Australia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Australia


Australia ni bara pia ni nchi huru ya Oceania. Ikiwa na eneo la km² 7,617,930 ni bara dogo kuliko yote duniani, na ni kisiwa kikubwa kuliko vyote. Kama nchi ni ya sita kwa ukubwa.

Iko kusini kwa Indonesia na Papua Guinea Mpya na iko magharibi kwa New Zealand. Mara nyingi visiwa vya New Zealand huhesabiwa kuwa sehemu ya bara la Australia. Vilevile Australia huangaliwa pamoja na visiwa vya Pasifiki katika orodha ya mabara ya dunia kama "Australia na Pasifiki".

Idadi ya wakazi ni 25,970,200 (mwaka 2022).

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Hali ya hewa Australia kufuatana na Köppen classification.

Bara la Australia linakaa juu ya sehemu imara ya bamba la Australia bila mipaka ya gandunia na kwa hiyo hakuna volkeno; matetemeko ya ardhi ni madogo tu.

Umbali kati ya magharibi na mashariki ni km 4,000, na kati ya kaskazini na kusini umbali ni km 3,700.

Australia huzungukwa na bahari ya Hindi, bahari ya Pasifiki na Bahari ya Kusini. Kwa jumla ina pwani yenye urefu wa kilomita 34,218.

Great Barrier Reef mbele ya pwani ya mashariki-kaskazini ni vipwa vya matumbawe vikubwa duniani; ina urefu wa kilomita 2,000.

Sehemu kubwa ya bara ni jangwa au maeneo yabisi sana. Takriban asilimia 40 ya eneo limefunikwa na matuta ya mchanga. Ardhi yenye rutuba iko kusini-mashariki na kona ya kusini-magharibi pamoja na hali ya hewa isiyo na joto kali. Hali ya hewa kaskazini ni ya kitropiki na huko kuna misitu minene pamoja na savana na jangwa.

Sehemu kubwa ya uso wa nchi ni tambarare na majangwa. Kwenye pwani ya mashariki na pia upande wa magharibi kuna safu za milima inayopanda hadi kimo cha mita 2,200. Sehemu ya juu kabisa huitwa milima ya theluji au Alpi za Australia na mlima Kosciuszko unafikia kimo cha mita 2,229. Huko kuna barafuto za kudumu.

Sehemu ya chini iko kwenye beseni la ziwa Eyre iliyopo mita 17 chini ya usawa wa bahari. Tako la beseni hilo mara nyingi ni kavu kabisa, huwa pamejaa maji mara chache tu baada ya mvua kubwa sana.

Mahali pakavu kabisa ni jangwa la Simpson lenye usimbishaji chini ya 200 mm kwa mwaka.

Mito muhimu inaanza katika Alpi za Australia: ni Murray na Darling inayomwagilia beseni la Murray-Darling na hii ni eneo muhimu la kilimo cha Australia.

Mingine ni Mto Snowy na Mto Murrumbidgee, halafu mto Fitzroy (Queensland), mto Ord, mto Swan (Australia ya Magharibi), mto Derwent, mto Tamar (Tasmania) na mto Hawkesbury (New South Wales).

Sehemu kubwa ya bara haina watu. Wakazi wengi pamoja na miji yote wako kwenye pwani ya mashariki na kusini.

Miji mikubwa ni Sydney (wakazi milioni 3.7), Melbourne (wakazi milioni 3.6), Brisbane (wakazi milioni 1.7), Perth (wakazi milioni 1.4) na Adelaide (wakazi milioni 1.1).

Mji mkuu, Canberra (wakazi 308,700), ulijengwa kati ya Sydney na Melbourne kwa sababu miji hiyo miwili ilishindwa kukubaliana ni upi unaostahili kuwa mji mkuu.

Uchumi katika maeneo yabisi ni hasa ufugaji wa kondoo milioni 130 na ng'ombe milioni 25.

Ekolojia[hariri | hariri chanzo]

Australia ilitengana na mabara mengine miaka milioni mingi iliyopita. Kwa sababu hiyo kuna aina nyingi za pekee za mimea na wanyama zisizopatikana penginepo duniani. Wanyama wa pekee ni kwa mfano kanguru na koala. Miti ya Australia kama vile mkalitusi imepelekwa kote duniani katika nchi zenye hali ya hewa ya kufaa.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Watu wa kwanza walifika Australia takriban miaka 65,000 iliyopita[1]. Walitunza utamaduni wa wawindaji-wakusanyaji hadi kufika kwa wakoloni (1606).

Hakuna habari kama watu wa Asia walifikia Australia lakini tangu karne ya 17 BK Waholanzi halafu Waingereza walifika kwa jahazi zao.

Australia ikawa mahali pa koloni la kigereza na wafungwa kutoka Uingereza walipelekwa huko katika karne ya 19. Baadaye walifika pia walowezi huru.

Idadi ya Waustralia asilia imepungua sana kutokana na magonjwa mapya wakiambukizwa na Wazungu, pia walitendewa vibaya na kufukuzwa katika sehemu kubwa ya nchi yao.

Australia ilipata uhuru wake mwaka 1901 lakini inaendelea kumkubali malkia ya Uingereza kama Mkuu wa Dola akiwasilishwa na Gavana Mkuu. Mamlaka imo mikononi mwa waziri mkuu na serikali yake.

Serikali[hariri | hariri chanzo]

Muundo wa utawala ni wa shirikisho. Kuna majimbo 6 ya kujitawala pamoja na maeneo ambayo yako moja kwa moja chini ya serikali ya shirikisho.

Lugha[hariri | hariri chanzo]

Australia haina lugha rasmi, lakini 72% ya wakazi nyumbani wanaongea Kiingereza cha Kiaustralia tu. Lugha nyingine zinazotumika na zaidi ya 1% ya wakazi ni ni Kichina, Kiarabu, Kivietnam, Kipanjabi n.k. Wachache nyumbani wanaongea mojawapo kati ya lugha asili za Australia. Angalia pia Orodha ya lugha za Australia.

Dini[hariri | hariri chanzo]

Katika sensa ya mwaka 2021, Wakristo walikuwa 43.9% ya wakazi wote, wakiongozwa na Wakatoliki (20%) na Waanglikana (9.8). Waislamu walikuwa 3.2%, Mabanyani 2.7%, Wabuddha 2.4%, Singasinga 0.8%, Wayahudi 0.4% n.k. 38.9% walisema hawana dini yoyote.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Marejeo mengine[hariri | hariri chanzo]

  • Denoon, Donald, et al. (2000). A History of Australia, New Zealand, and the Pacific. Oxford: Blackwell. ISBN 0-631-17962-3
  • Goad, Philip and Julie Willis (eds) (2011). The Encyclopedia of Australian Architecture Cambridge University Press, Port Melbourne, Victoria. ISBN 978-0-521-88857-8
  • Hughes, Robert (1986). The Fatal Shore: The Epic of Australia's Founding. Knopf. ISBN 0-394-50668-5.
  • Powell JM (1988). An Historical Geography of Modern Australia: The Restive Fringe. Cambridge, U.K.: Cambridge University Press. ISBN 0-521-25619-4
  • Robinson GM, Loughran RJ, and Tranter PJ (2000) Australia and New Zealand: economy, society and environment. London: Arnold; NY: OUP; 0340720336 paper 0-340720328 hard.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]


Makala hii kuhusu eneo fulani bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu eneo hilo kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Je, unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.


Usitaje majina ya madiwani na viongozi au maafisa wengine wa sasa maana wanabadilika haraka mno.

  1. Clarkson, Chris; Jacobs, Zenobia; Marwick, Ben; Fullagar, Richard; Wallis, Lynley; Smith, Mike; Roberts, Richard G.; Hayes, Elspeth; Lowe, Kelsey; Carah, Xavier; Florin, S. Anna; McNeil, Jessica; Cox, Delyth; Arnold, Lee J.; Hua, Quan; Huntley, Jillian; Brand, Helen E. A.; Manne, Tiina; Fairbairn, Andrew; Shulmeister, James; Lyle, Lindsey; Salinas, Makiah; Page, Mara; Connell, Kate; Park, Gayoung; Norman, Kasih; Murphy, Tessa; Pardoe, Colin (2017). "Human occupation of northern Australia by 65,000 years ago". Nature. 547 (7663): 306–310. Bibcode:2017Natur.547..306C. doi:10.1038/nature22968. hdl:2440/107043. ISSN 0028-0836. PMID 28726833.