Mafuta ya petroli

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Chupa cha mafuta ya petroli; chupa chenyewe ni cha plastiki inayotengenezwa na mafuta hii
Pampu ya mafuta ya petroli

Mafuta ya petroli (pia petroliamu kutoka Kilatini petra = mwamba na oleum = mafuta au mafuta ghafi) ni kiowevu kizito chenye rangi nyeusi hadi ya kijani. Inatokea kiasili katika ardhi na inawaka rahisi.

Ni chanzo cha petroli, fueli mbalimbali, dawa nyingi na plastiki: hivyo ni kati ya vyanzo muhimu kabisa vya nishati vinavyotumiwa na binadamu kama fueli ya usafiri na ya kutengeneza umeme.

Kikemia mafuta ya petroli ni mchanganyiko wa dutu, hasa hidrokaboni mbalimbali. Inatumiwa kwa njia ya ukenekaji (distillation) ikipashwa moto na sehemu zake kutenganishwa zikifikia kiwango cha kuchemka kwa nyakati mbalimbali.

Chanzo cha mafuta ya petroli[hariri | hariri chanzo]

Petroliamu hupatikana ndani ya maganda ya mwamba. Wataalamu wengi hukubaliana ya kwamba iliundwa baharini. Maji ya bahari yamejaa algae na planktoni inayoishi kutokana na uwezo wake wa usanisinuru. Viumbehai hao wadogo wanakufa na kuzama chini katika vilindi vya bahari vikifunika tako la bahari kama ganda. Katika kina kirefu cha mita elfu kadhaa mabaki yale hayawezi kuoza kutokana na uhaba wa oksijeni, hivyo yanageuka kuwa ganda la matope.

Kila baada ya muda mashapo mineralia (kama vile mchanga, vumbi ya hewani) yanashuka pia hadi tako la bahari na kufunika matope yaliyotokea na planktoni. Maganda yale ya mashapo mineralia yanaweza kuwa manene na mazito hadi yakaanza kukandamiza tope na kuisababisha kuwa moto. Katika mazingira ya shindikizo na joto molekuli ndefu za hidrati kabonia za biomasi zinavunjwa kuwa molekuli fupi katika mchakato unaoigwa na teknolojia ya mvevusho.

Molekuli hizo fupi zinatembea katika vinyweleo ndani ya mwamba ya mashapo hadi kufikia aina ya mwamba penye nafasi ndogondogo ambako molekuli nzito zakusanya kama petroliamu na molekuli nyepesi sana kama gesi asilia. Kama kuna ganda la mwamba imara lililopo juu ya mwamba vinyweleo akiba ya petroliamu na gesi inaanza kutokea na mara nyingi molekuli nyepesi za gesi huwa kama "kofia" ya gesi asilia juu ya "ziwa" la petroliamu. Hii ni sababu ya kwamba mara nyingi gesi asilia inapatikana pamoja na petroliamu.

Historia ya matumizi yake[hariri | hariri chanzo]

Tangu nyakati za kale mafuta ya petroli ilitokea kiasili kutoka ardhi katika nchi kama Mesopotamia kusini. Pale ilipoonekana kama ziwa iliunganika na oksijeni ya hewa na kuganda kuwa lami. Ile lami asilia iliwahi kutumiwa na watu wa kale; kwa kuikoroga na mchanga watu waliweza kuziba mapengo kati ya Mbao za jahazi.

Pia wenyeji wa Babeli walimwaga tayari mafuta ya petroli asilia juu ya barabara za udongo kwa shauri la kuimarisha uso wake.

Baadaye Waroma wa Kale na Wabizanti walitumia mafuta hayo kama silaha za kumwaga moto dhidi ya maadui hasa baharini.

Lami na mafuta ya petroli zilitumiwa pia kama tiba ya maradhi mbalimbali.

Wakati wa karne ya 19 daktari Mkanada Abraham Gesner aligundua ya kwamba aliweza kutengeneza mafuta ya taa kutoka kwa mafuta hayo. Hadi wakati ule ni hasa mafuta ya nyangumi yaliyotumiwa kama mafuta ya taa lakini ilizidi kuwa ghali. Mafuta mpya yalipokelewa haraka, yalipatikana kwa bei nafuu na katika nchi nyingi watu walianza kutafuta chemchemi asilia za mafuta ya petroli.

Mwishoni mwa karne ya 19 Carl Benz alibuni motokaa iliyotumia injini ya mwako wa ndani kwa kutumia petroli. Kutokana na juhudi za Henry Ford za kujenga motokaa kwa bei ndogo mahitaji ya petroli yaliongezeka tena.

Usambazaji wa motokaa ulisababisha kuzalishwa kwa petroli kwa wingi na haja ya kukwa na mafuta ya petroli kuongezeka.

Uzalishaji wa petroliamu[hariri | hariri chanzo]

Jedwali linalofuata linaorodhesha nchi ambako petroliamu hutolewa ardhini kufuatana na wingi wa uzalishaji.

Kipimo cha wingi ni kiasi kinachohesabiwa kwa "mapipa" kwa siku kwa Kiingereza: "barrels per day" - kifupi "bbl/d") ambako "pipa" moja linalingana na lita 159. Hali halisi mapipa hayatumiwi tena na mafuta husafirishwa kwa njia ya bomba.

# Nchi ya kuzalisha mafuta ya petroli 1,000 bbl/d (2006) 1,000 bbl/d (2007) 1,000 bbl/d (2008) 1,000 bbl/d (2009) Asilimia ya uzalishaji duniani
mwaka 2009
1 Saudia 10,665 10,234 10,782 9,760 11.8%
2 Urusi 1 9,677 9,876 9,789 9,934 12.0%
3 marekani 1 8,331 8,481 8,514 9,141 11.1%
4 Nigeria 4,330 4,138 4,290 4,300 6.3%
5 Uajemi (OPEC) 4,148 4,043 4,174 4,177 5.1%
6 China 3,845 3,901 3,973 3,996 4.8%
7 Kanada 2 3,288 3,358 3,350 3,294 4.0%
8 Mexico 1 3,707 3,501 3,185 3,001 3.6%
9 Falme za Kiarabu (OPEC) 2,945 2,948 3,046 2,795 3.4%
10 Angola 3,109 2,890 2,803 2,507 3.2%
11 Kuwait (OPEC) 2,675 2,613 2,742 2,496 3.0%
12 Venezuela (OPEC) 1 2,803 2,667 2,643 2,471 3.0%
13 Norwei 1 2,786 2,565 2,466 2,350 2.8%
14 Brazil 2,166 2,279 2,401 2,577 3.1%
15 Iraq (OPEC) 3 2,008 2,094 2,385 2,400 2.9%
16 Algeria (OPEC) 2,122 2,173 2,179 2,126 2.6%
17 Libya (OPEC) 1,809 1,845 1,875 1,789 2.2%
18 Ufalme wa Maungano
(Uingereza na Uskoti)
1,689 1,690 1,584 1,422 1.7%
19 Kazakhstan 1,388 1,445 1,429 1,540 1.9%
20 Qatar (OPEC) 1,141 1,136 1,207 1,213 1.5%
21 Indonesia 1,102 1,044 1,051 1,023 1.2%
22 Uhindi 854 881 884 877 1.1%
23 Azerbaijan 648 850 875 1,012 1.2%
24 Argentina 802 791 792 794 1.0%
25 Oman 743 714 761 816 1.0%
26 Malaysia 729 703 727 693 0.8%
27 Misri 667 664 631 678 0.8%
28 Kolombia 544 543 601 686 0.8%
29 Australia 552 595 586 588 0.7%
30 Ecuador (OPEC) 536 512 505 485 0.6%
31 Sudan 380 466 480 486 0.6%
32 Syria 449 446 426 400 0.5%
33 Guinea ya Ikweta 386 400 359 346 0.4%
34 Thailand 334 349 361 339 0.4%
35 Vietnam 362 352 314 346 0.4%
36 Yemen 377 361 300 287 0.3%
37 Denmark 344 314 289 262 0.3%
38 Gabon 237 244 248 242 0.3%
39 Afrika Kusini 204 199 195 192 0.2%
40 Turkmenistan (hakuna takwimu) 180 189 198 0.2%

Chanzo: U.S. Energy Information Administration Archived 10 Julai 2008 at the Wayback Machine.

1 Uzallishaji wa mafuta umeshapita kilele chake katika nchi hii kutokana na jumla ya akiba zake.

2 Uzalishaji kutokana na akiba za kawaida unapungua katika Kanada, lakini uzalishaji kutokana na mchanga mwenye mafuta unaongezeka; pamoja na mafuta yaliyopo ndani ya mchanga akiba za Kanada ni kubwa dunani baada ya Saudia.

3 Iraki ni mwanachama wa OPEC lakini uzalishaji wake haukuhesabiwa katika takwimu za OPEC tangu 1998.

Petroliamu na siasa[hariri | hariri chanzo]

Mafuta ya petroli yalijulikana tangu karne nyingi yakawa na matumizi mbalimbali. Tangu mapinduzi ya viwandani umuhimu wake uliongezeka kama mafuta ya kutia grisi kwenye injini pia kama mafuta ya taa katika miji iliyokua haraka. Baada ya kupatikana kwa injini ya mwako wa ndani umuhimu wake uliongezeka tena. Mwingereza Winston Churchill alitangulia kuhakikisha utawala wa kampuni ya Kiingereza juu ya maeneo ya mafuta katika Uajemi kusini mnamo mwaka 1911. Tangu Vita kuu ya kwanza ya Dunia wanasiasa wengine wengi walielewa umuhimu wake wa kijeshi na kiuchumi kwa jumla.

Lakini mafuta ya petroli yanapatikana katika nchi kadhaa tu, tena si kila mahali kwa viwango vikubwa. Hivyo kulitokea mashindano baina ya nchi kubwa namna za kutawala upatikanaji wa mafuta yale. Rais Coolidge wa Marekani alisema mwaka 1924 "kipaumbele cha mataifa kitaonekana kwa utawala wao juu ya mafuta ya petroli na bidhaa zinazotengenezwa kutokana nayo"[1]

Wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia maazimo mbalimbali yalitawaliwa na shabaha za kukamata au kutetea maeneo yenye petroliamu[2]. Nchi za jangwa za Waarabu kwenye Ghuba la Uajemi kama Saudia, Kuwait na Falme za Kiarabu zenye wakazi wachache zilikuwa maskini lakini tangu upatikanaji wa petroliamu zimekuwa tajiri. Wakati uleule zilipaswa kukubali uhusiano wa karibu sana na Uingereza na baadaye hasa na Marekani uliofanana wakati mwingine na usimamizi.

Wakati wa Vita ya Yom Kippur kwenye mwaka 1973 nchi za Waarabu walitumia mafuta ya petroli kama silaha wakasababisha mgogoro wa bei ya mafuta walipokataa kwa miezi kadhaa kuuza mafuta kwa nchi zilizosaidia Israel vitani, hasa Marekani na nchi za Ulaya Magharibi. Mgogoro huo ulisababisha matatizo ya kiuchumi kote duniani.[3]

Matatizo ya matumizi ya petroliamu[hariri | hariri chanzo]

Petroliamu ni fueli yenye faida nyingi; inatolewa ardhini kwa urahisi, inasafirishwa haraka na kuwa na nafasi nyingi za kuitumia kwa manufaa ya binadamu. Ilikuwa fueli iliyowezesha maendeleo ya kiuchumi ya karne ya 20.

Siki hizi kuna wasiwasi mwingi kuhusu matumizi yake kama fueli kwa sababu ni fueli kisukuu maana ikitumiwa haiongezeki tena wala kurudi; ilionekana ya kwamba akiba zake zitaishia siku moja. Hapa wasiwasi mkubwa ni ya kwamba uchumi wa dunia umejengwa juu ya msingi unaoendelea kufifia na kuna hatari ya kwamba uchumi utapata mshtuko mkubwa kama akiba za mafuta ya petroli zitaendelea kupungua na bei zake kupanda.

Vilevile matumizi yake yanatoa gesi nyingi hewani amabazo zinaleta hasara kwa mazingira, hasa gesi ya dioksidi kabonia inayochangia kupanda kwa joto duniani kwenye hatari nyingi.

Hapo ndipo sababu kuu za utafiti mwingi kugundua vyanzo vya nishati mbadala.

Kurasa nyingine[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Robert McNally 2017), Crude Volatility: The History and the Future of Boom-Bust Oil Prices, uk. 56, ISBN 9780231178143, online hapa
  2. Oil Strategy in World War II Archived 15 Agosti 2009 at the Wayback Machine., tovuti ya oil150.com, Aug 24, 2007, iliangaliwa Aprili 2019]
  3. Oil Embargo, 1973–1974, tovuti ya history.state.gov, iliangaliwa Aprili 2019

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons

Takwimu[hariri | hariri chanzo]