Kiwango cha kuchemka

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Maji yachemkayo

Kiwango cha kuchemka ni halijoto ambako kiowevu huchemka.

Kiwango hiki ni halijoto ya juu ambako dutu yaendelea kuwa kiowevu. Kuongezeka kwa kiasi kidogo sana cha nishati kutabadilisha kiowevu kuwa gesi.

Kugeuka kwa kiowevu kuwa gesi hutokea pia chini ya kiwango cha kuchemka kwa njia ya uvukizaji lakini hii inahusu molekuli karibu na uso wa kiowevu tu.

Kwenye kiwango cha kuchemka molekuli mahali popote ndani ya kiowevu huanza kugeukia kuwa gesi hivyo kutokea kwa viputo ndani yake ambavyo ni gesi inayopanda juu.

Kimo, kanieneo na kiwango cha kuchemka[hariri | hariri chanzo]

Halijoto ya kiwango cha kuchemka hutegemea kanieneo au shindikizo la angahewa juu ya uso wa kiowevu. Kwa kanieneo sanifu kiwango cha kuchemka kwa maji ni 100 °C. Lakini mlimani halijoto hii inapungua kwa sababu mlimani urefu wa nguzo ya hewa juu ya uso wa kiowevu umepungua na hivyo pia kanieneo hupungukiwa.

Ongezeko la kimo juu ya UB la mita 300 hupunguza halijoto ya kiwango cha kuchemka kwa takriban sentigredi moja. Maana yake maji yakichemka Dar es Salaam na Mombasa (0 m juu ya UB) kwa 100 °C yatachemka Nairobi au Mbeya (1,700 m juu ya UB) kwenye 94 - 95 °C na kwenye kilele cha mlima Kilimanjaro (5,895 m juu ya UB) kwenye 80-81 °C.


Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kiwango cha kuchemka kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.