Vita

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Vita: Mfalme Ramses II mnamo 1274 KK, Mfalme Gustav Adolf mnamo 1623, Faru ya Marekani M1 2005

Vita ni mapambano baina ya nchi, mataifa au angalau vikundi vikubwa vya watu yanayoendeshwa kwa nguvu ya silaha.

Mchoro wa Pier Gerlofs Donia na Wijerd Jelckama wakipigana kwa ajili ya uhuru wa watu.

Katika vita kuna pande mbili au zaidi. Husababisha mateso, vifo na kuharibika kwa mali ya watu pamoja na mazingira asilia.

Mwanamgambo wa Kipalestina akiwa ameshika silaha aina ya M16 rifle, mwaka 2009.

Asili ya vita ilikuwa mapambano kwa silaha kati ya makabila au vijiji mbalimbali. Baada ya kutokea kwa madola ilikuwa zaidi serikali au watawala wa madola walioamua juu ya vita.

Mlipuko wa silaha ya nyuklia mwaka 1951.

Aina za vita

Kuna aina tofauti za vita:

  • vita kati ya nchi mbili au zaidi kwa niaba ya serikali zao
  • vita vya wenyewe kwa wenyewe ndani ya nchi nzima kwa msingi wa itikadi au maslahi tofauti
  • vita ya uhuru ambako watu wa eneo fulani wanapambania dola ya pekee, kwa mfano
    • vita ya wenyeji wa koloni au nchi lindwa dhidi ya serikali ya kikoloni au nchi inayotawala
    • vita ya watu wa sehemu moja ya nchi dhidi ya serikali ya nchi nzima

Watekelezaji wa vita

Watekelezaji wa vita huitwa askari au wanajeshi. Historia imejua vipindi ambapo wanaume wote wa nchi fulani walitakiwa kushika silaha na kushiriki katika mapigano. Palikuwa pia na vipindi na utamaduni ambapo wapiganaji walikuwa watu wa pekee wenye jukumu hilo ama kwa sababu walipaswa kuwa askari kufuatana na sheria za nchi au kwa sababu walikodiwa kwa kazi hii.

Wanajeshi rasmi huwa chini ya kanuni za vita lakini sehemu kubwa na vita inashirikisha watu wasiofuata kanuni hizo kama wanamgambo hasa katika vita za wenyewe kwa wenyewe.

Silaha

Wanadamu wametumia akili nyingi kuboresha vifaa vya vita, yaani silaha, na mbinu za vita. Maendeleo ya silaha yamesababisha kupungua kwa idadi ya askari wanaopigana moja kwa moja lakini uharibifu wa silaha umeongezeka.

Silaha za kale zilitegemea nguvu ya mkono wa mtu zikifikia umbali mdogo. Silaha zimebadilika kulenga mahali ambapo ni mbali zaidi na zaidi. Silaha kali za kisasa zina uwezo wa kuharibu nchi yote; jumla ya silaha za nyuklia inatosha kuua uhai wote duniani.

Jitihada za kuepa au kupunguza athari za vita

Kutokana na uharibifu mkubwa unaosababishwa na vita palikuwa tena na tena na makubaliano juu ya kanuni za vita. Kanuni hizo hulenga kupunguza hasara inayosababishwa na mapigano. Lakini historia imejaa pia mifano ambapo kanuni hizo zilivunjwa au kupuuzwa.

Katika karne ya 20 mataifa mengi yalipatana mikataba ya kimataifa juu ya kanuni za vita. Chanzo kilikuwa Mapatano ya Geneva baada ya kuundwa kwa Kamati ya Kimataifa ya Msalaba Mwekundu mwaka 1863.

Baada ya vita kuu ya kwanza ya dunia nchi nyingi ziliunda Shirikisho la Mataifa kwa shabaha ya kuzuia vita lakini hii ilishindikana baada ya nchi kubwa kama Urusi, Ujerumani na Italia kupuuza maazimio yake. Kuundwa kwa Umoja wa Mataifa kulikuwa jaribio jipya la kuwa na taasisi ya kimataifa yenye uwezo wa kuzuia vita.

Vasili Vereshchagin: Ufaulu wa Vita (1871)

Misemo juu ya vita

  • "Inawezekana kuanza vita unapotaka lakini haiwezekani kuimaliza unapotaka." - Niccolò Machiavelli
  • "Vita ni baba wa vitu vyote." - Heraklitos
  • "Vita ni aina ya siasa kwa kutumia mbinu tofauti." - Carl von Clausewitz
  • "Ukitaka amani andaa vita." - Vegetius
  • "Si vita, bali amani ni baba wa vitu vyote." - Willy Brandt
  • "Vita abadan!" - Yohane Paulo II
  • "Vita ilipokwisha askari alirudi nyumbani. Lakini alipokosa chakula akamwona mwenye chakula. Akamwua. "Lakini huruhusiwi kumwua mtu!" alisema hakimu. "Kwa nini?" aliuliza askari." - Wolfgang Borchert