Waha

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Wajiji)
Waha katika ramani

Waha ni kabila kubwa [1][2] la watu wa Tanzania wanaoishi katika Mkoa wa Kigoma hadi mpakani kwa Burundi.

Lugha yao ni Kiha, jamii ya Kirundi, Kinyarwanda na Kihangaza katika kundi la lugha za Kibantu.

Katika kipindi cha kuhamahama kwa ajili ya kutafuta masilahi kama vile chakula na kukimbia vita, wazazi wa kabila hilo, baada ya kufika kando ya ziwa Tanganyika na maeneo yote yanayolizunguka Ziwa Tanganyika waliweza kukaa na kuanzisha shughuli mbalimbali kama vile kilimo, uvuvi, ufugaji na uwindaji.

Waha walipoanza kuyazoea mazingira, walijigamba na kujidai kwa makundi ya kikoo kuwa yana nguvu, kila mmoja kwa nafasi yake. Kila ukoo ulijigamba kwa kutumia majina ya wanyama, wadudu, ndege, milima n.k.

Waha wanagawanyika kati ya Wahambwe (Waha wa Kibondo), Wayungu (Waha wa Kakonko), Washingo (Waha wa Heru Bushingo) na Wanyaheru (Waha wa Heru Juu) mbali na Wamanyema (ambao si Waha, wana asili ya Kongo). Hao wote, pamoja na kuwa wavuvi na wachuuzi, ni wakulima wa mazao mbalimbali kama vile mahindi, maharage, mtama, karanga, viazi, mihogo n.k.

Waha pia ni wavuvi wa samaki katika ziwa Tanganyika, mto Malagarasi, Mto Rwiche, Mto Mkoza, na mito mingine midogomidogo kama vile, Nyajijima, Mresi, Kazingu, n.k.

Waha ni wafugaji wa ng'ombe, mbuzi, kuku, bata, nguruwe, sungura, mbwa, paka, n.k.

Biashara zao ni mazao wanayoyalima, samaki, na bidhaa nyingine za kawaida.

Usafiri wao wa asili ulikuwa wa miguu yao wenyewe, ambapo kuna imani ilikuwepo pia ya kusadikika kuwa walitumia ungo kusafiria kama ndege yao ya asili.

Utamaduni wao, yaani mavazi yao ilikuwa ni magome ya miti yaliyojulikana kama impuzu, na nyumba zao za msonge, udongo na miti, kulingana na sehemu mbalimbali, maana kuna sehemu zenye joto kama vile bondeni, na sehemu zenye baridi kama vile nyanda za juu. Kwa sasa wanatumia zaidi kitenge.

Historia ya jina

Historia ya Waha ilianzia katika kijiji kiitwacho Buha kilichopo Heru: hapo ndipo Waha walipofikia baada ya kutoka maeneo ya Burundi, Rwanda na Kongo.

Inafahamika kuwa Waha ni moja ya makabila kutoka Wabantu wa mashariki. Wabantu hao walipata kufika maeneo hayo hata kabla ya miaka ya 600 yaani kabla ya Wamanyema. Wamanyema na Waha ndio wenyeji wa Kigoma. Uenyeji huu tunaouzungumza ni miaka ya zamani sana: hata kabla ya kuanza kwa ukoloni hawa watu tayari walikuwa wakiishi pamoja na walikuwa wakipendana na kuthaminiana. Kuna vitu Waha waliwafundisha Wamanyema na pia kuna vitu Wamanyema waliwafundisha Waha na wote hawa waliipigania Tanganyika kutoka mikononi mwa serikali ya kikoloni. Hata mradi wa kuligawa bara la Afrika kati ya nchi kadhaa za Ulaya ulikuwa bado kabisa Wamanyema na Waha walikuwa wakiishi pamoja.

Ifahamike kuwa asilimia kubwa ya makabila mengi yaliyopo hapa Afrika yalipata majina kulingana na wageni walivyoelewa au walivyoona. Kuna makabila yaliyopata majina kutokana na namna wanavyopigana, yapo makabila yaliyopata majina namna wanavyopiga makelele na wengine walipewa majina kulingana na lugha yao au matamshi yao. Kwa upande wa kabila la Waha, ambao wanapatikana katika mkoa wa Kigoma, ukweli ni kwamba kabila hili ni miongoni mwa makabila ambayo yana historia kubwa sana tangu walipofika katika ardhi hiyo na pia ni kabila lenye umaarufu mkubwa nchini.

Kipindi watu hawa wanafika maeneo ya Afrika Mashariki hawakujulikana kama kabila la Ha na hawakuja wakiwa kundi moja. Bali walikuja kwa mtindo wa koo na kila ukoo ulikuwa na jina lake.

Koo zilizokuwa hapo zilipata kumiliki ardhi. cha msingi ni kwamba watu hao walifanikiwa kuitwa majina ya maeneo waliyokaa kutokana na mazingira yake. Kwa mfano kuna ukoo uliokaa sehemu zenye udongo (Bayungu) walijiita Wayungu na wale waliokaa sehemu za mwinuko (Heru) walijiita Wanyaheru. Lakini mpaka kufikia miaka ya 1800, koo hizo ziliungana na kuishi sehemu na kutawaliwa na chifu mmoja. Ndipo watu hao walipoanza kupata jina moja lililowatambulisha kwa wageni.

Sasa kwa nini watu hao waliitwa Waha? Hii ndiyo mitazamo iliyosimulia asili ya neno Waha au Ha.

1. Wapo waliodai kuwa asili ya neno Waha au Ha ni pale wageni walipofika katika ardhi ya Kigoma na kuwauliza watu hao kuwa “ninyi ni wakina nani” na ndipo watu hao walipojibu “tur; Abhaha” wakimaanisha "sisi ni wazaliwa wa hapa hapa". Hapo wageni hao walikariri kuwa Waha kwa kuchukua neno “ha”,,, Kiuhalisia Waha na Wamanyema ni watu wamoja: tangu enzi na enzi walipendana na kuthaminiana.

2. Wapo wanaodai kuwa wageni walipokuja na kukuta ufalme wa Buha umekua na ulikuwa na watu wengi, walimuuliza mfalme wao kuwa “hawa ni wakina nani”, na ndipo mfalme wa Buha alipojibu kuwa, “N’abhaha” akimaanisha kuwa “hawa ni wenyeji wa hapahapa” na hapo wageni hao walipata neno “Ha” na walipoandika waliaandika hivyo.

Maelezo hayo yalitolewa na watu waliokuwa wamekutwa katika ardhi ya Buha. Kwa upande mwingine, historia inafafanua kuwa, Watusi walikuwa watawala wa kabila la Waha na kuna mahusiano makubwa sana kati ya Watusi na Waha. Hivyo hata neno Waha bado lilionekana kuhusiana na Watusi.

Kwa Watusi neno Abaha lina maana ya mtu yeyote “anaowapa ardhi” na kwa Watusi aliyekuwa akitoa ardhi alifahamika kwa jina la Mtoke. Na mteko alikuwa akitoa ardhi kwa Watusi, walifahamika kwa jina moja la Uwaha.

Waliolima shamba moja na Mteko walijiita “Abhaha”, hata kuna baadhi ya Watusi hujiita “Waha” na ndiyo maana hata walivyotawala walijiita hivyo.

Tanbihi

Marejeo

  • J.H. Scherer, Marriage and Bride-Wealth in the Highlands of Buha (Tanganyika). Diss. Utrecht University, 1965.

Viungo vya nje