Yohane wa Msalaba

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kuhariri Yohane wa Msalaba

Yohane wa Msalaba (Fontiveros, Castilia, Hispania, 24 Juni 1542 - Ubeda, Hispania, 14 Desemba 1591) ni jina la kitawa la Juan de Yepes Álvarez, padri wa Kanisa Katoliki na mwanzilishi (pamoja na Teresa wa Yesu) wa urekebisho wa shirika la Wakarmeli maarufu kama Wakarmeli Peku.

Anaheshimiwa kama mtakatifu na mwalimu wa Kanisa.

Sikukuu yake inaadhimishwa kila mwaka tarehe 14 Desemba[1].

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Utoto na ujana[hariri | hariri chanzo]

Yohane alizaliwa Fontiveros, kijiji cha mkoa wa Castilia (Hispania), tarehe 24 Juni 1542 akafariki Ubeda tarehe 14 Desemba 1591.

Baba yake, Gonzalo de Yepes, wa ukoo maarufu wa Toledo wenye asili ya Kiyahudi, alifukuzwa na familia yake na kunyimwa urithi kwa sababu ya kumuoa mfumaji fukara, Catalina Álvarez. Hivyo hali yao ilikuwa ngumu sana kiuchumi.

Tangu utotoni Yohane alielekea huruma kwa maskini na hasa sala.

Kati ya 1551 na 1559 alipata elimu na ufundi huko Medina del Campo (kituo cha biashara na masomo karibu na Valladolid), ambapo familia yake ilikuwa imehamia kufuatana na kifo cha baba yake.

Baadaye akawa seremala, mshonaji, mchoraji, mchongaji, nesi msaidizi namtumishi wa altare, kufuatana na vipawa vyake na maendeleo yake katika masomo.

Akiwa na miaka 18 aliingia shule mpya ya bweni iliyoanzishwa na Wajesuiti huko Medina del Campo akasoma lugha na mengineyo kwa miaka mitatu. Alipomaliza alikuwa na hakika kuhusu wito wake wa kitawa.

Miaka ya kwanza utawani[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1563 alijiunga na shirika la Wakarmeli, wakati maisha ya jumuia yalipokuwa yamelegea sana, na wakati wa joto wa mwaka huo alianza unovisi hukohuko Medina del Campo akichukua jina la Yohane wa Mt. Matia.

Kati ya 1564 na 1567 akasoma lugha na falsafa katika chuo kikuu maarufu cha Salamanca.

Mwaka 1567 alipata upadirisho akarudi Medina del Campo kuadhimisha Misa ya shukrani kati ya wanafamilia.

Huko akakutana na Teresa wa Yesu, ambaye alimfanya amuunge mkono katika kurekebisha shirika hilo lirudi kwenye juhudi za awali “kwa utukufu mkubwa zaidi wa Mungu”. Upande wake Teresa alianza kumheshimu sana akamuita "baba wa roho" yake, ingawa alimtania pia kutokana na silika yake ngumu na makini.

Kwa miezi kadhaa walishirikishana mawazo na malengo kwa ajili ya kuanza urekebisho mapema iwezekanavyo.

Juhudi kwa ajili ya urekebisho[hariri | hariri chanzo]

Tarehe 9 Agosti 1568, alikwenda Valladolid ilipoanzishwa monasteri ya kwanza ya Masista Wakarmeli Peku akabaki huko hadi Oktoba ili kujifunza maisha ya urekebisho, halafu akaenda Duruelo (Segovia), akageuza nyumba ya wakulima kuwa konventi ya kwanza ya Wakarmeli Peku wanaume (28 Desemba).

Mwanzoni walikuwa wanne. Waliporudia nadhiri zao kadiri ya kanuni asili ya shirika, kila mmoja alijichagulia jina jipya, naye akajiita “Yohane wa Msalaba”.

Mwishoni mwa mwaka 1572, kwa ombi la Teresa, akawa muungamishi na makamu wa monasteri ya Umwilisho mjini Avila iliyongozwa na Teresa mwenyewe.

Ilifuata miaka ya urafiki wa kiroho na ushirikiano mkubwa kwa faida ya wote wawili. Ndipo vitabu bora vya Teresa na vile vya kwanza vya Yohane vilipoandikwa.

Kati ya mateso ya kimwili na ya kiroho yaliyompata kwa kupigania urekebisho, mbali ya kufukuzwa konventini, mojawapo ni lile la kufungwa miezi minane kwa tuhuma ya uongo katika gereza la shirika la Toledo (kuanzia tarehe 2 Desemba 1577 hadi alipotoroka usiku wa kuamkia tarehe 17 Agosti 1578). Humo alinyanyaswa kwa namna mbalimbali.

Hata hivyo humohumo aliangaziwa na Mungu kutunga baadhi ya mashairi yake bora, yaliyompatia nafasi kati wa washairi mashuhuri wa lugha ya Kihispania.

Kisha kujisalimisha katika nyumba ya Wakarmeli Peku ya Toledo, Teresa na wenzake walishangilia sana uhuru wake. Baada ya muda mfupi wa pumziko kwa ajili ya kupata tena nguvu, alipangiwa kwenda katika mkoa wa Andalusia, alipoishi miaka 10 katika konventi mbalimbali, hasa Granada.

Alizidi kupewa vyeo muhimu shirikani hata kuwa makamu wa mkuu wa kanda, pia alikamilisha maandishi yake ya kiroho.

Halafu akarudi katika mkoa wake asili kama mmoja wa halmashauri kuu ya shirika la Teresa ambalo lilikuwa limeshapata uhuru kamili kisheria. Aliishi katika Karmeli ya Segovia kama mkuu wa jumuia.

Miaka ya mwisho ya maisha yake alijikuta ameachwa na wafuasi wake walio wengi.

Mateso hayo yote yalimfundisha kuvumbua fumbo la msalaba na kusonga mbele katika njia ya sala ya juu kabisa, hata akaweza kuielekeza kwa kufafanua hatua zake.

Kifo[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1591 aliondolewa majukumu yote na kupangiwa aende katika kanda mpya ya Meksiko barani Amerika. Akiwa anajiandaa kwa safari hiyo ndefu pamoja na wenzake 10, tarehe 28 Septemba 1591 akiwa mgonjwa alisafiri kwenda kujifungia katika konventi ya Úbeda (karibu na Jaén), alipozidi kuugua kwa mateso makali na uvumilivu mkubwa hadi alipofariki usiku kati ya tarehe 13 na 14 Desemba 1591.

Wakati wenzake walipokuwa wanaimba Kipindi cha Masomo, aliaga, “Leo naenda kuimba Masifu mbinguni”.

Masalia yake yalihamishiwa Segovia.

Sala yake[hariri | hariri chanzo]

Roho yangu ni kavu ndani mwangu kwa sababu imesahau kujilisha wewe.

Teolojia yake[hariri | hariri chanzo]

Pamoja na kuwa mshairi, Yohane alikuwa hasa mwanateolojia, aliyetunga vitabu mbalimbali kuhusu maisha ya Kiroho, yaani sala na safari ya kumuelekea Mungu kwa njia ya mkato (kupitia hatua ya utakaso, hatua ya mwanga na hatua ya muungano).

Kufuatana na mapokeo ya Ukristo, alifundisha namna ya kubandukana na wote na vyote ili kuungana na Mungu tu aliye kwa pamoja «mwanga wenye giza na giza angavu», kwa kuwa mwanga wake ni mkali mno kwa macho yetu mabovu.

Mojawapo ya semi zake ilikuwa kwamba: «Mungu anamnyenyekesha sana mtu ili kumuinua sana».

Maandishi na sifa yake baada ya kifo[hariri | hariri chanzo]

Maandishi yake ni kama ifuatavyo:

  • Wimbo wa Kiroho
  • Usiku wenye giza wa roho
  • Kupanda mlima Karmeli
  • Mwali hai wa upendo
  • Mawazo juu ya upendo na amani
  • Barua

Katika “Wimbo wa Kiroho”, Yohane anaeleza maendeleo ya utakaso wa roho kama njia ya kuzidi kumpata Mungu kwa furaha, hadi mtu anapotambua kwamba anampenda kwa upendo uleule ambao anapendwa naye.

“Mwali Hai wa Upendo” kinaendeleza mada hiyo kwa kufafanua zaidi hali ya muungano na Mungu unaomgeuza mtu ndani yake. Mfano unaotumika tena na tena ni ule wa moto: kama vile huo unavyozidi kuwaka kwa nguvu na kushika ukuni hata kuugeuza mwali, Roho Mtakatifu naye, kisha kutakasa roho katika usiku wenye giza, anaiangaza na kuiwasha kama mwali wa moto. Maisha ya roho ni adhimisho la mfululizo la Roho Mtakatifu ambalo mtu anaanza kuonja utukufu wa kuungana na Mungu milele.

“Kupanda Mlima Karmeli” kinaelekeza roho katika utakaso wake wa hatua kwa hatua, unaohitajika ili kupanda hadi vilele vya ukamilifu wa Kikristo, unaomaanishwa na mlima huo. Utakaso huo unapendekezwa kama safari ambapo mtu anashirikiana na Mungu ili kubandukana na lolote lililo kinyume na matakwa yake matakatifu. Utakaso huo, unaotakiwa kuwa kamili uweze kufikia muungano wa upendo na Mungu, unaanza na hisi, halafu unaendelea na maadili ya Kimungu (imani, tumaini na upendo) ili kutakasa pia akili, kumbukumbu na utashi.

“Usiku Wenye Giza wa Roho” kinafafanua kazi ya Mungu mwenyewe katika kuitakasa kikamilifu roho ya mtu na kuiandaa iweze kuungana naye kwa upendo. Hiyo inahitajika kwa sababu juhudi za binadamu haziwezi kutosha kufikia mizizi mirefu ya maelekeo na mazoea mabaya aliyonayo. Mtu anaweza kuyadhibiti, lakini si kuyang’oa kabisa. Hiyo ni kazi ya Mungu tu: mtu anapaswa kukubali afanyiwe, lakini ni Roho Mtakatifu ambaye kama mwali wa moto anateketeza uchafu wowote. Katika hali hiyo mtu anajaribiwa kwa kila namna, kama kwamba angejikuta katika usiku wenye giza nene.

Mihtasari hiyo ya vitabu muhimu zaidi vya Yohane wa Msalaba inatusaidia kutambua mafundisho yake makuu kuhusu maisha ya Kiroho, yaliyoelekeza kwa hakika njia ya utakatifu ambao Mungu anawaitia wote, Kwake viumbe vyote ni vyema, na kwa kuvipitia tunaweza kumfahamu Muumba aliyeacha athari yake ndani ya hivyo vyote. Lakini ni imani tu inayotuwezesha kumjua Mungu jinsi alivyo kwa ndani, yaani katika umoja wa Nafsi tatu. Yale yote aliyotaka kuwashirikisha binadamu aliyatoa katika Yesu Kristo, Neno wake aliyefanyika mwili: ndiye njia pekee ya kumfikia Baba.

Viumbe vyote si kitu kabisa vikifananishwa na Mungu, kwa hiyo ili tufikie upendo kamili wa Mungu, ni lazima mapendo mengine yote yalinganishwe nao ndani ya Kristo. Ndiyo sababu Yohane anasisitiza haja ya utakaso na uvuaji kamili ili kugeuzwa ndani ya Mungu, lengo la ukamilifu.

Safari ndefu na ngumu ya utakaso inadai juhudi za mtu, lakini mtendaji mkuu ni Mungu: mtu anapaswa hasa kujiandaa afanyiwe kazi bila kuizuia. Hasa atekeleze maadili ya Kimungu ambayo yanakua pamoja na maendeleo ya utakaso na muungano na Mungu, hadi mtu ageuzwe ndani ya Mungu.

Akifikia lengo hilo, mtu anazama ndani ya Utatu Mtakatifu na kumpenda Mungu kwa upendo uleule anaopendwa naye, yaani anampenda kwa Roho Mtakatifu. Anajisikia amezama katika upendo wa Mungu na kuufurahia bila kipimo. Anafahamu yote kumpitia Mungu, asihitaji tena kuvipitia viumbe ili kumfikia.

Maandishi yake yalitolewa kwa mara ya kwanza mwaka 1618, akatangazwa na Papa Klementi X kuwa mwenye heri tarehe 25 Januari 1675, halafu mtakatifu na papa Benedikto XIII tarehe 27 Desemba 1726 na hatimaye mwalimu wa Kanisa na Papa Pius XI tarehe 24 Agosti 1926.

Kulinganisha maandishi yake na yale ya Teresa wa Yesu[hariri | hariri chanzo]

Tangu tusome mara ya kwanza maandishi ya Teresa wa Yesu na Yohane wa Msalaba, ni rahisi tutambue tofauti ambazo zimesisitizwa mara nyingi. Zinatokana na tofauti za mitazamo yao.

Teresa alitegemea mang’amuzi yake binafsi, akidokeza neema za pekee alizojaliwa (njozi n.k.) asiwe makini kuzitofautisha na mambo yaliyo ya lazima katika “makao saba” ya jumba la Kiroho. Hivyo alitia maanani kuliko wengine matukio ya kihisi, ya nje na ya ziada yanayoweza yakaendana na sala ya kumiminiwa; vilevile alisisitiza kuzingatia ubinadamu wa Yesu.

Yohane pia alisema kwa mang’amuzi yake binafsi na ya watu aliowaongoza, lakini hakuyataja, akijitahidi kuyachimba kiteolojia, jambo ambalo ni muhimu ili kutofautisha yaliyo ya kawaida na yaliyo ya ziada. Alieleza sababu za hali mbalimbali za sala kwa mafundisho juu ya maadili ya Kimungu na ya vipaji vya Roho Mtakatifu vinavyoendana nayo.

Kwa mtazamo huo alizingatia yaliyo ya lazima katika safari ya kuelekea utakatifu, hasa matakaso ya Kimungu yanayohitajika kwa usafi kamili wa upendo. Hivyo hakuelekea kujali neema za pekee zinazoendana pengine na sala ya kumiminiwa, wala hakusisitiza kuzingatia ubinadamu wa Yesu, akilenga moja kwa moja shabaha kuu ya sala, yaani Mungu aliyemo mwetu, tunayemfikia katika giza la imani kwa njia ya ujuzi ambao anatumiminia na unafanana na mang’amuzi.

Kwa kufanya hivyo amekamilisha maandishi ya Teresa na kutusaidia tuyaelewe.

Hata hivyo, chini ya tofauti hizo kuna msingi mmoja, kwa kuwa Teresa alijua vya kutosha mang’amuzi ya wafuasi wake aweze kuelewa na kueleza nini inatokea kwa kawaida kwa watu wanaopitia hayo makao saba. Tukitumia maelekezo aliyoyatoa huko na huko tunaweza kubainisha zaidi yaliyo ya lazima na yaliyo ya ziada.

Kimsingi watakatifu hao walielewa vilevile sala ya kumiminiwa, muungano na Mungu unaotokana nayo, na matakaso ya Kimungu yanayohitajika ili kuufikia ule kamili.

Ikifaa kuonyesha tofauti zao, inafaa zaidi kuonyesha wanavyolingana na kutambua teolojia inavyoweza kusaidia katika masuala hayo magumu.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Maandishi yake kwa Kiingereza[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Sr. Pascale-Dominique Nau, When God Speaks: Lectio Divina in Saint John of the Cross and the Ladder of Monks (Rome: Lulu.com, 2011)

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]