Muungano wa Afrika

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Pan-Africanism)

Muungano wa Afrika (kwa Kiingereza: "Pan-Africanism") ni jina la harakati iliyolenga kuunganisha watu wote duniani walio Waafrika au wenye asili ya Afrika. Hao ni pamoja na wakazi wa Afrika yenyewe na watu wenye asili ya Kiafrika katika nchi za Amerika na sehemu nyingine ambao mababu wao walipelekwa huko wamefungwa wakiuzwa katika biashara ya watumwa.

Mara nyingine yalihesabiwa humo hata maslahi ya watu wa rangi nyeusi ambao ni wakazi asilia wa Melanesia ya Pasifiki.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Harakati hiyo ilianza kama harakati ya kiutamaduni ikaendelea kuwa harakati ya kisiasa iliyotaka kuunganisha nchi huru za Afrika baada ya mwisho wa ukoloni kwa lengo la kutengeneza nchi moja yenye serikali moja.

Wazo hilo lilianza kipindi cha mapambano ya kupigania haki za Waafrika katika dunia nzima, mapambano haya yaliungwa mkono na wanaharakati kama vile Marcus Garvey, William E. B. Du Bois ambao waliishi Marekani na Kwame Nkrumah wa Ghana na Julius Nyerere wa Tanzania.

Harakati zao zilianzia nje ya Afrika kwa kuwapigania Waafrika walioteswa kama watumwa hasa Marekani, zikaenea hadi Afrika ambapo mkutano wa kwanza ulifanyikia Ghana katika mji mkuu wake Accra. Mara tu baada ya Ghana kupata uhuru mwaka 1957, mwaka 1958 rais wa Ghana Kwame Nkrumah alitoa wazo la kuunda umoja wa Afrika.

Baada ya mazungumzo marefu wazo hilo lilikubaliwa na viongozi wa nchi huru za Afrika akiwemo MwalimuJulius Kambarage Nyerere wa Tanzania. Hivyo basi umoja wa Afrika OAU ambao sasa unaitwa AU uliundwa mwaka 1963 nchini Ethiopia iliyokuwa nchi ya pekee ya Afrika ambayo ilifaulu kujitetea dhidi ya uenezaji wa ukoloni katika karne ya 19. Addis Ababa ndipo makao makuu yake. Nyerere na Nkrumah walifikiri zaidi ni kwa vipi bara la Afrika lingeungana.

Msimamo wa Nyerere[hariri | hariri chanzo]

Nyerere na mwenzake Brazaville na kikundi cha Monrovia walitaka hatua hizo za kutengeneza nchi moja ya Afrika zisiharakishwe. Nyerere alitoa mawazo ambayo kwake yeye aliona yasingeruhusu muungano wa haraka kama alivyotaka Nkrumah.

Alisema kila nchi inayo haki ya kutengeneza uchumi na siasa yake ili kuifanya nchi hiyo kutambulika, lugha na tamaduni zake pia zingestahili kutambulisha nchi hizo. Hivyo basi alisema ni vigumu kuwaunganisha watu wenye tamaduni tofauti, lazima kwanza tofauti hizo za kitamaduni ziondolewe, kitu ambacho kilihitaji muda zaidi.

Pia alisema matatizo mbalimbali yanayozikumba nchi za Afrika, yakiwemo umaskini, vita vya wenyewe kwa wenyewe, ujinga na magonjwa mbalimali, pia njia tofautitofauti za utawala wa viongozi vingekuwa vikwazo kikubwa cha kuunda umoja huo.

Nyerere alitoa wazo la kuunda mashirika mbalimbali yanayoziunganisha nchi za Afrika kwanza kama hatua mojawapo ya kuelekea kuunda Afrika moja, hivyo mashirika kama vile SADC, ECOWAS, COMESA, EAC na kadhalika yaliundwa.

Msimamo wa Nkrumah[hariri | hariri chanzo]

Naye Nkrumah alikuwa na mawazo kadha wa kadha ambayo kwa kiasi fulani yalitofautiana na yale ya Nyerere kama vile: Nkrumah na wenzake kutoka nchi za Mali, Nigeria na Guinea walitaka kuharakishwa kwa umoja huo, vinginevyo waliona kuwa ni kupoteza muda.

Nkrumah alisema haya kwa vigezo vifuatavyo: Kuundwa kwa umoja wa Afrika hakuwezi kuzifanya nchi zikose uhuru bali itasaidia kuleta muungano baina ya Waafrika wenyewe. Pia aliendelea kusema tatizo la tamaduni tofauti halikustahili kukwamisha harakati za kuunda umoja wa Afrika kwani kuendelea kuchelewa kungetoa nafasi kwa wakoloni kurudi kuitawala Afrika kwa urahisi, hivyo umoja ulikuwa njia pekee ya kuwazuia wakoloni kutawala tena na hayo matatizo mengine mengi yangeendelea kutatuliwa huku umoja ukiwa umeshaundwa.

Nkrumah pia alisema muungano wa Afrika ungesababisha kujenga nchi huru na imara yenye kusimamia maamuzi yake kuhusu uzalishaji katika kilimo na bei katika soko la dunia ambayo ilimilikiwa na kupangwa na mabepari.

Kwa kuangalia na kutathmini mawazo hayo, viongozi hao walionekana kuwa chumvi ya Afrika kwa msaada wao katitika kujenga na kuleta uhuru miongoni mwa nchi za Afrika

Kwa kuhitimisha, viongozi hao, Nkrumah, Nyerere na wengineo kama vile Jomo Kenyatta wa Kenya, Kamuzu Banda wa Malawi na Nelson Mandela wa Afrika Kusini ni miongoni mwa viongozi wa Afrika wanaostahili kukumbukwa kwa mchango wao mkubwa katika kupigania uhuru wa Afrika.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]