Moyo

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Moyo wa binadamu baada ya kutolewa kwenye maiti kwa utafiti wa kiganga.
Moyo kama ishara ya upendo.
Muundo wa moyo wa binadamu
*1 Vena kava ya juu (damu inaingia kutoka mwilini)
*2 ateri ya mapafu (damu inatoka kwenda mapafu)
*3 vena ya mapafu (damu inarudi kutoka mapafu)
*4 Vali mitralia - 5 Vali ya aorta
*6 Ventrikali kushoto - 7 Ventrikali kulia
*8 Atiria kushoto - 9 Atiria kulia
*10 Aorta (damu inatoka kwenda mwilini)
*11 Vali kwa mapafu - 12 Vali triskupidia
*13 Vena kava ya chini (damu inaingia kutoka mwilini)

Moyo ni ogani ya mwili inayoendesha mzunguko wa damu mwilini. Kazi yake ni kama pampu ya damu. Hali halisi ni misuli inayosukuma damu kwenye mishipa kwa njia ya kujikaza.

Mioyo ya mamalia pamoja na binadamu huwa na pande mbili. Upande wa kulia unasukuma damu kwenda mapafu inapopokea oksijeni; upande wa kushoto unazungusha damu katika sehemu nyingine za mwili pale ambako oksijeni inahitajika.

Moyo ni ogani ya lazima kwa uhai.

Moyo na utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Katika masimulizi ya mataifa mengi moyo unajadiliwa kama mahali pa roho, mawazo au hisia, hasa pendo na chuki.

Sababu yake ni kwamba pigo la moyo ni dalili ya wazi ya uhai na bila pigo la moyo mtu amekufa, kwa hiyo moyo ulitazamwa kama mahali pa uhai wenyewe pamoja na nafsi ya mtu.

Siku hizi wataalamu wanaona moyo ni pampu tu, ni zaidi ubongo mahali pa nafsi ya mtu.

Muhtasari wa kazi ya moyo[hariri | hariri chanzo]

(Namba zinalingana na mchoro wa moyo)

Moyo unazungusha damu mwilini.

  • Damu isiyo na oksijeni inafika moyoni (kulia) kutoka viungo. (na. 1+13)
  • Moyo unapeleka damu hii kwenye mapafu inapoongezwa oksijeni. (na. 2)
  • Damu inarudi moyoni (kushoto) ikiwa na oksijeni (na. 3)
  • Kutoka moyoni (kushoto) unasukumwa kwenda mwilini tena na kubeba oksijeni (na. 10)

Mbali na kubeba oksijeni damu inapokea pia virutubishi kwenye utumbo na kuvipeleka seli vinapotakiwa, halafu inapokea pia homoni kutoka tezi mbalimbali na kuzisafirisha. Moyo inahakikisha mwendo huu wa damu unaendelea.

Muundo wa moyo wa binadamu[hariri | hariri chanzo]

Moyo wetu huwa na pande mbili na kila upande kuna vyumba viwili. Kwa jumla moyo huwa na vyumba vinne. Amfibia huwa na vyumba vitatu na samaki na vyumba viwili tu.

Damu kutoka mwilini isiyo na oksijeni tena inafika kwenye atiria ya kulia. Atiria inasogeza damu kwenda chumba cha pili au ventrikali ya kulia. Ventrikali inasukuma damu kwenda mapafu inapoongezwa oksijeni. Kutoka mapafu damu yenye oksijeni inarudi moyoni ikiingia atiria ya kushoto na kuendelea ventrikali ya kushoto. Ventrikali hii inasukuma damu mwilini.

Kila sehemu ya kuingia au kutoka kwa damu katika chumba kimoja kuwa na mlango wake na milango hii huitwa "vali" ya moyo. Vali huongezeka jina kufuatana na upande wao ama kulia na kushoto au ya mapafu na menginevyo.

Mishipa ya damu moyoni[hariri | hariri chanzo]

Mishipa ya damu moyoni huwa na majina maalumu. Kwa jumla kuna mishipa mikubwa kwa sababu damu yote inapaswa kupita humo. Kwa hiyo mishipa karibu na moyo ni kama barabara kuu za damu mwilini.

Mishipa yote inayopeleka damu kwenda moyoni huitwa "vena". Mishipa yote inayotoa damu kutoka kwa moyo kwenda penginepo huitwa "arteri".

Ateri kuu inayopeleka damu mwilini ni aorta.

Kuna pia ateri za nje zinazozunguka moyo mwenyewe; kama musuli inahitaji oksijeni kwa kazi yake. Ateri za nje zinafikisha damu yenye oksijeni moja kwa moja kwa seli za moyo yenyewe.

Mapigo ya moyo[hariri | hariri chanzo]

Pigo la moyo ni hatua ya kujikaza kwa misuli ya moyo. Misuli ikijikaza inapunguza nafasi ndani yake na hivyo kusukuma damu kwenda ama chumba kingine kutoka ateri au kwenda mishipa ya damu yaani ateri.

Computer generated animation of a beating human heart
moyo wa mwanadamu ukipiga

Baadaye misuli inalegea mahali ilipojikaza. Vali inafunguka na damu kutoka vena inaweza kuingia na kujaza chumba cha moyo. Shindikizo ya damu kutoka vena inapanusha chumba tena mpaka kujaa. Sasa vali ya kuingia inafungwa, chumba kinajikaza tena na vali ya kutoka inafunguliwa.

mzunguko wa damu kuoitia valvu

Mwendo huu wa kujikaza unasikika kama "pigo la moyo".

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: