Mama Teresa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mama Teresa mnamo mwaka 1990.

Mama Teresa wa Kolkata (26 Agosti 19105 Septemba 1997) alikuwa mtawa wa Kanisa Katoliki aliyejulikana kimataifa hasa kutokana na huduma zake kwa watu maskini katika mji wa Kolkata (Uhindi) na kwingineko iliyofanya apatiwe tuzo ya Nobel ya Amani mwaka 1979.

Tarehe 19 Oktoba 2003 alitangazwa na Papa Yohane Paulo II kuwa mwenye heri. Baada ya muujiza wa pili kufanywa na Mungu kwa maombezi yake, Papa Fransisko amemtangaza kuwa mtakatifu tarehe 4 Septemba 2016.

Sikukuu yake huadhimishwa kila mwaka tarehe 5 Septemba[1]. Siku hiyohiyo imetangazwa na mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa kuwa siku ya kimataifa ya upendo kuanzia mwaka 2013.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa tarehe 26 Agosti 1910 mjini Skopje (katika Dola la Kituruki, leo mji mkuu wa Makedonia Kaskazini) katika familia ya Waalbania akaitwa Agnes Gonxha Bojaxhiu. Alizaliwa katika familia ya Kikatoliki na alibatizwa siku moja baada ya kuzaliwa, yaani tarehe 27 Agosti 1910 na siku hiyo aliyobatizwa aliitazama siku zote kama siku yake ya kuzaliwa rasmi.[2]

Alipofikia umri wa miaka 18 alijiunga na shirika la Masista wa Loreto huko Ireland na mwaka 1929 alitumwa Uhindi kufanya utume wake kama mmisionari afundishe kwenye shule ya masista mjini Kolkata alipoendelea hata kuwa mkuu wa shule.

Hata hivyo aliguswa sana na hali ya mafukara nje ya shule akajaliwa neema ya wito wa pekee yaani kujitoa kwa ajili ya watu maskini sana na wale ambao jamii imewatenga, kwa kuwasaidia na kuishi pamoja nao. Wito huu mpya ulikuwa chanzo cha Shirika la Masista Wamisionari wa Upendo lililoanza rasmi mnamo 7 Oktoba 1950.[3] Na sasa limeenea sehemu mbalimbali duniani likiendeleza utume wa Mama Tereza.

Kwa kibali cha wakuu wa shirika lake na wa Kanisa mwaka 1948 alitoka jumuiya ya Loreto akaanzisha maisha duni kati ya wakazi wa mitaa ya vibanda.

Alianzisha shule lakini baada ya muda alitambua umuhimu wa kuzingatia zaidi hali ya watu ambao walikuwa wagonjwa na hatimaye kufa katika mitaa hiyo.

Mwaka 1950 alianzisha shirika la Masista Wamisionari wa Upendo ambalo mwanzoni lilikuwa jumuiya ndogo ya masista 12 tu.

Kati ya kazi zao za kwanza ilikuwa nyumba kwa watu mahututi; masista waliwakusanya wakiwa wamelala barabarani na kuwapeleka katika nyumba hiyo walipopata dawa, chakula na usaidizi mwingine.

Shirika lilikua haraka sana; hadi leo kuna masista 4,500 kwa jumla katika matawi mengi kote duniani.

Wanaendesha nyumba kwa watoto yatima, wagonjwa wa UKIMWI, wenye ukoma, walemavu, walevi, wenye kichaa na kila aina ya matatizo maishani.

Mwaka 1979 alipewa Tuzo ya Nobel ya Amani ambayo hutolewa na Umoja wa Mataifa kwa sababu jumuiya ya kimataifa iliweza kutambua mchango wake katika kutetetea haki za wanyonge.[4]. Mama huyu ni mfano halisi wa namna ya kuishi kama binadamu kwa sababu kila mwanadamu ni sura na mfano wa Mungu, hivyo kuwajali na kuwasaidia wale wasiojiweza na wale ambao kamwe hawawezi kurudisha kwetu chochote, huwasaidia watu hao kuiona sura halisi ya Mungu kupitia sisi. Kwa kweli maisha yake yalikuwa ushuhuda halisi wa upendo wa Mungu hapa duniani. Pia Mama Tereza ni mfano halisi wa kuishi kama Mkristo kwa sababu hata Kristo mwenyewe alijitoa kwa ajili ya wale ambao jamii haikuwathamini kwa kipindi kile ambao ni wachungaji, wavuvi, watoza ushuru na wenye dhambi, hivyo kujitoa kwa ajili ya wale wasiojiweza au wale ambao jamii haiwathamini tena inawasaidia wao kumwona na kumtambua Kristo kupitia sisi na huwawezesha kuuona uwezo mkuu wa Mungu kupitia matukio ya maisha yao.

Mnamo mwaka 1990 aling'atuka kuongoza shirika lake kama mkuu wa shirika kimataifa.

Alifariki akiwa na umri wa miaka 87 huko Calcutta, Bengal Magharibi nchini India tarehe 5 Septemba 1997 akafanyiwa mazishi ya kitaifa.

Sala zake[hariri | hariri chanzo]

Baba yetu, mwanao nipo hapa, tayari kwako unitumie ili kuendelea kupenda ulimwengu kwa kuupatia Yesu na, kwa njia yangu, kumtoa kwa kila mmoja na kwa ulimwengu.


Ee Bwana, utufanye tustahili kutumikia watu wenzetu ambao ulimwenguni kote wanaishi na kufa kwa ufukara na njaa.

Kwa mikono yetu uwape leo mkate wao wa kila siku; na kwa upendo wetu wenye kuelewa uwape amani na furaha.


Ee Bwana wangu, nakupenda, Mungu wangu, najuta, Mungu wangu, nakuamini, Mungu wangu, nakutumainia.

Utusaidie kupendana unavyotupenda.


Bwana Yesu, wewe ambaye uliumba kwa upendo, ulizaliwa kwa upendo, ulitumikia kwa upendo, ulitenda kwa upendo, uliheshimiwa kwa upendo, uliteseka kwa upendo, ulikufa kwa upendo, ulifufuka kwa upendo, nakushukuru kwa upendo wako kwangu na kwa ulimwengu wote, na kila siku nakuomba: unifundishe mimi pia kupenda! Amina.

Maandishi yake[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kifo chake maandishi yake yaliyotolewa hadharani yakafichua siri ya maisha yake ya ndani, yaani kwamba alipitia kwa karibu miaka 50 mfululizo katika hali ngumu inayoitwa usiku wa roho, bila ya hiyo kuweza kumzuia atabasamu muda wote.

  • Teresa, Mother et al., Mother Teresa: In My Own Words. Gramercy Books, 1997. ISBN 0-517-20169-0.
  • Teresa, Mother & Kolodiejchuk, Brian, Mother Teresa: Come Be My Light, New York: Doubleday, 2007. ISBN 0-385-52037-9.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mkristo huyu, kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Je, unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.