Anga

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Anga lenye mawingu.
Anga la mwezi ni jeusi; angani inaonekana dunia yetu. Kama dunia isingekuwa na angahewa kama mwezi rangi ya anga ingekuwa nyeusi pia.

Anga (mara nyingi pia: mbingu) ni uwazi ule mkubwa tunaoona juu yetu tukiinua kichwa nje ya jengo. Tukisimama kwenye tambarare au juu ya mlima kwenye mchana bila mawingu unaonekana kama nusutufe yenye rangi ya buluu. Ile buluu inaongezeka tukitazama juu zaidi kulingana na sehemu karibu na upeo. Wakati wa usiku anga ni jeusi lakini limejaa nuru za nyota.

Kwa lugha nyingine anga ni eneo la angahewa au upeo unaojaa hewa juu ya uso wa ardhi. Sehemu hiyo imejaa molekuli za gesi za angahewa hasa nitrojeni na oksijeni; ni molekuli hizo zinazoakisisha nuru ya jua na kusababisha rangi ya buluu ya anga wakati wa mchana. Bila hewa, anga lingekuwa jeusi muda wote jinsi lilivyo mwezini (linganisha picha).

Wakati wa mchana tunaona jua angani lisipofunikwa na mawingu. Wakati wa usiku tunaona mwezi na nyota zinazoonekana pia asubuhi na jioni ambako nuru ya jua haina nguvu bado au tena.

Mengine yanayoonekana angani ni mawingu, upinde wa mvua, ndege au eropleni.

Anga-nje[hariri | hariri chanzo]

Anga halina mwisho. Pale tunapojadili sehemu kubwa iliyoko nje ya angahewa tunaweza kuita anga-nje na hii ni upeo wa mwezi, sayari, jua na nyota. Sayansi ya astronomia inaifanyia utafiti.

Anga-nje ni karibu hali ya ombwe yaani utupu ambako kwa umbali mkubwa tu kuna magimba ya angani au vumbi. Lakini imejaa mnururisho wa aina mbalimbali na kani kama graviti.

Anga na mbingu[hariri | hariri chanzo]

Katika lugha ya kila siku maneno "anga" na "mbingu" mara nyingi yanatumiwa kwa maana moja: "Mawingu yanatembea angani - mawingu yanatembea mbinguni". Lakini mbingu huwa na maana ya ziada, yaani ya kidini, kwa kutaja pia upeo wa Mungu au hali inayopita maarifa ya duniani: "hapa ninajisikia kama mbinguni" ni tofauti sana na "hapa najisikia angani".

Katika wikipedia hii tunatumia neno "mbingu" zaidi kwa maana ya kidini.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Anga kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.