Kwame Nkrumah

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kwame Nkrumah pamoja na Martin Luther King.

Kwame Nkrumah (21 Septemba 1909 - 27 Aprili 1972) alikuwa Rais wa kwanza wa Ghana na mmoja wa viongozi wenye nia ya kujenga Muungano wa Afrika, tena mchochezi wa falsafa ya Umajinuni.

Maisha

Miaka ya kwanza katika Ghana

Kwame Nkrumah alizaliwa mnamo mwaka 1909 katika kijiji cha Nkroful kwenye koloni la Gold Coast (leo Ghana). Nkrumah mwenyewe aliandika ya kwamba tarehe ilikuwa 18 Septemba 1909 iliyokuwa siku ya Jumamosi. Hii inalingana na jina "Kwame" ambalo katika utamaduni wa Waakan ni jina la mwanamume aliyezaliwa siku hiyo. Ila tu aliposoma Marekani alijulikana kwa jina la Francis Nwia Kofi Nkrumah na "Kofi" ni jina la mwanamume aliyezaliwa siku ya Ijumaa.

Baba yake, ambaye jina lake halikuhifadhiwa, alikuwa na kazi ya fundi dhahabu. Mama yake aliitwa Nyanibah akaishi hadi kifo chake na kwa muda alitunza kaburi la mwanawe. [1][2].

Mtoto alilelewa kijijini pamoja na watoto wengine wa babake na ukoo. Mama alimsomesha katika shule ya msingi ya misioni ya Kanisa Katoliki. [3]. Alipita madarasa kumi katika muda wa miaka minane.

Mnamo 1925 alikuwa Mkristo aliyebatizwa akafundisha katika shule yake kama mwalimu msaidizi. Kutoka hapo alikaribishwa na mchungaji Alec Garden Fraser, mkuu wa chuo cha ualimu cha serikali mjini Accra kujiunga na masomo huko.[4] [5] Huko makamu wa mkuu Kwegyir Aggrey aliyewahi kusoma Marekani alimweleza mafundisho ya Marcus Garvey na W. E. B. Du Bois. Aggrey, Fraser na walimu wengine wa chuo walifundisha ya kwamba ushirikiano wa watu wa rangi zote ni shabaha kwa maendeleo ya Gold Coast. Lakini Nkrumah alifuata mwelekeo wa Marcus Garvey akiamini ya kwamba ni lazima nchi yake itawaliwe na Waafrika wenyewe.[6] [7]

Baada ya kumaliza masomo yake mwaka 1930 Nkrumah aliajiriwa kama mwalimu wa shule ya msingi ya Kikatoliki huko Elmina na baada ya mwaka 1 alikuwa mwalimu mkuu wa shule ya Axim. Huko alianza kushiriki katika majadiliano ya kisiasa akaanzisha "Nzima Literary Society". Mwaka 1933 aliendelea na kuwa mwalimu kwenye seminari ya Kikatoliki mjini Amissa.

Marekani

Alipokuwa mwanafunzi wa chuo Nkrumah alisikia hotuba ya mwandishi Nnamdi Azikiwe (baadaye alikuwa rais wa Nigeria). Alikutana naye, na Azikiwe alimpa ushauri kuendelea na masomo yake huko Marekani kwenye chuo cha Lincoln College alikowahi kusoma mwenyewe an kilichokuwa chuo kwa Waamerika Weusi. Nkrumah angependelea kusoma London (Uingereza) lakini alishindwa mitihani ya kuingia. Hivyo kwa msaada wa mjomba tajiri alisafiri Pennsylvania na kuanza masomo huko Lincoln kwenye Oktoba 1935.[8].

Hakuwa na pesa nyingi, hivyo alifanya kazi ndogo kama kusafisha vyombo hotelini. Siku za Jumapili alisali katika makanisa ya Weusi mjini Philadelphia na New York. [9] Mwaka 1939 alimaliza masomo akapokea digrii ya bachelor katika fani ya uchumi.

Chuo kikampa nafasi ya mhadhiri msaidizi kwa masomo ya falsafa akaendelea kusoma teolojia akachukua BA mwaka 1942. Alisoma pia Chuo Kikuu cha Pennsylvania alipomaliza digrii za master katika falsafa na ualimu.[10]. Wakati huohuo alishirikiana na mwanaisimu William Everett Welmers kutunga kitabu cha sarufi ya Fante iliyokuwa lugha yake ya kwanza.[11]

Wakati wa likizo Nkrumah alipenda kwenda Harlem (New York) iliyokuwa kitovu cha kiutamaduni kwa Waamerika Weusi. Hapa alienda kuzunguka mitaani na kusikiliza wahubiri wa barabarani.

These evenings were a vital part of Kwame Nkrumah's American education. He was going to a university—the university of the Harlem Streets. This was no ordinary time and these street speakers were no ordinary men .... The streets of Harlem were open forums, presided over [by] master speakers like Arthur Reed and his protege Ira Kemp. The young Carlos Cook, founder of the Garvey oriented African Pioneer Movement was on the scene, also bringing a nightly message to his street followers. Occasionally Suji Abdul Hamid, a champion of Harlem labor, held a night rally and demanded more jobs for blacks in their own community .... This is part of the drama on the Harlem streets as the student, Kwame Nkrumah walked and watched.[12]

Chuoni Nkrumah alikusanya wanafunzi kutoka nchi za Afrika na kuanzisha "African Students Association of America and Canada" akichaguliwa kuwa mwenyekiti wake. Katika majadiliano ya kundi hili alisisitiza haja ya nchi zote za Afrika kushikamana baada ya uhuru, si kufuata shabaha za pekee kwa kila koloni. [13] Nkrumah alishiriki pia katika Mkutano wa Umoja wa Afrika mjini New York wa mwaka 1944 uliosisitiza Marekani kusaidia nchi za Afrika kufikia uhuru baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia. [14]

Katika kipindi chake nchini Marekani Nkrumah alikutana pia na wafuasi wa Umarx, hasa wa mwelekeo wa Trotzki. Hasa C.L.R. James kutoka Trinidad alikuwa na athira juu yake. Nkrumah aliandika baadaye ni Johnson aliyemfundisha namna gani kufanya kazi ya kisasa kwa siri kama ni lazima.[15].

Wakati Nkrumah alitaka kurudi Afrika baada ya vita kwenye mwaka 1945, James alitunga barua ya kumtambulisha kwa marafiki huko London akiandika: "Huyu kijana anakuja sasa kwenu. Si mtu mwelekevu mno, lakini fanyeni mnachoweza kumsaidia; anataka kuwafukuza Wazungu kutoka Afrika". [16]

London

60 Burghley Road, Kentish Town, London, where Nkrumah lived when in London between 1945-1947

Nkrumah alfika London mwezi wa Mei 1945 akajiandikisha kwenye chuo cha London School of Economics kama mwanafunzi wa PhD katika anthropolojia. Aliacha baada ya mhula mmoja, akajiandikisha kwenye chuo kikuu kwa shabaha ya kufuata PhD ya falsafa lakini hakuendelea. Mwishoni alijaribu masomo ya sheria. Profesa wa falsafa Alfred Ayer hakumwona Nkrumah kuwa mwanafalsafa bora. Alisema juu yake: "Nilimpenda nikafurahi kujadili naye. Lakini kwangu hakuonekana kuwa na akili ya mchambuzi. Alitafuta majibu ya harakaharaka. Labda sehemu ya matatizo yake ilikuwa ya kwamba hajajikazia kuendeleza thesis yake. Kwake ilikuwa njia tu ya kupita muda hadi aliweza kurudi Ghana" [17]

Nkrumah alitumia nguvu nyingi kupanga mikutano ya siasa. Alikuwa kati ya waratibu walioandaa mkutano wa Pan-African Congress mjini Manchester (15-19 Oktoba 1945).[18] Wajumbe wa mkutano huu walipatana kuelekea kwa Shirikisho la Maungano ya Madola ya Afrika na kujenga utamaduni mpya kwa Afrika bila ukabila na siasa itakayounganisha usoshalisti au ukomunisti na demokrasia. [19] Kati ya wajumbe waliohudhuria walikuwa mzee W.E.B. Dubois pamoja na Waafrika walioendelea kuwa viongozi wa nchi zao baada ya uhuru kama vile Hastings Banda wa Nyasaland (Malawi), Jomo Kenyatta wa Kenya, Obafemi Awolowo wa Nigeria na C.L. R. James.[20]

Kurudi Ghana

Baada ya kurusi Gold Coast, Nkrumah kwenye mwaka 1947 alikuwa katibu mkuu wa chama cha United Gold Coast Convention (UGCC). Mwaka 1948 kulitokea ghasia ya "Accra Riots"; askari Waafrika wa jeshi la Kiingereza walioachishwa baada ya vita kuu walidai malipo waliyoahidiwa. Nkrumah alihutubia mkutano wao; baada ya maandamano yao kuvunjwa na polisi na watu kufa katika ghasia iliyofuata, polisi ilikamata viongozi wa chama cha UGCC.

Mwaka 1949 Nrumah alitoka katika UGCC akaunda Convention People’s Party (CPP) iliyokuwa na madai makali zaidi. Mwaka 1951 CPP ilipata kura nyingi katika uchaguzi baada ya kudai uhuru mara moja. Nkrumah aliyekuwa tena mbaroni aliruhusiwa kugombea, alipata asilimia 98,5 za kura mjini Accra akaachwa huru. Mwaka 1952 alichaguliwa na Halmashauri ya Kisheria kuwa waziri mkuu wa koloni.

Aliendelea kuongoza serikali na mwaka 1957 wakati wa uhuru alibadilisha jina la nchi kuwa Ghana. Hii ilikuwa koloni la kwanza kupata uhuru katika Afrika ya Magharibi, baada ya Liberia. Mwaka huohuo alifunga ndoa na Fathia Helen Ritzk, Mkristo wa Kikopti kutoka nchi ya Misri.

Baada ya uhuru

Nkrumah alianzisha mipango mingi ya kuendeleza Ghana kiutamaduni, kielimu na kiuchumi. Pamoja na Haile Selassie wa Ethiopia aliunda Umoja wa Muungano wa Afrika (kwa Kiingereza: Organisation of African Union - OAU). Alikaribia nchi za kikomunisti na kuajiri washauri na wahandisi kutoka Urusi na China.

Alijipatia maadui kati ya machifu waliokuwa na mamlaka kubwa wakati wa ukoloni lakini sasa wengi waliachishwa au kupinduliwa na serikali kama hawakufuata maagizo yote kutoka juu. Alipata pia maadui kati ya wakulima tajiri wa kakao kwa sababu aliongeza sana kodi wakati bei ya zao hili kwenye soko la dunia ilipanda juu. Mnamo mwaka 1960 bei za kakao zilishuka sana na hapo alikosa pesa kwa miradi mingi aliyoanzisha wakati mapato ya kakao yalikuwa juu.

Gharama za miradi kubwa zililipiwa kwa kukopa pesa nje ya nchi. Deni la taifa lilikua haraka. Baada ya bidhaa kadhaa kuwa haba, serikali ilijaribu kuongoza uchumi kwa mfano wa nchi za kikomunisti. Upinzani kati ya wananchi ulitazamwa kama uasi na watu wengi walikamatwa. Kodi zilipandishwa.

Inasemekana ya kwamba pia huduma za siri za CIA (Marekani) na MI5 (Uingereza) zilichochea wapinzani wa Nkrumah waliopanga kumpindua. Mwaka 1966 alipokwenda safari ya kutembelea China na Korea ya Kaskazini kamati ya siri ya upinzani pamoja na jeshi la ulinzi na polisi ya kitaifa ilipindua serikali.

Nkrumah alishindwa kurudi. Kwa miaka kadhaa alikaa Guinea. Baada ya kugonjeka alihamia kwa tiba huko Romania alipoaga dunia mwaka 1972.

Vitabu vilivyoandikwa na Kwame Nkrumah

A postage stamp from the Soviet Union marking the 80th anniversary of his birth
"The essence of neo-colonialism is that the State which is subject to it is, in theory, independent and has all the outward trappings of international sovereignty. In reality its economic system and thus its political policy is directed from outside." (Introduction)

Marejeo

  1. Birmingham, David (1998). Kwame Nkrumah: The Father of African Nationalism. Ohio University Press. ISBN 978-0-8214-1242-8., uk 3
  2. Addo, Ebenezer Obiri (1997). Kwame Nkrumah: A Case Study of Religion and Politics in Ghana. University Press of America. ISBN 978-0-7618-0785-8., uk 50-51
  3. Rooney, David (1988). Kwame Nkrumah: The Political Kingdom in the Third World. St. Martin's Press. ISBN 978-0-312-02479-6, uk 7–8
  4. Rooney uk. 7–8
  5. Owusu-Ansah, David (2014). Biographical Dictionary of Ghana (4th ed.). Rowman & Littlefield. ISBN 978-0-8108-7242-4, uk 239
  6. Rooney uk. 9
  7. Addo, Ebenezer Obiri (1997) uk. 53–54
  8. Rooney, uk. 9–12
  9. Birmingham uk. 4
  10. Rooney uk. 13–14
  11. A Descriptive Grammar of Fanti, by Welmers, William Everett; Linguistic Society of America 1946; uk. 7
  12. Clarke uk. 11
  13. Rooney uk.14–15
  14. Rooney uk.16
  15. "how an underground movement worked". Sherwood, Marika (1996). Kwame Nkrumah: The Years Abroad 1935–1947. Freedom Publications. ISBN 978-9988-7716-0-7. uk.114
  16. "this young man is coming to you. He is not very bright, but nevertheless do what you can for him because he's determined to throw Europeans out of Africa.” Sherwood uk. 114
  17. “I liked him and enjoyed talking to him but he did not seem to me to have an analytical mind. He wanted answers too quickly. I think part of the trouble may have been that he wasn't concentrating very hard on his thesis. It was a way of marking time until the opportunity came for him to return to Ghana.” Sherwood uk.115
  18. G. Martin African Political Thought ISBN 9781137062055 uk.
  19. Boni Yao Gebe, Ghana's Foreign Policy at Independence and Implications for the 1966 Coup D’état, Journal of Pan African Studies, volume 2, issue 3, date March 2008
  20. Rooney uk.23

Soma pia

Viungo vya nje

Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kwame Nkrumah kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.