Rangi za Umoja wa Kiafrika

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Rangi za Pan-African)
Aina mbili za rangi za Umoja wa Kiafrika (pan-African).

Kuna aina mbii za bendera zinazotumiwa kuonyesha Umoja wa Kiafrika au umoja wa watu wenye asili ya Afrika. Zote mbili ni tofauti na bendera rasmi ya Umoja wa Afrika, ambao ni maungano ya nchi 55 za Afrika na kutumia kijani pekee.

Aina moja inafuata mfano wa bendera ya Ethiopia iliyokuwa nchi pekee barani Afrika iliyoweza kujitetea dhidi ya uenezaji wa ukoloni kwa ushindi wa kijeshi dhidi ya Italia.

Aina nyingine ina asili katika harakati ya watoto na wajukuu wa watumwa kutoka Afrika huko Amerika ikaundwa na Marcus Garvey.

Kijani - Njano - Nyekundu kwa kufuata mfano wa Ethiopia[hariri | hariri chanzo]

Bendera ya Ethiopia yenye rangi tatu za kijani, njano na nyekundu.

Rangi tatu za kijani, njano na nyekundu huitwa rangi za umoja wa Afrika kwa sababu zinapatikana kwenye bendera ya Ethiopia, nchi pekee ya Afrika iliyofaulu kujitetea dhidi ya uvamizi wa kikoloni katika karne ya 19 BK.

Tangu kuenea kwa uhuru kwenye nchi za Afrika katika miaka ya 1950 na 1960 kuna nchi mbalimbali zilizochagua rangi zilezile kwa kuonyesha upendeleo wao kwa umoja wa Afrika. Ghana ilikuwa nchi ya kwanza ya kutoka katika ukoloni mwaka 1957 ikateua rangi za Ethiopia kwa bendera yake.

Bendera za nchi zifuatazo hutumia rangi za Ethiopia ama pekee au pamoja na rangi nyingine, ambayo mara nyingi ni nyeusi kama alama ya watu weusi.

Bendera za nchi kadhaa za Amerika zinatumia rangi zilezile kwa sababu wakazi wao ni watoto wa watumwa kutoka Afrika.

Nchi za Afrika zinazotumia rangi za Ethiopia[hariri | hariri chanzo]

Nchi za Amerika Kusini na Visiwa vya Karibi zinazotumia rangi za Ethiopia[hariri | hariri chanzo]

Nyekundu - Nyeusi - Kijani kwa kufuata mapokeo ya Marcus Garvey[hariri | hariri chanzo]

Bendera ya Umoja wa Kiafrika au Nguvu ya Watu Weusi iliyoundwa na Marcus Garvey.

Kuna seti nyingine ya rangi iliyoundwa kwa nia hiyohiyo lakini asili yake iko zaidi Amerika ambako imekuwa bendera ya watu wanaopigania haki za watu weusi ambao ni wajukuu wa watumwa wa zamani na umoja nao na Afrika. Hii bendera inatumia rangi nyekundu, nyeusi na kijani.

Hii ilikuwa bendera ua UNIA (Universal Negro Improvement Association and African Communities League) nchini Marekani. Ilipendekezwa na Marcus Garvey aliyeeleza mwaka 1921 "nyekundu ionyeshe urafiki na "wekundu kote duniani" (Wasoshalisti waliotumia bendera nyekundu walikuwa chama cha kupinga ubaguzi wa rangi), kijani ionyeshe urafiki wa watu wa Eire (wakati ule Waeire (wa Ireland) walipigania uhuru kutoka Uingereza wakitumia bendera ya kijani) na nyeusi kwa watu weusi"[1].

Baadaye rangi hizo zilielezwa hivi[2]:

  • nyekundu: damu inayounganisha watu wote wenye asili ya Afrika
  • nyeusi: watu weusi wanaotazamiwa kama taifa moja hata kama hawana dola la pamoja
  • kijani: utajiri asilia wa Afrika

Bendera zinazotumia rangi za pande zote mbili[hariri | hariri chanzo]

Bendera za nchi nyingine za Afrika na Visiwa vya Karibi zinachanganya sehemu ya rangi kutoka kila upande kwa mfano:

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. The Marcus Garvey and Universal Negro Improvement Association Papers, Vol. 2, p. 603.
  2. History of the Flag, History Red - Black - Green Archived 31 Oktoba 2019 at the Wayback Machine., tovuti ya The Universal Negro Improvement Association, iliangaliwa Oktoba 2019

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]