kurudisha umoja wa awali.

Wakatoliki

Zaidi ya nusu ya Wakristo wote wanashikamana katika imani na sakramenti chini ya maaskofu wenye ushirika kamili na yule wa Roma, ambaye kwa kawaida anaitwa Papa.

Kati yao umoja unazingatiwa sana kama sifa ya kwanza ya Kanisa inayotambulisha wanafunzi wa Yesu.

Neno "Katoliki" tunaendelea kulitumia zaidi kwa maana ya madhehebu maalumu yenye wafuasi wengi duniani. Kiteolojia linamaanisha "Kanisa lililopo popote, lililo moja tu kila mahali na kila wakati". Kwa maana hiyo kila Mkristo yumo katika Ukatoliki, kwani mbele ya Kristo Kanisa ni moja tu, kila mahali duniani.

Waanglikana, Walutheri, Wamoravia na wengineo huamini kabisa kwamba wenyewe ni sehemu ya Kanisa lile moja la Bwana Yesu lililopo mahali popote.

Upande mwingine, hata Kanisa “Katoliki" linaloongozwa na Askofu (Papa) wa Roma ni la "Kiinjili" kwani linakubali na kutangaza Injili (= “habari njema”) ya Yesu Kristo.

Waorthodoksi na Waorthodoksi wa Mashariki

Kanisa kuu la Kristo Mwokozi huko Moscow ni refu kuliko yote ya Waorthodoksi duniani.

Wakristo wengi walioishi upande wa mashariki wa Dola la Kirumi na ng'ambo ya mipaka yake ya mashariki walitengana na Wakatoliki hasa katika karne V (Waorthodoksi wa Mashariki) na karne XI (Waorthodoksi).

Hata hivyo msimamo wao wa imani si tofauti sana, kwa kuwa wanachanga mapokeo ya awali ya Kanisa la Mitume na la Mababu.

Waprotestanti

Utitiri wa madhehebu ya Waprotestanti ndio wenye tofauti kubwa zaidi kati yao wenyewe na kati yao na Wakristo waliotajwa kwanza.

Hiyo ilitokana na msimamo wa msingi wa urekebisho wa Kiprotestanti wa kutaka kila mmoja aweze kutafsiri Biblia alivyoielewa, bila kutegemea mapokeo wala mamlaka rasmi ya Kanisa, ila msaada wa Roho Mtakatifu.

Umoja halisi wa Kanisa unaweza kupatikana tu katika ukweli wa Injili ya Yesu Kristo. Ni habari mbaya kwamba katika karne ya 16 kuupigania ukweli huo kulivunja umoja wa Ukristo wa magharibi. Haiwezekani kushangilia mafarakano ya wafuasi wa Yesu.

Yale ya karne hiyo yalitokana na kuelewa tofauti kweli za imani ya Kikristo na yalikuwa na ukali kwa sababu pande zote zilisadiki kwamba kushikilia kwa usahihi ufunuo wa Mungu ni suala la wokovu wa milele. Kwa mfano, Martin Luther aliandika,«Sikubali mafundisho yangu yahukumiwe na yeyote, hata kama ni malaika. Asiyekubali mafundisho yangu hawezi kufikia wokovu».[11]

Pamoja na hayo, mambo mengi yalichangia farakano, si teolojia tu, bali siasa, uchumi, jamii na utamaduni. Wakati huo mara nyingi hoja za imani na malengo ya kisiasa vilichanganyikana: wanasiasa wengi walitumia hoja hizo ili kufikia malengo ya kiutawala, na vilevile wanateolojia walitumia siasa kutetea mafundisho yao ili kuvuta watu. Ndiyo sababu Luther alichorwa kama shujaa wa taifa la Ujerumani.

Mara nyingi pande zote zilipotosha maana ya wapinzani na kuwachora vibaya wakivunja amri ya nane inayokataza uongo dhidi ya jirani. Hata waliojitahidi kusema ukweli tu juu ya wengine kwa kawaida hawakujitahidi vya kutosha kuelewa msimamo wao na kuona kwamba pengine si mbaya zaidi. Kila mmoja alitaka ushindi akachangia ugomvi uliorithishwa kwa vizazi vilivyofuata.

Hivyo, kilichosababisha zaidi farakano si masuala ya imani yaliyojadiliwa na Waprotestanti, bali lawama zao dhidi ya hali mbaya ya Kanisa la wakati huo iliyokuwa inakera wengi na kuwaelekeza kuunga mkono urekebisho.

Hapo kale neno hilo (kwa Kilatini reformatio) lilihusu badiliko la hali mbaya iliyopo ili kurudia hali nzuri zaidi ya awali. Katika Karne za Kati lilitumika mara nyingi kwa marekebisho ya umonaki. Katika karne ya 15 haja ya urekebisho ilionekana wazi si tu kwa mashirika ya kitawa bali kwa Kanisa lote. Hasa Mtaguso wa Konstanz (1414-1418) ulidai kabisa ufanyike «katika kichwa na katika viungo». Lakini kwa jumla mitaguso yote ya Karne za Kati na mikutano mingi ya Bunge la Dola la Ujerumani ililenga urekebisho wa Kanisa.

Kwa kweli Karne za Kati zilikuwa na mchanganyiko wa mambo yaliyopingana: ibada za nje tu na za dhati kabisa; teolojia iliyoelekeza kutenda kwa msingi wa nipe nikupe na hakika ya kwamba binadamu anategemea kabisa neema ya Mungu; kutojali wajibu hata upande wa viongozi wa Kanisa na marekebisho safi ya mashirika ya kitawa.

Karne ya 15 ilikuwa kipindi cha umotomoto wa pekee katika Kanisa, ambapo walei wengi zaidi na zaidi walipata elimu nzuri, hivyo walitamani hotuba bora na mafundisho ya kuwasaidia kuishi Kikristo zaidi. Luther aliitikia haja hizo zilizomgusa sana kama mtu wa wakati wake.

Luther alitumia kwa nadra neno urekebisho, lakini likaja kuwa jina la kawaida la matukio yale mengi ya miaka 1517 - 1555, yaani kuanzia uenezi wa hoja 95 za Martin Luther hadi amani ya Augsburg. Kati yake chanzo, yaani mabishano ya Kikanisa yaliyosababishwa na teolojia ya Luther, yalichanganyikana mapema na siasa, uchumi na utamaduni, kutokana na hali halisi ya wakati huo, mbali kuliko mwenyewe alivyofikiri.

Viongozi mbalimbali wakaiga mfano wa Luther, ila juhudi zao zikatofautiana: ndio mwanzo wa madhehebu mengine yanayoitwa ya "Kiinjili". Jina hilo linataka kusisitiza kwamba yanasimama kwenye msingi wa Injili tu, kinyume cha Kanisa Katoliki lililoona mapokeo yake kuwa na umuhimu pamoja na Biblia.

Kumbe wafuasi wa Luther na wengineo waliitwa na Wakatoliki "Waprotestanti", maana yake "wapinzani" (to protest = kupinga): neno hilo lilianza kutumika tangu wafuasi wa Luther walipopinga azimio la bunge lililotaka Wajerumani wote warudi chini ya Papa wa Roma.

Tangu mwaka 1907 tapo la Wapentekoste limeenea duniani kote (linakadiriwa kuwa na waumini milioni karibu 300) na kuathiri hata madhehebu yote ya zamani (ambapo mara nyingi waumini wa aina hiyo wanaitwa "Wakarismatiki").

Kanisa leo

Nchi ambapo Wakristo ni 50% au zaidi zimechorwa rangi ya zambarau, na zile ambapo ni kati ya 10 na 50% zina rangi ya waridi
Nchi ambapo Ukristo ni dini rasmi:

     Ukristo wa Kiorthodoksi      Ukristo wa Kiprotestanti (pamoja na Anglikana)

     Ukristo wa Kikatoliki
Uwepo wa Wakristo duniani: Rangi nzito inaonyesha asilimia kubwa zaidi ya Wakristo[12]

Kwa miaka 100 ya mwisho asilimia za Wakristo kati ya watu wote zimebaki 33, yaani mmoja kwa watatu, lakini uwiano kati ya mabara umebadilika sana, kwa maana katika Afrika, Asia na nchi nyingine zinazoendelea Wakristo wameongezeka, kumbe Ulaya na Amerika Kaskazini wamepungua[13]Pew Research Center inakadiria kwamba mwaka 2050, watazidi bilioni tatu.[14]. Wakati huo Wakatoliki na Waprotestanti huenda wakalingana kwa idadi[15][16].

Kuhusu maeneo ambako Wakristo wanapungua, ni kwamba, kutokana na historia ya Kanisa kuwa na mchanganyiko wa mazuri na mabaya, wengine wanahisi kuwa halina maana tena. Pia kuna makundi kama Wakomunisti na Wamasoni ambayo yanakusudia kabisa kufuta Ukristo kwa kutangaza kasoro za waumini na viongozi wao, pamoja na kuhimiza watu kwenda kinyume cha maadili.

Hali hii inajionyesha hasa pale ambapo waamini wengi, hasa Ulaya, wameacha kwenda kanisani isipokuwa siku ya Krismasi na Pasaka au kwenye harusi na misiba.

Pia kutokana na mgawanyiko wa madhehebu, kumekuwa na mkanganyiko kuhusu kazi ambazo zinalipasa Kanisa la leo.

Sala na ibada

Padri akiadhimisha Misa katika Basilika la Bikira Maria, Bangalore, India.

Mafundisho ya Yesu kuhusu sala hayatii maanani taratibu maalumu. Badala yake yeye alisisitiza msimamo wa ndani wa kumuendea Mungu kwa imani na unyofu kama vitoto wanavyohusiana na baba zao. Ndivyo mwenyewe alivyosali katika Roho Mtakatifu aliyewaahidia wafuasi atawaongoza badala yake.

Kwa msingi huo, katika historia ya Kanisa namna nyingi za kusali zimetokea kwa maisha ya Kiroho ya Mkristo binafsi na kwa jumuia nzima pamoja. Kwa kawaida, taratibu za kuendesha ibada zinaitwa liturujia (kutoka maneno ya Kigiriki yenye maana ya “kazi ya hadhara”).

Wakatoliki, Waorthodoksi, Waorthodoksi wa Mashariki, Waanglikana, Wamethodisti, Walutheri na wengineo wanafuatilia desturi kama walivyozipokea. Mtiririko wa ibada zao huandikwa na hujulikana kama Liturujia.

Bendi ya Kiprotestanti ikiongoza ibada inayofanana na tamasha.

Madhehebu mengine, hasa yale ya Kipentekoste, huwa na ibada ambazo hazijaandikwa kitabuni: kiongozi wa ibada wa siku hiyo huja na madondoo yake na mtiririko wa ibada huenda kama "Roho" atakavyoongoza siku hiyo. Kwa sababu hiyo husema kwamba hawafuati desturi au mapokeo.

Ukiangalia zaidi utaona kuwa ibada zao pia huwa na mtindo na mtiririko fulani, kama vile kuimba mapambio ya harakaharaka wakiwa wanapiga makofi, kucheza na kurukaruka. Mapambio hayo hufuatiliwa na mengine ya taratibu wakiinua mikono kuabudu. Inawezekana kusema hao nao wana utaratibu au liturujia yao ingawa haijaandikwa kwenye vitabu.

Wakristo wanahesabu ufufuko wa Yesu kuwa msingi mkuu wa imani yao (1Kor 15:14): ndiyo sababu karibu wote wanaabudu hasa Jumapili, ambayo ndiyo siku ya tukio hilo kuu la historia yote. Ila asilimia 1 inashika Sabato, iliyo siku ya wiki ambapo Wayahudi hupumzika na kuabudu.

Haki na amani

Mama Teresa wa Kolkata.

Upande mwingine wanakanisa wanajaribu kuonyesha jitihada zao katika jamii, ikiwa ni pamoja na kuleta amani na maendeleo na kutoa misaada ya kijamii. Kuna uwezekano kwa madhehebu kadhaa kubadilisha mkazo wao kuutoa kwenye imani tu na kuuweka kwenye huduma za jamii au elimu: hii inafanya yaonekane kama moja ya mashirika ya hisani.

Katika nchi nyingi Kanisa limekuwa nguvu ya kutetea haki za binadamu. Tumesikia habari za Desmond Tutu kule Afrika Kusini au za Janani Luwum katika Uganda, jinsi walivyojaribu kutetea haki za wananchi dhidi ya utawala mbaya. Ikiwa Wakristo wanajisikia wito wa kusimama na kusema mbele ya wakubwa hukumbuka manabii wa Agano la Kale hadi Yohane Mbatizaji. Wanakumbuka pia Wakristo wengi katika historia walioweza kusimama mbele ya wafalme na kutetea haki za watu. Labda tunamkumbuka Askofu Ambrosi wa Milano (aliyemvuta kijana Agostino kuwa Mkristo) alivyomtenga Kaisari na Kanisa kwa sababu ya uuaji wa wananchi wengi wasio na kosa uliofanywa na wanajeshi wa serikali. Msingi wake ni katika mafundisho juu ya kazi ya uumbaji. Mbele ya Mungu tuko sawa: kuna msingi gani kuona wengine ni sawa zaidi?

Lakini si Wakristo wote wanakubali na kufurahia msimamo wa aina hiyo. Wengine huona imani ya Kikristo haihusiki na taratibu za dunia hii au huona ni wajibu wa Mkristo kutii serikali yoyote wakikumbuka maneno ya Mtume Paulo katika Rum 13. Pamoja na hayo katika Ukristo yapo mapokeo ya kutoshindana na wenye mamlaka bali kuwavumilia katika yote. Labda huona hofu ya kuwa dini inaingizwa mno katika siasa.

Binadamu wa karne ya 21 wanahitaji jibu litakalosaidia kuwakwamua kutoka matatizo yao. Wenye dini mbalimbali, hususan Wakristo, wanadai kujua ufumbuzi wa matatizo makuu ya binadamu, ingawa wachache tu wameweza kuonyesha dhahiri matatizo yaliyotatuliwa kabisa kwa dini. Wakati mwingine wanadini wenyewe wamekuwa chanzo cha matatizo badala ya kuyatatua.

Jibu linaweza kupatikana katika maneno ya Yesu mwenyewe, aliposema kwamba wafuasi wake ni chumvi ya dunia, ambayo ilete ladha katika maisha ya watu, lakini kama chumvi hiyo inapoteza ladha yake, haifai kitu, isipokuwa kutupwa na kukanyagwa kwa dharau. Hivyo changamoto ya Wakristo ni kufuata vema mafundisho ya imani yao ili kukidhi hitaji la nyakati hizi la kuishi kwa amani, furaha na upendo duniani kote .

Uhusiano na dini nyingine

Ukristo na dini nyingine zinahusiana kwa kiasi tofauti, kadiri ya mazingira asili, historia, mafundisho kuhusu imani na maadili, desturi, ibada n.k.

Ukristo na Uyahudi

Ni wazi kuwa Ukristo unahusiana zaidi na dini ya Uyahudi, kwa sababu unatokana nayo na kutumia vitabu vyake vitakatifu (Tanakh na pengine Deuterokanoni pia). Haiwezekani kumuelewa Yesu kwa kumweka nje ya mazingira ya Kiyahudi.

Dini hizo mbili zilitengana moja kwa moja miaka 50 hivi baada ya Yesu kuaga dunia. Ni kwamba Wayahudi wa shule ya Jabneh (mwaka 80 hivi B.K.) waliamua kuwatenga kama wazushi wananchi wenzao waliomuamini Yesu Kristo, hasa baada ya kuona hawakusaidia vita vya ukombozi dhidi ya wakoloni Warumi vilivyosababisha maangamizi ya Hekalu la pili na mji wa Yerusalemu mwaka 70 B.K.

Tangu hapo Wakristo hawakushiriki tena ibada pamoja na Wayahudi, wakazidi kuzingatia sakramenti ya Kumega Mkate katika Siku ya Bwana (Jumapili, siku inaposadikika Yesu alifufuka) badala ya Sabato (Jumamosi, siku ya pumziko ya Wayahudi). Kabla ya hapo Wakristo wa Kiyahudi walikuwa wanashika siku zote mbili.

Ukristo na Ubuddha

Hakuna uhusiano wa kihistoria kati ya Yesu na Ubuddha. Hata hivyo mambo kadhaa yanafanana.

Yesu alifundisha kuhusu nidhamu mbili zinazompelekea mtu kuwa mwadilifu na hatimaye kuurithi utukufu wa kiroho ambao karama yake ni uzima wa milele: hizo ni kumpenda Mungu kwa moyo wako wote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote, na jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.

Buddha alifundisha hali ya kutodhuru viumbe hai wowote, tena kuwa na moyo mkuu wa mapenzi kwa vitu vyote. Hii ni miongozo inayolenga mtu atambue tabu anazodumisha yeye mwenyewe, kwa matendo yake na upeo ulio na mipaka, katika maisha yake ya kila siku.

Baada ya hili, mafundisho ya Kristo yanatofautiana katika kuchukulia hali hii. Kwa mujibu wa Kristo, dhambi, matendo yenye kukosea kanuni za kiroho na hata za kimaumbile, hufutwa na toba; wakati katika mafundisho ya Buddha, makosa yote yanatokana na kutokuwa makini. Hivyo, kwa mujibu wa Buddha, njia pekee ya kumkomboa mtu na shida zake ni kufuata mwongozo wa Nguzo Nane ambazo humweka katika hali ya kuweza kuamka kiroho wakati utulivu wa kimwili na wa kiakili unapofikiwa. Haya ndiyo yanayofanya Ubuddha kuwa ni njia inayojali sana nidhamu ya mtu kimatendo, wakati Ukristo hufuata sana moyo wenye kukiri makosa, na kutafuta uadilifu wa kweli wa kiroho. Huu ni uzuri wa pekee kutoka kwenye mafundisho ya Yesu: Tubuni kwa kuwa saa ya ukombozi ni sasa...

Jingine lenye tofauti ni kuwa Kristo hufundisha kuhusu Upendo kwamba ni Mungu, kwa kuwa Upendo una maana kuliko elimu yote ya binadamu, nao ndio unaounganisha na kutunza vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Hilo hutambulika kupitia Kristo ambaye hujidhihirisha kwa yule mwenye kumpokea Roho wa Mungu. Upande wa Buddha, hukanusha nafsi na pia Mungu, akisema: Ni Buddha mwenye ufahamu wa milele, tena hana nafsi isipokuwa Utupu; na ni wenye furaha isiyo kifani izidiyo yote yenye kufanyika ulimwenguni, yaani Nirvana; kila mtu ni Buddha aliyesahau asili yake ya ndani kabisa.

Ukristo na Uislamu

Ukristo na Uislamu vinafanana zaidi kwa sababu Muhammad alifahamu Wayahudi na Wakristo wengi katika nchi yake na katika safari zake. Dini hizo tatu zinajulikana kwa kushika imani katika Mungu Pekee, muumba wa vitu vyote, na kwa kumchukua Abrahamu kama kielelezo cha imani na rafiki wa Mungu.

Mafundisho ya msingi ya Uislamu ni unyenyekevu kwa Mola mmoja aitwaye Allah , mwingi wa rehema na mwingi wa fadhila; nguzo ya Uislamu ni kumuabudu. Katika Uislamu, unyenyekevu wa mtu katika kumcha Mola kwa ibada na swala humpa kukirimika na kuhifadhika kwa Mola wake mwenye fadhila, ambaye atamtunuku haki yake. Naye mnyenyekevu kwa Mola ataishi kuona utukufu mwingi wa Mola wenye kutajwa katika Kurani kwa majina 99 ya Allah. Kati ya sifa na utukufu huo ulio na majina mengi, baadhi yake ni Al Rahman (kwa Kiarabu, "Mwenye rehema"), Al Nur ("Mwenye nuru") n.k. Hayo hufanana na neno la Nuru ya Bwana, rehema na ukombozi kuwa utukufu wa Mbingu katika mwongozo wa Kikristo.

Pia Uislamu unafundisha udugu miongoni mwa Waislamu yaani mzizi wa neno linalotumika sana katika Kurani: Waly (Wala, Wilayat, Mawla, Awla) katika kueleza jinsi Mwislamu apasavyo kuishi karibu na mwenzake. Nalo husisitiza upendo na kulindana kwa heri na pia kuepushana na shari. Hilo linafanana na upendo ambao katika Ukristo ndio adili kuu kuliko yote:

Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo... mimi si kitu kabisa. (1 Wakorintho 13:1-11).

Lakini katika Ukristo upendo hauna mipaka wala masharti. Unatakiwa kuenea kwa maadui pia na kusamehe kila mara kufuatana na mfano wa Baba wa Mbinguni.

Mwislamu kadiri ya wingi wa unyenyekevu na usafi wa moyo wake huakisi sifa za Mola wake. Uislamu hufundisha kuhusu vita vya ndani ambavyo muumini hupigana na nafsi yake yenye matamanio ya chini, ambayo huzaa chuki, dhuluma, wivu na maovu mengine ili kuishinda kwa utukufu wa Mola na kudumisha dini (mwongozo) yake katika ngazi zote za maisha.

Kabla yake Yesu alihimiza wote wafuate mfano wake wa upole na unyenyekevu wa moyo, akitoa kielelezo katika Heri Nane za hotuba ya mlimani. Tofauti ya msingi ni kuwa kwa mujibu wa Kristo, ni kwa neema ya imani katika Neno la Uzima kwamba mtu hukombolewa kutoka matamanio yake ya kibinadamu, mbali ya kwamba anapaswa kujitahidi asije akapotewa na neema hiyo na kurudia utumwa wa dhambi.

Ni imani ya Wakristo na ya Waislamu kwamba Yesu atarudi duniani kwa utukufu, ingawa jambo hilo wanalitafsiri kwa namna tofauti.

Uhusiano wa Wakristo na Waislamu una umuhimu wa pekee kwa ajili ya amani na maendeleo ya nchi. Katika sehemu mbalimbali Wakristo na Waislamu waliwahi kushirikiana vema katika mambo mengi ya kijamii lakini uhusiano huo umeanza kuwa mgumu.

Sababu moja ni mzigo wa historia tunaoubeba mara nyingi bila kujua. Mzigo huo ni urithi wa mahusiano magumu kati ya Waislamu na Wakristo kule Ulaya na Asia. Itakuwa muhimu sana kwa vijana wa leo kukataa mzigo wa historia na kuvumiliana.

Kwa mfano, Waislamu wanaweza kutumia neno "jihadi" wakiongea juu ya jitihada za kuimarisha jumuiya yao au kueneza imani yao, lakini Wakristo walio wengi wanasikia neno hilo vibaya kwa sababu "vita vitakatifu" vya Waislamu vilivyoitwa "jihadi" vilileta mateso mengi kwa Wakristo katika nchi mbalimbali. Kumbe neno halimaanishi vita hasa ila liliwahi kutumika hivyo tangu muda mrefu.

Vilevile Wakristo wengi hawaoni tatizo kutumia neno "Crusade" kwa ajili ya mikutano ya kiroho. Lakini Waislamu wanaweza kuchukua neno hili vibaya pia kwani kiasili "Crusade" (maana yake "Vita vya Msalaba") linamaanisha hasa kipindi cha miaka 800 hivi iliyopita. Wakati ule Wakristo wa Ulaya Magharibi walijaribu kufuta utawala wa Kiislamu katika nchi za Mashariki ya Kati kwa vita vilivyoendelea kwa kwikwi muda wa miaka 200.

Ukristo na Uislamu viko karibu katika mambo mengi lakini hutumia mafundisho yanayogongana katika sehemu nyingine, hivyo mpaka leo hii kwa Waislamu ni vigumu sana kupokea Injili. Wakati wa vita vya msalaba Fransisko wa Asizi aliona hakuna njia ya kuwavuta Waislamu kwa mabavu. Mashindano pekee yanayoruhusiwa kwa Mkristo ni yale ya upendo ya kumfuata Yesu.

Kwa jumla mawazo ya Mt. Fransisko yamethibitishwa na historia. Kwa hiyo si vibaya kujiandaa kushirikiana na Waislamu Kikristo kwa kufahamu kidogo imani yao na kutambua sifa nzuri zilizopo katika maisha na mafundisho yao pia.

Wakristo kwa jumla wasijivunie sifa zao kuwa bora kuliko za Waislamu. Anayesoma "Historia ya Kanisa" ataona mifano mingi ya jinsi Wakristo walivyosahau mafundisho ya Yesu na kutendeana kwa unyama. Kwa hiyo mtu asijivune kwamba Ukristo ni dini ya upendo au imani yenye maendeleo kama mwenyewe si mfano wa upendo huo na maendeleo hayo.

Kwa Wakristo wengi ni fumbo kwa nini Mungu alikubali kutokea kwa dini hiyo mpya. Lakini mwanzoni mwa Uislamu Mfalme Mkristo wa Ethiopia alipokea na kuhifadhi wakimbizi Waislamu kutoka Maka. Mapokeo ya Kiislamu yanasema mfalme huyu aliyekuwa na jina "Negasi" aligeukia Uislamu baadaye. Lakini "Negasi" si jina la mtu fulani, ni cheo cha wafalme wote wa Ethiopia hadi mwaka 1974 (kwa kawaida huandikwa "Negus"). Halafu hakuna kumbukumbu ya kwamba mfalme yeyote wa karne zile aliacha Ukristo wake.

Ukristo na dini za jadi

Kuhusu wanaofuata bado imani asilia pia ni kwamba wanatunza katika mila na desturi zao urithi wa utamaduni. Hata maadili mengine yanayofundishwa kwao yanalingana na sehemu za Biblia. Hakika si vema Wakristo wakiwacheka na kuwaita kwa majina ya dharau kama "Wapagani".

Hata juu ya imani hizo za jadi ni kweli kwamba zilimjua Mungu kwa namna fulani kutokana na uumbaji wake jinsi alivyoandika Mtume Paulo katika Rom 1.

Tazama pia

Tanbihi

  1. Neno "Mkristo" (Χριστιανός) lilitumika mara ya kwanza kuhusiana na wafuasi wa Yesu katika mji wa Antiokia [Mdo 11:26] mwaka 44 BK. Wenyewe walikuwa wanajiita "ndugu", "waamini", "wateule", "watakatifu". Katika mazingira ya Kisemiti waliendelea na bado wanaendelea kuitwa "Manasara", yaani "Wanazareti" kutokana na jina la kijiji alikokulia Yesu. Kumbukumbu ya kwanza ya mwandishi ya neno "Ukristo" (Χριστιανισμός) ni katika barua za Ignas wa Antiokia, mwaka 100 hivi. See Elwell/Comfort. Tyndale Bible Dictionary, pp. 266, 828.
  2. Taz. Catholic Encyclopedia (article "Monotheism"); William F. Albright, From the Stone Age to Christianity; H. Richard Niebuhr; About.com, Monotheistic Religion resources; Kirsch, God Against the Gods; Woodhead, An Introduction to Christianity; The Columbia Electronic Encyclopedia Monotheism; The New Dictionary of Cultural Literacy, monotheism; New Dictionary of Theology, Paul, pp. 496–99; Meconi. "Pagan Monotheism in Late Antiquity". p. 111f.
  3. Hinnells, The Routledge Companion to the Study of Religion, p. 441.
  4. Zoll, Rachel. "Study: Christian population shifts from Europe", December 19, 2011. Retrieved on 25 February 2012. 
  5. The Global Religious Landscape: Christianity. Pew Research Center (December 2012). Jalada kutoka ya awali juu ya 2015-09-24. Iliwekwa mnamo 2012-07-30.
  6. 33.39% of ~7.2 billion world population (under the section 'People') World. CIA world facts. Jalada kutoka ya awali juu ya 2010-01-05. Iliwekwa mnamo 2015-07-09.
  7. Christianity 2015: Religious Diversity and Personal Contact. gordonconwell.edu (January 2015). Jalada kutoka ya awali juu ya 2017-05-25. Iliwekwa mnamo 2015-05-29.
  8. Major Religions Ranked by Size. Adherents.com. Jalada kutoka ya awali juu ya 2013-06-22. Iliwekwa mnamo 2009-05-05.
  9. ANALYSIS (2011-12-19). Global Christianity. Pewforum.org. Iliwekwa mnamo 2012-08-17.
  10. Hitilafu ya kutaja: Invalid <ref> tag; no text was provided for refs named Armenia
  11. Martin Luther, Weim., X, P. Il, 107, 8-11
  12. ANALYSIS (2011-12-19). Table: Religious Composition by Country, in Percentages. Pewforum.org. Iliwekwa mnamo 2012-08-17.
  13. Werner Ustorf. "A missiological postscript", in McLeod and Ustorf (eds), The Decline of Christendom in (Western) Europe, 1750–2000, (Cambridge University Press, 2003) pp. 219–20.
  14. The Future of World Religions: Population Growth Projections, 2010-2050. Jalada kutoka ya awali juu ya 2015-05-06. Iliwekwa mnamo 2017-03-14.
  15. Johnstone, Patrick, "The Future of the Global Church: History, Trends and Possibilities", p. 100, fig 4.10 & 4.11
  16. Hillerbrand, Hans J., "Encyclopedia of Protestantism: 4-volume Set", p. 1815, "Observers carefully comparing all these figures in the total context will have observed the even more startling finding that for the first time ever in the history of Protestantism, Wider Protestants will by 2050 have become almost exactly as numerous as Roman Catholics – each with just over 1.5 billion followers, or 17 percent of the world, with Protestants growing considerably faster than Catholics each year."

Marejeo

  • Albright, William F. From the Stone Age to Christianity.
  • Alexander, T. Desmond. New Dictionary of Biblical Theology.
  • Bahnsen, Greg. A Reformed Confession Regarding Hermeneutics (article 6) Archived 4 Desemba 2014 at the Wayback Machine..
  • Ball, Bryan; Johnsson, William (ed.). The Essential Jesus. Pacific Press (2002). ISBN 0-8163-1929-4.
  • Barrett, David; Kurian, Tom and others. (ed.). World Christian Encyclopedia. Oxford University Press (2001).
  • Barry, John F. One Faith, One Lord: A Study of Basic Catholic Belief. William H. Sadlier (2001). ISBN 0-8215-2207-8
  • Benton, John. Is Christianity True? Darlington, Eng.: Evangelical Press (1988). ISBN 0-85234-260-8
  • Bettenson, Henry (ed.). Documents of the Christian Church. Oxford University Press (1943).
  • Bokenkotter, Thomas. A Concise History of the Catholic Church . Doubleday (2004). ISBN 0-385-50584-1
  • Bruce, F.F. The Canon of Scripture.
  • Chambers, Mortimer; Crew, Herlihy, Rabb, Woloch. The Western Experience. Volume II: The Early Modern Period. Alfred A. Knopf (1974). ISBN 0-394-31734-3.
  • Coffey, John. Persecution and Toleration in Protestant England 1558–1689. Pearson Education (2000).
  • Cross, F. L.; Livingstone, E. A. (ed.). The Oxford Dictionary of the Christian Church. Oxford University Press (1997). ISBN 0-19-211655-X.
  • Deppermann, Klaus. Melchior Hoffman: Social Unrest and Apocalyptic Vision in the Age of Reformation. ISBN 0-567-08654-2.
  • Dilasser, Maurice. The Symbols of the Church. Collegeville, MN: Liturgical Press (1999). ISBN 0-8146-2538-X
  • Duffy, Eamon. Saints and Sinners, a History of the Popes. Yale University Press (1997). ISBN 0-300-07332-1
  • Elwell, Walter A.; Comfort, Philip Wesley. Tyndale Bible Dictionary, Tyndale House Publishers (2001). ISBN 0-8423-7089-7.
  • Esler, Philip F. The Early Christian World. Routledge (2004).
  • Farrar, F.W. Mercy and Judgment. A Few Last Words On Christian Eschatology With Reference to Dr. Pusey's, "What Is Of Faith?". Macmillan, London/New York (1904).
  • Ferguson, Sinclair; Wright, David, eds. New Dictionary of Theology. consulting ed. Packer, James. Leicester: Inter-Varsity Press (1988). ISBN 0-85110-636-6
  • Foutz, Scott. Martin Luther and Scripture Archived 14 Aprili 2000 at the Wayback Machine. Martin Luther and Scripture.
  • Fowler, Jeaneane D. World Religions: An Introduction for Students, Sussex Academic Press (1997). ISBN 1-898723-48-6.
  • Fuller, Reginald H. The Foundations of New Testament Christology Scribners (1965). ISBN 0-684-15532-X.
  • Froehle, Bryan; Gautier, Mary, Global Catholicism, Portrait of a World Church, Orbis books; Center for Applied Research in the Apostolate, Georgetown University (2003) ISBN=1-57075-375-X
  • Funk, Robert. The Acts of Jesus: What Did Jesus Really Do?. Polebridge Press (1998). ISBN 0-06-062978-9.
  • Glenny, W. Edward. Typology: A Summary Of The Present Evangelical Discussion.
  • Gonzalez, Justo L. The Story of Christianity: The Early Church to the Dawn of the Reformation, Harper Collins Publishers, New York (1984).
  • Hanegraaff, Hank. Resurrection: The Capstone in the Arch of Christianity. Thomas Nelson (2000). ISBN 0-8499-1643-7.
  • Harnack, Adolf von. History of Dogma (1894).
  • Hickman, Hoyt L. and others. Handbook of the Christian Year. Abingdon Press (1986). ISBN 0-687-16575-X
  • Hinnells, John R. The Routledge Companion to the Study of Religion (2005).
  • Hitchcock, Susan Tyler. Geography of Religion. National Geographic Society (2004) ISBN 0-7922-7313-3
  • Kelly, J.N.D. Early Christian Doctrines.
  • Kelly, J.N.D. The Athanasian Creed. Harper & Row, New York (1964).
  • Kirsch, Jonathan. God Against the Gods.
  • Kreeft, Peter. Catholic Christianity. Ignatius Press (2001) ISBN 0-89870-798-6
  • Letham, Robert. The Holy Trinity in Scripture, History, Theology, and Worship. P & R Publishing (2005). ISBN 0-87552-000-6.
  • Lorenzen, Thorwald. Resurrection, Discipleship, Justice: Affirming the Resurrection Jesus Christ Today. Smyth & Helwys (2003). ISBN 1-57312-399-4.
  • McLaughlin, R. Emmet, Caspar Schwenckfeld, reluctant radical: his life to 1540, New Haven: Yale University Press (1986). ISBN 0-300-03367-2.
  • MacCulloch, Diarmaid, The Reformation: A History. Viking Adult (2004).
  • MacCulloch, Diarmaid, A History of Christianity: The First Three Thousand Years. London, Allen Lane. 2009. ISBN 978-0-7139-9869-6
  • Marber, Peter. Money Changes Everything: How Global Prosperity Is Reshaping Our Needs, Values and Lifestyles. FT Press (2003). ISBN 0-13-065480-9
  • Marthaler, Berard. Introducing the Catechism of the Catholic Church, Traditional Themes and Contemporary Issues. Paulist Press (1994). ISBN 0-8091-3495-0
  • Mathison, Keith. The Shape of Sola Scriptura (2001).
  • McClintock, John, Cyclopaedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature. Harper &Brothers, original from Harvard University (1889)
  • McGrath, Alister E. Christianity: An Introduction. Blackwell Publishing (2006). ISBN 1-4051-0899-1.
  • McGrath, Alister E. Historical Theology.
  • McManners, John. Oxford Illustrated History of Christianity. Oxford University Press (1990). ISBN 0-19-822928-3.
  • Meconi, David Vincent. "Pagan Monotheism in Late Antiquity", in: Journal of Early Christian Studies.
  • Metzger, Bruce M., Michael Coogan (ed.). Oxford Companion to the Bible. Oxford University Press (1993). ISBN 0-19-504645-5.
  • Mullin, Robert Bruce. A short world history of Christianity. Westminster John Knox Press (2008).
  • Norman, Edward. The Roman Catholic Church, An Illustrated History. University of California (2007) ISBN 978-0-520-25251-6
  • Olson, Roger E., The Mosaic of Christian Belief. InterVarsity Press (2002). ISBN 978-0-8308-2695-7.
  • Orlandis, Jose, A Short History of the Catholic Church. Scepter Publishers (1993) ISBN 1-85182-125-2
  • Ott, Ludwig. Grundriß der Dogmatik. Herder, Freiburg (1965).
  • Otten, Herman J. Baal or God? Liberalism or Christianity, Fantasy vs. Truth: Beliefs and Practices of the Churches of the World Today.... Second ed. New Haven, Mo.: Lutheran News, 1988.
  • Pelikan, Jaroslav; Hotchkiss, Valerie (ed.) Creeds and Confessions of Faith in the Christian Tradition. Yale University Press (2003). ISBN 0-300-09389-6.
  • Putnam, Robert D. Democracies in Flux: The Evolution of Social Capital in Contemporary Society. Oxford University Press (2002).
  • Riley-Smith, Jonathan. The Oxford History of the Crusades. New York: Oxford University Press, (1999).
  • Robinson, George. Essential Judaism: A Complete Guide to Beliefs, Customs and Rituals. New York: Pocket Books (2000).
  • Schama, Simon . A History of Britain. Hyperion (2000). ISBN 0-7868-6675-6.
  • Servetus, Michael. Restoration of Christianity. Lewiston, New York: Edwin Mellen Press (2007).
  • Simon, Edith. Great Ages of Man: The Reformation. Time-Life Books (1966). ISBN 0-662-27820-8.
  • Smith, J.Z. (1998).
  • Spitz, Lewis. The Protestant Reformation. Concordia Publishing House (2003). ISBN 0-570-03320-9.
  • Sproul, R.C. Knowing Scripture.
  • Spurgeon, Charles. A Defense of Calvinism Archived 10 Aprili 2008 at the Wayback Machine..
  • Sykes, Stephen; Booty, John; Knight, Jonathan. The Study of Anglicanism. Augsburg Fortress Publishers (1998). ISBN 0-8006-3151-X.
  • Ustorf, Werner. "A missiological postscript", in: McLeod, Hugh; Ustorf, Werner (ed.). The Decline of Christendom in Western Europe, 1750–2000. Cambridge University Press (2003).
  • Walsh, Chad. Campus Gods on Trial. Rev. and enl. ed. New York: Macmillan Co., 1962, t.p. 1964. xiv, [4], 154 p.
  • Woodhead, Linda. An Introduction to Christianity.

Marejeo mengine

Viungo vya nje

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu: