Wakinga

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mwanamke na Mwanaume wa Kikinga

Wakinga ni kabila la watu wa Tanzania wanaoishi hasa katika Mkoa wa Njombe, Wilaya ya Makete.

Makabila makubwa ya wenyeji mkoani Njombe ni Wabena, Wakinga na Wapangwa, na uwiano wao ni 37:11:3.

Kabila la Wabena liko wilaya ya Njombe na eneo la Malangali likiwa linapakana na wilaya ya Ulanga na wilaya ya Kilombero (Mkoa wa Morogoro), Wakinga wako wilaya ya Makete na Wapangwa wako eneo la Malangali.

Yapo pia makabila madogo kama vile Wamahanji, Wakisi, Wamanda, Wamagoma n.k. ambao kwa ujumla wao wanachukua asilimia 6 iliyosalia ya watu Mkoani Njombe.

Lugha ya Wakinga inaitwa Kikinga. Asili ya lugha hii ina mkanganyo kidogo: baadhi ya taarifa zinaeleza kuwa asili ya lugha hii ni misitu ya Kongo [1], huku taarifa nyingine zinaeleza kuwa asili ya jamii ya Wakinga ni Afrika Kusini na kwa waliingia Ukinga kwa kutokea mkoa wa Ruvuma.

Jamii ya Wakinga ina koo mbalimbali, kwanza ukoo wa Sanga, ambao ndio ukoo mkubwa na ndio uliokuwa unatawala jamii yote ya Wakinga. Koo nyingine ni pamoja na ukoo wa Kyando, Mahenge, Chaula, Tweve, Luvanda, Pila, Lwila, Ndelwa, Mlelwa, Mbilinyi, Msigwa na Mbwilo. Hizi ni baadhi tu ya koo za jamii ya Wakinga. [2]

Maendeleo[hariri | hariri chanzo]

Kwenye maendeleo Wabena na Wakinga ni wachapa kazi sana. Tanzania nzima mkoloni aligundua makabila matatu ndio wachapa kazi za mikono na wenye kujituma na waaminifu kazini kuliko makabila yote. Makabila hayo ni:

1. Wabena toka Njombe 2. Wakinga toka Makete 3. Waha toka Kigoma[3]

Wilaya ya Makete inategemea barabara mbili kuu ya kutoka Njombe na nyingine kutoka Mbeya, kipindi hiki moja ya kutoka Njombe inapitika, lakini barabara pacha zinazoingia mkoani Mbeya zimeharibika na haipitiki.

Ubovu wa barabara hizo umechangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha usafirishaji wa pembejeo na hivyo hazifiki kwa wakati. Lakini pia umechangia kushindwa usafirishaji mazao kama matunda, viazi, pareto, mazao ya mbao, ngano, mahindi na mengine kwenda sokoni.

Barabara wilayani humo kama katika wilaya nyingine kama zinapitika, zinachangia kukuza uchumi wa wilaya hiyo, lakini zinazopokuwa mbovu zinachangia kupunguza kasi ya kukua kwa uchumi, pato la wananchi na maendeleo wilaya hiyo.

Ubovu wa barabara wilayani humo umepandisha bei ya bidhaa za madukani ambazo zinaingizwa wilayani humo kupitia Mbeya na Njombe. Bei ya bidhaa nyingi ni za kuruka, hasa katika maeneo ambayo barabara zimeharibika.

Kutokana na ubovu wa barabara hizo, wananchi wa maeneo ya Bulongwa wanabeba matunda, ngano na bidhaa nyingine kwa kichwa umbali mrefu kwenda kuuza mkoani Mbeya ambako soko linapatikana.

Adha za ubovu wa barabara zimewakumba pia wakazi wa Ipepele, Iniho na Matamba wilayani humo, wamekuwa wakibeba viazi, mbao na mahindi vichwani umbali mrefu kwenda kufikisha kwenye maeneo ambako barabara zinafikika.[4]

Kutokana na ubovu wa barabara, mazao mengi ya wilaya ya Makete, yakiwamo ya mbao. yamekuwa yakikwama kusafirishwa na hivyo kukwamisha ukuaji wa uchumi wilayani na hivyo kuwakosesha wananchi kipato, ajira na mahitaji ya kila siku.

Pareto imekuwa ikisuasua kusafirishwa, hata kama hivi karibuni imefufuliwa baada ya miaka takribani kumi kufifia na wakulima kukata tamaa kutokana na soko la dunia la bidhaa hiyo kuanguka mwanguko wa mende.

Kufufuliwa kwa soko la zao hilo na kuanzishwa kwa malipo ya papo kwa hapo, kumechangia kuamsha ari ya wananchi kulima kwa wingi zao hilo, hata kama ubovu wa barabara unalazimisha baadhi ya mazao kuozea nyumbani.

Mahindi, ngano, shayiri na matunda ambayo yanalimwa kwa wingi Bulongwa na Matamba, yanaozea mitini. Watu wachache wenye uwezo wanabeba kichwani umbali mrefu kwenda kuuza. Wenyeji pia wana zao la miti ya ulanzi.[5]

Wakinga, ni wafanyabiashara maarufu katika mikoa mbalimbali nchini, hasa Mbeya, Iringa, Dar es Salaam, Ruvuma, Rukwa na maeneo mengine. Lakini, wamekuwa wakishindwa kuwekeza wilayani kwao kutokana na barabara nyingi kuwa mbovu na kutopitika wakati wote.

Barabara ni chanzo cha maendeleo: zikijengwa kwa lami, zitasaidia kuongeza haraka pato la wananchi, kukuza uchumi wa nchi na kuondoa umaskini.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. [1]
  2. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2024-01-13. Iliwekwa mnamo 2024-01-13.
  3. [2]
  4. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2018-07-09. Iliwekwa mnamo 2008-07-22.
  5. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-06-24. Iliwekwa mnamo 2008-07-22.
Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wakinga kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.