Tanganyika

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Tanganyika (nchi))
Bendera ya koloni ya Tanganyika.
Bendera ya Tanganyika tangu 1961 hadi 1964.
Historia ya Tanzania
Coat of Arms of Tanzania
This article is part of a series
Uendo
Historia ya Zanzibar
Afrika Mashariki 1800-1845
Ukoloni
Afrika ya Mashariki ya Kijerumani
Mkataba wa Zanzibar-Helgoland
Mkwawa
Vita vya Maji Maji
Vita vikuu vya kwanza Afrika Mashariki
Tanganyika
Mapambano ya uhuru Tanganyika
Uhuru
Uhuru wa Tanganyika
Mapinduzi ya Zanzibar
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
Julius Nyerere
Ujamaa
Tamko la Arusha
Vita vya Kagera
Ali Hassan Mwinyi
Benjamin Mkapa
Jakaya Kikwete
John Magufuli
Samia Suluhu Hassan

Tanzania Portal

Tanganyika ni jina la kihistoria la sehemu kubwa ya Tanzania ya leo, yaani ile yote isiyo chini ya serikali ya Zanzibar.

Kwa sababu za kisiasa, mara nyingi huitwa "Tanzania bara" ingawa ina visiwa pia, hasa Mafia na Kilwa.

Tanganyika ilikuwa sehemu kubwa ya koloni la Ujerumani hadi vita kuu ya kwanza ya Dunia. Baada ya mwaka 1916 ilivamiwa na Uingereza na Ubelgiji. Kuanzia mwaka 1922 Tanganyika ilikuwa eneo la kudhaminiwa kwa niaba ya Shirikisho la Mataifa lililokuwa chini ya Uingereza ikawa nchi huru kati ya miaka 1961 - 1964, mwaka wa kwanza kama ufalme, halafu kama jamhuri.

Mwaka 1964 iliungana na Zanzibar na kuwa sehemu ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.

Chanzo katika koloni la Kijerumani

Maeneo yaliyoitwa baadaye (1920) "Tanganyika" yaliunganishwa mara ya kwanza tangu mwaka 1886 kama koloni la Ujerumani lililoitwa Afrika ya Mashariki ya Kijerumani. Kabla ya kufika kwa ukoloni kulikuwa na madola madogo mbalimbali na maeneo madogo ya kikabila.

Kanda la pwani pamoja na njia za misafara kuelekea Ziwa Tanganyika vilikuwa chini ya athira ya Usultani wa Zanzibar.

Tangu mwaka 1885 Karl Peters, kwa niaba ya Shirika la Ukoloni wa Kijerumani (Gesellschaft für Deutsche Kolonisation) alianza kufanya mikataba na watawala wenyeji katika maeneo ya Usagara, Nguru, Useguha na Ukami iliyoweka msingi wa madai yake ya kuchukua utawala mkuu wa maeneo hayo. Mikataba hii ilikuwa ya udanganyifu maana Peters aliwahamasisha machifu kutia sahihi kwenye matini za Kijerumani ambazo hawakuelewa.

Uenezeaji wa Wajerumani uliendelea hasa baada ya kushinda upinzani katika vita ya Abushiri na vita dhidi ya Wahehe.

Koloni ile la Kijerumani ilikuwa kubwa kuliko Tanganyika ya baadaye, maana ilijumlisha pia maeneo ya Rwanda na Burundi pamoja na sehemu ndogo ya Msumbiji.

Wakati wa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia (1914 - 1918) koloni ya Kijerumani ilitekwa na majeshi ya Uingereza na Ubelgiji.

Mkataba wa Versailles wa mwaka 1919 ulikuwa na kanuni za kuchukua makoloni yote ya Ujerumani na kuzikabidhi kwa mataifa washindi wa vita. Sehemu kubwa ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani iliwekwa chini ya utawala wa Uingereza, kasoro maeneo ya Rwanda na Burundi yaliyokabidhiwa mikononi mwa Ubelgiji.

"Tanganyika Territory" ya Kiingereza baada ya kuondoka kwa Wajerumani

Tangu mwaka 1917/18 maeneo yote ya Tanganyika yalitawaliwa na jeshi la Uingereza. Mwaka 1922 yalipelekwa chini ya utawala wa kiraia wa Kiingereza[1] uliotekelezwa na gavana. Mwaka 1922 Shirikisho la Mataifa liliamua kukabidhi Tanganyika mikononi mwa Ufalme wa Maungano (Uingereza)[2] kama eneo la kudhaminiwa chini ya mamlaka ya Shirikisho la Mataifa kulingana na kifungo 22 cha mkataba wa Versailles.

Jina la eneo

Waingereza walihitaji jina jipya kwa ajili ya eneo hilo. Tangu mwaka 1919 ilipoeleweka kwamba koloni ya Kijerumani itabaki chini ya Uingereza idara ya koloni pale London (Colonial Office) ilijadili jina. Kati ya mapendekezo yalikuwepo:

  • Smutsland (kwa heshima ya jenerali Jan Smuts wa Afrika Kusini aliyeogoza uvamizi wa eneo katika Vita Kuu),
  • Eburnea na Azania ambayo hayakukubaliwa;
  • New Maryland, Windsorland (kwa heshima ya familia ya kifalme) na Victoria yalipingwa na waziri aliyetaka kuona jina la kienyeji;
  • kati ya majina ya kienyeji kama Kilimanjaro na Tabora hatimaye Tanganyika lilipendelewa.[3] na kuwa jina rasmi kuanzia Januari 1920. Kwa chaguo la "Tanganyika Territory" Waingereza walitumia jina la ziwa kubwa upande wa mashariki ya eneo. [4] Jina hilo lilitumiwa pia na Shirikisho la Mataifa katika azimio lake kuhusu eneo hilo.

Kuhusu asili ya jina "Tanganyika" ona hapa: Tanganyika_(ziwa)#Jina

Tanganyika chini ya Uingereza

tazama pia: Orodha ya Magavana wa Tanganyika

Katika Vita Kuu ya Pili, wananchi 100,000 hivi waliungana na jeshi la Uingereza[5] wakiwa kati ya Waafrika 375,000.[6] Watanganyika walipiga vita katika vikosi vya King's African Rifles huko Somalia, Uhabeshi, Madagascar na Burma.[6] Pia Tanganyika ilikuwa chanzo kikubwa cha chakula[5].Jambo hilo lilisababisha mfumuko wa bei usio wa kawaida.[7]

Uhuru na Muungano na Zanzibar

(Tazama pia Historia ya Muungano wa Zanzibar na Tanganyika, Historia ya Tanzania)

Tanganyika ilipata uhuru wake tarehe 9 Desemba 1961.

Mwaka 1964 imeunganika na Zanzibar kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Leo hii neno "Tanganyika" linatumiwa wakati mwingine kutaja sehemu ya Tanzania isiyo Zanzibar, hasa na watu ambao hawapendi muundo wa serikali mbili tu (ile kuu na ile ya Zanzibar) ndani ya muungano na wanadai kuwa na serikali ya tatu, yaani ile ya Tanganyika.

Marejeo

  1. Quincy Wright: Mandates under the League of nations, Chicago, Ill. : The University of Chicago press, [1930], online hapa kwenye tovuti ya hathitrust.org, uk. 413
  2. Azimio: tazama Quincy Wright: Mandates under the League of nations, uk. 611 ff
  3. Iliffe, A modern History of Tanganyika, uk. 247
  4. Linganisha makala "Tanganyika Territory" katika Encyclopedia Britannica, 12th edition, vol 32, uk 676
  5. 5.0 5.1 Jay Heale; Winnie Wong (2010). Tanzania. Marshall Cavendish. ISBN 978-0-7614-3417-7. 
  6. 6.0 6.1 "African participants in the Second World War". mgtrust.org.
  7. "Tanzania: British rule between the Wars (1916–1945)" Archived 4 Februari 2015 at the Wayback Machine.. eisa.org.za.