Sudan

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Sudani)
Sudan


Ramani ya Sudan ikionyesha majimbo yake

Sudan (jina rasmi: Jamhuri ya Sudan) ni nchi ya tatu kwa ukubwa katika bara la Afrika na ya kumi na sita duniani

Imepakana na Misri kaskazini, Bahari ya Shamu kaskazini-mashariki, Eritrea na Ethiopia mashariki, Sudan Kusini kusini-mashariki, Afrika ya Kati na Chadi magharibi, na Libya kaskazini-magharibi.

Kijiografia nchi hii huhesabiwa kama sehemu ya Afrika ya Kaskazini.

Mji mkuu ni Khartoum.

Majimbo ya Sudan Kusini yalikuwa sehemu ya nchi hiyo lakini yalipiga kura ya kujitenga yakapata kuwa nchi huru kuanzia tarehe 9 Julai 2011.

Aliyekuwa makamu wa Rais John Garang, ambaye awali aliongoza wanamgambo wa Sudan Kusini kupigania uhuru wa majimbo ya kusini.

Jiografia

Ona pia: Orodha ya mito ya Sudan, Orodha ya miji Sudan

Mlima wa Dair eneo ya kati, Sudan
Bwawa kusini mwa Sudan

Sudan iko upande wa Afrika ya kaskazini, ina pwani kwenye bahari ya Shamu kati ya Misri na Eritrea. Imetamalikiwa zaidi na mto Nile na mikono yake.

Ina eneo la kilomita mraba 1,886,068 (sq mi 728,215).

Ardhi yenyewe ni kiwara, lakini kuna milima upande wa mashariki na magharibi.

Hali ya anga ni ya mwangaza kusini, na mikuranga kaskazini.

Mvua yapatikana miezi ya Aprili na Oktoba.

Uharibifu wa mazingira hasa ni kwa sababu ya mmomonyoko wa udongo na utapakazi wa jangwa.

Majimbo

Nchi imegawiwa katika wilaya 18, zilizogawiwa tena katika kata 133.

Historia

Makala kuu: Historia ya Sudan
Sanamu ya Mfalme wa Wanubi, Sudan
Muhammad al-Mahdi
Dola la Mahdi 1881-1898

Historia ya awali

Nchi ilikuwa na makazi ya kudumu kuanzia milenia ya 8 KK.

Katika milenia ya 5 KK watu walizidi kuhama Sahara ikigeuka jangwa wakasogea katika eneo la Sudan ya sasa (bonde la mto Nile).

Mchanganyiko wa watu hao uliunda ufalme wa Kush kwenye 1700 KK. Makao makuu yalikuwa Kerma.

Katika karne ya 8 KK watu wa ufalme huo waliteka Misri na kuitawala kwa karne moja hadi waliposhindwa na Waashuru.

Baadaye makao makuu yalikuwa Meroe, ambapo ufalme uliendelea hadi karne ya 4 BK ukiwa maarufu kwa uhunzi kwa jina la Ethiopia.

Ufalme kusambaratika

Ufalme huo uliposambaratika, zilitokea falme mbalimbali katika eneo lake, mmojawapo ukiwa ule wa Nubia.

Huko Ukristo ulienea katika madhehebu tofauti: yale ya Kikopti kutoka Misri na yale ya Kibizanti kutoka Roma ya mashariki.

Baadaye Uislamu pia ulijitokeza katika falme hizo ukazidi kuenea hadi kuanzisha usultani wa Sennar.

Mwaka 1821 mtawala wa Misri chini ya himaya ya Waturuki aliteka Sudan kaskazini.

Katika miaka ya 1870 juhudi za Wazungu za kukomesha biashara ya utumwa zilisababisha kutokea kwa Mahdi.

Dola la Mahdi

Dola la Mahdi (kwa Kiarabu المهدية, "mahdiyya") lilianzishwa na Muhammad Ahmad Al-Mahdi mwaka 1881 alipojitangaza kuwa mahdi kufuatana na imani ya Kiislamu akaongoza uasi dhidi ya Misri iliyotawala Sudan ikisimamiwa yenyewe na Uingereza.

Muhammad Ahmad Al-Mahdi alifaulu kukusanya wafuasi wengi na kushinda Wamisri. Tarehe 26 Januari 1885 jeshi lake lilitwaa mji mkuu Khartum na kumwua gavana Gordon Pasha.

Al-Mahdi alianzisha mji mkuu mpya ng'ambo ya mto Nile kwa kuunda Omdurman. Wamisri na Waingereza wakatoka nje ya Sudan.

Baada ya ushindi wake Al-Mahdi alikufa na homa ya matumbo.

Ugomvi ulitokea kati ya makamu wake hadi 1891 wakati Abdallahi ibn Muhammad mwenye sifa ya kuwa aliongoza jeshi la mahdi wakati wa mashambulio dhidi ya Khartum alikubaliwa wa viongozi wa mahdiyya akajiita "khalifa".

Khalifa Abdullahi aliimarisha utawala wake wa kuwaua wapinzani bila neema, kati yao wanafunzi na ndugu za mahdi mwenyewe. Akajenga jumba mjini Omdurman linalosimama hadi leo.

Khalifa Abdullahi alijaribu kutumia teknolojia mbalimbali. Akanunua meli za mvuke za mtoni alizoziona Waingereza walizitumia pia akajenga kiwanda cha kutengenezea bunduki. Akaanzisha nyaya za mawasilaino kwa simu. Lakini kwa ujumla vita na utawala wa mahdiyya zilikuwa ziliharubu uchumi iliyoendelea kuzorota.

Khalifa alifaulu kupanua utawala wake juu ya maeneo karibu yote ya Sudan ya leo lakini alishindwa kufikia jimbo la Ikweta ambako Emin Pasha aliendelea kutetea mabaki ya Sudani ya Kimisri.

Jeshi la Mahdiyya

Itikadi ya kupanua utawala wa mahdiyya kwa njia ya jihad ilimsababisha khalifa kushambulia nchi jirani ya Ethiopia iliyotawaliwa na kaisari wa Kikristo. Mwaka 1887 akaongoza jeshi la askari 60,000 hadi Gondar. Waethiopia wakajibu kwa kushambulia Sudan mwaka 1889. Kifo cha Kaisari Yohane IV katika mapigano ya Metemma tarehe 9 Machi 1889 ililazimisha Waethiopia kurudi kwao. Lakini jeshi la mahdiyya lilipoteza wanajeshi wengi pia likadhoofika.

Wakati huohuo jemadari wa khalifa Abd ar-Raħmān an-Nujumī alishambulia Misri lakini alishindwa kwenye mapigano ya Tushkah. Hii ilikuwa mara ya kwanza ya jeshi la mahdiyya kushindwa.

Majaribio ya vita za jihadi dhidi ya Wabelgiji katika jimbo la Ikweta na dhidi ya Waitalia katika Eritrea yalishindikana pia.

Mapigano ya Omdurman 2 Septemba 1898

Mwaka 1895 mkuu wa jeshi la pamoja la Misri na Uingereza, jenerali Horatio Kitchener aliamua kulipiza kisasi kwa vita ya 1885 akaongoza jeshi kubwa dhidi ya Sudan. Kwa kutumia meli za mvuke kwenye mto Nile na kujenga reli akasongea mbele hadi Omdurman.

Tarehe 2 Septemba 1898 jeshi la mahdiyya lilishindwa kabisa katika mapigano ya masaa matano. Safari hiyo Waingereza waliandaliwa vizuri zaidi, pia silaha mpya kama bunduki ya mtombo ziliwapa ushindi. Upande wa khalifa walikufa askari 11,000, upande wa Waingereza na Wamisri watu 400 pekee.

Khalifa mwenyewe alitoroka akajenga jeshi upya na kutawala kusini mwa Sudan, lakini akauawa mwaka 1899 katika mapigano ya Umm Diwaykarat.

Hivyo Waingereza walitawala Sudan pamoja na Misri hadi 1956, na Kitchener akawa gavana mkuu wa kwanza.

Baada ya Uhuru

Ramani ya siasa ya Sudan kabla ya Sudan Kusini kujitenga.

Baada ya uhuru wa nchi (1956), makabila ya kusini, ambayo hayakukubali kusilimishwa, yalipigania vita ndefu hadi kupata uhuru wao.

Darfur ni eneo lenye majimbo matatu ambayo imeathiriwa na vita vya kisiasa, vita vya Darfur.

Kutokana na vita nyingi serikali hazikuwa imara na kulikuwa na mabadiliko ya mara kwa mara baada ya uhuru. Mapinduzi ya kijeshi ya kwanza yalitokea mwaka 1958, kisha jenerali Ibrahim Abboud alitawala hadi 1964 wakati alipopaswa kujiuzulu kutokana na upanuzi wa vita katika Sudan Kusini na upinzani wa wananchi kwenye mji mkuu.

Utawala wa Nimeiry

Kilichofuata kilikuwa kipindi cha serikali 3 za kiraia hadi 1969. Tarehe 25 Mei 1969 jeshi, chini ya kanali Gaafar Nimeiry, lilipindua tena serikali. Nimeiry alikuwa waziri mkuu, wakati bunge na vyama vyote vilipigwa marufuku. Nimeiry alitawala hadi 1985, na tangu 1971 alikuwa rais. Mwaka 1972 alifaulu kumaliza awamu ya kwanza ya vita ya wenyewe kwa wenyewe dhidi ya Sudan Kusini kwa mapatano ya Addis Ababa. Sudan Kusini ilipewa mamlaka ya kujitawala katika mambo ya ndani chini ya serikali ya kieneo.

Mwanzoni Nimeiry alijaribu kuiga siasa ya Gamal Abdel Nasser nchini Misri na kutekeleza sera kadhaa za ujamaa. Utawala wake uliona upinzani kutoka kwa Wakomunisti na pia kutoka Waislamu wenye itikadi kali. Baada ya kupinduliwa kwa siku kadhaa na Wakomunisti alivunja ushirikiano na Urusi na kuanza kupokea wanasiasa wenye mwelekeo wa Uislamu mkali katika serikali yake.

Tangu miaka ya 1980 alisogea zaidi upande wa Uislamu wa kisiasa. Mwaka 1983 alitangaza sharia kuwa msingi wa sheria zote na kubadilisha sheria za jinai ipasavyo. Hatua hii ilisababisha upinzani katika sehemu za nchi zisizokaliwa na Waislamu. Alivunja pia serikali ya kieneo kwa Sudan Kusini na hivyo vita ya wenyewe kwa wenywewe ilianza upya.

Nimeiry alitangaza hali ya dharura iliyompa tena mamlaka za kidikteta. Mwaka 1985 aliruhusu kunyongwa kwa mwanafalsafa Mwislamu Mahmoud Mohammed Taha kwa kosa la "uasi dhidi ya Uislamu". Miezi minne baadaye Nimeiry alipinduliwa kwenye mwaka huohuo.

Utawala wa Bashir

Sudan ilirudi kwa miaka michache chini ya serikali ya kiraia. Mapinduzi yaliyofuata mwaka 1989 yalileta utawala wa jenerali Omar al-Bashir. Vita ya wenyewe kwa wenye iliendelea hadi mwaka 2005 ikamalizika kwa Mapatano ya Naivasha baina ya Sudan na SPLA. Sudan Kusini ilipewa miaka hadi 2011 kujitawala halafu kuwa na kura ya wananchi wa kusini kuhusu uhuru uliotangazwa mwaka uleule.

Tangu mwaka 2003 Bashir alisimamia pia vita ya jeshi lake na wanamgambo dhidi ya wakazi wasio Waarabu wa Darfur waliopinga utawala wake.

Tarehe 11 Aprili 2019 Bashir alipinduliwa na jeshi lake baada ya wiki kadhaa za maandamano ya wananchi wa Khartum na miji mingine dhidi yake. Kupinduliwa kwake pamoja na kipindi cha serikali ya mpito ya kijeshi vilitangazwa na waziri wa ulinzi, jenerali Awad Mohammed Ibn Auf. Ilhali waandamanaji waliendelea kupinga serikali ya kijeshi, Ibn Auf alijiuzulu tarehe 12 Aprili na siku iliyofuata, tarehe 13 Aprili, jenerali Abdel Fattah Burhan alitangaza wanajeshi wanatafuta ushirikiano wa karibu na wapinzani wa utawala wa awali[1].

Watu na makabila

Kadiri ya sensa za mwaka 2008, wakazi walihesabiwa kuwa zaidi ya milioni 21.6.

Kadirio ni kwamba wakazi ni karibu milioni 48 mwaka 2022.

Umma wa miji kama Khartoum (pamoja na Omdurman, na Khartoum ya kaskazini) waongezeka zaidi: umma wa miji hiyo yakadiriwa milioni 6-7 na wengine wahamiaji milioni 2 ambao wamekimbia vita vya kusini, magharibi, mashariki na pia wengine kwa sababu ya ukame.

Sudan ina aina mbili za utamaduniWaafrika walio na Uarabu na Waafrika wasio Waarabu — na maelfu ya makabila na migao ya kabila, lugha tofautitofauti kwa makundi au kabila – migawanyiko hii uleta siasa za utengo na ubaguzi.

Majimbo ya Kaskazini hasa ndio makubwa nchini Sudan, na pia miji mikubwa iko katika majimbo haya. Zaidi ya milioni 22 wanaoishi katika majimbo haya ni Waislamu-Waarabu na wanaongea Kiarabu, lakini wengi pia huongea lugha 70 za kikabila hasa Kinubi, Kibeja, Kifur, Kinuban, Kiingessana, kwa kikundi hiki kuna wale wavutia zaidi kama: Wa-Kababish kutoka Kordofan kaskazini, watu hawa wanaofuga ngamia; Ga’alin (الجعلين), Rubatab (الرباطاب), Manasir (المناصير) and Shaiqiyah (الشايقيّة); makabila ambao makao yao ni karibu na mito ni kama Baggara wa Kurdufan na Darfur; Wakiham Beja eneo ya bahari ya Shamu na Wanubi wa Nile kaskazini, ambao wengine wamehamishwa karibu na mto Atbara. Eneo la Shokrya kwa Wabutana, Wabataheen wamepakana na Waga’alin na Washorya, upande wa kusini-magharibi eneo ya Butana. Pia kuna Warufaa, Wahalaween na makabila mengine mingi eneo la Gazeera na kwa ufuo wa Bluu Nile na eneo ya Dindir. Hata Wanubi kusini mwa eneo la Kurdufan na Wafur upande wa magharibi.

Makabila makuu

Lugha

Nchini Sudan kuna lugha zaidi ya 70. Kati yake, muhimu zaidi ni Kiarabu, ambacho ndicho lugha rasmi pamoja na Kiingereza. (Angalia Orodha ya lugha za Sudan.)

Dini

Dini kubwa zaidi nchini ni Uislamu (97%).

Wakristo ni hasa Waorthodoksi wa Mashariki (Wakopti, Waethiopia na Waeritrea, lakini pia Waarmenia), halafu Waorthodoksi, Wakatoliki na Waprotestanti.

Elimu

Vyuo Vikuu vya Sudan ni kama vile:

Tazama pia

Marejeo

Tanbihi

  1. Kiongozi wa baraza la kijeshi la mpito nchini Sudan ameapa kuung'oa utawala, BBC News Swahili 13-04-2019

Vitabu

Makala

  • "Quo Vadis bilad as-Sudan? The Contemporary Framework for a National Interim Constitution". Law in Africa (Cologne; 2005). Vol. 8, pp.  63–82.

Viungo vya nje

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:

Serikali

Maarifa ya kawaida

Habari

Picha

Utalii

Mengineyo


Nchi za Afrika Bara la Afrika
Afrika ya Kati (Jamhuri ya) | Afrika Kusini | Algeria | Angola | Benin | Botswana | Burkina Faso | Burundi | Cabo Verde | Chad | Cote d'Ivoire | Eritrea | Eswatini | Ethiopia | Gabon | Gambia | Ghana | Guinea | Guinea Bisau | Guinea ya Ikweta | Jibuti | Kamerun | Kenya | Komori | Kongo (Jamhuri ya) | Kongo (Jamhuri ya Kidemokrasia ya) | Lesotho | Liberia | Libya | Madagaska | Malawi | Mali | Misri | Morisi (Visiwa vya) | Mauritania | Moroko | Msumbiji | Namibia | Niger | Nigeria | Rwanda | Sahara ya Magharibi | Sao Tome na Principe | Senegal | Shelisheli | Sierra Leone | Somalia | Sudan | Sudan Kusini | Tanzania | Togo | Tunisia | Uganda | Zambia | Zimbabwe
Maeneo ya Afrika ambayo ni sehemu za nchi nje ya Afrika
Hispania: Kanari · Ceuta · Melilla | Italia: Pantelleria · Pelagie | Ufaransa: Mayotte · Réunion | Uingereza: · St. Helena · Diego Garcia | Ureno: Madeira
Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Sudan kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.