Nubia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kuhusu kabila la watu la kusini mwa Sudan, tazama Wanuba

Farao Ramses II akipigana na Wanubia (mchoro wa mwaka 100 BK hivi).
Falme za Kikristo katika Nubia kabla ya Uvamizi wa Waarabu.

Nubia (kutokana na jina la wakazi walioteka nchi katika karne ya 4: kwa Kiarabu نوبة nuba / noba) ni eneo lilipo kando ya mto Naili katika Misri (kusini kwa mji wa Aswan) na Sudan (kaskazini kwa Khartoum). Zamani ilijulikana kwa jina la Kushi na hata Ethiopia.

Katika historia ilikuwa mahali pa falme mbalimbali, na milki za Kushi na Meroe zilikuwa kubwa kati ya hizo.

Tangu zamani Wanubia walikuwa majirani wa Misri ya Kale upande wa kusini. Kulikuwa na vipindi ambako Misri ilitawala sehemu kubwa za Nubia, na pia vipindi ambako Misri ya Kale ilishindana na majirani hao kwa vita.

Kutokana na picha za ukutani katika makaburi ya Misri inaonekana ya kwamba Wanubia walikuwa Waafrika weusi. Jeshi la Misri ya kale lilikuwa na vikosi vya Wanubia mara kwa mara. Kutokana na picha hizo inaonekana ya kwamba kulikuwa na mafarao (wafalme) wenye asili ya Nubia mara kadhaa.

Mnamo mwaka 700 KK Wanubia walivamia na kuteka Misri na wafalme wao walitawala milki ya Misri kama nasaba ya 25 hadi kufukuzwa katika Misri na uvamizi wa Waashuru.

Tangu mnamo 600 KK Nubia ilipata kitovu chake upande wa kusini zaidi katika mazingira ya Meroe.

Waroma wa Kale waliotawala Misri baada ya Julius Caesar walipigana pia mara kadhaa na Wanubia.

Biblia inamtaja Towashi Mwethiopia kama waziri wa "malkia wa Kushi" aliyetembelea Yerusalemu na kuwa Mkristo katika kitabu cha Matendo ya Mitume, mlango wa 8.

Inajulikana ya kwamba tangu karne ya 6 BK Nubia ilikuwa nchi ya Kikristo. Falme wa Kikristo ziliendelea zikipigana na Waarabu walivamia na kuteka Misri katika karne ya 7.

Polepole Uislamu ulianza kuenea pamoja na wavamizi Waarabu na milki ya Kikristo ya mwisho katika Nubia ilitekwa na Waislamu mnamo mwaka 1504.

Polepole sehemu kubwa ya Wanubia waliacha lugha yao na kutumia Kiarabu lakini kuna maeneo ambako Kinubia kinazungumzwa hadi leo.

Vilevile walizidi kuacha Ukristo na kusilimu (mchakato huo ulimalizika katika karne ya 19).

Kwa sasa kuna vita vikubwa katika eneo la Nubia baina ya Waarabu na wakaaji wa eneo hilo. Waarabu wanataka kuwanyang'nya Wanubian sehemu yao. Jambo ambalo limezusha vita kwa muda wa miaka na miaka huko Wanubia wakipigania eneo lao.

Viungo vya Nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Nubia kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.