Utetezi wa Kanisa Katoliki

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Hii ni sehemu ya mfululizo kuhusu
Kanisa Katoliki
Imani

Umoja wa Mungu
Utatu (Baba, Mwana, Roho Mtakatifu)
Umwilisho Maisha ya Yesu
Msalaba Ufufuko Kupaa
Historia ya Wokovu Ufunuo
Biblia Mapokeo Ualimu Dogma
Neema Dhambi Wokovu Sakramenti
Watakatifu Bikira Maria

Muundo

Papa: Fransisko
Urika wa maaskofu Mitaguso mikuu
Kundi la Makardinali
Kanisa la Kilatini
Makanisa Katoliki ya Mashariki

Historia

Historia Ukristo
Ukatoliki Mlolongo wa Kitume
Sifa nne za Kanisa Utetezi Ekumeni
Maisha ya kiroho Amri Kumi Utawa
Sala Falsafa Teolojia
Muziki Sanaa Sayansi

Ibada

Liturujia Mwaka wa Kanisa
Ekaristi Liturujia ya Vipindi

Mapokeo ya liturujia

Liturujia ya Kilatini (Roma Liturujia ya Trento Milano Toledo Braga Lyon Canterbury)
Liturujia ya Armenia Liturujia ya Misri
Liturujia ya Ugiriki Liturujia ya Antiokia
Liturujia ya Mesopotamia

Utetezi wa Kanisa Katoliki ni sehemu ya teolojia ya Ukristo inayolenga kutoa hoja za kutetea imani na maisha ya Kanisa Katoliki dhidi ya zile za watu wa madhehebu au dini nyingine au za wale wasio na dini yoyote wanaolenga kuthibitisha kasoro zake ili kukomesha imani katika asili yake ya Kimungu.

Kwa kutaja utetezi wa namna hiyo katika lugha nyingi limetoholewa neno la Kigiriki ἀπολογία, apologia, "utetezi wa sauti, hotuba ya utetezi"[1].

Ni tofauti kidogo na hoja zinaotumiwa na Wakatoliki dhidi ya dini, madhehebu na itikadi nyingine ili kuonyesha vilivyo na kasoro[2][3].

Historia[hariri | hariri chanzo]

Mt. Yustino katika picha takatifu ya Urusi.

Utetezi wa Ukristo ulihitajika mapema dhidi ya hoja za Wayahudi na wengineo, hivyo unajitokeza katika Agano Jipya lenyewe, kwa mfano katika nyaraka za Mtume Paulo.

Baadaye uliendelea katika maandishi ya Mababu wa Kanisa kama vile Yustino mfiadini, Tertullianus, Origen na Agostino wa Hippo. Baadhi yao walitetea Ukristo dhidi ya dhuluma za serikali ya Dola la Roma na kwa hiyo wanaitwa Mababu watetezi (wa imani).

Baadaye kazi hiyo iliendelezwa na walimu wa Kanisa wa Karne za Kati, kama vile Anselm wa Canterbury, Thoma wa Akwino na wengineo wa Teolojia ya shule.

Juhudi za pekee zilihitajika na kufanyika wakati wa Matengenezo ya Kiprotestanti, yaliyoelekea kusambaratisha Kanisa kwa msingi wa ufafanuzi mpya wa Biblia na kwa kutegemea itikio la wengi dhidi ya makwazo yaliyotolewa na baadhi ya viongozi wa ngazi zote, hata Mapapa. Wakati huo walijitokeza hasa Wajesuiti kama vile Petro Kanisi na Roberto Bellarmino.

Wakati wa Falsafa ya mwangaza kati ya watetezi wa Kanisa dhidi ya falsafa hiyo iliyopinga kabisa imani yoyote ya dini, anakumbukwa hasa Blaise Pascal.

Katika karne za mwisho kuna walei walioongokea Ukatoliki kama John Henry Newman na Gilbert K. Chesterton huko Uingereza, Scott Hahn na mke wake huko Marekani na wengine wengi.

Siku hizi, mbali ya vitabu, magazeti, vipeperushi, kanda n.k., kuna tovuti mbalimbali za kutetea Kanisa Katoliki, ambazo kati yake labda maarufu zaidi ni ile Catholic Answers.

Mbinu[hariri | hariri chanzo]

Mama Teresa mwaka 1988.

Watetezi hao na wengineo wametumia hoja za kifalsafa, za kihistoria na za fani nyingine, mbali ya madondoo ya Biblia, kadiri ya hoja zilizotumiwa na wapinzani, ambao pengine wanakanusha mafundisho ya Kanisa, pengine wanalaumu zaidi matendo ya wanakanisa, hasa viongozi.

Hata hivyo, utetezi mkuu ni utakatifu wa maisha ya waamini, ambao kila unapopatikana unakumbusha neno la Yesu kwamba matunda yanathibitisha ubora wa mti kuliko hoja za akili. Kati ya hao kuna waamini milioni 30 hivi waliofia dini yao huku wakisamehe watesi wao.

Ugumu wa kazi hiyo[hariri | hariri chanzo]

Ugumu wa kutetea Kanisa hilo una sababu mbalimbali.

Upande wa imani na maadili, ni kwamba Kanisa Katoliki lina mafundisho mengi sana kutokana na juhudi za miaka 2000 hivi za kuwa na uwiano kati ya mitazamo inayopingana. Kanisa hilo halikubali kurahishisha mafundisho kwa kusisitiza upande mmoja unaoeleweka zaidi na kuweka kivulini upande wa pili. Hivyo, kwa mfano, unakiri kuwa Yesu ni Mungu kweli na papo hapo mtu kweli katika umoja wa nafsi yake. Kufafanua fumbo hilo kwa mtu asiyesadiki ni jambo gumu kuliko kumueleza kwamba ni Mungu tu au mtu tu.

Tena, katika ulimwengu wa kisasa, Kanisa Katoliki linajikuta mstari wa mbele katika kutetea uhai na haki duniani, pamoja na kupinga maovu mbalimbali yaliyoenea kwa faida kubwa ya kiuchumi ya makundi mbalimbali, kama vile wanaouza binadamu, wanaonyanyasa wanyonge, wanaotoa mimba za wanawake n.k. Hivyo si ajabu kwamba linakabiliwa na chuki na upinzani mkubwa.

Upande wa maisha, ugumu ni kwamba Kanisa Katoliki linakaribia kutimiza miaka 2000 ya uwepo wake, likiwa na muundo unaoonekana, ulioenea sasa duniani kote. Ndani yake hadi sasa wameishi bilioni kadhaa za Wakristo, wakiwemo milioni kadhaa za wakleri na watawa katika mazingira mbalimbali, pengine machafu na ya kikatili sana, yaliyoweza kuwaathiri kwa urahisi.

Kwa kuwa hao pia ni binadamu, si ajabu kwamba kati yao wengine walishindwa uaminifu, lakini ni rahisi kuwanyoshea kidole ili kulaumu Kanisa lenyewe. Yesu alikuwa amesema kwamba adui yake atapanda magugu kati ya ngano aliyosia yeye shambani mwake. Pamoja na hayo, maovu yanazidi kukwaza watu wasiamini. Ingekuwa rahisi zaidi kutetea kundi dogo lililoanza juzijuzi tu.

Maelekezo ya kisasa[hariri | hariri chanzo]

"Tunahitaji utetezi wa aina mpya, kulingana na madai ya leo, ambayo izingatie kwamba jukumu letu si kushinda hoja, bali kuokoa watu, ni kuwajibika katika mapambano ya kiroho, si katika mabishano ya nadharia, ni kutetea na kukuza Injili, si sisi wenyewe".[4]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. "ἀπολογία". Blue Letter Bible-Lexicon. Iliwekwa mnamo 7 May 2012.  Check date values in: |accessdate= (help)
  2. Kahlos, Maijastina (2007). Debate and Dialogue : Christian and Pagan Cultures c. 360-430. Aldershot: Ashgate. ku. 7–9. ISBN 0-7546-5713-2. 
  3. Ernestine, van der Wall (2004). "Ways of Polemicizing: The Power of Tradition in Christian Polemics". Katika T L Hettema and A van der Kooij. Religious Polemics in Context. Assen: Royal Van Gorcum. ISBN 90-232-4133-9. 
  4. Papa Yohane Paulo II, hotuba kwa Maaskofu wa Karibi, 7 Mei 2002

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu Kanisa Katoliki bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Utetezi wa Kanisa Katoliki kama historia yake au maelezo zaidi?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.