Dhamiri

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Dhamiri ni kipawa cha binadamu kinachomwezesha kuamua kuhusu uadilifu au uovu wa tendo fulani analolikabili au alilolitenda.

Dhamiri hiyohiyo inamsukuma daima kutenda lililo adilifu na kukwepa lililo ovu.

Katika falsafa ya maadili wengi wanakubali kwamba uamuzi wa dhamiri unategemea ukweli ambao upo nje ya mhusika na ambao yeye anatakiwa kuutambua.

Baadhi ya wataalamu wa elimunafsia wanashika msimamo kuwa uamuzi wa dhamiri unategemea zaidi malezi na mang'amuzi ya mtu.

Katika Ukristo[hariri | hariri chanzo]

Katika dini, Ukristo unatia maanani sana dhamiri iliyozungumziwa na mtume Paulo kama sheria ya ndani ya mtu.

Mtaguso wa pili wa Vatikano ulifundisha: Ndani mwa dhamiri binadamu anakuta sheria anbayo hajipatii, bali anapaswa kuitii na ambayo sauti yake, inayomuita daima apende na kutenda maadilifu na kukimbia maovu inapotakiwa, inasema wazi katika masikio ya moyo wake [...]. Kwa kweli mtu ana sheria iliyoandikwa na Mungu katika moyo wake [...]. Dhamiri ni kiini cha siri zaidi na patakatifu pa mtu, ambapo anabaki peke yake na Mungu, ambaye sauti yake inasikika kwa ndani kabisa (Gaudium et Spes 16).

Kwanza kabisa, mtu yeyote anapaswa kufuata daima dhamiri yake, inayomdai atende mema na kuepa maovu. Sauti hiyo ya ndani inajitokeza utotoni na kumuelekeza uadilifu siku zote atakapokuwa na akili timamu. “Neno li karibu nawe sana, li katika kinywa chako na moyo wako, upate kulifanya” (Kumb 30:14). “Watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe, yakiwashtaki au kuwatetea” (Rom 2:14-15).

Katika kupima tendo fulani, dhamiri ilizingatie kwanza lenyewe, kwa sababu baadhi ni maovu daima, hivi kwamba hayawezi kamwe kuwa halali. “Ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya: uasherati, wivi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, ukorofi, hila, ufisadi, kijicho, matukano, kiburi, upumbavu. Haya yote yaliyo maovu yatoka ndani, nayo yamtia mtu unajisi” (Mk 7:21-23). “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu” (Gal 5:19-21).

Katika kupima tendo fulani, dhamiri izingatie pia uadilifu wa lengo na wa nafasi yake. Katika hayo mawili moja likiwa baya, hata tendo jema linakuwa ovu. “Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni” (Math 6:1).

Dhamiri inapopima uadilifu wa tendo fulani inaweza kukosea, kutokana na ujinga, udhaifu na misimamo miovu tuliyonayo. “Walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza” (Rom 1:21). “Mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi” (Eb 3:13).

Basi, kwa kuwa dhamiri inayotuongoza inaweza kukosea, tuiunde mfululizo kwa kuzingatia na kutekeleza ukweli uliofunuliwa na Mungu. "Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu” (Zab 119:105). “Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati, wala mchafu, wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu. Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana... Msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana” (Ef 5:5-6,17)[1].

Wakati tunapozidi kuunda dhamiri yetu, tusiache kuifuata, isije ikawa butu. Tuwafundishe watoto wazoee mapema kufanya hivyo daima: wakijali dhamiri yao watakuwa waaminifu. “Ingekuwa heri leo msikie sauti yake: ‘Msifanye migumu mioyo yenu’” (Zab 95:7-8). “Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe” (Rom 14:5). “Mimi kwa dhamiri safi kabisa nimeishi mbele za Mungu hata leo hivi... Nami ninajizoeza katika neno hili niwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele ya watu sikuzote” (Mdo 23:1; 24:16).

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Wakatoliki hasa wanasisitiza tulizingatie Neno la Mungu namna linavyofundishwa na waandamizi wa Mitume, waliopewa mamlaka ya kutuelekeza katika maadili pia. “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi” (Math 28:19-20). Tusipokubali kufundishwa nao, ujinga, udhaifu na uovu wetu vitatudanganya tena tulielewe Neno la Mungu namna inayoupendeza umimi wetu. Tena waandamizi wa Mitume wanaweza kututungia sheria pia ili kutusaidia tusiyumbe. Baadhi yake zinaitwa amri kuu za Kanisa. “Amin, nawaambieni: Yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni, na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni” (Math 18:18). “Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike” (Mdo 16:4).

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]