Historia ya Rwanda

Historia ya Rwanda inahusu eneo la Afrika Mashariki ambalo wakazi wake leo wanaunda Jamhuri ya Rwanda.
Historia ya kale
[hariri | hariri chanzo]Rwanda imekuwa nchi yenye rutuba na uoto wa kijani kwa maelfu ya miaka; sehemu ya Msitu wa Nyungwe ilikuwa ikipokea maji yaliyotoka barafu za milima ya Rwenzori. Ingawa haijulikani binadamu wa kwanza walifika lini hasa, inaaminika kuwa waliingia nchini baada ya enzi za barafu, aidha wakati wa kipindi cha Neolithiki (takriban miaka 10,000 iliyopita), au kipindi cha unyevunyevu kilichofuata hadi mwaka 3000 KK[1].
Watu wa kwanza kuishi Rwanda walikuwa jamii ya Watwa, waliokuwa wawindaji-wakusanyaji wa matunda msituni. Walijulikana kwa kuwa na miili mifupi na waliishi karibu na misitu. Hadi leo, baadhi ya watu wa jamii hii bado wanaishi Rwanda na wanatambulika kama wakazi wa asili wa nchi hiyo.[2]
Uchunguzi wa akiolojia uliofanywa tangu miaka ya 1950 umebaini ushahidi wa makazi ya watu wachache waliokuwa wawindaji-wakusanyaji katika Enzi ya Mawe ya Mwisho. Baadaye, walikuja wakaaji wengi zaidi wa Zama za Chuma walioacha zana za chuma na vyungu vya udongo vilivyochongwa.
Mnamo mwaka 3000 KK, wakulima na wafugaji waliotumia lugha za Sudani ya Kati walikaa kaskazini na magharibi mwa Rwanda (pamoja na Burundi ya magharibi). Wachungaji wa Sudani ya Mashariki, waliokuwa na uhusiano na watu wa lugha za Kuliak, walihamia kusini mwa Rwanda na maeneo ya mashariki na magharibi ya Mto Ruzizi mnamo 2000 KK[3].
Mnamo 1000 KK, jamii za Wabantu wa Mashariki wenye ujuzi wa kilimo na uhunzi zilifika Rwanda kupitia Bonde la Kivu. Kabla ya 800 KK, baadhi ya wafugaji wa Kikushi kutoka Kusini walikaa sehemu za mashariki mwa Rwanda. Ifikapo 500 KK, jamii ya watu wa Maziwa Makuu, ambao ni mababu wa wasemaji wa lugha ya Kinyarwanda-Kirundi, walikaa kati ya Ziwa Kivu na Ziwa Rweru.
Hatimaye, jamii ya Wabantu wa Maziwa Makuu waliunganisha makundi yote ya awali ya Waniloti wa Sahara na Wakushi wa Kusini, na kufanya Rwanda kuwa nchi inayozungumza lugha za Kibantu pekee.
Karne nyingi zilizopita, jamii ya Watwa ilianza kupoteza nafasi yao ya awali baada ya kuwasili kwa Wabantu, ambao walikuwa wakulima wakaanza kusafisha misitu ili kujenga makazi ya kudumu. Hata hivyo, asili ya uhamiaji wa tatu mkubwa, wa jamii ya wachungaji wa mifugo, inabaki kuwa suala lenye utata mkubwa. Wataalamu mbalimbali hawakubaliani kuhusu ni lini na kwa njia gani Watutsi waliingia Rwanda, na iwapo walikuja kwa njia ya amani au kwa ushindi wa kijeshi.
Kabla ya Ukoloni
[hariri | hariri chanzo]Rwanda ilikuwa chini ya utawala wa kifalme tangu karne nyingi kabla ya kufika kwa ukoloni. Mwanzo wake ni katika eneo la Ziwa la Muhazi. Watawala wenye cheo cha "mwami" kutoka kikundi cha wafugaji (Watutsi) walitanua eneo lao tangu miaka ya karne ya 16 BK hadi kufika eneo la leo. Wafugaji wa ng'ombe Watutsi walikalia nchi pamoja na wakulima wa Kihutu na wavindaji Watwaa.
Ukoloni wa Kijerumani
[hariri | hariri chanzo]Ukoloni ulichelewa kufika Rwanda; mwaka 1890 Ujerumani na Uingereza walipatana ya kuwa Rwanda na Burundi ni sehemu ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani. Lakini ilikuwa mwaka 1908 tu ya kwamba Wajerumani walimtuma afisa wa kudumu aliyekaa Rwanda kama mwakilishi wa serikali ya Ujerumani. Mwaka 1916Ubelgiji na Uingereza walivamia Rwanda katika Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia. Baadaye ikawa chini ya Ubelgiji pamoja na Burundi kama "Rwanda-Urundi" katika hali ya eneo la kudhaminiwa kutokana na azimio la Shirikisho la Mataifa.
Ukoloni wa Ubelgiji
[hariri | hariri chanzo]Utawala wa Wabelgiji ulikuwa wa moja-kwa moja na mkali zaidi kuliko Wajerumani. Wabelgiji walijaribu kutoa faida ya kiuchumi wakilazimisha wenyeji kupanda mikahawa na kutekeleza kazi za serikali ya kikoloni. Katika utawala wao Wabelgiji walitumia zaidi Watutsi wakiwapa nafasi za elimu na kuwatumia katika shughuli za serikali. Wataalamu wengine huamini ya kwamba siasa hii ilisababisha kukua kwa chuki dhidi ya Watutsi kwa upande wa wakulima Wahutu iliyoleta kumwaga kwa damu baadaye.
Katika miaka ya 1950 ilionekana ya kwamba ukoloni unaelekea mwisho wake. Uhusiano kati ya Wahutu na Watutsi ukawa vigumu kwa sababu Wabelgiji walibadilisha siasa yao yakupendelea Watutsi wakidai haki zaidi kwa ajili ya Wahutu waliokuwa wengi. Na hasa wamisionari wa katoliki Mapadre Weupe walisimama upande wa Wahutu wakiona ndio wagandamizwa.
Mwami Mutara Rudahigwa aliyejiita pia Charles alijaribu kuleta upatanishi kati ya vikundi katika nchi. Mwaka 1954 aligawa nchi ya kifalme kati ya Wahutu na Watutsi. Lakini alikuwa na wapinzani Watutsi waliomuua mwaka 1959.
Mtoto wake Mwami Kigeri V aliwekwa kwenye kiti chake. Tendo hili lilisababisha ghasia na vurugu nchini kwa sababu Wahutu walidai kuwa na neno katika mabadiliko ya serikali. Mwezi wa Novemba 1959 Mwami Kigeri V. alilazimishwa kuondoka nchini akikimbilia Uganda. Watutsi wenye siasa kali walijaribu kumwua kiongozi wa Mouvement Democratique Republicain (MDR) chama kikubwa cha Wahutu. Wahutu walijibu kwa kuwashambulia na kuua Watutsi. Wabelgiji walitumia wanajeshi wao kupoza hali hiyo nchini. Katika uchaguzi wa kwanza wa halmashauri ya tarafa na miji kabla ya uhuru ndicho chama cha Parmehutu kilichopata kura nyingi. Viongozi wa Parmehutu walitangaza serikali mpya mwaka 1961. Uchaguzi wa Bunge ulileta kura ya 77% kwa ajili ya chama cha Parmehutu kilichomchagua kiongozi wake Grégoire Kayibanda kuwa Raisi.
Uhuru
[hariri | hariri chanzo]Tarehe 1 Julai 1962 Rwanda ilipata uhuru wake wa kisiasa. Wakati huu zaidi ya Watutsi 350,000 walikuwa wakikimbilia nchi jirani. Mwaka uliofuata vikundi vya Watutsi kutoka nchi hizi za jirani walijaribu kushambulia utaratibu mpya. Iliyofuata ilikuwa uangamizaji wa kwanza wa Watutsi; zaidi ya 100,000 waliuawa na Wahutu. Hata katika miaka iliyofuata mauaji dhidi ya Watutsi yaliendelea. Wanasiasa Wahutu walizoea kuwaita Watusi ndio "Wadudu". Kila kitu kilichokuwa si sawa kilielezwa ni kosa la Watutsi waliokuwa raia bila haki. Idadi kubwa ya Watutsi walikimbilia Burundi, Uganda na Tanzania.
Mwaka 1973 jenerali Habyarimana alimpindua rais Kayibanda na kuanzisha serikali ya kijeshi akijaribu kupatanisha vikundi ndani ya taifa. Lakini hata mwaka uliofuata 1974 mauaji ya Watutsi yalitokea tena.
Mnamo 1990 ilikuwa wazi ya kwamba Rwanda ilikuwa na hali ngumu. Kwa upande mmoja nchi za nje zilisukuma serikali za Afrika kuruhusu kura huru za kisiasa; katika Rwanda ongezeko la wakazi lilileta msongamano mkubwa na uhaba wa ardhi ya kilimo. Uchumi ilikuwa duni. Wakati huohuo wapinzani Wahutu walikusanyika nje ya nchi na kudai demokrasia. Na kati ya watoto wa Watutsi waliokuwa walitoka nchini sauti zikasikika zilizodai warudi tena.
Habyarimana alijaribu kutafuta suluhisho akanza kujadiliana na Watutsi wa nje lakini alikuta pia upinzani kwa upande wa Wahutu wakali waliochukia uelewano wa Watutsi.
RPF ilipojaribu kurudi Rwanda kutoka Uganda
[hariri | hariri chanzo]Mnamo Oktoba 1990 Watutsi waliokaa Uganda walianzisha chama cha RPF (Rwanda Patriotic Front) wakiwa na wafuasi wahutu wachache wakavamia Rwanda kwa silaha. Kiongozi wao alikuwa Paul Kagame aliyeondoka Rwanda akiwa mtoto wa miaka minne. Alikuwa amejiunga na jeshi la Yoweri Museveni na kupanda ngazi katika jeshi la Uganda hadi kuwa mkuu wa huduma ya usalama wa jeshi la Uganda. Walitaka kulazimisha serikali ibadilishe hali ya Watutsi kuwa raia bila haki. Lakini uvamizi huu ulisababisha kuongezeka kwa ukali dhidi ya Watutsi ndani ya Rwanda na siasa kali kwa upande wa viongozi Wahutu. Kikundi cha kihutu cha Interahamwe kilipatiwa silaha hali iliyopelekea vifo vya maelfu ya Watutsi Wanyarwanda.
Vita kati ya wapinzani kutoka Uganda na jeshi la serikali viliendelea mpakani hadi pande zote mbili zilipokutana huko Arusha na kupatana kuacha vita mwaka 1992 chini ya uangalizi wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika.
Sehemu ya viongozi wa Rwanda walijiandaa kutafuta utaratibu mpya lakini wengine walifanya mipango ya kumaliza swala la Watutsi kabisa wakipanga kuua Watutsi wote nchini.
Kifo cha Juvenal Habyarimana na mauaji ya watu milioni moja
[hariri | hariri chanzo]Tarehe 6 Aprili 1994 rais Juvenal Habyarimana alirudi nchini kutoka safari ya Tanzania. Ndege yake ilipigwa risasi kabla ya kuteremka ikaanguka chini akafa. Haipingiki kwamba Watutsi wakali (RPF) ndio waliomuua.
Tendo hili lilikuwa mwanzo wa mauaji ambayo hayakuwahi kutokea Afrika. Viongozi wa Interahamwe, wa jeshi la kitaifa na vikundi vikali vya Kihutu walitekeleza mipango ya kukusanya Watutsi kila mahali na kuwaua. Haiwezekani kuwa na idadi kamili lakini makadirio ya chini yanataja Watutsi 750.000 na Wahutu wasio wakali zaidi ya 600000 waliuawa na Interahamwe na wanajeshi wa serikali ya Kihutu. Watu walikimbilia na kutafuta hifadhi makanisani lakini hata huko walichinjwa bila huruma. Wahutu waliokataa kushiriki katika mauaji hayo waliuawa pia.
RPF chini ya uongozi wa Paul Kagame iliamua kutumia nguvu zote kulipiza kisasi kwa kuwaua Wahutu wenye msimamo mkali na wengine wengi kufungwa maisha katika jela zenye hali mbaya sana, akilenga kulipiza kisasi cha mauaji. Kwa miezi miwili mauaji na vita vilikwenda sambamba hadi RPF iliposhinda mnamo Julai 1994 na kuchukua madaraka ya serikali.
Jeshi, Waparmehutu na serikali ya kihutu walikimbilia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wakiwalazimisha wakazi wengi kuongozana nao hali iliyosababisha kutokea kwa makambi ya wakimbizi makubwa sana katika Kongo ya mashariki yaliyokuwa na idadi ya wahutu milioni mbili. Walio wengi wamerudi Rwanda baada ya kuimarika kwa serikali mpya.
Rwanda mpya
[hariri | hariri chanzo]Tangu ushindi wa kijeshi mwaka 1994 RPF walianzisha serikali ya umoja wa kitaifa. Rais alikuwa Pasteur Bizimungu mwanasiasa Mhutu aliyeshikamana na RPF, Kagame akiwa makamu wake. Baada ya kupinduliwa kwa Bizimungu mwaka 2000 Kagame akawa Rais.
Mwaka 2003 palitokea uchaguzi wa kwanza.
Jeshi la Rwanda limeendelea kuwa na vita ndani ya Kongo ikipigana na mabaki ya Interahamwe walioshambulia Rwanda mara kwa mara kutoka Kongo.
Ndani ya Rwanda mahakama za vijijini zinazoitwa "gachacha" zimejaribu kutoa hukumu juu ya wauaji wa mwaka 1994.
Rais D. Gasangwa wa Eacu alisisitiza [4] kwamba ilikuwa "Ethnic cleansing", si "Holocaust" kama ilivyoandikwa na Wazungu wa magazeti ya Ulaya. Watu karibu 600,000 waliuawa Rwanda, na Mkoa wa Kivu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Utengamano wa siasa mpya lazima utoe nafasi ya kujenga nchi mpya.
| Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu. Je, unajua kitu kuhusu Historia ya Rwanda kama enzi zake au matokeo yake? Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa? Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari. |
- ↑ Kingdom of Rwanda – Encyclopaedia Britannica
- ↑ Kingdom of Rwanda – Encyclopaedia Britannica
- ↑ Wahutu wa Maziwa Makuu ya Afrika – Qiraat Africa
- ↑ "Sometime in April (2004)" movie