Umwilisho

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Evangelismos, picha takatifu ya Kiorthodoksi, 1825, Thessaloniki, Ugiriki.
Mfululizo wa kurasa juu ya Yesu
Jesus
Yesu Kristo na Ukristo

Umwilisho  • Utoto wa Yesu  • Ubatizo
Arusi ya Kana • Utume wa Yesu • Mifano ya Yesu  • Miujiza ya Yesu
Kugeuka sura • Karamu ya mwisho • Msalaba wa Yesu  • Maneno saba
Kifo cha Yesu  • Ufufuko wa Yesu
Kupaa mbinguni  • Ujio wa pili
Injili  • Majina ya Yesu katika Agano Jipya  • Yesu kadiri ya historia  • Tarehe za maisha ya Yesu • Kristolojia

Mazingira ya Yesu

Wayahudi • Kiaramu • Bikira Maria • Yosefu (mume wa Maria) • Familia takatifu • Ukoo wa Yesu • Ndugu wa Yesu • Yohane Mbatizaji

Mitazamo juu ya Yesu

Mitazamo katika Agano Jipya · Mitazamo ya Kikristo • Mitazamo ya Kiyahudi • Mitazamo ya Kiislamu • Yesu katika sanaa

Umwilisho (kwa Kiingereza "incarnation" kutoka Kilatini "incarnatio") ni neno la teolojia linalotumika kulitaja fumbo la imani ya Ukristo la kwamba Mwana wa Mungu alijifanya binadamu kweli kwa kutwaa roho na hata mwili kama vile vya mtu yeyote.

Mkazo juu ya mwili unatokana na dibaji ya Injili ya Yohane inayosisitiza ajabu la tukio hilo ikisema: "Neno akawa mwili akakaa kwetu" (1:14).

Kwa msingi huo Kanuni ya imani ya Nisea-Konstantinopoli inafundisha kukiri:

Alishuka toka mbinguni kwa ajili yetu sisi wanadamu na kwa ajili ya wokovu wetu, akapata mwili kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwake yeye Bikira Maria akawa mwanadamu.

Umwilisho ulifanyika pale ambapo Maria alikubali wito wa Mungu kwake alivyoletewa na Malaika Gabrieli katika kijiji chake, Nazareti . Habari inasimuliwa hivi (Lk 1:26-38):

26 Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, 27 kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. 28 Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. 29 Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? 30 Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. 31 Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. 32 Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. 33 Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho. 34 Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? 35 Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. 36 Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; 37 kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu. 38 Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake.

Dini nyingine ziliwahi kusimulia juu ya mungu fulani kuja duniani akionekana kama mtu (kwa mfano Avatar katika Uhindu), lakini umwilisho ni wa pekee kwa kuwa unatokana na imani ya kuwa Yesu tangu alipotungwa tumboni mwa mama yake ni binadamu halisi kama mwingine yeyote, ingawa nafsi yake ni ya milele kama ile ya Mungu Baba na ya Roho Mtakatifu.

Imani hiyo inaongoza kumkiri Yesu kuwa Mungu kweli milele yote na mtu kweli tangu alipotwaa mwili. Kwa sababu hiyo, Wakristo wengi (Wakatoliki, Waorthodoksi, Waorthodoksi wa Mashariki na baadhi ya Waprotestanti) wanamuita Maria "Theotokos" (yaani "Mzazi wa Mungu" au "Mama wa Mungu", kwa maana ni mama aliyemzaa mtu ambaye tangu milele ni Mungu, si kwamba aliweza kumzaa Mungu kama Mungu).

Picha za Mtoto Yesu mikononi mwa Maria[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Umwilisho kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.