Nenda kwa yaliyomo

Mkoa wa Tanga

Mkoa wa Tanga
Mahali paMkoa wa Tanga
Mahali paMkoa wa Tanga
Mahali pa Mkoa wa Tanga katika Tanzania
Majiranukta: 5°0′S 38°15′E / 5.000°S 38.250°E / -5.000; 38.250
Nchi Tanzania
Wilaya 6
Mji mkuu Tanga
Serikali
 - Mkuu wa Mkoa Martin Shigela
Eneo
 - Jumla 27,348 km²
Idadi ya wakazi (2022)
 - Wakazi kwa ujumla 2,615,597
Tovuti:  http://www.tanga.go.tz/
Tanga.
Milima ya Usambara Magharibi.

Mkoa wa Tanga ni mojawapo ya mikoa 31 ya Tanzania uliopo kaskazini-mashariki mwa nchi, ukiwa na makao makuu katika jiji la Tanga. Mkoa una eneo la km² 27,348 ambalo linaunganisha sehemu za pwani pamoja na milima. Unapakana na Mkoa wa Kilimanjaro upande wa kaskazini-magharibi, Mkoa wa Manyara upande wa magharibi, Mkoa wa Morogoro kusini-magharibi, na Mkoa wa Pwani upande wa kusini. Kwa upande wa mashariki, mkoa huu unapakana na Bahari ya Hindi, jambo linaloufanya kuwa na fursa nyingi za kiuchumi kupitia bandari, uvuvi, na utalii wa fukwe. Tanga ni miongoni mwa mikoa ya zamani zaidi nchini, ikiwa na historia tajiri ya biashara ya pwani na urithi wa Kiswahili. Uchumi wa mkoa unategemea kilimo cha mazao kama mkonge, biashara, na utalii unaotokana na vivutio kama Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, na Milima ya Usambara. Mwaka 2022 wakazi waliohesabiwa katika sensa walikuwa 2,615,597 [1] kutoka 2,045,205 wa mwaka 2012[2]. 5°18′15″S 38°19′3″E / 5.30417°S 38.31750°E / -5.30417; 38.31750

Eneo la mkoa

[hariri | hariri chanzo]

Tanga ni kati ya mikoa midogo ya Tanzania ikiwa na msongamano mkubwa wa wakazi ndani ya eneo lake, hasa wilaya ya Lushoto kwenye ardhi yenye rutuba nzuri.

Eneo linalofaa kwa kilimo ni km² 17,000.

Kuna wilaya 11 ambazo ni Bumbuli, Handeni Vijijini, Handeni Mjini, Kilindi, Korogwe Vijijini, Korogwe Mjini, Lushoto, Mkinga, Muheza, Pangani na Tanga Mjini.

Hali ya hewa

[hariri | hariri chanzo]

Kwa jumla hali ya hewa ni joto lenye unyevu. Handeni kuna joto kavu zaidi. Milima ya Usambara hakuna joto sana.

Miezi ya Desemba - Machi halijoto huko Tanga inafikia sentigredi 30-32 mchana na 26-29 usiku. Wakati wa Mei hadi Oktoba halijota inapoa: ni sentigredi 23-28 mchana na 20-24 usiku. Unyevu iko juu kati ya asilimia 100 na asilimia 65.

Maeneo mengi ya mkoa hupokea angalau milimita 750 za mvua kwa mwaka au zaidi. Pwani ni zaidi: takriban milimita 1,100 hadi 1,400 ikipungua sehemu za ndani isipokuwa milima ya Usambara ambako mvua inaweza kuzidi milimita 2000 kwa mwaka.

Makabila makubwa mkoani Tanga ni Wasambaa, Wazigua, Wabondei na Wadigo. Mengine ni Wapare, Wataita, Wambugu, Wasegeju na Wanago. Pia kuna Waarabu wengiwengi wenye asili ya Oman.

Wasambaa ndio kabila kubwa lililoko katika milima ya Usambara, Muheza, Korogwe na Lushoto. Kwa jumla ndio asilimia 40 ya wakazi wote wa mkoa.

Wazigua ni kabila kubwa huko Handeni na sehemu za Korogwe na Pangani. Wabondei wako hasa Muheza na sehemu za Pangani. Wadigo ndio wengi Tanga yenyewe na sehemu za pwani.

Katika mkoa huu elimu inahitaji kuboreshwa zaidi, hasa maeneo ya vijijini, maana watu wengi wa mkoa huu hufanya shughuli zao za kimila na kushindwa kuendelea na zile za maendeleo katika taifa la Tanzania.

Mkulima akionyesha pilipili mtama kutoka kwenye shamba lake, Magoroto - Tanga.

Wakazi wengi hutegemea kilimo cha riziki pamoja na ufugaji na uvuvi.

Mazao ya chakula hasa ni mahindi, muhogo, ndizi, maharagwe na mpunga.

Tanga ilikuwa na viwanda vingi kiasi katika miaka ya 1960 na 1970 lakini karibu vyote vimekwama kutokana na siasa ya Ujamaa na uchumi wake ulioiga mfumo wa nchi za kisoshalisti. Viwanda vichache vilivyobaki havizalishi mali kulingana na uwezo wao. Kilichobaki hasa ni kiwanda cha saruji Tanga.

Utalii umeanza kupanuka kidogo, hasa katika eneo la Pangani, Mapango ya Amboni na kituo cha Makumbusho Urithi Tanga.

Wilaya ya Handeni kuna machimbo ya madini.

Majimbo ya bunge

[hariri | hariri chanzo]

Wakati wa uchaguzi mkuu wa Tanzania mwaka 2015 mkoa huu ulikuwa na majimbo ya uchaguzi yafuatayo:

Tazama pia

[hariri | hariri chanzo]
  1. "Nakala iliyohifadhiwa". Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2022-11-07. Iliwekwa mnamo 2022-11-15.
  2. "Population Distribution by Administrative Units, United Republic of Tanzania, 2013" (PDF). National Bureau of Statistics, Ministry of Finance, Dar es Salaam and Office of Chief Government Statistician, President’s Office, Zanzibar. Machi 2013. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo (PDF) mnamo Juni 12, 2013. Iliwekwa mnamo 2017-08-22.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)

Viungo vya nje

[hariri | hariri chanzo]


Makala hii kuhusu maeneo ya Mkoa wa Tanga bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Mkoa wa Tanga kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.
Tafadhali usiingize majina ya maafisa au viongozi wa sasa maana wanabadilika mno.