Teresa wa Yesu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Rukia: urambazaji, tafuta
Mt. Teresa alivyochorwa na Pieter Paul Rubens
Livio Mehus, Mtakatifu Petro wa Alkantara akimkomunisha mtakatifu Teresa wa Avila; picha ya mwaka (1683) inayotunzwa Prato (Italia)
Teresa nje ya nafsi yake alivyochorwa na Gianlorenzo Bernini katika basilika la Santa Maria della Vittoria, Roma.

Teresa wa Yesu ni jina la kitawa la Teresa Sánchez de Cepeda Ávila y Ahumada, maarufu pia kwa jina la Teresa wa Avila.

Alizaliwa Avila (Hispania) tarehe 28 Machi 1515, akafariki Alba de Tormes tarehe 15 Oktoba 1582.

Ni kati ya watu muhimu zaidi katika ya historia ya Kanisa ya karne ya 16, katika historia ya utawa na katika teolojia ya Kiroho kutokana na urekebisho aliouanzisha katika shirika la Wakarmeli (wanawake na wanaume vilevile) na kutokana na maandishi yake juu ya maisha ya kiroho.

Anaheshimiwa na Kanisa Katoliki kama mtakatifu mwenye sifa za bikira na mwalimu wa Kanisa.

Yaliyomo

[hariri] Maandishi

Maandishi ya Teresa, yaliyokusudiwa kufundisha hasa masista wenzake, ni kati ya vitabu bora vya Kanisa Katoliki:

  • Maisha yake mwenyewe (Autobiografia), yaliyoandikwa baada ya mwaka 1567 chini ya padri Pedro Ibáñez, muungamishi wake;
  • Safari ya ukamilifu (Camino de perfecciòn), iliyoandikwa vilevile baada ya mwaka 1567 chini ya muungamishi wake;
  • Jumba la ndani (Castillo interior, Las Moradas), kitabu kilichoandikwa mwaka 1577, ambamo anafananisha mtu wa sala na jumba lenye vyumba 7 vinavyofikiwa kimoja baada ya kingine;
  • Ripoti, nyongeza ya kitabu cha maisha yake kwa mtindo wa barua juu ya mang'amuzi yake ya ndani na ya nje;
  • Mawazo ya upendo
  • Mishangao
  • Barua 342 nzima na sehemu 87 za nyingine.

[hariri] Kulinganisha maandishi yake na yale ya Yohane wa Msalaba

Tangu tusome mara ya kwanza maandishi ya Teresa wa Yesu na Yohane wa Msalaba, ni rahisi tutambue tofauti ambazo zimesisitizwa mara nyingi. Basi, tuone hasa asili yake.

Zinatokana na tofauti za mitazamo yao. Teresa alitegemea mang’amuzi yake binafsi, akidokeza neema za pekee alizojaliwa (njozi n.k.) asiwe makini kuzitofautisha na mambo yaliyo ya lazima katika “makao saba” ya jumba la Kiroho. Hivyo alitia maanani kuliko wengine matukio ya kihisi, ya nje na ya ziada yanayoweza yakaendana na sala ya kumiminiwa; vilevile alisisitiza kuzingatia ubinadamu wa Yesu.

Yohane pia alisema kwa mang’amuzi yake binafsi na ya watu aliowaongoza, lakini hakuyataja, akijitahidi kuyachimba kiteolojia, jambo ambalo ni muhimu ili kutofautisha yaliyo ya kawaida na yaliyo ya ziada. Alieleza sababu za hali za sala kwa mafundisho juu ya maadili ya Kimungu na ya vipaji vya Roho Mtakatifu vinavyoendana nayo.

Kwa mtazamo huo alizingatia yaliyo ya lazima katika safari ya kuelekea utakatifu, hasa matakaso ya Kimungu yanayohitajika kwa usafi kamili wa upendo. Hivyo hakuelekea kujali neema za pekee zinazoendana pengine na sala ya kumiminiwa, wala hakusisitiza kuzingatia ubinadamu wa Yesu, akilenga moja kwa moja shabaha kuu ya sala ya kumiminiwa, yaani Mungu aliyemo mwetu, ambaye tunamfikia katika giza la imani kwa njia ya ujuzi ambao anatumiminia na unafanana na mang’amuzi.

Kwa kufanya hivyo amekamilisha maandishi ya Teresa na kutusaidia tuyaelewe.

Hata hivyo, chini ya tofauti hizo kuna msingi mmoja, kwa kuwa Teresa alijua vya kutosha mang’amuzi ya wafuasi wake aweze kuelewa na kueleza nini inatokea kwa kawaida kwa watu wanaopitia hayo makao saba. Tukitumia maelekezo aliyoyatoa huko na huko tunaweza kubainisha zaidi yaliyo ya lazima na yaliyo ya ziada.

Kimsingi watakatifu hao walielewa vilevile sala ya kumiminiwa, muungano na Mungu unaotokana nayo, na matakaso ya Kimungu yanayohitajika ili kuufikia ule kamili.

Ikifaa kuonyesha tofauti zao, inafaa zaidi kuonyesha wanavyolingana na kutambua teolojia inavyoweza kusaidia katika masuala hayo magumu.

[hariri] Nukuu

« Usivurugwe na lolote, usitishwe na lolote. Yote yanapita, Mungu habadiliki. Subira inapata yote. Aliye na Mungu hakosi lolote. Mungu tu anatosha. »
(Teresa wa Yesu, Shairi, 9)

[hariri] Vyanzo

  • Teresa of Avila, "The Book of Her Life" (Translated, with Notes, by Kieran Kavanaugh, OCD and Otilio Rodriguez, OCD. Introduction by Jodi Bilinkoff). Indianapolis/Cambridge: Hackett Publishing Company, 2008. ISBN 978-0-87220-907-7
  • "The Delighted Angel" drama about Teresa of Ávila and Rabija al-Adavija by Dževad Karahasan, Vienna-Salzburg-Klagenfurt, ARBOS 1995.
  • "The Interior Castle (Edited by E. Allison Peers)," Doubleday, 1972. ISBN 978-0-385-03643-6
  • "The Way of Perfection (Translated and Edited by E. Allison Peers)," Doubleday, 1991. ISBN 978-0-385-06539-9
  • "The Life of Teresa of Jesus: The Autobiography of Teresa of Avila (Translated by E. Allison Peers)," Doubleday, 1991. ISBN 978-0-385-01109-9
  • "Teresa of Avila: An Extraordinary Life", Shirley du Boulay, Bluebridge, 1995 ISBN 978-0-9742405-2-7
  • "Teresa: Outstanding Christian Thinkers," Rowan Williams, Continuum, 1991. ISBN 0-8264-5081-4
  • "The Eagle and the Dove" Saint Teresa of Avila and Saint Thérèse of Lisieux. by Vita Sackville-West. First published in 1943 by Michael Joseph LTD, 26 Bloomsbury Street, London, W.C.1

[hariri] Viungo vya nje

Vifaa binafsi
Maeneo ya wiki

Vibadala
Vitendo
Urambazaji
Vifaa
Lugha zingine