Gedi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Maghofu ya msikiti
Kaburi la mwaka 1399 kati ya maghofu ya Gedi

Gedi (pia: Gede) ni kijiji cha wakazi 600 kwenye pwani ya Kenya takriban kilomita 16 kusini kwa Malindi. Ni mahali maarufu pa maghofu ya mji wa Waswahili wa Kale ndani ya msitu wa Arabuko-sokole.[1]

Kuna maeneo 116 ya Waswahili yanayonyooka kutoka kusini mwa Somalia mpaka Vumba kuu katika mpaka wa Kenya na Tanzania.[2] kutokana na uvumbuzi wa magofu ya Gedi uliofanywa na wakoloni miaka ya 1920, Gede imejulikana kama mji uliotambulika zaidi na maeneo yake kufanyiwa utafiti zaidi kando na maeneo ya Shanga, Manda, Ungwana, Kilwa na visiwa vya Komoro.

Gedi ya kihistoria[hariri | hariri chanzo]

Kando ya kijiji cha leo kuna eneo kubwa la maghofu. Kuta za mawe zinaonekana kati ya miti. Nyumba za watu, jumba la mkubwa -labda mfalme-, msikiti na makaburi huonekana vizuri. Mji wote ulikuwa na takriban ekari 45 na mabaki ya ukuta uliozunguka yote yaonekana hadi leo lakini nyumba nyingi zilikuwa za watu maskini zilizojengwa kwa kutumia udongo na mbao tu hazionekani tena.

Hakuna uhakika Gedi ya Kale ilianzishwa lini lakini wataalamu hukadiria umri wa nyumba za kwanza zinazopatikana hadi leo kuwa wa mnamo karne ya 13/14. Kuna maandiko ya Kiarabu kwenye makaburi yanayosaidia makadirio hayo. Hakuna habari za kimaandishi juu ya mji, kwa hiyo taarifa zote zimetegemea matokeo ya akiolojia.

Inaonekana Gedi ilikuwa mji tajiri uliostawi kwa biashara. Kuna mabaki ya bidhaa kutoka Uhindi (taa ya chuma), China (jagi la kauri la kipindi cha Ming), Venezia, Italia (ushanga wa kioo), na Hispania (mkasi).

Idadi ya wakazi inakadiriwa ilikuwa hadi 2,500. Nyumba kubwa za matajiri zilikuwa na vyoo vya maji na bafu.

Mnamo karne ya 16 mji uliachwa na wakazi wake. Hakuna uhakika kuhusu sababu yake.

Maghofu ya Gedi yalitangazwa kuwa hifadhi ya taifa na siku hizi yatawaliwa na idara ya makumbusho ya Kenya.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • James Kirkman. 1975. Gedi. Historical monument. Museum Trustees of Kenya, Nairobi.
  • James Kirkman. 1963. Gedi, the palace. Studies in African history, Mouton, Den Haag.
  • James Kirkman. 1954. The Arab City of Gedi. Oxford University Press, Oxford.
  • Eric P. Mitchell. 2011. "Gedi: The Lost City Revisited" World Explorer Magazine, Vol. 6, No. 2, pp. 33–36.
  • Rudolf Fischer. 1984. Korallenstädte in Afrika. Die vorkoloniale Geschichte der Ostküste. Edition Piscator, Oberdorf. pp. 107–121.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]