Burundi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Republika y'u Burundi (Kirundi)
République du Burundi (Kifaransa)
Jamhuri ya Burundi
Bendera ya Burundi Nembo la Burundi
(Bendera ya Burundi) (Nembo la Burundi)
Lugha rasmi Kifaransa, Kirundi, Kiswahili
Mji Mkuu Gitega au Bujumbura
Serikali Jamhuri
Rais Évariste Ndayishimiye
Eneo km² 27,834
Eneo la Rwanda Kazembe km² 123.553
Idadi ya wakazi 10,395,931 (2014)
Wakazi kwa km² 373.4
Pesa Burundi franc
Wimbo wa Taifa Burundi Bwacu (Burundi yetu)
Burundi katika Afrika
Ramani ya Burundi

Jamhuri ya Burundi (iliyojulikana zamani kama Urundi) ni nchi ndogo ambayo iko katika eneo la Maziwa Makubwa ya Afrika. Burundi imepakana na Rwanda upande wa kaskazini, Tanzania upande wa mashariki, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo upande wa magharibi.

Burundi ni mwanachama wa Umoja wa Afrika na wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Jina[hariri | hariri chanzo]

Jina lenyewe la nchi hii, limetokana kwa msingi na kutanuka kwa lugha ya Kirundi ambacho ni lugha ya Kibantu kama vile Kiswahili ambacho pia kinatumika sana.

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Burundi ni kati ya nchi ndogo zaidi zilizomo barani Afrika. Eneo lote ni km² 27,834 pekee.[1] Wakazi milioni 10 ni wengi kulingana na eneo dogo la nchi, msongamano wa watu ni wakazi 314.3 kwenye kila kilomita ya mraba.

Ingawa Burundi haina bahari, sehemu ya mpaka wake eneo la mashariki unaishia kwenye mwambao wa Ziwa Tanganyika.

Eneo lote ni nyanda za juu zenye kimo cha mita 1700 juu ya UB kwa wastani. Sehemu ya juu zaidi ni kilele cha mlima Heha chenye mita 2685 juu ya uwiano wa bahari uliopo katika safu ya milima inayopakana na bonde la ufa la Afrika ya Mashariki.

Sehemu ya magharibi ya nchi ni sehemu ya bonde la ufa yenye kimo cha mita 760-850 juu ya uwiano wa bahari. Sehemu ya kusini ya bonde la ufa katika Burundi imejaa maji ya Ziwa Tanganyika.

Upande wa mashariki wa safu ya milima inayopakana na bonde la ufa kuna chanzo cha mto Ruvyironza (pia: Luvironza) unaoishia katika mto Kagera na hivyo huhesabiwa kati ya vyanzo vya mto Naili.[2]

Hali ya hewa ni ya kitropiki: kuna vipindi viwili vya mvua. Joto linapungua kutokana na kimo cha nchi. Kuna mvua kwa wastani wa milimita 1,000 kwa mwaka.

Matumizi ya ardhi ni kwa ajili ya kilimo au mifugo. Msongamano wa watu umesababisha kuenea kwa ukataji wa misitu, mmomonyoko wa ardhi na kupotea kwa ardhi yenye rutuba[3]. Eneo la misitu lililobaki ni kilomita cha mraba 600 pekee linalopungua kwa kasi ya asilimia 9 kwa mwaka[4].

Viboko kwenye hifadhi ya taifa Rusizi

Kuna hifadhi mbili za taifa ambazo ni Hifadhi ya Taifa ya Kibira kwenye kaskazini-magharibi (inapakana na Msitu wa Nyungwe huko Rwanda), na Hifadhi ya Taifa ya Ruvubu upande wa kaskazni-mashariki karibu na mto Rurubu (pia Ruvubu au Ruvuvu). Hifadhi zote mbili zilianzishwa mwaka 1982 kwa shabaha ya kuhifadhi wanyamapori[5].

Watu[hariri | hariri chanzo]

Idadi ya watu ni takriban milioni 10 na nusu. Asilimia 46 kati yao hawajamaliza miaka 15. Umri wa wastani ni miaka 16.7 hivi.

Idadi ya watoto wanaoaga dunia mapema, ni 62 kati ya 1000 wanaozaliwa (mwaka 2007). Kwa umri wa kifo kwa wastani ni miaka 54 tu. Takriban 1.2% za wananchi wana UKIMWI[6].

Familia ni imara kuliko zile za nchi zote za Afrika.

Wanawake wanazaa kwa wastani watoto 6: hii nafasi ya juu ya tano duniani kote.

Piramidi ya umri kwa Burundi

Jamii ya Burundi ni jamii ya vijijini, ni asilimia 13 pekee wanaoishi katika miji.[7]

Vikundi kati ya wakazi ni hasa Wahutu (~80%), Watutsi (~14%) na Watwaa (mbilikimo) (chini ya 1%). Wote wanatumia lugha ya Kirundi.

Pamoja na hayo, kuna Warundi wachache wanaojinasibu kuwa wao si Watutsi wala Wahutu bali ni Waswahili (~5%). Hilo kabila lilikuwepo toka enzi za tawala za kifalme nchini humo, na ndio wenyeji wa jiji la Bujumbura, waliomsaidia Mwanamfalme Louis Rwagasore katika harakati za kutafuta uhuru wa Burundi.

Dini[hariri | hariri chanzo]

Upande wa dini, Wakristo ni 80-90% kati ya wakazi wote, hasa Wakatoliki (65%), halafu Waprotestanti (26%). Asilimia 5 wanafuata dini za jadi na 3 Uislamu.

Wapiga ngoma za jadi wa Burundi
Askari wa mwami Kasliwami, mnamo 1910

Historia[hariri | hariri chanzo]

Historia ya awali[hariri | hariri chanzo]

Wakazi wa kwanza huaminiwa kuwa wawindaji wa jamii ya Wasani na ya Wabilikimo.

Katika karne za BK walifika wahamiaji Wabantu wenye ujuzi wa kilimo na uhunzi.

Ufalme wa Burundi[hariri | hariri chanzo]

Dola la kwanza katika eneo hili lilikuwa Ufalme wa Burundi. Katika mapokeo ya wenyeji ulianzishwa katika karne ya 17 na mtu kwa jina la Cambarantama aliyefika ama kutoka Rwanda ama kutoka Buha katika Mkoa wa Kigoma, Tanzania ya leo.

Ufalme huo ulitawaliwa na kundi la Watutsi waliokuwa wafugaji wa ng'ombe na kutawala wenyeji waliokuwa wakulima Wabantu. Watutsi walikuwa tabaka la kikabaila. Mfalme au mwami alikuwa mkuu wa makabaila hao ambao walitazamiwa kama mabwana wa ardhi iliyolimwa na watu wa kawaida. Hao wakulima waliruhusiwa kulima nchi wakipaswa kutoa huduma na sehemu ya mavuno kwa mabwana waliopaswa kuwatetea dhidi ya maadui.

Ufalme huo ulienea katika karne zilizofuata. Mwami Ntare IV Rutaganzwa Rugamba aliyetawala tangu mwaka 1796 hadi 1850 aliweza kupanua mipaka ya ufalme wake hadi kushika sehemu kubwa ya eneo la leo.

Ukoloni[hariri | hariri chanzo]

Wazungu wa kwanza waliofika walikuwa wapelelezi Waingereza Richard Burton na John Hanning Speke mnamo mwaka 1854. Lakini habari za falme kwenye eneo kati ya maziwa makubwa hazikuenea sana. Wakati wa Mkutano wa Berlin 1885 Wajerumani hawakujua ya kwamba falme za Burundi na Rwanda zilikuwepo ndani ya eneo waliotegemea kutwaa. Waliitambua baadaye tu.

Mwaka 1894 Mjerumani wa kwanza alipita Burundi aliyekuwa Oskar Baumann. Wakati ule Ujerumani uliwahi tayari kuanzisha koloni ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani lakini Wajerumani walichelewa kufika kaskazini-magharibi mwa maeneo waliyotazama kuwa sehemu yao.

Katika Burundi kikosi cha kwanza cha Kijerumani kilifika mnamo 1896 wakakuta ufalme wa mwami wakaridhika kumwacha mwakilishi mkazi (resident) katika mji mkuu Gitega ambaye hakuhusika na mambo ya utawala wa ndani. Wakati ule eneo lilijulikana kwa jina "Urundi". Hapa sawa na Rwanda na Bukoba Wajerumani walitumia mbinu ya eneo lindwa ingawa walikuwa pia na majadiliano kuingiza falme hizi za kienyeji moja kwa moja ndani ya koloni lao.

Baada ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia Burundi pamoja na Rwanda ilikabidhiwa kwa Ubelgiji kwa niaba ya Shirikisho la Mataifa kama eneo la kudhaminiwa lililoitwa Ruanda-Urundi. Kimsingi Wabelgiji waliendelea na mfumo wa Wajerumani uliomwachia mtemi mamlaka kubwa. Waliweka Ruanda-Urundi chini ya serikali ya Kongo ya Kibelgiji.

Lakini baadaye walianza kuingilia zaidi, na ilhali wakati ule walipendelea Watutsi, karibu machifu wote walikuwa Watutsi, na Wahutu walipotea katika nafasi za uongozi kimahali.

Tangu mwaka 1946 Shirikisho la Mataifa lilikwisha na Ubelgiji ilipokea wito wa kutawala Ruanda-Urundi na Umoja wa Mataifa.

Jiji la Bujumbura

Uhuru[hariri | hariri chanzo]

Mwaka moja kabla ya uhuru kulikuwa na uchaguzi wa kwanza chini ya usimamizi ya UM na chama mshindi kilikuwa UPRONA kilichoongozwa na mwanamfalme Mtutsi Louis Rwagasore aliyemwoa mwanamke wa Kihutu na chama kiliunganisha pande zote mbili. Lakini miezi michache baadaye Rwagasore aliuawa na chama chake kilitengana kufuatana na ukabila.

Mwaka 1962 Umoja wa Mataifa uliamua kuipa Ruanda-Urundi uhuru kamili, lakini kila nchi pekee.

Baada ya uchaguzi wa 1965 mapigano yalitokea kwa silaha, na kikundi cha Watutsi wakali kilichukua serikali.

Mwaka 1966 mwami alipinduliwa na mwanasiasa Michel Micombero aliyejitangaza kuwa rais na nchi kuwa jamhuri. Kuanzia hapo wanasiasa na watumishi wakubwa walio Wahutu walifukuzwa, kukamatwa au kuuawa.

Soko la Mbuzi, Karuzi, Burundi

Hali ya nchi kijamii na kisiasa[hariri | hariri chanzo]

Burundi ilundwa kama ufalme ulioongozwa na Watutsi waliotawala Wahutu. Lakini kabla ya ukoloni mipaka kati ya makundi hayo haikuwa imara mno; Wahutu matajiri katika utumishi wa mwami waliweza kupanda ngazi na kuwa Watutsi na pia Watutsi maskini waliweza kushuka ngazi na kuhesabiwa kati ya Wahutu, hasa baada ya kuoa au kuolewa na mtu wa upande mwingine. Uhusiano wa makundi hayo ulifanana zaidi na ule wa matabaka si wa makabila tofauti, pia kwa sababu lugha ilikuwa moja kwa wote.

Utawala wa kikoloni uliimarisha mipaka kati ya makundi hayo mawili maana kila mtu aliandikishwa na kupangwa katika moja kati ya makundi hayo. Pia Wabelgiji walipendelea Watutsi na kuangalia wapate nafasi zote za uchifu ambako walipaswa kutoa kibali. Kuhamia katika kundi lingine kulikwisha. Uhusiano kati ya makundi ulianza kufanana zaidi na ukabila.

Mwishoni mwa ukoloni Wabelgiji walibadilisha msimamo na kupendelea Wahutu.

Katika hali hiyo Burundi ilikaribia uhuru. Vyama vya siasa viliundwa vilivyofuata ugawaji wa kimbari kati ya Watutsi na Wahutu. Mapigano ya kwanza kati ya Wahutu na Watutsi yalitokea mwaka 1959 kabla ya uhuru yakakomeshwa na Wabelgiji.

Baada ya uhuru katika Burundi, kinyume na Rwanda, utawala ulibaki upande wa Watutsi kwa sababu jeshi lilikuwa mikononi mwao. Vipindi vya mashambulio kati ya vikundi vilifuata.

Mwaka 1972 malaki ya Wahutu waliuawa na jeshi la Kitutsi waliolenga hasa Wahutu wenye elimu.

Mwaka 1993 uongozi wa Kitutsi ulikubali tena uchaguzi huru ambako Mhutu Melchior Ndadaye alichaguliwa kuwa rais. Alipouawa na wanajeshi Watutsi malaki ya Watutsi waliuawa na Wahutu wakali.

Kipindi kilichofuata kilikuwa cha Vita ya wenyewe kwa wenyewe katika sehemu mbalimbali za nchi.

Uwanja wa Ndege, Bujumbura

Tangu mwaka 1995 Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa zilijitahidi kujenga mapatano kati ya vikundi. Marais na wanasiasa walioshiriki katika jitihada hizo walikuwa pamoja na Julius Nyerere, Boutros Boutros-Ghali, Nelson Mandela, Thabo Mbeki na rais wa Marekani Bill Clinton.

Mapatano yalifikiwa na kusainiwa mwaka 2000 na washiriki karibu wote huko Arusha. Majadiliano yaliendelea hadi mwaka 2003 hatimaye vita ilisimamishwa. Mapatano yaliyofikiwa yanasema ya kwamba Watutsi pamoja na Watwa, ambao ni asilimia 15 za wananchi, watakuwa na asilimia 40 ya nafasi kwenye bunge na ya kwamba jeshini kila upande utashika asilimia 50 za nafasi. Pia kwenye senati ya bunge kila upande utakuwa na asilimia 50. [8]

Rais atachaguliwa na wananchi wote lakini mapatano yalisema rais wa kwanza atachaguliwa na bunge.

Rais Nkurunziza mwaka 2006

Siasa[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 2005 uchaguzi wa kwanza wa bunge baada ya vita ya wenyewe kwa wenyewe ulifanyika. Chama cha CNDD-FDD kilipata kura nyingi na kiongozi chake Pierre Nkurunziza alichaguliwa na bunge kuwa rais wa taifa. Vyama vya UPRONA na FRODEBU vilivyotangulia kuongoza serikali ya mpito vilipata kura chache kwa sababu vilishtakiwa kuwa na rushwa na upendeleo wa kindugu.

Chama tawala kinajaribu kufuata siasa ya mapatano ya ndani, lakini ina uvumilivu mdogo tu kwa upinzani na mawazo yanayopinga siasa yake.

Mwezi Aprili 2009 chama cha Palipehutu FNL hatimaye kilisimamisha upinzani kwa silaha kikakubaliwa kama chama cha kisiasa cha FNL.

Nkurunziza alichaguliwa tena kwa kura ya wananchi wote mwaka 2010. Chama cha upinzani FNL kilikataa kukubali ushindi wa CNDD-FDD.

Mwaka 2015 rais Nkurunziza alipendekezwa kugombea tena urais katika uchaguzi akakubali. Hatua hiyo ilisababisha upinzani mkali wa wananchi walioandamana wakiona hii inavunja mapatano ya amani ya Arusha.

Tarehe 13 Mei jenerali Godefroid Niyombare alitangaza kufukuzwa kwa Nkurunziza kutoka urais wakati huyo alikuwa safarini Tanzania, lakini uasi huu wa kijeshi ulikandamizwa.

Nkurunziza alirudi na kutangaza ya kwamba kura inatakiwa kufanyika jinsi ilivyopangwa tarehe 26 Mei 2015 kwa bunge na tarehe 26 Juni kwa urais.

Taasisi ya kimataifa na nchi jirani walitamka wasiwasi kuhusu mwelekeo wa hali ya kisiasa katika Burundi. Nkosazana Dlamini-Zuma, mwenyekiti wa kamati tendaji ya Umoja wa Afrika, aliomba kuahirishwa kwa kura nchini Burundi hadi hali iwe imetulia.

Tarehe 24 Julai 2015 Tume ya Uchaguzi ilimtangaza Nkurunziza mshindi wa uchaguzi kwa 69.41% za kura. Agathon Rwasa alishika nafasi ya pili kwa 18.99% ingawa alikuwa amehimiza wananchi wasipige kura.

Kilichofuata kimesababisha wananchi 200,000 wakimbie, huko rais akikataza Umoja wa Afrika usitume askari kulinda amani na haki nchini, wakati wanajeshi wanaendelea kuua na kunyanyasa Watutsi wakielekea mauaji ya kimbari.

Utawala[hariri | hariri chanzo]

Burundi imegawiwa katika mikoa 17 (kwa Kifaransa province, kwa Kirundi: IProvense) inayoitwa kufuatana na miji yenye makao makuu ya utawala.

*Angalia Mikoa ya Burundi

Mikoa imegawiwa kwa wilaya inayoitwa "communes" na hii imegawiwa kwa "collines" (vilima).

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Kama Burundi ingekuwa Mkoa wa Tanzania, ingekuwa kwenye na nafasi ya 14 kwa ukubwa, maana ni ndogo kuliko Mkoa wa Pwani na kidogo kubwa kuliko Mkoa wa Tanga; kama ingekuwa wilaya ya Kenya ingekuwa na nafasi ya sita kwa eneo maana ni ndogo kuliko Wilaya ya Mto Tana na kubwa kuliko Mandera.
  2. [Klohn, Wulf and Mihailo Andjelic. [http://www.fao.org/ag/AGL/AGLW/webpub/lakevic/LAKEVIC4.htm Lake Victoria: A Case in International Cooperation]. Food and Agriculture Organization of the United Nations. Retrieved on July 20, 2008]
  3. [Bermingham, Eldredge, Dick, Christopher W. and Moritz, Craig (2005). ''Tropical Rainforests: Past, Present, and Future''. Chicago, Illinois: [[University of Chicago]] Press, p. 146. ISBN 0-226-04468-8]
  4. [http://www.mongabay.com/deforestation.htm Worldwide Deforestation Rates] Food and Agriculture Organization of the U.N.: The State of the World's Forests 2003. Published on Mongabay.com. Retrieved on June 29, 2008.
  5. East, Rob (1999). ''African Antelope Database 1998''. [[Gland, Switzerland]]: [[International Union for Conservation of Nature]], p. 74. ISBN 2-8317-0477-4.
  6. UNDP Human Development Index; wastani ya Tanzania ni miaka 64. Jalada kutoka ya awali juu ya 2015-06-01. Iliwekwa mnamo 2015-05-14.
  7. World Fact Book 2008. Jalada kutoka ya awali juu ya 2018-01-28. Iliwekwa mnamo 2015-05-14.
  8. Mapatano ya Arusha ya 2000 kuhusua mani na upatanisho kwa ajili ya Burundi, uk. Protocoll II, I, 11, 4a, Appendix I,I B 2-4. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-02-25. Iliwekwa mnamo 2015-05-13.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Mambo mengi ya Burundi yamepatikana kutoka CIA World Factbook 2000 na 2003 U.S. Department of State website.
  • Burundi: Ethnic Conflict and Genocide Reni Lemarchand and Lee H. Hamilton

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:

Serikali[hariri | hariri chanzo]

Habari[hariri | hariri chanzo]

Overviews[hariri | hariri chanzo]

Maendelezo[hariri | hariri chanzo]

Vinginevyo[hariri | hariri chanzo]


Nchi za Afrika Bara la Afrika
Afrika ya Kati (Jamhuri ya) | Afrika Kusini | Algeria | Angola | Benin | Botswana | Burkina Faso | Burundi | Cabo Verde | Chad | Cote d'Ivoire | Eritrea | Eswatini | Ethiopia | Gabon | Gambia | Ghana | Guinea | Guinea Bisau | Guinea ya Ikweta | Jibuti | Kamerun | Kenya | Komori | Kongo (Jamhuri ya) | Kongo (Jamhuri ya Kidemokrasia ya) | Lesotho | Liberia | Libya | Madagaska | Malawi | Mali | Misri | Morisi (Visiwa vya) | Mauritania | Moroko | Msumbiji | Namibia | Niger | Nigeria | Rwanda | Sahara ya Magharibi | Sao Tome na Principe | Senegal | Shelisheli | Sierra Leone | Somalia | Sudan | Sudan Kusini | Tanzania | Togo | Tunisia | Uganda | Zambia | Zimbabwe
Maeneo ya Afrika ambayo ni sehemu za nchi nje ya Afrika
Hispania: Kanari · Ceuta · Melilla | Italia: Pantelleria · Pelagie | Ufaransa: Mayotte · Réunion | Uingereza: · St. Helena · Diego Garcia | Ureno: Madeira
Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Burundi kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.