Makaa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa fueli inayochimbwa ardhini tazama makaa mawe

Kuni huwa zinapangwa kwa rundo linalofunikwa baadaye kwa udongo.
Makaa yakiwaka.

Makaa ni dutu mango yenye kiwango kikubwa cha kaboni inayotumiwa kama fueli. Kwa kawaida inapatikana kwa kupashia moto kuni na kuzia hewa isiingie. Ilikuwa chanzo cha nishati ya kupikia na kupashia moto katika nchi nyingi za dunia kabla ya makaamawe kusambaa kwa urahisi zaidi tangu upatikanaji wa usafiri wa kisasa kama treni na meli. Bado ni fueli muhimu kwa watu wengi katika nchi za Afrika.

Makaa huwa na faida kuliko kuni hasa kutokana na kiwango kikubwa cha nishati ndani yake kulingana na uzito na mjao wake. Faida nyingine ni ya kwamba inawaka bila kutoa ulimi wa moto.

Kwa hiyo matumizi yake yameongezeka kwenye miji iliyo mbali na misitu kutokana na gharama za kusafirisha mizigo. Matumizi ya makaa yalisababisha uharibifu wa misitu katika nchi nyingi.

Makaa hutengenezwa kwa kupanga kuni kavu kama rundo na kulikanda kwa udongo mbichi. Kuni zinachomwa chini, lakini udongo huzuia kuwaka kwake, hivyo joto la ndani linaangamiza unyevu wa kuni na gesi zote zilizomo ndani ya kuni na kulisha ulimi wa moto. Inayobaki ni karibu kaboni tupu yenye mashimo mengi ndani yake yanayosaidia kushika moto baadaye wakati makaa yanapowashwa.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]