Jumuiya ya Afrika Mashariki

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Jumuia ya Afrika Mashariki)
Jumuiya ya Afrika Mashariki
English: East African Community
Wito: Taifa Moja Mustakabali Mmoja
English: "One People One Destiny"
Wimbo wa taifa: Jumuiya Yetu
Makao makuuArusha, Tanzania
Lugha rasmi Kiswahili, Kiingereza
Aina Shirika la kimataifa
Uanachama Bendera ya Burundi Burundi
Bendera ya Kenya Kenya
Bendera ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Democratic Republic of the Congo
Bendera ya Rwanda Rwanda
Bendera ya Somalia Somalia
 South Sudan
Bendera ya Tanzania Tanzania
Bendera ya Uganda Uganda
Viongozi
 -  Mwenyekiti Salva Kiir Mayardit
 -  Mwenyekiti wa Baraza Shem Bageine
 -  Rais wa Mahakama Harold Nsekela
 -  Spika wa Bunge Margaret Zziwa
 -  Katibu Mkuu Richard Sezibera
Bunge Bunge la EAC (EALA)
Maanzilisho
 -  Mara ya kwanza 1967 
 -  Kufutwa 1977 
 -  Mara ya pili 7 July 2000 
Eneo
 -  Jumla 4,810,363 km2 (7th a)
1,857,292 sq mi 
 -  Maji (%) 4.14
Idadi ya watu
 -  2022 makisio 312,362,653 a (4th)
 -  Density 58.4/km2
151.3/sq mi
Pato la Taifa makisio 2020 
 -  Total US$ 602.584 billion[1] (34tha)
 -  Per capita US$ 3,286
GDP (nominal) 2020 estimate
 -  Total US$ 220.783 billion (50tha)
 -  Per capita US$ 1,185 a
Currency
Saa za eneo CAT / EAT (UTC+2 / +3)
Tovuti
eac.int
a. If considered as a single entity.
b. To be replaced by the East African shilling
Nchi tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki

Jumuiya ya Afrika Mashariki au Mtangamano wa Afrika Mashariki (kwa Kiingereza East African Community, kifupi EAC) ni muundo wa kisiasa unaounganisha nchi nane za kanda ya Maziwa Makuu ya Afrika Mashariki: Burundi, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Rwanda, Somalia[2], Sudan Kusini[3], Tanzania na Uganda.[4]

Kwa sasa eneo la Mtangamano ni km2 4,810,363, likiwa na wakazi 312,362,653 (kadirio la mwaka 2022), hivi kwamba ingekuwa nchi moja tu ingekuwa ya nne duniani.

Jumuiya yenye jina hilo imepatikana mara mbili katika historia: jumuia ya nchi tatu kati ya hizo ilianzishwa mwaka 1967, lakini ilisambaratika mwaka 1977[5][6][7] ikafufuliwa rasmi tarehe 7 Julai 2000.[8]

Jumuiya ya kwanza

Nchi tatu za Afrika ya Mashariki zilizokuwa chini ya utawala wa Uingereza zilianza uhuru wao kwa kuendeleza ushirikiano wa karibu uliorithiwa kutokana na utawala wa pamoja wakati wa ukoloni.

Baada ya kupata uhuru mwaka 1961 nchi hizo ziliunda Mamlaka ya Huduma za Pamoja za Afrika ya Mashariki (kwa Kiingereza East African Common Services Organisation – kifupi EACSO).

Ushirikiano ulihusu fedha (East African Shilling), forodha (Customs Union), huduma za reli (East African Railway), ndege (East African Airways), mabandari, posta na simu na elimu ya juu (Chuo Kikuu cha Afrika ya Mashariki chenye kampasi Makerere, Dar es Salaam na Nairobi). Mkataba ulilenga pia mahakama kuu ya pamoja na sera ya kiuchumi ya soko la pamoja. Haya yote yalitakiwa kuwa chini ya Bunge la Afrika Mashariki.

Tangu 1965 umoja huo ulianza kurudi nyuma kila nchi ilipoanzisha pesa yake.

Mwaka 1967 nchi tatu zilijaribu upya kuimarisha umoja wao kwa Mkataba wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki wakiita umoja wao "Jumuiya ya Afrika ya Mashariki" ikiwa na makao makuu Arusha, Tanzania.

Lakini mielekeo ya nchi zote tatu zilitofautiana mno: Kenya iliendelea kwa njia ya upebari lakini Tanzania ilijaribu kujenga Ujamaa (usoshalisti) kuanzia mwaka 1967. Uganda uliingia katika kipindi cha udikteta kali ya Idi Amini aliyeharibu uhusiano na majirani alipoanza kudai sehemu za maeneo yao.

Sababu nyingine ni madai ya Kenya ya kuwa na viti zaidi kuliko Uganda na Tanzania katika kamati za maamuzi,[9] huku kukiwa na kutokuelewana kulikosababishwa na udikteta wa Idi Amin nchini Uganda, Usoshalisti huko Tanzania, na soko huria nchini Kenya,[6] hivyo wanachama hawa watatu wakapoteza ushirikiano wa miaka zaidi ya sitini na manufaa ya ukubwa wa jumuiya hii kiuchumi. Kila mmoja wa wanachama hawa ilimbidi kuanza kutoa huduma na kujenga viwanda ambavyo hapo awali vilikuwa chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hivyo mwaka 1977 Jumuiya ya Afrika Mashariki ilikoma kufanya kazi yoyote na 1983 ilifutwa rasmi. Mali iliyobaki iligawanywa kati ya nchi zote tatu.

Kufufuka kwa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki tangu 1993

Tangu miaka ya 1990 majaribio ya kujenga umoja mpya yalionekana tena.

Marais Daniel arap Moi wa Kenya, Ali Hassan Mwinyi wa Tanzania, na Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda walipatana katika Mkataba wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki huko Arusha, tarehe 30 Novemba 1993, na kuanzisha Tume ya Ushirikiano ya nchi hizi tatu. Shughuli ya kuzileta pamoja nchi hizi kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni, utafiti na teknolojia, ulinzi, usalama, masuala ya kisheria na kimahakama ilianza.

Mkataba wa kufufua jumuiya ulitiwa sahihi tarehe 30 Novemba 1999 ukaanza kuwa rasmi tarehe 7 Julai 2000.

Vyombo vya Jumuiya mpya ya Afrika ya Mashariki vilianza kufanya kazi mnamo Januari 2001 penye makao makuu ya jumuiya hii huko Arusha.

Mkataba 2004 uliweka msingi wa Umoja wa Forodha ulioanzishwa 2005.

Kuna tena Bunge la Afrika ya Mashariki linalojumuisha wabunge waliochaguliwa na mabunge ya nchi wanachama.

Pia Mahakama Kuu ya Afrika ya Mashariki imeundwa upya.

Mwaka 2008, baada ya majadiliano na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Southern Africa Development Community, kifupi SADC) na Soko la Pamoja la Mashariki na Kusini mwa Afrika (Common Market for Eastern and Southern Africa, kifupi COMESA), Mtangamano huo ulikubali nchi zote za miundo hiyo mitatu ziunde eneo pana la biashara huria. Kwa sasa Jumuiya ya Afrika Mashariki ni mojawapo ya nguzo muhimu za hiyo Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika (African Economic Community, kifupi AEC).

Mwaka 2010, Mtangamano ulitangaza soko la pamoja kwa bidhaa, kazi na mitaji kati ya nchi hizo tano, kwa lengo la kuanzisha pesa ya pamoja na hatimaye Shirikisho kamili.[10]

Kuna majadiliano ya kuanzisha shilingi mpya ya pamoja kwa nchi za Jumuia ya Afrika ya Mashariki. Kwanza ilitarajiwa kuanzishwa mwaka 2012, halafu mwaka 2015, sasa mwaka 2024. Mwaka 2013 ulisainiwa mkataba wa kuamua kuanzisha hiyo pesa ndani ya miaka 10.[11]

Nchi wanachama na jinsi zilivyojiunga

Kutoka kushoto: Rais Yoweri Museveni wa Uganda, Rais Mwai Kibaki wa Kenya na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania wakati wa mkutano wao Arusha, mnamo Novemba 2006.
Rais wa Rwanda Paul Kagame katika mkutano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka wa 2006. Rwanda ilijiunga na Jumuiya ya Afrika mashariki tarehe 1 Julai 2007

Kenya, Tanzania na Uganda zina historia ya ushirikiano tangu mwanzoni mwa karne ya 20, wakati wa ukoloni, ikiwa ni pamoja na Umoja wa Forodha baina ya Kenya na Uganda mwaka 1917, Tanganyika ilijiunga mnamo mwaka 1927, katika Ubalozi wa Afrika Mashariki (1948-1961), 'East African Common Services Organisation' (1961-1967) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (1967-1977).[12]

Jumuia ambayo ilianzishwa baada ya uhuru ilidumu miaka 10 tu, lakini ilifufuliwa kwa mkataba wa tarehe 30 Novemba 1999, ulioanza kufanya kazi tarehe 7 Julai 2000, miaka 23 baada ya kifo cha ile ya kwanza.

Burundi na Rwanda, ambazo ziliwahi kuwa koloni moja na Tanzania bara kabla ya Vita vikuu vya kwanza, zilijiunga na Mtangamano tarehe 6 Julai 2009.[13]

Mara baada ya kupata uhuru mwaka 2011, Sudan Kusini iliomba kujiunga na Jumuia, lakini haikukubalika hadi Machi 2016 kutokana na hali ya vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.

Tarehe 23 Novemba 2021 Baraza la Mawaziri la EAC limependekeza kwa Wakuu wa nchi wanachama wakubali ombi la kujiunga la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo [14], nao wakakubali rasmi tarehe 29 Machi 2022.

Hatua kubwa ya awali katika kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki ni muungano wa forodha katika mataifa husika uliotiwa saini mnamo Machi 2004 na ulioanza kutumika tarehe 1 Januari mwaka 2005. Chini ya masharti ya mkataba, Kenya, ambayo ndiyo nchi inayopata mauzo bora zaidi nje ya nchi katika kanda ya Afrika Mashariki, iliendelea kulipa ushuru kwa bidhaa zake zinazoingia nchi nyingine wanachama hadi mwaka 2010, kwa kiwango kilichopungua na wakati. Mfumo sawa wa ushuru utatumika kwa bidhaa kutoka nchi ambazo si wanachama.

Vipingamizi kuelekea shirikisho

Kwa ujumla, mataifa wanachama kwa kiasi kikubwa wanaona neema ya Shirikisho la Afrika Mashariki, lakini utafiti usio rasmi unaonyesha kwamba Watanzania wengi (asilimia themanini ya wakazi wake) wana mtazamo hasi.[15]

Tanzania imekuwa na historia ya amani tangu kunyakua uhuru, ikilinganishwa na fujo na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoshuhudiwa katika mataifa ya Kenya, Rwanda, Burundi, na Uganda. Wakati huu Afrika Mashariki inajaribu kudumisha utulivu na mafanikio katikati ya migogoro inayoendelea katika nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Pembe ya Afrika na Sudan Kusini.

Pia ni kwamba Tanzania ina ardhi kubwa, na baadhi ya Watanzania wana hofu ya unyakuzi wa ardhi na wakazi wa sasa wa mataifa mengine wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.[16] [17] [18]

Uhaba wa ardhi ni suala nyeti katika eneo la Afrika Mashariki, hasa nchini Kenya, ambako mapigano ya wenyewe kwa wenyewe upande wa Mlima Elgon mwaka 2007 yaliwaacha zaidi ya watu 150 wamefariki na kulazimisha takriban watu wengine 60,000 kugura makazi yao.[19]

Mahakama ya Afrika Mashariki

Mahakama ya Afrika Mashariki ndiyo mahakama inayosimamia kesi zote katika eneo hilo. Kwa sasa imo mjini Arusha, Tanzania.

Bunge la Afrika Mashariki

Bunge la Afrika Mashariki ndicho kitengo cha kutengeneza sheria katika eneo la Afrika Mashariki. Ina wajumbe 27 ambao wote wamechaguliwa na mabunge ya nchi wanachama. Linahusika na masuala yote ambayo yanahusu Jumuiya hii kama vile kujadili bajeti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na masuala yote ya Jumuiya na kutoa mapendekezo kwa Baraza juu ya mambo wanayoyadhani muhimu kwa utekelezaji wa mkataba, kushirikiana pamoja na Bunge husika na kuanzisha kamati kwa makusudi kama vile wanavyodhani ni muhimu. Tangu uzinduzi wake mwaka 2001, bodi hii imekuwa na vikao kadhaa mjini Arusha, Kampala na Nairobi.

Pasipoti ya Afrika Mashariki

Pasipoti ya Afrika Mashariki ilizinduliwa rasmi tarehe 1 Aprili 1999 ili kurahisisha usafiri na kuvuka mipaka ya nchi husika.[20][21] Ni halali kwa kusafiri ndani ya eneo la Afrika Mashariki (Kenya,Uganda na Tanzania) na kutoa haki ya kuingia na kukaa kwa miezi sita katika nchi yoyote na kisha unaweza ukaitumia tena.[20] Pasipoti hii inapatikana katika Makao Makuu ya Idara ya Uhamiaji katika miji ya Nairobi, Kampala na Dar es Salaam. Ni raia tu wa Afrika Mashariki wanaoweza kuomba pasipoti hii.[20][21] Gharama ya pasipoti hii ni dola 10 za Marekani au pesa sawa ukibadilisha kwa sarafu za nchi za Afrika mashariki.[21] Baada ya kujaza fomu za kupata pasipoti hii itachukua muda wa wiki mbili au tatu kuipata tayari kwa matumizi. Ingawa pasipoti hii ni halali tu ndani ya Afrika Mashariki, majadiliano yalifanywa ili kuwa na hati sawa za kusafiri kwa watu wote wa Afrika Mashariki.[20]

Viza moja kwa watalii

African Union

Makala hii imepangwa kwa mfululizo:
Siasa na serikali ya
the African Union



Nchi zingine · Atlasi

Lilikuwa tarajio la wengi kuwa kabla ya 2006 kungekuwa na viza moja kwa watalii wote wanaozuru Afrika Mashariki, iwapo mpango huo ungeidhinishwa na mamlaka ya sekta husika chini ya jumuiya hiyo. Iwapo ingekubalika basi viza hiy ingetumika kote katika ardhi ya wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Chini ya pendekezo hili viza yoyote mpya ya Afrika Mashariki ingeweza kupokewa kutoka ubalozi wowote katika eneo la Afrika Mashariki.

Mtandao

Matumizi ya wavuti katika eneo la Afrika Mashariki bado yako chini mno yakilinganishwa na mataifa yaliyostawi kiuchumi.

Eneo la Afrika Mashariki ni kituo kizuri kiuchumi huku likikadiriwa kuwa na wakazi zaidi ya milioni 150. Inakadiriwa kuwa asilimia 10 ya wakazi wa Afrika Mashariki - milioni 15 - huutumia Mtandao.

Mkakati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki unasisitiza ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo kwa kuzingatia uwezo wa kijamii.

Wengi wa wakazi wa Afrika Mashariki hutumia mtandao kuangalia habari, kusoma barua pepe na kwenye mitandao mingine ya kijamii.

Hivi karibuni kumekuwa na majukwaa mengi yanayoibuka katika eneo hili kwa lengo la kuileta pamoja Afrika Mashariki.

Kasi ya mawasiliano kupitia kwa mtandao pia iko chini mno katika eneo la Afrika Mashariki, ikilinganishwa na mataifa yaliyostawi. Hii labda ni mojawapo ya vikwazo vya maendeleo ya mawasiliano ya mtandao Afrika Mashariki.

Jiografia

Mtangamano ungekuwa nchi moja tu, ungekuwa ya 7 duniani kwa eneo (kilometa mraba 4,812,618).

Lake Victoria
Ziwa Victoria kati ya nchi za Mtangamano.
Mount Kilimanjaro
Mlima Kilimanjaro, mrefu kuliko yote ya Afrika, uko Tanzania.

Sudan Kusini, Uganda, Rwanda na Burundi hazina pwani baharini, lakini zina mvua za kutosha.

Huku inapatikana minne kati ya milima mirefu zaidi barani Afrika: Mlima Kilimanjaro (Tanzania), Mlima Kenya (Kenya), milima ya Rwenzori (Uganda/DRC) na Mlima Meru (Tanzania).

Ziwa Turkana, Kenya, ndiyo ziwa la jangwani kubwa na lenye maji ya chumvi nyingi kuliko yote duniani.

Ziwa Victoria linaunganisha nchi za Kenya, Uganda na Tanzania na ni la pili duniani kwa eneo.

Ziwa Tanganyika kati ya Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni la pili duniani kwa kina.

Kenya pekee ina jangwa, jangwa la Chalbi katika Kaunti ya Marsabit.

Wildebeest#Migration
Uhamaji wa wanyamapori ni ajabu la kimaumbile la 7 duniani
Mount Kilimanjaro
Ziwa Nakuru, maarufu kwa flamingo.
Dar es Salaam, ukiwa na watu milioni 4 ndio mji mkubwa kuliko yote ya Mtangamano baada tu ya Kinshasa.
Nairobi, kitovu cha biashara cha Mtangamano

Ugatuzi katika nchi za Jumuia ya Afrika Mashariki (E.A.C.)

Burundi

  1. Bubanza
  2. Bujumbura Mjini
  3. Bujumbura Vijijini
  4. Bururi
  5. Cankuzo
  6. Cibitoke
  7. Gitega
  8. Karuzi
  9. Kayanza
  10. Kirundo
  11. Makamba
  12. Muramvya
  13. Muyinga
  14. Mwaro
  15. Ngozi
  16. Rutana
  17. Ruyigi

Kenya

  1. Mombasa
  2. Kwale
  3. Kilifi
  4. Tana River
  5. Lamu
  6. Taita–Taveta
  7. Garissa
  8. Wajir
  9. Mandera
  10. Marsabit
  11. Isiolo
  12. Meru
  13. Tharaka-Nithi
  14. Embu
  15. Kitui
  16. Machakos
  17. Makueni
  18. Nyandarua
  19. Nyeri
  20. Kirinyaga
  21. Murang'a
  22. Kiambu
  23. Turkana
  24. West Pokot
  25. Samburu
  26. Trans-Nzoia
  27. Uasin Gishu
  28. Elgeyo-Marakwet
  29. Nandi
  30. Baringo
  31. Laikipia
  32. Nakuru
  33. Narok
  34. Kajiado
  35. Kericho
  36. Bomet
  37. Kakamega
  38. Vihiga
  39. Bungoma
  40. Busia
  41. Siaya
  42. Kisumu
  43. Homa Bay
  44. Migori
  45. Kisii
  46. Nyamira
  47. Nairobi

Rwanda

  1. Kigali
  2. Kaskazini
  3. Kusini
  4. Magharibi
  5. Mashariki

Somalia

  1. Awdal
  2. Bari
  3. Nugal
  4. Mudug
  5. Galguduud
  6. Hiran
  7. Shebeli wa Kati
  8. Banaadir
  9. Shebeli wa Chini
  10. Togdheer
  11. Bakool
  12. Woqooyi Galbeed
  13. Bay
  14. Gedo
  15. Juba wa Kati
  16. Juba wa Chini
  17. Sanaag
  18. Sool

Sudan Kusini

  1. Bahr el Ghazal Kaskazini
  2. Bahr el Ghazal Magharibi
  3. Lakes
  4. Warrap
  5. Western Equatoria
  6. Central Equatoria
  7. Eastern Equatoria
  8. Jonglei
  9. Greater Upper Nile
  10. Unity
  11. Upper Nile
  12. Eneo la Abyei
  13. Eneo la Pibor
  14. Eneo la Ruweng

Tanzania

  1. Arusha
  2. Dar es Salaam
  3. Dodoma
  4. Geita
  5. Iringa
  6. Kagera
  7. Katavi
  8. Kigoma
  9. Kilimanjaro
  10. Lindi
  11. Manyara
  12. Mara
  13. Mbeya
  14. Morogoro
  15. Mtwara
  16. Mwanza
  17. Njiombe
  18. Pemba Kaskazini
  19. Pemba Kusini
  20. Pwani
  21. Rukwa
  22. Ruvuma
  23. Shinyanga
  24. Simiyu
  25. Singida
  26. Songwe
  27. Tabora
  28. Tanga
  29. Unguja Kaskazini
  30. Unguja Mjini Magharibi
  31. Unguja Kusini

Uganda

  1. Mkoa wa Kaskazini
  2. Mkoa wa Kati
  3. Mkoa wa Magharibi
  4. Mkoa wa Mashariki

Wakazi

Jumla ya wakazi wote ilikuwa 312,362,653 mnamo 2022.

Katika Mtangamano, hasa nchini Tanzania, zinapatikana jamii zote za makabila ya Afrika kusini kwa Sahara: Khoisan, Wakushi, Wabantu, Waniloti.

Asilimia ya wakazi wanaoishi mijini ni 20 tu, lakini wanaongekeza kwa 4.71% kila mwaka.

Nchi Mji mkuu Kujiunga Wakazi Eneo (km2) GDP
(US$ bn)​[22]
GDP
kwa mtu
(US$)[22]
GDP PPP
(US$ bn)[23]
GDP PPP
kwa mtu
(US$)[23]
Bendera ya Burundi Burundi Gitega 2007 &0000000012722976.00000012,722,976 &0000000000027834.00000027,834 3.4 &0000000000000272.400000272.4 10.8 &0000000000000855.600000855.6
Bendera ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Kinshasa 2022 &0000000095944984.00000095,944,984 &0000000002344858.0000002,344,858 51.2 &0000000000000669.400000669.4 127.4 &0000000000001315.9000001,315.9
Bendera ya Kenya Kenya Nairobi 2000 &0000000056553921.00000056,553,921 &0000000000580367.000000580,367 114.7 &0000000000002252.0000002,252 308.7 &0000000000006061.4000006,061.4
Bendera ya Rwanda Rwanda Kigali 2007 &0000000013705697.00000013,705,697 &0000000000026338.00000026,338 12.1 &0000000000000910.000000910 37.2 &0000000000002807.6000002,807.6
Bendera ya Somalia Somalia Mogadishu 2024 &0000000016500000.00000016,500,000 &0000000000637657.000000637,657 12.49 &0000000000000756.980000756.98 34.02 &0000000000002060.0000002,060
Bendera ya South Sudan South Sudan Juba 2016 &0000000011501583.00000011,501,583 &0000000000644329.000000644,329 5.7 &0000000000000392.700000392.7 13.5 &0000000000000927.400000927.4
Bendera ya Tanzania Tanzania Dodoma 2000 &0000000063732235.00000063,732,235 &0000000000945087.000000945,087 77.5 &0000000000001260.1000001,260.1 206.6 &0000000000003358.3000003,358.3
Bendera ya Uganda Uganda Kampala 2000 &0000000049135753.00000049,135,753 &0000000000241550.000000241,550 46.4 &0000000000001060.4000001,060.4 129.5 &0000000000002960.5000002,960.5
&0000000303397152.000000303,397,152 &0000000004810363.0000004,810,363 325 1106.3 834 2,841.4

Lugha kubwa zaidi katika Mtangamano ni Kiswahili, ambacho kutoka pwani ya Somalia, Kenya na Tanzania kimeenea kwa namna moja au nyingine katika nchi zote nane na nje yake pia. Lugha rasmi ni Kiswahili, Kiingereza na Kifaransa.

Upande wa dini, unaongoza Ukristo (77.64%), ukifuatwa na Uislamu (17.1%) na dini asilia za Kiafrika (3.38%). Kati ya Wakristo, Wakatoliki wanaongoza nchini Burundi na Sudan Kusini, kumbe Waprotestanti wanaongoza Kenya, huku aina hizo mbili zikilingana katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Tanzania, Uganda na Rwanda. Somalia ni nchi pekee ya Kiislamu hasa.

Tazama pia

Tanbihi

  1. [1]
  2. https://www.mwananchi.co.tz/mw/habari/kitaifa/somalia-yatambuliwa-rasmi-eac-viongozi-kuvalia-njuga-migogoro-4545254
  3. "South Sudan admitted into EAC", Daily Nation, 2 March 2016, reprinted at nation.co.ke, accessed 4 March 2016
  4. Joint Communiqué of the eighth Summit of EAC Heads of State
  5. – Born in anonymity. Ms.dk. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-04-15. Iliwekwa mnamo 2010-07-01.
  6. 6.0 6.1 East African trade zone off to creaky start, Christian Science Monitor, 9 Machi 2006
  7. We Celebrated at EAC Collapse, Says Njonjo.
  8. East African Community – Quick Facts. Eac.int. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-03-19. Iliwekwa mnamo 2010-07-01.
  9. ms.dk - Born in anonymity. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-04-15. Iliwekwa mnamo 2009-12-03.
  10. "FACTBOX-East African common market begins", 1 July 2010. Retrieved on 1 July 2010. Archived from the original on 2012-01-18. 
  11. "East African trade bloc approves monetary union deal", Reuters, 30 November 2013. Retrieved on 2015-01-23. Archived from the original on 2015-09-24. 
  12. From Co-operation to Community (eac.int)
  13. EAC Update E-newsletter. www.eac.int. Directorate of Corporate Communications and Public Affairs. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-04-26. Iliwekwa mnamo 10 December 2011.
  14. https://www.eac.int/press-releases/2288-eac-council-of-ministers-green-light-report-on-drc-verification-mission-for-consideration-by-eac-heads-of-state
  15. allAfrica.com: Tanzania: Fast-Tracking Political Federation
  16. EAC federation fears justified? Tanzania's Daily News On Saturday; 5 Mei 2007
  17. Kenya: Tears for Mt Elgon as Schools Re-Open
  18. Sabiny Demand Land as Karamajong Raid Reduce
  19. AlertNet Archived 20 Juni 2010 at the Wayback Machine. Kenya land clashes kill 60, displace thousands
  20. 20.0 20.1 20.2 20.3 EAC News .... Jalada kutoka ya awali juu ya 2004-12-21. Iliwekwa mnamo 2004-12-21.
  21. 21.0 21.1 21.2 Travelling in East Africa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2004-07-01. Iliwekwa mnamo 2004-07-01.
  22. 22.0 22.1 Report for Selected Countries and Subjects.
  23. 23.0 23.1 Report for Selected Countries and Subjects.

Viungo vya nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu: