Roho Mtakatifu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Roho Mtakatifu akionekana kama njiwa, katika Basilika la Mt. Petro, Vatikano. Kazi ya Gian Lorenzo Bernini.

Roho Mtakatifu katika mapokeo ya dini ya Israeli, Ukristo na Uislamu ni roho ya Mungu pekee.

Kwa madhehebu karibu yote ya Kikristo, Roho Mtakatifu ni upendo wa Mungu, nafsi ya tatu ya Utatu Mtakatifu, mwenye Umungu mmoja na Baba na Mwana. “Pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi” (Rom 5:5). Ametumwa kwetu atufanyie kazi pasipo kuonekana. “Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho” (Yoh 3:8). “Wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu” (Rom 8:14).

Hata hivyo, tofauti katika teolojia ya madhehebu hayo kuhusu Roho Mtakatifu ni kubwa kuliko zile zilizopo kuhusu Nafsi mbili za kwanza (Mungu Baba na Mungu Mwana)[1].

Kwa jumla Roho Mtakatifu anasadikiwa kuvuviwa milele na Baba kwa njia ya Mwana awe mwalimu wa wanadamu kwa kuwafundisha, kuwakumbusha na kuwazuia kufanya mambo mabaya au dhambi.

Kazi zote za Roho Mtakatifu zinahusiana na Yesu na kulenga hasa kuandaa watu wampokee, wamfuate na kumshuhudia katika umoja wa kundi lake, Kanisa. “Ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia” (Yoh 15:26-27).

Jina[hariri | hariri chanzo]

Kwa Kiebrania רוח ("ruah") ni jina la kike linalomaanisha roho, lakini pia upepo, pumzi. "Roho Mtakatifu" ni רוח הקודש, "ruah hakodesh".

Vilevile kwa Kigiriki neno ni "πνευμα" ("Pneuma"; kutokana na "πνεω", "pneō", yaani "kupumua/kupuliza/kuwa hai").

Kwa Wayahudi jina hilo linataja Nguvu za Mungu zinazoweza kujaza watu (kwa mfano manabii.

Wazo hilo lilistawishwa na Waeseni, halafu na Yohane Mbatizaji na hasa Yesu Kristo.

Mifano[hariri | hariri chanzo]

Kwa kuwa Nafsi ya tatu ni fumbo gumu kueleweka kuliko mengine, Biblia inamfananisha na vitu mbalimbali: maji, mpako, moto, wingu, mwanga, mhuri, mkono, kidole, njiwa.

Katika Agano la Kale[hariri | hariri chanzo]

Tangu ukurasa wa kwanza wa Biblia ya Kiebrania uwepo wa Roho wa Mungu unatajwa kuhusu uumbaji wa ulimwengu, kwamba alitua juu ya maji (Mwa 1:2).

Katika Agano Jipya[hariri | hariri chanzo]

Humo Roho Mtakatifu anafunuliwa na Yesu kikamilifu.

Ni hasa Injili ya Yohane (7:37-39; 14:16-17; 14:26; 15:7,26) inayomtambulisha kama παρακλητος, (kwa Kigiriki, paracletos), yaani Nafsi ambaye baada ya Yesu kupaa mbinguni anafariji/anatetea/anasimamia waamini badala yake.

Lakini hata Injili Ndugu, hasa Injili ya Luka, zinaonyesha uhusiano wa Roho Mtakatifu na Kristo tangu mwanzo wa maisha yake, yaani kuanzia umwilisho (Mt 1:18; Lk 1:34-35), kwa kupitia ubatizo (Mt 3:13-17; Mk 1:9-11; Lk 3:21-22; Yoh 1:31-33), miujiza (Mt 12:15-21; Mt 12:28; Mk 3:22-30) hadi kifo cha msalabani (Mt 27:50; Mk 15:37; Lk 23:46; Yoh 19:30).

Baada ya Yesu kumtoa kwa Bikira Maria, Mtume Yohane na wengineo wakati wa kufa na baada ya yeye kuwavuvia mitume wake jioni ya Jumapili ya ufufuko (Aprili 30 au 33), Roho Mtakatifu alidhihirika kwa kishindo kwenye Pentekoste ya mwaka ule (Mdo 2:1-11), haohao na wengineo walipokuwa wakimngojea wakisali kwa umoja.

Hapo Mtume Petro na wenzake walianza kutangaza habari njema kwa watu wa lugha mbalimbali waliokuwa Yerusalemu ama kama wakazi ama kwa ajili ya hija.

Roho Mtakatifu kama Paji lisiloumbwa[hariri | hariri chanzo]

Neema inayotia utakatifu, ambayo ni zawadi iliyoumbwa, inapita tayari vipawa vyovyote vya kibinadamu (k.mf. ubunifu, akili na utashi) hata kama ni vikubwa namna gani. Neema hiyo inapita pia umbile la malaika na karama za nje (k.mf. kutenda miujiza). Zaidi tena basi, Roho Mtakatifu kama paji lisiloumbwa linapita kiwango chochote cha upendo na cha utukufu.

Kwanza ni paji lisiloumbwa kama tunda la mwisho na la milele la uzima wa Mungu Baba na Mwana. Baba, aliye mwema pasipo mipaka, kwa kumzaa milele Neno anamshirikisha umungu wake wote, awe Mungu aliyetoka kwa Mungu, mwanga kwa mwanga. Baba, akiwa na Mwana, anatokwa na Upendo-nafsi aliye Roho Mtakatifu. Hivyo Nafsi ya tatu ya Mungu inatokana na upendano wa Baba na Mwana; ni paji lisiloumbwa ambalo hao wawili wanatoleana, paji pekee linalotokana na uvuvio wa milele ambao unamshirikisha Roho Mtakatifu umungu wote. Roho Mtakatifu anaitwa Paji-nafsi kwa sababu, ikiwa kila zawadi inatolewa bure kwa msingi wa upendo, kitu cha kwanza tunachokitoa zawadi ni upendo ambao tunamtakia fulani mema.

Hilo paji kuu, ambalo Nafsi mbili za kwanza zinatoleana milele, limetolewa kwetu pia katika historia. Kisha kutujalia ekaristi katika karamu ya mwisho na kutumwagia damu yake azizi msalabani; kisha kutujalia neema kwa njia ya sakramenti zote, Bwana alipenda kutuvuvia Paji kuu akamilishe fadhili zake zote. Mwokozi alitustahilia matokeo yote ya uteule wetu: wito wa kuishi Kikristo, uongofu na utakaso, kufa katika urafiki na Mungu na utukufu wa waliokombolewa kwa damu yake; zaidi ya hayo akapenda kutujalia paji lisiloumbwa, yaani Roho Mtakatifu. Ndiye anayefariji katika huzuni za maisha, katika mahangaiko yanayoweza yakafikia hali ya mafadhaiko. Ndivyo alivyowafariji mitume walipoondolewa uwepo wa Bwana kimwili na walipokabili ugumu mkubwa wa kuanza kazi yao. Walipompokea waliangazwa, waliimarishwa, walidumishwa katika neema na kugeuzwa; hivyo chini ya uongozi wake wakawa waaminifu hadi kufia dini. Pentekoste inafanyika upya kwa kila Mkristo siku ya kipaimara.

Kazi ya paji lisiloumbwa ndani mwetu[hariri | hariri chanzo]

Tumepokea kweli paji kuu na tunaweza kulifurahia kwa njia ya upendo na ya kipaji cha hekima, ambavyo unatokea ujuzi unaofanana na mang’amuzi kuhusu uwemo ndani mwetu wa Nafsi za Kimungu zisizotenganika kamwe. Inafaa tusisitize matokeo makuu ambayo tunamsifu hasa Roho Mtakatifu, ingawa yanasababishwa na Baba na Mwana pia, kama tokeo lolote la uweza wa Kimungu ambao ni wa Nafsi tatu pamoja.

Kwanza paji lisiloumbwa linathibitisha, linadumisha na kukuza ndani mwetu zawadi iliyoumbwa ya neema inayotia utakatifu, “maji yaliyo hai… yakibubujikia uzima wa milele” (Yoh 4:10-14). Kinyume cha maji ya birika au mtaro, maji hai hayatenganiki na chemchemi na kwa msukumo wake yanatiririkia daima bahari. Vivyo hivyo neema inayotia utakatifu haitenganiki na chemchemi ya Roho Mtakatifu: ndiye anayeidumisha ndani mwetu na kuisukuma ielekee bahari ya uzima wa milele. “Pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi” (Rom 5:5).

Kwa hiyo pengine anampatia mtu aliyekamilika hakika fulani kuhusu hali yake ya kuwa na neema hiyo: “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu” (Rom 8:16). Anatoa ushahidi huo kwa njia ya upendo wa kitoto ambao anausababisha ndani mwetu na hivyo kutufanya tumsikie kama uhai wa maisha yetu. Hata hivyo hakika hiyo ya muda si ya wazi, kwa kuwa hatuwezi kutofautisha kikamilifu huo upendo wa kitoto unaotokana na Roho Mtakatifu na tendo la kibinadamu tu la kumpenda Mungu kwa namna isiyozaa matunda.

Mwanga wa Roho Mtakatifu haufikiwi bali unaonekana giza kwetu kwa jinsi ulivyo mkali; ila uvuvio wake unaimarisha imani yetu na kuifanya ipenye na kunogewa. “Sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu” (1Kor 2:12). Kutokana na hayo Roho Mtakatifu anathibitisha pia hakika ya tumaini letu, ambayo si bado hakika ya kufikia wokovu, bali ni hakika ya kuuelekea ambayo inaongezeka kadiri tunavyokaribia mwisho wa safari. Hatimaye na hasa Roho Mtakatifu, akiwa ndiye Upendo-nafsi, anachochea katika waliokamilika upendo wa kumiminiwa kwa Mungu na kwa jirani ulio tofauti na mapendo mengine. Ni upendo tusioweza kuufikia kwa msaada wa neema za kawaida; unahitaji uvuvio maalumu, yaani neema inayotenda iliyo ya juu zaidi, ambapo Roho Mtakatifu anatokeza moyoni mwetu upendo huo ambao yeye ni kwa pamoja mwanzo na mwisho wake. Hatutaweza kamwe kumpenda Mungu kama anavyotupenda kwa upendo usioumbwa na wa milele; hata hivyo kati yake na sisi kuna usawa fulani wa upendo Roho Mtakatifu anapotokeza ndani mwetu upendo wa kumiminiwa ambao anautakasa na kuuimarisha hadi kuingia mbinguni.

Bwana alimuambia Katerina wa Siena, “Ndani ya waliokamilika Roho Mtakatifu analia machozi ya moto” hasa akiona dhambi zinazopeleka watu kwenye maangamizi; mara nyingi machozi hayo ya Kiroho yanajaliwa madhambi makubwa yasamehewe. Ndiyo sababu anaitwa Baba wa maskini, hasa wa wale wanaopenda ufukara mtakatifu. “Roho Mtakatifu anamlisha mwadilifu, anamlevya kwa utamu, anamjaza utajiri usiopimika… hapo mtu anakubali huzuni zote, hakuna cha kumkatisha tamaa, hakuna cha kumtikisa: anapokea nguvu kubwa na kuanza kuonja uzima wa milele” (Katerina wa Siena). “Watakatifu wanahisi ndani mwao kama utupu usio na mipaka, ambao viumbe vyote haviwezi kuujaza na ambao unaweza kujazwa tu na hali ya kumfurahia Mungu. Walipotenganika naye wanasikitika na kuteseka kama kwa kifodini cha muda mrefu, ambacho wasingekivumilia pasipo faraja ambazo Roho Mtakatifu anawapatia mara kadhaa” (Alois Lallemant).

Yeye anawatia upendo kwa msalaba, yaani kwa Yesu msulubiwa, kwa mateso yake, kwa kuangamia kwake kitakatifu; anawapa hamu ya kuushiriki kadiri ya maongozi ya Mungu, na katika hamu hiyo anawafanya waone amani, nguvu na pengine hata furaha. Anawalinganisha na msulubiwa, akiokoa watu kwa njia yao na ya mateso yao. Anawaelewesha thamani ya miangaza yake ya Kimungu ambayo isipopingwa inafikishia utakatifu halisi. Hapo inazidi kueleweka jinsi matokeo ya kujiweka wakfu kwake yanavyoweza kuwa makubwa. Hatimaye anaweza akawapa waliokamilika zaidi hakika fulani ya uteule wao, kwa ufunuo wa pekee au neema inayolingana nao, akiwajalia mwonjo wa uzima wa milele ambao wanang’amua neema inayotia utakatifu kama mbegu ya utukufu.

Vipaji vya Roho Mtakatifu[hariri | hariri chanzo]

Mapokeo ya Kikristo, yakitumia Isa 11:2, yanaorodhesha vipaji saba vinavyoombwa hasa wakati wa kipaimara: hekima, akili, shauri, nguvu, elimu, ibada na uchaji wa Mungu.

Kwa vipaji hivyo Roho Mtakatifu anamuongoza kila mmoja katika safari ya kumfuata Kristo hadi kuchuma yale yanayoitwa na Mtume Paulo matunda ya Roho Mtakatifu: "upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi" (Gal 5:22).

Tofauti na vipaji na matunda ni karama mbalimbali ambazo Roho Mtakatifu anazigawa anavyotaka kwa ujenzi wa Kanisa: karama yoyote si ya lazima kwa wokovu wa mtu, wala hailengi kwanza utakatifu wake, bali faida ya wengine, hasa kupitia umoja wa Kanisa ambao anausababisha kwa kutia upendo mioyoni mwa waamini na kwa njia ya sakramenti, hasa ekaristi, mkate wa uzima.

Roho Mtakatifu, kupitia vipaji vyake hivyo, ndiye asili ya maisha yetu ya sala na ya utendaji. “Vipaji saba vinafungamana na upendo; kwa hiyo, sawa na maadili ya kumiminiwa, vinakua pamoja na upendo, kama viungo vya mwili mmoja, au kama vidole vitano vya mkono mmoja” (Thoma wa Akwino) au kama mabawa yanayokua pamoja na ndege. Lakini marudio ya dhambi nyepesi yanavifunga, hata tukaja kupima mambo kwa aina ya upofu iliyo kinyume cha sala ya kumiminiwa.

Uvuvio wake maalumu, ambao vipaji vinatuandaa kuupokea, ni tofauti na neema ya msaada ya kawaida inayotusukuma kutekeleza maadili. Neema inayotusaidia kutenda, ambayo tunatenda toka ndani, ni tofauti na neema inayotenda, ambayo tunatenda kwa kukubali tu msukumo wa Roho Mtakatifu. Katika ile ya kwanza utendaji wetu unazidi, kumbe katika ile ya pili utendaji wake ndani mwetu ndio unaozidi.

Usikivu kwa Roho Mtakatifu unafanana na ule wa mtiifu kamili anayepokea mara kwa hiari na stahili agizo la kiongozi wake, bila kufikiria na kuamua kwanza afanye nini. Kiongozi anatenda kwa njia yake, ila mwenyewe ana stahili za utiifu, unaozidisha nguvu zake, kwa kuwa akitii hadanganyiki wala hakataliwi neema anazohitaji atekeleze agizo.

Kwa uvuvio huo inatokea pia kwamba vipaji vinatumika pamoja na kazi ya maadili kufanyika: hapo ni kama upepo mzuri unaorahisisha kazi ngumu ya wapigakasia. Kwa mfano, uvuvio unaweza ukatukumbusha Injili wakati akili yetu inapofikiria la kufanya; kumbe pengine busara inajitambua haiwezi kutatua tatizo kubwa la dhamiri, hivyo inatuongoza kumuomba Roho Mtakatifu ambaye uvuvio wake unatufanya tuone na kutenda yanayofaa. Basi, tunapaswa kuwa wasikivu zaidi na zaidi kwake.

Mpangilio wa vipaji kuanzia chini[hariri | hariri chanzo]

Aina za uvuvio ni mbalimbali, tunavyoona katika orodha ya Isaya ambamo vipaji vimepangwa kuanzia juu, yaani kuanzia kile cha hekima kinachoongoza vingine vyote. Wimbo huo wa zamani uliojaa utamu unafanana na noti saba za muziki zilizopangwa vizuri.

1. Kipaji cha uchaji ni cha kwanza kudhihirisha athari ya Roho Mtakatifu kwa mtu aliyeongoka. Kinafidia upungufu wa adili la kiasi na kumsaidia apambane na mivuto ya anasa na ya moyo. Uchaji huo mtakatifu ni kinyume cha kuogopa watu, tena ni bora kuliko hofu ya kitumwa inayomsaidia mkosefu atubu kwa kuogopa adhabu za Mungu. Kipaji cha uchaji kinaogopa dhambi kuliko adhabu zake. Pengine mtu anauhisi kwa nguvu isiyoweza kusababishwa na tafakuri wala somo lolote, isipokuwa na Roho Mtakatifu ndani mwake. Mbinguni watakatifu hawaogopi tena kumchukiza Mungu, ila wanatetemeka pamoja na malaika wakiuheshimu ukuu wake; hata katika roho ya Yesu hisi hiyo ilikuwemo na bado imo. Uchaji huo, uliosababisha malipizi makubwa ya watakatifu, unahusiana na heri ya maskini ambao kwa kumcha Mungu wanabandukana na anasa na heshima za dunia.

2. Kwa namna fulani uchaji una elekeo hasi maana unatufanya tukwepe dhambi; lakini mtu anahitaji kumuelekea zaidi Mungu kama mwana. Kipaji cha ibada ndicho kinachotutia upendo wa namna hiyo kwa Baba wa mbinguni, halafu kwa Yesu, bikira Maria na watakatifu wanaotulinda. Kipaji hicho kinafidia upungufu wa adili la ibada linalompatia Mungu heshima inayotakiwa. Hakuna juhudi ya Kiroho inayodumu pasipo kipaji hicho kinachotuzuia tusiishie faraja za kihisi katika sala, bali tufaidike na huzuni na ukavu vinavyokusudiwa kutufanya wa Kiroho zaidi. “Mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, ‘Aba!’ yaani, ‘Baba!’… Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa” (Rom 8:15,26). Kipaji hicho kinatuonjesha ladha ipitayo maumbile hata katika tabu za ndani; kinajitokeza hasa katika sala ya utulivu, ambamo utashi unatekwa na mvuto wa Mungu, ingawa mara nyingi akili inalazimika kupambana na mitawanyiko ya mawazo. Kwa utamu wake kinatufanya tufanane na Kristo mpole na mnyenyekevu wa moyo, na kinaleta heri ya wapole watakaorithi nchi ya walio hai.

3. Lakini ili tuwe na ibada imara, ambayo inakwepa udanganyifu na kutawala ubunifu na miguso, tunahitaji kipaji cha juu zaidi, kile cha elimu. Hicho kinatuandaa kupokea mwanga bora kuliko ule wa elimudunia na wa teolojia. Ni kama hisi ipitayo maumbile ambayo tunapima vizuri mambo ya kibinadamu kadiri yanavyoashiria yale ya Kimungu au yanavyopingana nayo. Kwa kipaji hicho baadhi wanaona hasa vitu vinavyoonekana kama alama za visivyoonekana; baadhi wanaona hasa ubatili wa viumbe na wa yote yapitayo (k.mf. vyeo na sifa), pamoja na ubaya usio na mipaka wa dhambi ya mauti. Kwa kuonyesha uovu huo kipaji cha elimu kinatufanya tusiogope tu dhambi, bali tutishwe nayo na kuihuzunikia sana. Kinatufahamisha pia jinsi malimwengu yasivyotokana na Mungu tu, bali na sababu zenye kasoro (katika hilo kinatofautiana na hekima). Kinaleta ujuzi halisi wa mema na mabaya, si kama Adamu na Eva waliodanganywa na Ibilisi wakapata elimu chungu ya kung’amua uasi wao na matokeo yake. Tukimfuata Roho Mtakatifu tunakuja kufanana na Mungu anayejua maovu ili kuyachukia na maadili ili kuyatimiza. Mara nyingi elimudunia inavimbisha; kinyume chake kipaji cha elimu kinaimarisha tumaini kwa kutuonyesha udhaifu wa msaada wowote wa kibinadamu na ubatili wa malimwengu, na kwa kutuhimiza tutamani kwenda mbinguni kwa kumtegemea Mungu tu. Kinahusiana na heri ya machozi ya majuto na kutupa msimamo mzuri kati ya kutegemea mema bure na kutazamia mabaya tu hata kukata tamaa. Elimu hiyo ya thamani ilikuwa nao wote waliofanya utume mkubwa, k.mf. Dominiko Guzman aliyelia mara nyingi akiona hali ya watu aliowahubiria.

4. Juu kuliko elimu kipo kipaji cha nguvu, kwa kuwa haitoshi tupambanue mema na mabaya, bali ni lazima tuepe ya kwanza na kutimiza ya pili kwa udumifu. Tunapaswa kupiga vita vikali dhidi ya mwili, ulimwengu na shetani, maadui hatari kwa uovu, ujanja na uwezo. Tukiogopa vicheko vya watu na maneno yao tutatekwa na yule anayejitahidi kutupoteza kadiri tulivyo na wito bora. “Mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama, bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama” (Ef 6:10-13). Kipaji cha nguvu kinainua moyo wetu katika hatari na kusaidia subira yetu katika majaribu marefu. Kiliwategemeza wafiadini kikiwatia udumifu usioshindika hata watoto na mabikira. Kinahusiana na heri ya wenye njaa na kiu ya haki wanaodumisha ari takatifu kati ya vipingamizi vingi.

5. Lakini katika nafasi ngumu, yanapotimizwa matendo bora ya kipaji cha nguvu, tunapaswa kukwepa ushupavu wa kilokole: kwa ajili hiyo tunahitaji kipaji cha juu zaidi, kile cha shauri. Hicho kinafidia upungufu wa busara, k.mf. inaposita ikijiuliza, Ni afadhali niendelee kuvumilia au nionyeshe msimamo? Katika shida za namna hiyo tumkimbilie Roho Mtakatifu anayeishi mwetu. Kipaji hicho hakitukatazi tusiombe shauri la viongozi wa nje na wa roho, bali kinatukinga dhidi ya kufuata silika bila kufikiri na dhidi ya utovu wa moyo; kinatujulisha pia yale ambayo viongozi hawawezi kutuambia, hasa namna ya kulinganisha maadili yanayoonekana kupingana. Pengine Roho Mtakatifu anatuonya tusiseme neno fulani; tukienda kinyume, mara nyingi litasababisha vurugu, hasira, upotevu wa muda mwingi, mambo yaliyokuwa rahisi kuyaepa. Madogomadogo ndiyo yanayokwamisha katika njia ya ukamilifu: k.mf. zoea fulani linalozuia ukusanyaji wa mawazo, unyenyekevu au heshima kwa wengine. Vipingamizi hivyo vinaondolewa na uvuvio wa kipaji cha shauri, kinachohusiana na heri ya wenye huruma, kwa kuwa hao ni washauri hodari wanaoacha kujijali ili wainue wenye huzuni na wakosefu.

6. Ni lazima tupande juu zaidi ili kipaji kingine kifidie upungufu wa imani. Ni kwamba adili hilo linafikia mafumbo ya Kimungu kwa njia ya matamko ya kinadharia tu, tena mengi; tungependa yajumlishwe na moja ambalo lituambie vizuri Mungu ni nani. Basi, kipaji cha akili kinatusaidia mwanga wa ndani unaotuwezesha kupenya mafumbo ya wokovu na kuhisi ukuu wake. Pasipo mwanga huo mara nyingi tunasikia mahubiri na kusoma vitabu vya dini tusielewe maana yake ya dhati. Maneno hayo tunayatunza kwa heshima katika kumbukumbu, lakini ukweli wake hautugusi, hauna mwanga zaidi, ni kama nyota ya mbali angani. Hapo maneno ya ulimwengu yanatushawishi kwa urahisi kwa kuwa hatulishwi vya kutosha na kweli hizo za Kimungu. Kinyume chake, mtu sahili aliyemsujudia Mungu ataelewa mafumbo yake, si kwa ajili ya kuyafafanua, bali kwa kuyaishi. Roho Mtakatifu ndiye anayemjalia ujuzi huo wenye kupenya na kuishi kweli za imani unaomwezesha kuchungulia uzuri mkubwa ajabu wa maneno ya Yesu. Ndiye anayemjalia kuelewa kwa ndani wito wake akimkinga na udanganyifu wowote. Kipaji hicho hakipatikani kwa kiasi kikubwa pasipo usafi mkubwa wa moyo na wa nia. Kinahusiana na heri ya wenye moyo safi, ambao kwanzia hapa duniani wanamuona Mungu kwa namna fulani katika Maandiko matakatifu, ambayo pengine yanakuja kung’aa kama kwa kupigiwa mstari wa mwanga.

7. Hatimaye, kipaji cha hekima ndicho cha juu kuliko vyote, kama vile upendo, unaohusiana nacho, ulivyo adili bora kuliko yote. Hicho kinaelekeza kupima mambo kuhusiana na Mungu, aliye asili na lengo kuu la yote, si tu teolojia inavyofanya, bali kwa uelekevu kwa mambo ya Mungu unaotokana na upendo. Kwa uvuvio wake Roho Mtakatifu anatumia uelekevu huo ili atuonyeshe uzuri, utakatifu na utimilifu mwangavu wa mafumbo ya wokovu, yanayoitikia matamanio yetu ya dhati na ya juu zaidi. Kumbe ni utovu wa hekima: kukwazwa na msalaba unaoendelea kuwepo katika maisha ya Kanisa; kutothamini vya kutosha sala, sakramenti na majaribu yanayovumiliwa kwa upendo; kujali mno elimudunia; kuchanganya upendo na urahisi wa kuruhusu maovu, au imani na msimamo mkali. Kipaji cha hekima, asili ya sala ya kumiminiwa inayoongoza utendaji, kinaonjesha wema wa Mungu na kuudhihirisha katika matukio yoyote, hata yaliyo machungu zaidi. Kinaonyesha uhusiano wa sababu na malengo, pamoja na mpangilio wa tunu, kwa kukumbusha kwamba si yote yanayong’aa ni dhahabu: kinyume chake, maajabu kadhaa ya neema yamefichika katika sura duni, kama ile ya Benedikto Yosefu Labre. Kinafanya watakatifu watazame kwa upendo maongozi ya Mungu wasifadhaishwe na giza lililomo, wakitambua amefichama humo. Kama vile nyuki anavyojua afyonze wapi katika maua, kipaji cha hekima kinaona wema wa Mungu katika mambo yote. Kinakumbusha kuwa “tata elfu haziundi shaka moja” (Yohane H. Newman) kabla hazijatikisa msingi wenyewe wa hakika. Hivyo magumu elfu katika ufafanuzi wa Biblia hayasababishi shaka yoyote kuhusu asili ya Kimungu ya Ukristo. Basi, hekima inatia amani kubwa, yaani utulivu wa utaratibu wa mambo yaliyotazamwa upande wa Mungu. Ndiyo sababu inahusiana na heri ya wapatanishi ambao wanatunza amani hata wengine wanapofadhaika, na ambao wanaweza kuwatia amani waliovunjika moyo. Ni dalili mojawapo ya kuungana na Mungu.

Wengi, ambao waliishi katika neema inayotia utakatifu na walipokea ekaristi miaka mingi, hawaonyeshi vipaji vya Roho Mtakatifu katika mwenendo wao, bali wana uchu wa sifa, wanachukizwa na neno dogo na kuishi kibinadamu mno. Sababu ya ulegevu wao ni kwamba dhambi nyepesi, wanazozitenda mara nyingi pasipo kujali makosa hayo na maelekeo yanayotokana nayo, zinawavuta chini na kuvifunga vipaji vyao kama mabawa yaliyokunjwa. Hawako macho wapokee miangaza ya Roho Mtakatifu, hivyo inawapita tu na kuwaacha gizani. Wanaambiwa, “Ingekuwa heri leo msikie sauti yake: ‘Msifanye migumu mioyo yenu’” (Zab 95:7-8).

Namna ya kusikia sauti ya Roho Mtakatifu[hariri | hariri chanzo]

Ili tuisikie sauti hiyo ni lazima tukusanye mawazo, tujibandue na ulimwengu na umimi, tutunze moyo na tufishe matakwa na maoni yetu. Roho yetu isipokuwa na kimya ndani mwake, au ikivurugwa na mapendo ya kibinadamu mno, haiwezi kupokea miangaza ya huyo mlezi wa ndani. Ndiyo sababu Bwana anazifanyia kazi hisi zetu, pengine kwa dhati, kama kwa kuzisulubisha, ili hatimaye zinyamaze na kutii kikamilifu utashi uliohuishwa na upendo. Ikiwa kwa kawaida tunajifikiria tu, tutajisikiliza au tutasikiliza sauti nyingine mbovu na ya hatari zaidi inayotaka kutupotosha. Ndiyo sababu Bwana ametualika tujifie kama chembe ya ngano ardhini.

Lakini, hata tukipata kimya ndani mwetu, sauti ya Roho Mtakatifu ni ya fumbo: “Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho” (Yoh 3:8). Maneno hayo yanatutaka tuwe tayari kupokea mivuto ambayo inatoka kwa Bwana na ni kama mbegu ya mambo yajayo katika maongozi yake. Ni mivuto ya kujikatalia na kusali kwa ndani, yenye thamani kubwa kuliko tunavyodhani; k.mf. kuna wasomi wanaowahi kuvutiwa na sala ya moyo, ambayo peke yake huenda ikawakinga na kiburi kwa kuwapatia roho ya kitoto inayohitajika ili kuingia katika ufalme wa Mungu. Inaanza kama elekeo lisilo wazi, lakini tukidumu kwa unyenyekevu katika matakwa yake, tutakuja kutambua inatoka kwa Mungu. Mara nyingi mivuto ya kwanza inatambulisha wito: mwanga wa alfajiri unaweza ukawa mkubwa na kuongoza hija yetu ya kwenda mbinguni.

Ili tujiandae kuwa wasikivu hivyo:

1° Tutii kwa uaminifu matakwa ya Mungu tuliyokwishayajua kwa njia ya amri na mashauri yanayolingana na wito wetu. Tukitumia vizuri tuliyokwishayajua, Mungu atatuzidishia ujuzi.

2° Turudie mara nyingi azimio la kufuata matakwa yote ya Mungu. Hivyo tutajivutia neema mpya. Tukariri maneno ya Yesu, “Chakula changu ndicho hiki: niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake” (Yoh 4:34).

3° Tuombe mfululizo mwanga na nguvu ya Roho Mtakatifu ili kutimiza matakwa ya Baba. Tena inafaa kujiweka wakfu kwa Roho Mtakatifu, ili tujitie mikononi mwake kwa imani. Hasa katika nafasi ngumu na kazi mpya muhimu, tumuombe atuangaze, tukiwa na nia nyofu ya kutimiza matakwa ya Mungu tu. Halafu, tusipojaliwa miangaza mipya, tuendelee kutenda tunavyoona vema.

Hatimaye tuangalie kwa makini misukumo mbalimbali ya roho yetu ili kuchambua iliyo ya Mungu na isiyo yake. Katika roho inayotii neema, kwa kawaida ile ya Mungu ni mitulivu, kumbe ile ya shetani ni ya nguvu na kusababisha vurugu na fadhaiko.

Usikivu kwa Roho Mtakatifu, utiifu na busara[hariri | hariri chanzo]

Baadhi ya Wakristo wanataka kufuata mwanga wa binafsi kuliko Kanisa pia; kumbe usikivu kwa Roho Mtakatifu haukubali chochote kinyume cha mamlaka ya Kanisa, bali unalenga kutimiza imani na maadili mengine. Vivyo hivyo uvuvio wa Roho Mtakatifu haufuti utiifu kwa viongozi, bali unasaidia kuutekeleza, tena unatakiwa kueleweka daima kwa sharti la kwamba utiifu usiagize lingine. “Hofu pekee ni kwamba viongozi wanaweza wakafuata mno busara ya kibinadamu, na pasipo upambanuzi wakapinga miangaza ya Roho Mtakatifu kama udanganyifu na ndoto... Hata katika nafasi hiyo utiifu unatakiwa, ila Mungu atajua kurekebisha kwa wakati wake mawazo finyu ya hao wanaojiamini kipumbavu, akiwafundisha kwa uchungu wao kwamba hawatakiwi kulaumu neema zake bila kuzijua wala kuweza kuzitambua” (Alois Lallemant).

Tusidhani usikivu kwa Roho Mtakatifu hauhitaji maamuzi ya busara wala mashauri ya watu wenye mang’amuzi. Kinyume chake, mlezi wa ndani anatuambia tuangalie vizuri yale tunayoweza kuyaona wenyewe, na tuombe shauri la watu wenye mwanga, pamoja na kumkimbilia yeye. Mtume Paulo alitumwa kwa Anania aambiwe la kufanya. Basi, usikivu huo unapatana na utiifu, busara na unyenyekevu, tena unayakamilisha.

Matunda ya usikivu kwa Roho Mtakatifu[hariri | hariri chanzo]

Ukamilifu wetu wote unategemea uaminifu huo. “Wengine wanafuata ibada nyingi nzuri na kutenda mengi maadilifu; tunaweza kusema wanajitosa katika utekelezaji wa nje wa maadili. Hayo yanafaa kwa wanaoanza; lakini ni ukamilifu mkubwa zaidi sana kufuata uvuvio wa ndani wa Roho Mtakatifu na kutenda kwa kufuata misukumo yake” (A. Lallemant). Tukijitakasa moyo na kuondoa yale yote yanayopingana na neema tunaweza kuufikia ukamilifu kwa nusu ya muda wake.

“Shabaha ambayo tuilenge kisha kujizoesha sana katika usafi wa moyo, ni kujiachilia tutawaliwe na kuongozwa na Roho Mtakatifu, hata mwenyewe tu awe anaongoza vipawa vyote vya nafsi yetu na hisi zetu zote, na kuratibu yote yanayotokea ndani mwetu na nje yetu, wakati sisi tunapojiachilia kabisa kwake kwa kujinyima Kiroho matakwa yetu yanayoturidhisha binafsi… Wachache wanajua kufikia neema zote walizopangiwa na Mungu, au kufidia baadaye hasara ya kuzipoteza. Walio wengi wanakosa moyo katika kujitawala na uaminifu katika kutumia vema zawadi za Mungu. Kisha kushika njia ya uadilifu, mwanzoni tunatembea gizani, lakini tukifuata neema kwa uaminifu na udumifu, kwa hakika tutafikia mwanga mkubwa kwa faida yetu na ya wengine… Pengine inatokea kwamba, kisha kupata toka kwa Mungu mwanga mzuri, mara tunajisikia kushambuliwa na ukinaifu, shaka, wasiwasi na ugumu kutoka ndani ya umbile letu lililoharibika na maono yetu yenye kupingana na uvuvio wa Mungu. Tukiupokea mwanga huo kwa utiifu kamili wa moyo, utatujaza ile amani na faraja ambayo Roho wa Mungu analeta naye daima na ambayo anawashirikisha wale wasiopinga… Ni ukweli wa imani kwamba hata uvuvio mdogo kabisa wa Mungu ni azizi na bora kuliko ulimwengu wote, kwa sababu unapita maumbile na kutokana na damu na mauti ya Mungu. Lo, upumbavu mkubwa kweli! Tunapuuzia miangaza ya Mungu kwa sababu ni ya Kiroho na ya juu mno kuliko hisi. Hatuijali, tunapendelea vipawa vya umbile, kazi za heshima, sifa za watu, starehe zetu ndogondogo na kujiridhisha binafsi. Lo, udanganyifu mkubwa mno ambao wengi wanaung’amua saa ya kufa tu! Kwa kufanya hivyo tunamnyang’anya kimatendo Roho Mtakatifu uongozi wa roho yetu; na ingawa moyo ni wa Mungu tu, tunaujaza viumbe, kwa hasara yake; hivyo badala ya kuupanua bila mwisho kwa uwemo wa Mungu, tunaubana upeo kwa kuuhusisha na mambo madogo yasiyo na maana. Ndicho kinachotuzuia tusifikie ukamilifu” (A. Lallemant).

Usikivu kwa Roho Mtakatifu unatuonyesha alivyo kweli Mfariji katika wasiwasi juu ya wokovu wetu na katika vishawishi na huzuni za maisha haya. Kwa kuwa hatuwezi kustahili kifo chema, tunahitaji uongozi, ulinzi na faraja ya Roho Mtakatifu “aliye arabuni ya urithi wetu” (Ef 1:14). Mpako wake rohoni unatuliza tabu, unaimarisha utashi dhaifu na pengine kuonjesha ladha halisi ya Kimungu katika msalaba. “Roho Mtakatifu anatufariji katika mateso ya hapa uhamishoni, tulipo mbali na Mungu, jambo linalosababisha waadilifu wawe na huzuni isiyosemekana; kwa kuwa ndani mwao wanahisi sana utupu usiopimika uliomo na usioweza kujazwa na kiumbe chochote, ila na furaha ya Mungu tu. Muda wote ambao wametengana naye wananyong’onyea na kuteseka kama kwa kifodini chenye mateso, hata wasingeweza kuvumilia pasipo faraja ambazo Roho Mtakatifu anawajalia mara kadhaa” (A. Lallemant). Tone moja tu la utamu ambao Roho Mtakatifu anaumimina rohoni linatosha kuilevya kitakatifu.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Pontifical Council for Promoting Christian Unity: The Greek and the Latin Traditions regarding the Procession of the Holy Spirit Archived 3 Septemba 2004 at the Wayback Machine. and same document on another site

Vyanzo[hariri | hariri chanzo]

Marejeo mengine[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.