Upole

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sanamu inayodokeza upole huko Milano, kanisa la San Carlo al Corso.

Upole (kwa Kiingereza: meekness[1]) ni tawi la adili la kiasi ambalo linasisitwa na dini mbalimbali kama Ubuddha[2] na Ukristo[3][4]. Upole unatakiwa kuendana na subira lakini unatofautiana nayo kwa kuwa tokeo lake maalumu ni kuzuia vurugu za hasira, si kuvumilia tabu.

Upole wa Kikristo na matunda yake[hariri | hariri chanzo]

Adili la upole ni tofauti na silika ya upole kwa sababu linaratibu kwa mwanga wa akili (na wa imani) hisi zilizotikiswa na hasira. Adili hilo ni bora kuliko tabia hiyo ya kisaikolojia, kama vile usafi wa moyo ulivyo bora kuliko elekeo la haya, na adili la huruma kuliko ulaini wa moyo. Mara nyingi tabia ya upole inajitokeza kwa watu wanaopendeza, lakini inaendana na ukali kidogo kwa wasiopendeza. Kumbe adili la upole linaondoa ukali na uchungu kwa wote na katika nafasi yoyote. Tena linaingiza utulivu fulani hata unapotakiwa ukali: kwa kuwa linategemea adili la kiasi, linapenda kutozidisha.

Upole huo unakusudiwa kutawala si maneno na mwenendo tu, bali moyo pia, la sivyo ni bandia. Ukisababishwa na lengo lipitalo maumbile na ukitekelezwa hata kwa watu wakali, upole ni “ua la upendo” (Fransisko wa Sales). Katika mmea ua ndiyo sehemu ya kuvutia zaidi, na ingawa ni dhaifu lina kazi muhimu ya kutunza tunda linaloundika ndani yake. Vivyo hivyo upole ndio unaovutia zaidi katika utekelezaji wa upendo. Ndiyo sura yake ambayo inajitokeza katika macho, tabasamu, mwenendo na maneno, ikizidisha thamani ya huduma inayotolewa. Pia unatunza matunda ya upendo na ari, kwa kufanya mashauri na maonyo yapokewe vizuri. Tunaweza tukawa na ari kwa jirani, lakini tusipotumia upole hatutaonyesha tunawapenda, na nia zetu njema zitashindikana kwa sababu tutaonekana kusema kwa hasira kuliko kwa busara na hekima.

Upendo unastahili kwa namna ya pekee unapotumiwa kwa wanaotutesa; hapo kwa hakika si wa kibinadamu, bali unatoka kwa Mungu na pengine unamgusa aliyetukasirikia bure. Sala ya Stefano (taz. Mdo 7:60) ilimvutia Saulo neema ya uongofu, na upole unawaondolea silaha wakatili. “Hakuna kinachoweza kumtuliza tembo aliyekasirika kuliko sura ya mwanakondoo, na hakuna kinachozuia nguvu ya mzinga kuliko sufu” (Fransisko wa Sales). Pengine upole wa Kikristo unaogeuza shavu la pili unamtuliza mwenye hasira walau kidogokidogo.

“Ni afadhali kuunda watubu kwa kutumia upole kuliko kuunda wanafiki kwa kutumia ukali… Mjitahidi kutekeleza upole mnyenyekevu unaowapasa kwa wote, kwa kuwa ndio adili bora alilotusisitizia Bwana wetu. Ikiwatokea kukosa dhidi yake, msifadhaike, bali kwa tumaini kubwa muinuke tena na kuendelea na safari kwa amani na upole kama awali” (Fransisko wa Sales). Tunashika nzi wengi zaidi kwa tone la asali kuliko kwa pipa la siki. Inahitajika ari, lakini yenye upole na subira. Basi, tuepe ari chungu ya kukaripia daima ambayo inasababishwa na kiburi na iliharibu marekebisho mengi utawani. Dhidi yake Yohane wa Msalaba alisema, “Pasipokuwa na upendo wa kutosha, mpatie upendo, nanyi mtavuna upendo”.

Heri ya upole inahusiana na kipaji cha ibada ambacho kinatutia mvuto wa upendo wa kitoto kwa Mungu tuzidi kumuona kama Baba mpendwa; hivyo kinatufanya tuone watu kuwa ndugu, watoto wa Baba yuleyule, si watu tusiohusiana nao wala wapinzani. Kipaji hicho kinatusemesha kwa dhati zaidi na zaidi, “Baba yetu uliye mbinguni…”, tukitamani ufalme wake uimarike ndani yetu na ya ndugu zetu; hamu hiyo inasababisha upole unaong’aa kwa jirani.

Ili tutekeleze vizuri adili hilo, tunapaswa kulizingatia lilivyo ndani ya Yesu, upole upitao maumbile ambao umetokana na ari ya kuokoa watu bila kuipunguza, kama alivyotabiriwa, “Hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima” (Isa 42:2-3). Alipobatizwa alishukiwa na Roho Mtakatifu kwa sura ya njiwa, akatambulishwa kuwa “Mwanakondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu” (Yoh 1:29). Hatimaye msalabani akawasamehe watesi wake kwa kuwaombea. Ndio upole katika tendo kuu la nguvu; tabasamu ya Msulubiwa ndiyo sura bora ya wema hapa duniani. Upole wa namna hiyo ni moja ya dalili zinazobainisha zaidi wafiadini wa kweli. Watu wengine wanayafia mawazo yao, na kiburi kinawafanya wavumilie mateso; ndani mwao haupatikani ulinganifu wa maadili yanayoonekana kupingana. Kumbe wafiadini ni wapole hata kwa watesi na wanawaombea; sasa kusahau mateso yao wenyewe ili kufikiria wokovu wa watesi ni dalili ya upendo mkuu unaolinganisha maadili yote ndani yake.

Tumuombe Bwana adili hilo pamoja na unyenyekevu wa moyo; tumuombe kwenye komunyo, katika ule muungano wa dhati wa roho yetu na yake, wa akili yetu na yake, wa moyo wetu na wake uliofurika upendo. Tumuombe mara nyingi, halafu tukipata nafasi tuyatekeleze maadili hayo kwa bidii. Hapo yatatimia maneno yake: “Mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo, nanyi mtapata raha nafsini mwenu” (Math 11:29). Wakati wa ukinaifu na mahangaiko tung’amue raha hiyo kwa kusamehe kabisa waliotukosea. Kwa msaada wa neema tutarudi mahali petu mbele ya Bwana na ya jirani, kwenye utulivu wa utaratibu tuliopangiwa na kwenye amani ya dhamiri nyofu iliyounganika na Mungu wake. Katika upendo tutaona amani itokayo kwa Mungu, tofauti na ile ya nje tu inayopatikana ulimwenguni kwa kukubaliana na maadui wa Mungu na maelekeo yetu mabaya, kwa kutengana na waadilifu na kusambaratika kwa ndani: hiyo ni amani ya mauti inayoendana na uwozo. Kumbe amani aliyotuachia Bwana ni ya dhati na inadai tupambane mfululizo na tabia zetu mbovu, na ulimwengu na shetani: “Sikuja kuleta amani, bali upanga” (Math 10:34). Hakika, hatuwezi kuwa wanyenyekevu na wapole kwa wote tusipotumia nguvu juu yetu. Lakini, hata kama upendo wake una masharti makali, tunang’amua ukweli wa maneno yake: “nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi” (Math 11:30). Uzito wa mzigo huo unapungua kadiri yanavyostawi maadili ambayo ni namna za upendo. “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari, haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote, huamini yote; hutumaini yote, hustahimili yote” (1Kor 13:4-7). Upole huo wa Kimungu unaandaa kuzama katika sala, ni utangulizi wa heri isiyo na mwisho.

Kwa njia ya adili hilo likifikia kiwango cha ushujaa, mtu anafikia kujitawala kikamilifu, hata kushinda ubaya kwa wema badala ya kuupinga kwa hasira. Ngazi za juu za upole ni kutofadhaishwa na matusi, kufurahia kitakatifu matokeo bora yanayotokana nayo, na hatimaye kumhurumia mtukanaji kwa matokeo mabaya yanayoweza kumpata. Ndivyo Yesu alivyolia juu ya Yerusalemu kwa kuwa ulikosa shukrani; alisikitikia maangamizi ya mji huo kuliko kifo kikatili kitakachompata.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. The Free Dictionary, Meekness
  2. J. B. Carman, Majesty and Meekness (1994) p. 124
  3. C. S. Titus, Resilience and the Virtue of Fortitude (2006) p. 320
  4. The Free Dictionary, Usages of meekness
Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.