Nyangumi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Nyangumi
Nyangumi kibyongo akiruka baharini karibu na Boston, Marekani
Nyangumi kibyongo akiruka baharini karibu na Boston, Marekani
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Chordata (Wanyama wenye ugwe wa neva mgongoni)
Ngeli: Mamalia (Wenye viwele wanaonyonyesha wadogo wao)
Ngeli ya chini: Eutheria
Oda ya juu: Laurasiatheria
Oda: Artiodactyla
Nusuoda: Whippomorpha (Viboko na nyangumi)
Ngazi za chini

Makundi 3:

Nyangumi ni wanyama wa bahari, na pengine wa maji matamu, katika oda Cetacea wanaofanana na samaki, lakini ni mamalia: kwa hivyo hawatagi mayai kama samaki bali huzaa watoto kama mamalia wote na huwanyonyesha.

Pamoja na nguva, wanyama hawa ni mamalia pekee wanaoishi kwenye maji tu.

Oda yao ina spishi 80 hivi. Spishi ndogo huitwa pomboo kwa kawaida na spishi kadhaa za pomboo huishi kwenye maji matamu ya mito mikubwa kama Ganges au Amazonas.

Mwili wote unalingana na maisha ya majini. Nyangumi wanaotupwa kwenye nchi kavu wanakufa haraka: wanakauka, uzito wa mwili unagandamiza mapafu kwa sababu wanakosa ueleaji wa maji.

Hata hivyo muundo wa mwili ni sawa na mamalia wengine:

  • wanapumua kwa kutumia mapafu; kutegemeana na spishi zinaweza kuzama na kukaa chini ya maji kuanzia dakika kadhaa hadi masaa mawili.
  • Huwa na moyo wenye vyumba vinne unaoweza kusambaza oksijeni mwilini mwote.
  • Nyangumi huwa na damu moto yaani wanaweza kutunza halijoto ya wastani mwilini, tofauti na samaki wanaobadilika halijoto ya mwili kulingana na halijoto ya mazingira.
  • Wanazaa watoto waliokamilika tayari na kuwanyonyesha maziwa yenye mafuta mengi kwa kutumia viwele vyao. Mimba hukua mwilini mwa mama hadi kuwa mnyama kamili jinsi ilivyo kwa mamalia wengi.
Nyangumi mama na mtoto wake.

Spishi nyingi za nyangumi ni kubwa sana. Nyangumi buluu (Blue whale) anaweza kufikia uzito wa tani 200 na urefu wa mita 33. Nyangumi wadogo ni hasa familia ya pomboo ambao wale wadogo wanafikia urefu wa mita na nusu tu.

Mara nyingi spishi za nyangumi zinatofautishwa kutokana na meno yao:

  • wale wanaowinda samaki au wanyama wakubwa wengine wa bahari wana meno ya kawaida.
  • wale wanaokula planktoni (viumbe hai vidogo sana baharini) hawana meno, bali mifupa ya kinywani ambao si mifupa ya kweli, ila inaundwa na kitu kinachofanana na kucha za vidole. Mifupa hiyo inakaa kama meno ya chanuo na inafanya kazi ya filta; nyangumi huyo anafungua mdomo na kujaza nafasi maji pamoja na yote yaliyomo kama uduvi wadogo sana; ulimi unasukuma maji kupitia chanua ya mifupa ya kinywani na windo unabaki ndani kama chakula.

Nyangumi ni jina la jumla la mamalia wa majini wa oda ya Cetacea. Neno nyangumi wakati fulani humaanisha wanyama wote wa oda ya Cetacea, lakini katika lugha ya kawaida huwaacha wanyama wa familia ya Delphinoidea, kama vile pomboo. [1]

Spishi ndogo hizi huwa ndani ya oda ndogo ya Odontoceti (nyangumi wenye meno), ambayo hujumuisha nyangumi kadhaa.

Oda nyingine ndogo ya Cetacea ni Mysticeti, ambayo hujumuisha nyangumi wa bluu, ambaye ndiyo mnyama mkubwa kuliko wote aliyeripotiwa kuishi, nyangumi mwenye nundu, na wanyama wengine wanaokula kutoka kwenye maji ya baharini kutumia michirizi mirefu iliyopo badala ya meno, ambayo ndiyo walikopatia jina lao.

Viungo vyake[hariri | hariri chanzo]

Kama mamalia wengine, nyangumi hutumia mapafu kupumua, wana damu joto, wananyonyesha watoto wao kwa kutumia viwele, wana vinyweleo, japo kidogo sana.

Mwili wa nyangumi umeungana. Miguu ya mbele, imekaa muundo wa kasia. Mwishoni mwa mkia kuna tiara, au pezi la mkia, ambalo lina saidia kwenye mwendo hasa wima tofauti na kwa mwendo mlalo wa samaki. Japokuwa nyangumi hawana miguu ya nyuma, lakini baadhi yao wanamiguu isiyokamilika; iliyojificha ndani ya miili yao. Spishi nyingi za nyangumi wana pezi migongoni mwao inayojulikana kama pezi la mgongoni.

Chini ya ngozi yao wana utando wa mafuta. Mafuta haya ni kwaajili ya kuhifadhi nishati na kuzuia upotevu wa joto. Nyanguumi pia wana moyo wenye vyumba vinne. Nao pia wana uti wa mgongo japo pingili za shingoni pia zimeungana kwaajili ya kuimarisha uwezo wa kuogelea na kuongeza uhuru wa kufanya hivyo. Wanao pia mfupa wa nyonga usiokuwa na kazi maaluum.

Nyangumi wanapumua kutumia matundu ya hewa, yaliyo juu ya vichwa vyao ili kuwawezesha kupumua huku wakiwa wamezama majini. Nyangumi wa baleen wanayo mawili; na nyangumi wenye meno wana moja tu. Kupumua hujumuisha kutoa maji zaidi kutoka kwenye matundu hayo ya hewa na, na kuunda bubujiko la maji. Bubujiko hizi huwa na maumbo mbalimbali na wakati mwingine hutumika kuwatofautisha na hatimaye kuwatambua baadhi ya nyangumi.

Nyangumi wa bluu ndiye mamalia mkubwa zaidi aliyepata kuishi, na pia mnyama mkubwa, kufikia mpaka mita 35 kwa urefu na uzito wa tani 150.

Nyangumi kwa wastani wanaishi miaka 40 mpaka 90, kulingana na aina zao na mara chache hufanikiwa kiushi zaidi ya karne moja. Hivi karibuni kipande cha kamba kilichokuwa kinatumiwa na wavuvi wa nyangumi wa karne ya 19, kilipatikana kwa nyangumi huko Alaska, na kuonesha kuwa nyangumi yule alikuwa na umri kati ya miaka 115 na 130. [2] kwa kutumia mbinu ya kupima umri kwa kuangalia kiwango cha aspatiki asidi kwenye macho ya nyangumi, pamoja na kipande cha chusa, vilionesha umri wa miaka 211 kwa nyangumi mmoja, na kuwafanya nyangumi pia kuwa wanyama wanaoishi kwa muda mrefu zaidi. .[3][4] Mkia wa nyangumi unaweza kuwa pia kama alama ya kuwatambua, kama ilivyo kwa nyangumi wenye nundu mgongoni.

Meno ya nyangumi wenye meno kama vile nyangumi aitwaye sperm, yana seli za sementamu zilizo juu ya seli za dentaini. Tofauti na binadamu wenye meno yenye kiasi kikubwa cha enameli kwenye sehemu ya nje ya jino, nyangumi wana sementamu nje ya fidhi. Ni kwa nyangumi wakubwa pekee ambao enameli yao huonesha pale ambapo sementamu ilipotoka kwenye sehemu ya jino[5]

Tabia[hariri | hariri chanzo]

Nyangumi kibyongo akijitokeza.

Nyangumi huonwa kama ni wawindaji mara zote, lakini chakula chao ni kuanzia plankitoni mpaka samaki wakubwa kabisa, na wakati mwingine wanyama wengine wa baharini, hata nyangumi wengine. Nyangumi hasa wale wenye nundu mgongoni na wale wa bluu wanakula tu kwenye maji ya aktiki, ambapo humeza vitoweo vyao pamoja na maji mengi, na baadae kutoa maji kupitia baleen huku wakibakiza vitoweo vyao kinywani. [6]

Nyangumi hawanywi maji ya baharini na badala yake hutengeneza maji kutoka kwenye chakula chao kwa metabolizimu ya mafuta. [7]

Nyangumi wengi huonesha tabia nyingi za majini kama vile kujitokeza juu na kupigiza mkia.

Kulingana na mazingira yao (tofauti na na wanyama wengine), nyangumi hupumua kwa hiari yao, wanaamua ni wakati gani wa kupumua. Mamalia wote hulala lakini nyangumi hawawezi kulala kwa muda mrefu sababu wanaweza zama majini na kufa. Husemekana ni nusu tu ya ubongo wa nyangumi hulala na sehemu nyingine hufanyakazi, hivyo nyangumi huwa halali moja kwa moja lakini hupumzika vya kutosha. Mara nyingi nyangumi hulala huku jicho moja tu likiwa limefungwa. Baadhi ya nyangumi huwasiliana kwa sauti za kimuziki, zikijulikana kama nyimbo za nyangumi. Sauti hizi zaweza kuwa kubwa sana kutegemeana na spishi zao. Nyangumi waitwao sperm husikika wakitoa sauti za kugonga gonga tu, kwasababu wao wana meno na hutoa pia mwangwi unaoweza kusikika kwa maili nyingi. [8]

Nyangumi jike huzaa ndama mmoja tu. Muda wa kumkuza ndama huyo ni zaidi ya mwaka mmoja kwa spishi nyingi na hujumuisha uhusiano mkubwa kati ya mama na ndama. Nyangumi huwa tayari kuzaa wakiwa na miaka saba mpaka kumi. Mtindo huu huruhusu watoto wachache tu lakini wakiwa na uwezo mkubwa wa kuishi.

Viungo vya uzazi vya nyangumi huzama na kujificha ndani ya nafasi za mwili wakati wa kuogelea, kuongeza mwendo kasi na kuzuia majeraha. Nyangumi wengi hawana wenzi wa aina moja; na majike wengi hubadilisha madume kadhaa kila msimu. Watoto wa nyangumi huzaliwa kwa kutoa mkia kwanza utaratibu unaopunguza hatari ya kufa maji. [9] [10]

Nyangumi pia hujulikana kwa uwezo wao wa kufundisha na kujifunza, pamoja na kushirikiana na hata kuonekana kuhuzunika. [11]

Uwindaji wa nyangumi[hariri | hariri chanzo]

Kwa karne nyingi nyangumi wamekuwa wakiwindwa kwa ajili ya nyama na malighafi. Kati ya karne ya 20, hata hivyo, viwanda vingi vya nyangumi vilisababisha kuwa hatarini kwa spishi nyingi za nyangumi, na uwindaji wa nyangumi ukakomeshwa mara moja katika nchi nyingi isipokuwa chache.

Mashirika kadhaa yameanzishwa kwa ajili ya kuzuia uwindaji wa nyangumi na hatari nyingine kwa maisha ya nyangumi. [12][13]

Asili na uainishaji[hariri | hariri chanzo]

Cetacea wote, kujumuisha na nyangumi na pomboo, ni kizazi kilichotokana na mamalia wa nchi kavu wa oda ya Artiodactyl. Kwa pamoja cetacea na artiodactyls sasa wanaainishwa chini ya oda moja ya Cetartiodactyla inayojumuisha viboko na nyangumi. Kimsingi, nyangumi wana ukaribu mkubwa na viboko; wote ni chimbuko la uzao mmoja, Indohyus, miaka takriban milioni 48 iliyopita na wanyama wenye kwato shufwa kutoka Kashmir, India, karibu miaka milioni 54 iliyopita. [14][15]

Nyangumi waliingia majini karibia miaka milioni 50 iliyopita. [16]

Cetacea wamegawanywa kwenye makundi mawili:

Spishi za Afrika[hariri | hariri chanzo]

Spishi za mabara mengine[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mnyama fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Nyangumi kama uainishaji wake wa kibiolojia, maisha au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.