Uingereza

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Mwingereza)
Uingereza
England
English Flag English Coat of Arms
(Bendera ya Uingereza) (Nembo la Uingereza)
Wito (Kifaransa): Dieu et mon droit
("Mungu na haki yangu")
Uingereza katika Ulaya
Uingereza kwenye visiwa vya Britania
Mahali pa Uingereza (kijani cheusi) kwenye visiwa vya Britania ndani ya Ufalme wa Muungano (kijani nyeupe) pamoja na Jamhuri ya Eire (buluu) upande wa magharibi
Lugha Kiingereza
Mji Mkuu London
Mji Mkubwa London
Mfalme Charles III wa Uingereza
Waziri Mkuu Rishi Sunak
Eneo
– jumla

130,395 km²
Wakazi

2004
–sensa ya 2001
– Msongamano wa watu

50.1 millioni [1]

49,138,831 [2]
377/km²

Umoja wa nchi yote 927 BK na mfalme
Athelstan
Dini rasmi Church of England (Anglikana)
Pesa Pound sterling (£) (GBP)
Masaa UTC / (GMT)
Summer: UTC +1 (BST)
Ua la Taifa Waridi ya Tudor (nyekundu, nyeupe)
Mtakatifu wa kitaifa Mt George

Uingereza (pia: Ingilandi kutoka Kiingereza: England) ni nchi kubwa ndani ya Ufalme wa Muungano yenye wakazi milioni 50 (83% ya wakazi wote wa Ufalme) na eneo lake ni takriban km² 130,000 (theluthi mbili za kisiwa cha Britania).

Jina[hariri | hariri chanzo]

Katika lugha ya kila siku "Uingereza" hutaja mara nyingi Ufalme wote au kisiwa chote cha Britania. Lakini kwa usahihi "Uingereza" ni ile sehemu kubwa zaidi kusini mwa kisiwa, tofauti na nchi za Welisi (Wales, upande wa magharibi) na Uskoti (Scotland, upande wa kaskazini).

Mji Mkuu London

Asili ya jina la Kiswahili ni neno إنجليزي injilisi (matamshi ya Kimisri: ingilisi)" katika lugha ya Kiarabu; Waarabu walisikia jina "inglish" wakirahisisha matamshi kuwa "inglis", wakaongeza sauti fupi kati ya "g" na "l", hivyo kufikia kwa "ingilis" ambako "i" ya pili ni fupi kiasi cha kusikia pia "e" na hivyo ilipokewa na Waswahili. Kwa namna ya Kibantu sauti ya "l" ikawa "r": ingelesi kuwa ingereza.

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Mazingira ya vilima vya Devon, kusini-magharibi ya Uingereza

Uingereza iko kwenye kisiwa cha Britania ambacho ndicho kisiwa kikubwa cha Ulaya. Inapakana na Welisi upande wa magharibi na Uskoti upande wa kaskazini.

Upande wa magharibi iko Bahari ya Eire, na ng'ambo yake kisiwa cha Eire (Ireland). Upande wa mashariki iko Bahari ya Kaskazini, ng'ambo yake Denmark, Ujerumani na Uholanzi; upande wa kusini uko Mfereji wa Kiingereza halafu kusini-magharibi Bahari Atlantiki, ng'ambo yake Ufaransa na Ubelgiji. Tangu mwaka 1994 chini ya mfereji huo kuna njia ya reli kwa tobwe inayounganisha Uingereza na Ufaransa.

Uingereza ina visiwa vingi vidogo; kikubwa ni Isle of Wight katika kusini. Pwani zake ni ndefu, hakuna mahali palipo mbali zaidi ya km 113 kutoka baharini.

Sehemu kubwa ya nchi ni ama tambarare au vilima vidogo; mwinuko wa juu ni Scafell Pike yenye kimo cha mita 978. Kumbe milima mirefu ya Britania iko Welisi na Uskoti.

Tabianchi[hariri | hariri chanzo]

Tabianchi ya Uingereza inaathiriwa na mahali pake baharini inayopitiwa na Mkondo wa Ghuba na latitudo ya kaskazini. Athari hizo zinaleta tabianchi fufutende ya kibahari; kwa wastani baridi haishuki chini ya 0 °C na joto halipandi juu ya 32 °C. Hata hivyo vipindi vya jeledi au joto kali zaidi vinaweza kutokea kwa siku kadhaa. Miezi ya baridi ni Januari na Februari. Julai kwa kawaida ni mwezi wenye joto zaidi. Hali ya hewa mara nyingi ni nyevunyevu na mvua inaweza kutokea mwaka wote. Vipindi vya mvua na jua hubadilishana haraka.

Miji ya Uingereza[hariri | hariri chanzo]

Mji mkuu ni London. Kati ya miji mikubwa ya Uingereza ni: London (wakazi 9,787,426), Manchester (2,553,379), Birmingham (pamoja na West Midlands 2,440,986), Leeds (pamoja na West Yorkshire 1,777,934), Sheffield, Bradford na Liverpool.

Mito ya Uingereza[hariri | hariri chanzo]

Mto Thames katika London mnamo mwaka 1750
Makala kuu: Mito ya Uingereza

Kutokana na tabianchi yenye mvua ya kutosha kuna mito mingi nchini. Mito mirefu ni Thames (km 346) na Severn (km 350).

Mikoa ya Uingereza[hariri | hariri chanzo]

Makala kuu: Mikoa ya Uingereza

Kihistoria Uingereza iligawiwa katika kaunti (counties) na miji (boroughs).

Nchi yote imegawiwa leo katika mikoa (regions) 9. Mikoa kadhaa huwa na mamlaka fulani ya kiutawala, lakini si yote. Vinginevyo utawala wa kieneo kunatokea hasa kwenye ngazi ya kaunti na halmashauri ndani ya kila mkoa.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Uingereza ilikaliwa na makabila ya Wabritania wenye lugha za Kikelti na kuvamiwa na Dola la Roma katika karne ya 2 BK. Ikawa sehemu ya Dola la Roma hadi karne ya 5 BK. Wakati ule Waroma walipaswa kuondoa wanajeshi wao kisiwani kwa ajili ya ulinzi wa nchi za bara.

Uvamizi wa Waanglia-Saksoni[hariri | hariri chanzo]

Katika karne za 5 na 6 BK makabila ya Kigermanik walivamia kisiwa hasa Wasaksoni, Waangli na Wadenmark. Walileta lugha zao za Kigermanik zilizochukua nafasi ya lugha ya Wabritania.

Wabritania na Waroma waliokuwa wamebaki walihamia maeneo ya kando kama Welisi au Cornwall au kuvuka mfereji wa Uingereza kwenda Britania Ndogo (Kiingereza: Brittany; Kifaransa: Bretagne).

Karne zilizofuata kisiwa kiliona madola madogo na hali ya vita. Mwaka 937 Mfalme Athelstan aliweza kuunganisha karibu eneo lote la Uingereza ya leo.

Uvamizi wa Wanormani[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1066 wanajeshi Wanormani kutoka kaskazini mwa Ufaransa walivamia Uingereza na kuiteka yote chini ya mtemi William Mshindi. Wavamizi walitawala wakitumia aina ya Kifaransa. Lugha zote mbili za wananchi na za mabwana ziliendelea pamoja sambamba hadi kuwa lugha moja cha Kiingereza.

Ufalme wa Muungano[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka 1601 mfalme James VI wa Uskoti alichaguliwa kuwa mfalme wa Uingereza pia. Nchi jirani zote mbili ziliendelea na wafalme wa pamoja hadi mwaka 1707. Mwaka ule Uingereza pamoja na Welisi na Uskoti ziliunganishwa kuwa Ufalme wa Muungano wa Britania.

Tangu mwaka 1801 jina likawa Ufalme wa Muungano wa Britania na Eire (United Kingdom of Great Britain and Ireland) hadi 1927 wakati sehemu kubwa ya Eire ikapata uhuru wake. Tangu hapo Uingereza ni sehemu ya Ufalme wa Muungano wa Britania na Eire ya Kaskazini (United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland).

Mji wa Liverpool

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Office for National Statistics - UK population approaches 60 million
  2. Office for National Statistics - 2001 census Population profile - England.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]