Ufunuo

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Ufunuo ndio tukio au mchakato ambao mawasiliano kati ya Mungu na binadamu yanafanyika. Ufunuo ni pia yaliyomo katika ujumbe unaotokana na Mungu.

Ni kwamba katika dini mbalimbali kuna imani ya kwamba Mungu anaweza kujifunua kwa binadamu na kuwafunulia matakwa yake kwao.

Pengine ufunuo huo unakuja kuandikwa katika kitabu kitakatifu, kama vile Biblia kwa Wayahudi na Wakristo, na Torati, Zaburi, Injili na Kurani kwa Waislamu.

Ufunuo una umuhimu mdogo katika dini nyingine, isipokuwa katika Ubuddha.

Mpokeaji

Nabii ndiye jina la mtu anayepokea ufunuo huo ili kuwajulisha wengine.

Namna za kutolewa

Namna za ufunuo kufanyika zinaweza kuwa mbalimbali, kama vile:

Kutokana na asili yake isiyo ya kimaumbile, ufunuo hauwezi kuchunguzwa na mbinu za sayansi. Hata hivyo ni muhimu kupambanua ufunuo wa kweli na ule bandia ambao mtu anaweza kudanganyika au kudanganya.

Mada

Ufunuo unaweza kuhusu:

  • matukio yajayo (k.mf. mwisho wa dunia);
  • mambo ya mbinguni kuhusu Mungu, malaika n.k.;
  • ufafanuzi wa matukio ya wakati uleule.

Uyahudi

Kadiri ya dini ya Kiyahudi, Mungu alijifunua mara nyingi katika historia ya taifa lao kama Historia ya Wokovu, kuanzia mababu wao, lakini hasa kumpitia Musa, asili ya Torati (vitabu vitano vya kwanza vya Biblia ya Kiebrania).

Baada yake walitokea manabii wengi waliokubalika kuwa wa kweli na ambao vitabu vyao vilipokewa na wengi kama vitakatifu.

Tanakh ilikamilika kwa vitabu vingine vilivyoongezwa kabla ya Yesu Kristo.

Wayahudi wanaendelea kumsubiri Masiya atakayekamilisha ufunuo wao.

Ukristo

Wakristo wanapokea ufunuo wa Mungu kwa taifa la Israeli, wakiona ujio wa Yesu kuwa ndio kilele chake, ambapo Mungu alijifunua si kwa njia ya manabii, bali kwa njia ya Mwana wake, aliye Neno wa milele. Katika yeye ufunuo umekamilika usiweze kuboreshwa tena. Ufunuo huo unajitokeza hasa katika Agano Jipya.

Kwa imani hiyo, Mungu aliwahi kujifunua kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Eva, akaendelea hasa kwa taifa la Israeli, hadi alipomtuma Mwanae ajifanye mtu wa taifa hilo teule. “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana” (Eb 1:1-2).

Baada ya hapo, ufunuo wa Mungu hauendelei, kwa sababu alikwisha kuukamilisha kwa kumtuma duniani Neno wake wa milele. “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote; Mungu Mwana pekee aliye katika kifua cha Baba, huyu ndiye aliyemfunua” (Yoh 1:17-18). Baada yake hauwezekani ufunuo mpya. Hatutakiwi kumuamini yeyote akidai eti, ametumwa kukamilisha kazi ya Yesu; kwa kuwa mwenyewe alisema, “Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe” (Math 24:35). “Ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yoyote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe! Kama tulivyotangulia kusema, na sasa nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yoyote isipokuwa hiyo mliyoipokea, na alaaniwe!” (Gal 1:8-9).

Msimamo wa Kanisa Katoliki

Ufunuo huo wa Mungu unatufikia kupitia Kanisa lake, lililokabidhiwa Mapokeo ya Mitume na linaloongozwa na Roho Mtakatifu hadi ukweli wote. Yesu aliahidi kwamba, “Yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake” (Yoh 16:13). “Maana Roho huchunguza yote hata mafumbo ya Mungu” (1Kor 2:10).

Hivyo tupokee ufunuo wa Mungu kwa kusadiki mafundisho ya Kanisa lake, ili tuzidi kumjua na kuambatana naye bila kudanganyika. Yesu aliwaambia Mitume wake, “Awasikilizaye ninyi anisikiliza mimi, naye awakataaye ninyi anikataa mimi; naye anikataaye mimi amkataa yeye aliyenituma” (Lk 10:16). “Sisi nasi twamsukuru Mungu bila kukoma, kwa kuwa, mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kwelikweli, litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini” (1Thes 2:13).

Tukipata mafundisho ya Kanisa tunapaswa kuyasadiki kwa moyo mmoja tupate uzima wa milele, kwa kuwa Yesu aliwaambia Mitume, “Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa” (Mk 16:16).

Tunapaswa kusadiki hasa Utatu wa Mungu pekee, kwamba ni Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Milele yote Baba kwa jinsi alivyo ndani mwake anamzaa Mwana na kumvuvia Roho Mtakatifu, kama vile jua linavyotoa mwanga na joto lisitenganike navyo. Mwana, ambaye “ni mng’ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake” (Eb 1:3), alisema: “Nimekuja kutupa moto duniani” (Lk 12:49). Naye Roho aliwashukia wafuasi wake “kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu” (Mdo 2:3-4).

Katika teolojia ya Kikristo neno ufunuo lina maana ya jumla ya dogma zote, yaani kweli zilizofunuliwa na zinazodai imani ya kila mtu ili kupata wokovu.

Kwa Kanisa Katoliki kweli hizo zinapatikana katika Biblia pamoja na Mapokeo ya Mitume vinavyofafanuliwa na Ualimu wa kanisa.

Kanisa Katoliki linatofautisha pia huo ufunuo wa hadhara na mafunuo ya binafsi ambayo si lazima watu wengine wayasadiki.

Uislamu

Uislamu pia unakubali ufunuo wa Mungu kwa Wayahudi kupitia manabii, Isa (Yesu) akiwa mmojawao, lakini unaamini ufunuo huo umekamilishwa kupitia Muhammad, nabii wa mwisho na mkuu kuliko wote, na umeandikwa katika Kurani, inayohesabiwa "neno la Mungu" kwa maana kamili, kwa kuwa limetoka kwake na kuandikwa bila mabadiliko.

Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.