Peter Damian

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Petro Damiani amechorwa chini kulia.

Petro Damiani (Ravenna, Italia, 1007Faenza, Italia, 21 Februari 1072) alikuwa mmonaki wa urekebisho wa Wabenedikto wakaapweke wa Camaldoli nchini Italia.

Mmonaki halisi na mwenye msimamo pengine mkali, alitoa ushuhuda wazi wa umuhimu wa kumpa Mungu nafasi ya kwanza na kulenga utakatifu bila kupatana na uovu hata kidogo.

Aliwarudisha wamonaki kwenye madai ya maisha ya sala, waklero kwenye maadili safi na waumini wote kwenye umoja na Papa.

Kutokana na juhudi zake kubwa kwa urekebisho wa Kanisa lote ulioanzishwa na Mapapa wa wakati wake mgumu, alifanywa kardinali askofu na kuwa kati ya watu muhimu zaidi wa karne XI. Athari yake inadumu hata leo katika Kanisa Katoliki.

Tangu zamani ametambuliwa kuwa mtakatifu.

Mwaka 1828 Papa Leo XII alimuongezea sifa ya mwalimu wa Kanisa.

Sikukuu yake inaadhimishwa kila mwaka tarehe 21 Februari[1].

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Opera omnia, 1743

Utoto na ujana (1007-1022)[hariri | hariri chanzo]

Petro Damiani alizaliwa mwaka 1007 mjini Ravenna nchini Italia katika familia ambayo iliwahi kuwa maarufu, lakini baadaye ikawa na hali duni kidogo.

Alikuwa wa mwisho kati ya ndugu 7: mkubwa wao aliiitwa Damian, ambaye baadaye akawa padri na mmonaki.

Alibaki yatima mapema, akalelewa na wakubwa wake, hasa dada Roselinda na Damian aliyemfanya mwanae. Kama shukrani kwake akajiongezea jina la Damiani, yaani wa Damian.

Masomo (1022-1032)[hariri | hariri chanzo]

Damian alijitahidi kumsomesha mdogo wake huko Ravenna, halafu Faenza, alipobaki tangu mwaka 1022 hadi 1025. Baadaye Petro alihamia Parma ili kusoma lugha ya Kilatini, aliyoimudu vizuri sana, na sayansi za jamii (1026-1032).

Ualimu (1032-1035)[hariri | hariri chanzo]

Kisha kuhitimu masomo yake alianza kazi ya ualimu, halafu akarudi Ravenna akafundisha kwa miaka mitatu, iliyotosha kumpatia umaarufu, wanafunzi wengi na pesa. Inawezekana kwamba kwa wakati huo ameshaingia ukleri kwa daraja ndogo au hata ushemasi. Upadrisho alipewa na askofu mkuu Gebeardo wa Eichstätt (1027-1044).

Wito wa kimonaki (1035)[hariri | hariri chanzo]

Wakati alipoendelea na ualimu, alizidi kuvutiwa na umonaki akaanza kutimiza desturi kadhaa za kitawa (kukesha, kufunga n.k.) akizidi kujitenga na ulimwengu na kuzama katika sala.

Uamuzi wa kubadili maisha ulifikiwa alipotambua anajipendea bado kwa sababu akiwa mezani na kipofu alimpa mkate wa kifukara kuliko ule aliojipatia.

Basi, baada ya kukutana na wakaapweke wawili wa Fonte Avellana, palipokuwepo monasteri maarufu iliyoanzishwa na mtakatifu Romwald miaka michache ya nyuma, akawafuata aishi upwekeni huko, kulipokuwa na hali ngumu kabisa.

Monasteri hiyo ilikuwa wakfu kwa Msalaba mtakatifu, fumbo alilolipenda kuliko yote, hata akajiita “Petro, mtumishi wa watumishi wa msalaba wa Kristo”. Alisema, “Wasiopenda msalaba wa Kristo, hawampendi Kristo”.

Baadaye alipaswa kwenda kuhubiria watu na kurekebisha monasteri mbalimbali. Ili aweze kurekebisha wengine, hakuacha kujirekebisha kwa maisha ya uadilifu.

Mmonaki huko Fonte Avellana (1035-1043)[hariri | hariri chanzo]

Monasteri ya Fonte Avellana.

Huko Fonte Avellana aliombwa awafundishe na kuwalea Wakamaldoli wenzake, kazi aliyoendelea nayo hata katika Abasia ya Pomposa (1040 - 1042), akijitahidi kukomaza roho zao.

Mwaka 1042 priori wa Fonte Avellana alimtuma kurekebisha monasteri ya Mt. Vinsenti huko Furlo (karibu na Urbino), ambako aliandika maisha ya mtakatifu Romwald.

Priori wa Fonte Avellana (1043-1057)[hariri | hariri chanzo]

Mwishoni mwa mwaka 1043 alirudi Fonte Avellana, akachaguliwa kuwa priori wa jumuiya hiyo yenye wamonaki 20 hivi, kazi aliyoifanya kwa miaka 14, akihimiza uzingatifu wa upweke hapo na katika sehemu nyingine za Italia.

Wakati huo mgumu aliwasaidia Mapapa kwa maandishi yake, pia alichangia kulirekebisha Kanisa pamoja na mmonaki mwingine, Ildebrando wa Soana (ambaye baadaye akawa Papa Gregori VII).

Sura ya Kanisa kama “Bibiarusi wa Kristo” aliyoichora vizuri katika maandishi yake haikulingana na hali halisi. Ndiyo sababu hakusita kulaumu upotovu wa wamonaki na wakleri, hasa kutokana na desturi ya vyeo vya kidini kutolewa na watawala wa kisiasa.

Kwa ajili hiyo alitembelea majimbo mbalimbali ya Italia akionya maaskofu na hata kumfanya Papa awaondoe madarakani baadhi yao.

Alikwenda pia Ujerumani mara kadhaa kama mgeni wa Kaisari.

Alihudhuria sinodi za Roma za miaka 1047, 1049, 1050, 1051 na 1053 kuhusu dhambi ya usimoni, akafaulu hasa kwa kupitisha sheria ya kuwa Papa achaguliwe na makardinali tu, bila kuingiliwa na viongozi wa siasa wala watu wengine.

Mwaka 1049 aliandika Liber gomorrhianus kuhusu aina za uasherati dhidi ya maumbile.

Chini ya Papa Leo IX (1049-1054) na waandamizi wake Papa Stefano IX, Papa Nikolasi II na Papa Aleksanda II upana wa juhudi zake uliongezeka tena, akafanywa pia priori wa Ocri.

Askofu wa Ostia na mshauri wa Papa (kuanzia 1057)[hariri | hariri chanzo]

Hatimaye mwaka 1057 alifanywa na Papa Stefano IX kuwa kardinali askofu wa Ostia awe mshauri wake wa karibu kabisa (alipewa uaskofu mwaka 1058).

Petro Damiani hakufurahia uteuzi huo, kwa jinsi alivyojisikia wito wa kuishi upwekeni, lakini akatii na kuhamia Roma.

Mrekebishaji[hariri | hariri chanzo]

Akitumwa na Papa sehemu mbalimbali za Italia na Ufaransa, Petro Damiani alistawisha urekebisho hasa kwa:

  • kupambana na serikali zilizojiingiza katika uteuzi wa viongozi wa Kanisa, tena mara nyingi kwa njia ya rushwa;
  • kusisitiza mamlaka ya juu ya Papa, kiini cha miundo ya Kanisa;
  • kurudisha elimu na maadili katika maisha ya mapadri, akiwaelekeza kufuata mifano ya wamonaki.

Kurudia monasterini na miaka ya mwisho[hariri | hariri chanzo]

Petro Damiani alimuomba mara kadhaa Papa amruhusu kurudi upwekeni.

Baada ya miaka 10 alikubaliwa arejee Fonte Avellana 1067 na kuacha vyeo vyake vyote.

Kumbe miaka miwili baadaye akatumwa tena Frankfurt, Ujerumani (1069) ili kujaribu kumzuia Kaisari Henri IV asimpe talaka mke wake Bertha.

Mwaka 1071 alikwenda Montecassino ili kutabaruku kanisa la abasia hiyo.

Mwanzoni mwa mwaka uliofuata alirudi Ravenna ili kuleta amani ndani ya Kanisa baada ya Papa kukataza ibada zote ili kumuadhibu askofu mkuu wa huko aliyemuunga mkono Antipapa.

Akiwa njiani kurudi, ugonjwa wa ghafla ulimlazimisha kusimama katika monasteri ya Santa Maria Vecchia Fuori Porta karibu na Faenza ambapo alifariki usiku wa tarehe 22 Februari 1072.

Mara baada ya kifo chake alianza kuheshimiwa kama mtakatifu kwa jinsi alivyotumia nguvu zake zote, za kiroho na za kimwili, kwa Kristo na Kanisa, akibaki kujiona daima “Petro, mtumishi wa mwisho wa wamonaki”.

Mafundisho[hariri | hariri chanzo]

Aliandika vitabu muhimu vya aina mbalimbali vilivyoenea sana kuhusu liturujia, teolojia na maadilidini, mbali ya maisha ya Mt. Romwald, kanuni kwa ukaapweke, barua, hotuba na sala. Ndiye mwandishi bora wa karne XI.

Katika kanuni hiyo alisisitiza nidhamu ya mkaapweke ambaye, katika kimya cha ugo ana wito wa kuishi usiku na mchana katika sala, akifunga chakula vikali na kirefu; lakini pia anapaswa kutekeleza kwa bidii upendo wa kidugu kwa kumtii priori mara na kwa moyo wote.

Akisoma na kutafakari kila siku Maandiko matakatifu, Petro alitambua maana ya fumbo ya Neno la Mungu na kukuta humo lishe yake ya Kiroho. Kuhusu jambo hilo alifananisha chumba cha mkaapweke na “sebule ambamo Mungu anaongea na watu”.

Kwake, ukaapweke ni kilele cha maisha ya Kikristo, “hali bora” kwa kuwa mmonaki, kisha kupata uhuru kutoka vifungo vya maisha ya kidunia na vya nafsi yake mwenyewe, anapokea “mahari kutoka kwa Roho Mtakatifu na roho yake yenye heri inakuwa imeunganika na Bwanaarusi wake wa kimbingu”.

Mtu wa sala hasa, Petro alikuwa pia mwanateolojia safi: fikra zake juu ya mada mbalimbali zilimuongoza kwenye hatima muhimu. Kwa mfano, alifafanua imani kuhusu Utatu mtakatifu kwa namna wazi na hai.

Uchunguzi wa kitaalamu wa fumbo hilo ulimfanya azame katika maisha ya ndani ya Mungu kama mzunguko wa upendo kati ya Nafsi zake tatu, halafu ahitimishe na maadili kwa maisha ya kijumuia na kwa mahusiano kati ya Wakristo wa Mashariki na wa Magharibi waliotenganika kuhusu mada hiyo.

Vilevile tafakuri yake juu ya Kristo ina athari za maana kwa maisha ya kila siku, kwa kuwa ndiye kiini cha Maandiko yote, hivyo anatakiwa kuwa kiini cha maisha ya mmonaki ili “Kristo aweze kusikika katika maneno yetu, Kristo aweze kuonekana katika maisha yetu, naye aweze kuhisika katika mioyo yetu”. Muungano wa dhati na Kristo unawapasa pia wale wote waliobatizwa, ambao wasizamie kabisa shughuli zao, matatizo na mahangaiko yao ya kila siku hata kusahau kwamba Yesu anatakiwa kuwa kweli kiini cha yote.

Jinsi alivyopenda uzuri, alitazama ulimwengu wote kama msanii, akivumbua ndani yake mifano mingi sana ya maisha ya Kiroho na ya umungu. Kwa nadra vinapatikana vitabu vya kupendeza na kusisimua kama vya kwake.

Kwa ajili hiyo na kwa mchango wake katika urekebisho wa Kanisa, Papa Leo XII alimtangaza mwalimu wa Kanisa mwaka 1828.

Maandishi[hariri | hariri chanzo]

Vita Beati Romualdi
  • Vita beati Romualdi
  • Liber Gratissimus
  • Disceptatio Synodalis
  • Liber Gomorrhianus
  • De sancta simplicitate
  • De divina omnipotentia
  • Dominus vobiscum

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Vyanzo[hariri | hariri chanzo]

  • Berger, David, "St. Peter Damian. His Attitude Toward the Jews and the Old Testament," The Yavneh Review, 4 (1965) 80-112.
  • Owen J. Blum, "The Monitor of the Popes: St. Peter Damian," in Studi Gregoriani vol. 2 (1947), pp 459–76.
  • John Boswell, Christianity, Social Tolerance, and Homosexuality Chicago (1980).
  • Pierre J. Payer, 1962. Book of Gomorrah : An Eleventh-Century Treatise against Clerical Homosexual Practices, Waterloo, Ontario: Wilfrid Laurier University Press.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]