Jinsia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Uzazi wa kijinsia wa binadamu na wanyama wengi unafanyika kwa mbegu mojawapo kati ya nyingi zinazobebwa na manii ya mzazi wa kiume kuungana na kijiyai cha mzazi wa kike. Picha hii iliyokuzwa sana inaonyesha mbegu inayojipenyeza katika kijiyaji cha duara.
Sehemu ya mfululizo wa makala kuhusu mapendo

Moyo katika mapokeo ya Ulaya
ni mchoro unaowakilisha mapendo.
Vipengele Msingi
Mapendo kadiri ya sayansi
Mapendo kadiri ya utamaduni
Upendo (fadhila)
Upendo safi
Kihistoria
Mapendo ya kiuchumba
Mapendo ya kidini
Aina za hisia
Mapendo ya kiashiki
Mapendo ya kitaamuli
Mapendo ya kifamilia
Mapendo ya kimahaba
Tazama pia
Mafungamano ya binadamu
Jinsia
Tendo la ndoa
Maradhi ya zinaa
Siku ya wapendanao

Jinsia ni hali ya viumbe hai wengi kuwa wa kiume au wa kike, jambo muhimu katika mpango wa kuendeleza uhai kupitia uzazi. Hata hivyo, si viumbe vyote vinaendeleza uhai kwa njia ya uzaliano kijinsia:

Kuna pia njia ya kujizalisha ambayo ni namna ya pekee ya uzalioni kijinsia. Mimea kama karanga na pia wanyama kadhaa mfano vyawa na samaki kadhaa wanaweza kuanzisha wadogo bila manii ya kiume. Wanyama kama mategu ni huntha wanaobeba manii pamoja na vijiyai mwilini na wanazaa ndani yao.

Binadamu[hariri | hariri chanzo]

Kati ya wanadamu hali ya kuwa mwanamume au mwanamke inategemea nukta ya utungaji mimba na kudumu moja kwa moja.

Inatokana na milioni za mbegu zilizomo kwa kawaida katika shahawa ya mwanamume, ambazo baadhi yake ni za kiume (zenye chembeuzi Y) na baadhi za kike chembeuzi X.

Kijiyai cha mwanamke hakichangii uainishaji wa jinsia ya mtoto, kwa kuwa kina pea ya chembeuzi X tu.

Ikiwa mbegu inayowahi kujipenyeza katika kijiyai cha mwanamke ni ya kiume, mimba itakuwa ya kiume (XY), kumbe ikiwahi moja ya kike, mimba itakuwa ya kike (XX).

Kulingana na tofauti hiyo, binadamu huyo mpya atazidi kukua na kutokeza viungo maalumu vya uzazi kama:

Viungo hivyo vitakomaa wakati wa ubalehe.

Ni pia muhimu kazi ya chachu za jinsia (homoni za jinsia) zilizo tofauti kwa mwanamume na mwanamke.

Sehemu fulani ya tofauti kati ya jinsia mbili hutegemea pia utamaduni.

Hali za watu zisizo za kawaida[hariri | hariri chanzo]

Katika kila jamii, hasa zilizoendelea, kuna idadi fulani ya watu ambao utambuzi wa jinsia si wa kawaida kutokana na hali ya pekee ya chembeuzi (hasa XYY na XXY) au uwepo wa homoni za jinsia nyingine ndani yao au uwepo wa viungo vya uzazi mchanganyiko au visivyo kamili au visivyoeleweka. Hata hivyo chembeuzi Y inathibitisha kuwa mhusika ni wa kiume.

Watu wengine wana tatizo la utasa, ambalo linazidi kuongezeka hasa katika nchi zilizoendelea hata kuvuka asilimia 10 ya wakazi.

Wengine, kwa sababu zisizoelezeka vya kutosha na biolojia wala saikolojia, hawajisikii ipasavyo na jinsia yao (hasa ubaridi wa kijinsia na elekeo la ushoga na usagaji).

Usawa wa wanawake na wanaume na tofauti zao[hariri | hariri chanzo]

Siku hizi watu huongea mara nyingi juu ya usawa wa jinsia mbili. Hakika kuna usawa wa hadhi kati ya mwanamke na mwanamume. Kwa mfano, Biblia inatangaza usawa huo wa binadamu wote tangu sura yake ya kwanza (Mwa 1:26-30). Humo tunajifunza kwamba: wote wameumbwa na Mungu, tena kwa sura na mfano wake, wote wametiwa roho, wote wana akili na utashi, wote wamepata baraka yake ili kuongezeka na wote wamepewa uwezo wa kutawala dunia pamoja na vyote vilivyomo. Hata hivyo, kila mmoja ni sura na mfano wa Mungu kwa namna fulani tu, hivi kwamba mwanamke anafanana zaidi na Mungu katika baadhi ya sifa zake na mwanamume vilevile katika sifa nyingine.

Kutambua tofauti za maumbile ya mwanamke na mwanamume ni msaada mkubwa kwa ajili ya kuelewana na kushirikiana vizuri. Ujuzi huo unamwezesha mtu kufahamu kwa nini mwingine anawaza, anasema na kutenda tofauti naye. Mradi ujuzi wa udhaifu wa kila upande usimfanye yeyote ajikuze na kumdharau mwenzake, wala ajisikie mnyonge, bali uamshe ndani yake juhudi za kukamilika kwa kushinda udhaifu alionao. Hata hivyo mwenzake aelewe kwamba juhudi hizo haziwezi kufaulu mia kwa mia kutokana na umbile lilivyo.

Tofauti za maumbile na tabia kati ya wanawake na wanaume zinajitokeza tayari katika mbegu za kike na za kiume, ambazo zote zinatengenezwa na mwili wa mwanamume, lakini za kwanza ni fupi zaidi, zinakwenda polepole zaidi ila zinadumu kirefu kuliko za pili baada ya kutoka mwilini mwa baba. Ni hizo mbegu ambazo zinamiminwa kwa mamilioni ndani ya mwili wa mama na kushindana ili ziwahi kufikia kijiyai kilichoiva, ambacho kwa kawaida ni kimoja tu na kinasubiri mgeni wake.

Mbegu yoyote ya mwanamume, iwe ya kike au ya kiume, inapopenya kijiyai cha mwanamke, mara inapatikana mimba ya seli moja ambayo tayari ina jinsia yake isiyoweza kubadilika tena kwa namna yoyote ile, hata baada ya mtoto kuzaliwa, kukua na hatimaye kufa. Seli zake zote zitakuwa daima za jinsia ile. Utambulisho huo wa msingi unasababishwa na baba tu.

Kadiri seli ya kwanza inavyozidi kujigawa, viungo vya mwili vinazidi kupatikana na tofauti zifuatavyo zinazidi kutokea upande wa jinsia kulingana na mbegu ilivyokuwa:

  • Chembeuzi kwa jumla (kwa kawaida ni 46) zinabeba jeni zote (25,000 hivi) zinazoongoza utengenezaji wa seli zinazounda mwili jinsi ulivyo. Watu wote wana chembeuzi ya jinsia X (walau moja), ila kama ipo chembeuzi ya jinsia Y pia (inayobeba jeni maalumu za kiume) inamfanya mtu kuwa mwanamume, la sivyo ni mwanamke. Hivyo mwanamume ana jeni nyingi kuliko mwanamke, kwa kuwa yeye tu ana chembeuzi Y.
  • Ubongo una mwelekeo wa kike, ila unajenga tabia za kiume ukiingiwa na chachu ya testosteroni wakati wa mimba na wa ubalehe.
  • Katika mwanamke daraja kati ya pande mbili za ubongo (kulia na kushoto) ni nene, hivyo mawasiliano kati ya nusu hizo ni bora kuliko kwa mwanamume, ambaye daraja lake ni jembamba, ila ubongo wake ni mkubwa zaidi kwa asilimia 10 hivi.
  • Mwanamke anaweza kuongea kuliko mwanamume kwa sababu ndani ya ubongo wake usimamizi wa usemi na hisi pamoja na utendaji wote wa akili umeenea katika nusu zote mbili, kumbe kwa mwanamume unafanyika katika maeneo maalumu yaliyotengwa kwa ajili hiyo, hivyo kwake ni rahisi zaidi kupatwa na kigugumizi.
  • Mwanamke anamshinda mwanamume katika uwezo wa kufahamu kwa njia ya kusikia, kuonja, kunusa na kugusa; k.mf. mwanamke anaweza kuona pembeni kuliko mwanamume. Hata hivyo mwanamke ni mzito kuliko mwanamume kung’amua mahusiano ya umbali wa vitu.
  • Mwanamke ana uwezo hafifu kuliko mwanamume wa kuratibu macho na mikono.
  • Ubongo wa mwanamke unapokea zaidi hisia, hivyo analia kuliko mwanamume na maitikio yake yote yanajitokeza kwa nguvu hata kupitiliza, kumbe ya mwanamume yamepoa zaidi.
  • Mwanamke anajali uhusiano na viumbe hai, hasa watu: anavutwa na maongezi, hisia, urafiki kuliko mwanamume.
  • Uwezo wa mwanamke wa kutofautisha hoja na hisia ni mdogo kuliko ule wa mwanamume; hata hivyo anaweza akafikia mahitimisho sahihi zaidi ingawa ya mwanamume yana mantiki zaidi.
  • Mwanamke ni dhaifu katika hisabati kuliko mwanamume.
  • Mwanamke amezoea masumbuko na kuvumilia kuliko mwanamume, lakini katika shida na uchungu anahitaji kufarijiwa. Mwamamume anakabili tabu kwa kupanga na kutekeleza ili kubadili hili na hili, hapendi kujisikia anashindwa, hujitahidi kuhakikisha anafanikiwa.
  • Mwanamke huamua haraka, bila kufuata sheria wala hoja zaidi, kumbe mwanamume huamua mambo baada ya kuyafanyia utafiti, akihoji na kutafuta sababu: “Ilikuwaje? Nikifanya hivi itakuwaje? Na kikitokea hiki nitafanya nini?” Hivyo anaweza kuchukua muda mrefu kuamua. Akikwama asijue la kufanya, huenda akaonekana hajali au anapuuzia jambo, kumbe anatafuta bado mbinu mbadala.
  • Uamuzi wa mwanamke si wa moja kwa moja, ana wasiwasi, uko tayari kupokea mashauri au maoni ya watu, hata kuongozwa kama si kutawaliwa nao; pengine tabia hiyo humfikishia pabaya, kwani ni mwepesi kushawishika. Kumbe mwanamume hutaka kuongoza daima, hufanya mambo kwa kujiamini zaidi, kama kwamba hahitaji shauri.
  • Hamasa ya kushindana na kutawala kwa mwanamke ni pungufu: hivyo haelekei kufanya vurugu wala kuwa mhalifu kama mwanamume, na maradhi ya akili yanayosababisha ukatili hayampati mwanamke mara nyingi kama mwanamume.
  • Ubinafsi wa mwanamke ni mdogo zaidi: anaguswa na misiba ya wengine, anaona huruma na kutafuta amani kuliko mwanamume. Ikitokea ajali, mwanamke anauliza mara, “Je, kuna mtu aliyeumia?”, kumbe mwanamume anaweza akauliza kwanza, “Je, walikuwa na bima?”
  • Tangu utotoni, mwanamke anaelekea kushughulikia watu: anacheza na mwanasesere au mtoto wa gunzi, anambeba na kumuogesha, anamnyonyesha n.k., anapika chakula kwa kutumia mchanga. Mwanamume anamzidi kwa vipaji vya ufundi, kwa kuwa anajali zaidi vitu visivyo hai kama kisu, jembe, redio, fedha n.k.: anatazama aina za magari na namba zake, anaendesha makopo kama gari au baiskeli, anajenga nyumba. Kama anavyopenda kuvimiliki vitu, ndivyo anavyopenda wanadamu wawe chini yake: kwake hao ni karibu sawa na vitu.
  • Mwanamke anaweza kuzingatia mtu au jambo moja tu siku nzima au hata majuma kadhaa, kumbe mwanamume anasahau haraka mtu au jambo pekee, kwa kuwa anaelekea kuzingatia mengi pamoja.
  • Hata akiwa na kazi nyingi, mke anaweza kumkumbuka mumewe kutwa nzima, kumbe mume ni mwepesi kumsahau mke wake akishikwa na kazi.
  • Mke anaelekea uaminifu kwa mwenzi mmoja kuliko mume, kwa kuwa anatarajiwa kubeba mimba na kumtunza mtoto, kumbe mwenzie ana msukumo wa kusambaza mbegu zake kadiri iwezekanavyo.
  • Mwanamke haangalii sana faida na hasara ya jambo, halengi mafanikio kama mwanamume, ambaye yuko tayari kujitolea kila kitu (muda, afya, furaha na mahusiano) ili kufikia malengo yake.
  • Umbile lote la mwanamke ni katika umama: si tumbo lake tu limeumbwa kwa kazi ya kuzaa watoto, bali mabadiliko yote ya mzunguko wa kila mwezi unahusika na upatikanaji wa mimba. Tena si mwili tu, bali ubongo wake pia unalilia umama ambamo hisani na ukarimu vinang’aa upeo. Kumbe mwanamume, hata akiwa mwema vipi, hawezi kuelewa, kutunza na kutuliza watoto vizuri kama mwanamke.
  • Mwanamke ana mwili laini na mifupa midogo: hali hii humzuia asifanye kazi ngumu mno. Kwa nguvu hawezi kushindana na mwanamume, ambaye yupo tayari kufanya kazi yoyote, hata iwe nzito kiasi gani.
  • Mwanamke hufanya kazi mbalimbali (kulima, kuuguza, kufundisha, kutunza watu) kadiri awezavyo, hata saa 12-15 kwa siku: ni wa kwanza kuamka na wa mwisho kulala. Ingawa kazi zake ni nyepesi, hana muda maalumu wa kupumzika. Mwanamume anajua ni jukumu lake kuipatia familia mahitaji yake; hata hivyo anafanya kazi saa 8 au 9 tu, halafu huwa amechoka.
  • Viungo vya uzazi vya mwanamke vimo ndani ya mwili wake ili kupokea viungo vya mume na mbegu zake zinazomtia mimba. Kumbe viungo vya uzazi vya mwanamume viko nje ili kuzamia mwili wa mke na kuutia mbegu za uzazi. Tofauti hizo zinaonyesha wazi kwamba viungo vyao vinalenga kuungana na kukamilishana; ndivyo ilivyo pia kwa nafsi zao katika utendaji wote maishani.
  • Mwanamke anajitahidi kuwa mzuri daima ili azidi kupendwa; anataka awe mpendwa pekee: mbinu zake ni za kujivutia. Mwanamume anataka aheshimiwe na kusifiwa kwa nguvu yake hata katika ngono: mbinu zake ni za kuteka.
  • Kwa mwanamke mawazo, hisia na mwili ni kitu kimoja: hujitoa kiakili, kihisia na kwa mwili wake wote, si kwa sehemu tu. Hivyo, katika kufanya mapenzi, huchukua muda mrefu kupata ashiki, huona butwaa mwanamume yupo tayari zamani, kwa kuwa ni mwepesi kusisimka, huamshwa tamaa hata na jambo dogo, k.mf. kuona sehemu ambazo kwa kawaida hazitakiwi kuonekana.
  • Ashiki ya mwanamke hufanana na moto uwakao katika majani mabichi kwa kuwa inaenea katika mwili mzima, huamka polepole, pia huchukua muda mrefu kupoa. Kumbe ashiki ya mwanamume hufanana na moto uwakao katika majani makavu kwa kuwa imo hasa katika uume wake, huwaka kwa nguvu sana na hupoa haraka vilevile.
  • Kwa mwanamke tendo la ndoa huanza moyoni panapotokea pendo. Mwanamume hujikuta mbinafsi hata katika mapenzi: anadai kutoshelezwa katika ashiki asijali kutoshelezana kwa kumsubiri mwenzake.
  • Katika kufanya mapenzi, mwanamke hujitoa kabisa kwa yule ampendaye hata kujiachia na kutendewa zaidi. Kumbe mwanamume hutaka kummiliki mwenzake: humwona kama chombo cha halali yake.

Kutokana na tofauti hizo na nyinginezo, wanawake wanafaa zaidi kwa kazi kadhaa na wanaume kwa kazi nyingine. Mwanamke hawi bora anapofaulu kufanana na mwanamume, bali anapokuwa mwenyewe kama alivyo, yaani alivyoumbwa na Mungu kwa ajili ya umoja wa wawili tofauti. Si suala la ubaguzi, bali ni maumbile, hivyo ni hekima ya Mungu.

Jinsia mbili zinaposhirikiana kwa upendo na heshima bila kushindana, familia na jamii zinakwenda vizuri kwa michango maalumu ya jinsia zinazokamilishana. Kinyume chake, pale ambapo wanawake wanataka kushindana na wanaume ili washike nafasi yoyote, sisi sote tunakosa ule mchango maalumu wa jinsia ya kike hata kuliko wanapobaguliwa na kuzuiwa wasiutoe.

Katika Ukristo[hariri | hariri chanzo]

Kwa msingi huo unaweza ukaeleweka uamuzi wa Yesu wa kuteua wanaume tu kuwa mitume ingawa aliwaheshimu sana wanawake, kuanzia Mama yake, Bikira Maria. Huyo, aliye kielelezo cha wanawake wote, kwa upendo wake kamili alichangia na anazidi kuchangia ustawi wa Kanisa na wa ulimwengu kuliko mtume yeyote yule. Kwa kuwa Yesu ametuonyesha kuwa jambo bora si kutawala, bali kupenda na kutumikia kama mwenyewe alivyofanya akiongozwa na Roho Mtakatifu, ambaye ndani ya Mungu ni Upendo-Nafsi, ni Zawadi-Nafsi anayekamilisha umoja wa Baba na Mwana. Ndiyo sababu anatusukuma kupenda na kujitoa badala ya kutaka kutawala. Katika hilo wanawake wanaelekea zaidi.

Kimsingi zaidi, inafaa tujitahidi kuelewa fumbo la Mwana wa Mungu kujifanya mwanamume awe bwanaarusi wa Kanisa linalokusudiwa kumzalia watu wote kabisa. Ingawa Mungu hana mwili, na kwa sababu hiyo hana jinsia, Yesu Mwanae ni mwanamume na ametushirikisha uhusiano wake na Mzazi wa milele aliyemuita Baba. Hilo si bure: ndiye aliyetangulia kutupenda na ndiye anayetuwezesha kufanya lolote. Kazi yetu ni hasa kuwa tayari kupokea upendo wake na utendaji wake wowote ili uzima ustawi ndani mwetu na kandokando yetu.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]