Wahangaza

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Wahangaza ni kabila la watu wa Tanzania wanaoishi katika Mkoa wa Kagera, hasa kwenye wilaya za Ngara na Biharamulo. Nje na wilaya hizo wanaishi pia sehemu za Kigoma na Karagwe.

Lugha yao ni Kihangaza.

Kwa sehemu kubwa Wahangaza ni wafugaji na wakulima. Hapo mwanzo chakula chao kikuu kilikuwa ni ndizi kwa maharage, lakini hivi sasa wamejifunza kula vyakula vya makabila mengine pia kama vile ugali.

Wahangaza ni kabila la watu wakarimu sana, wenye upendo na roho za kujali wageni. Wana utamaduni sawia na makabila mengi ya nchini Tanzania yenye kujumuisha mila na desturi zinazoelekeana. Haya yanadhihirika katika sherehe za ndoa, kuzaliwa watoto, vifo, matambiko, mavuno na hata kusimikwa kwa viongozi.

Sherehe hizo hufanyika kila tukio hili linapojitokeza na muktadha wa tukio husika likafanyika na kundi fulani kama vile ukoo na pengine kundi la watu fulani wanaofanya kazi fulani maalum kama tiba, ufinyanzi, kilimo ama ufugaji.

Historia ya jina[hariri | hariri chanzo]

Historia ya jina "Hangaza" kwa mujibu wa historia ya mababu wao linatokana na neno la Kirundi/Kinyarwanda la "Hangaaza neza ulibe yo bali" yaani "angalia kwa makini uone walipo". Historia ya maneno haya yalitoka kipindi cha vita kati ya dola la Bugufi na madola ya Urundi na Uruanda.

Kwa mujibu wa simulizi za mababu hao ni kwamba hapo zamani kulikuwa na watemi wawili wa nchi mbili tofauti yaani Burundi na Rwanda kwa sasa; watemi hao walikuwa mtemi Mwambutsa wa Burundi na mtemi Kigeri wa Rwanda ambao waliamua kuunganisha nguvu ili kuvamia dola la Bugufi. Watemi hao wawili walikuja kupigana na mtemi Kinyamazinge wa Ngara, watu wa Ngara walibuni vita Vya kupigania mpakani (boarder defensive) ambapo walishinda mchana kutwa wakikata miti na usiku ambao ndio ulikuwa muda wa vita walikoka moto mkubwa. Sasa wale Warundi na Wanyarwanda walipokuja kupigana vita vya ana kwa ana (full force attack) walishangaa kuona moto mkubwa ukiwaka wakati muda huo wapiganaji wa Ngara wakiwatazama vizuri na kuwapiga mishale kwa urahisi sababu ya mwanga wa moto. Ndipo neno "Hangaaza" lilipozaliwa likiwa na maana ya tazama kwa umakini kwa lugha ya Kiswahili.

Neno hilo lilianzia pale maana Warundi na Wanyarwanda hawakuweza kuwaona vizuri maadui maana walikuwa kando kidogo na moto huo hivyo wakawa wanaambizana "hangaaza neza ulibe yo bali" yaani "angalia kwa makini uone walipo". Na pia kipindi hicho lilitumika zaidi kumaanisha mwanga wa vita kuanzia hapo watu wa Burundi na Rwanda, baada ya kushindwa vita hivyo, ndipo walipoanza kuwaita Wahangaza (yaani walioweza kuona), na ndipo ulipoanzia msemo wa kilugha unaosema "Utazi umhangaza amuhanga amaso".

Toka hapo jina "Hangaza" lilianza kutumika kuwatambulisha kabila lao.

Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wahangaza kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.