Zaka

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Zaka (kutoka neno la Kiarabu زكاة, zakat, lenye maana ya "kinachotakasa"; kwa Kiingereza: Tithe) ni toleo la sehemu ya mapato ambalo muumini wa dini fulani anapaswa kutoa kwa Mungu, kwa viongozi wa dini husika au kwa maskini.

Katika Biblia

Kutoa zaka hekaluni, mchoro wa Pierre Monier.

Desturi ya Mashariki ya Kati ya kutoa sehemu moja ya kumi kwa makuhani iliingia katika Uyahudi kuanzia Abrahamu aliyempa Melkisedek mfalme wa Salem aliyekuwa pia kuhani wa El Elyon (Mungu Mkuu).

Habari hiyo inasimuliwa katika Kitabu cha Mwanzo 14:18-20 [1] na kusisitizwa na Waraka kwa Waebrania 7:5 [2].

Zaka (kwa Kiebrania מעשׂר, ma‛ăśêr, kwa Kigiriki δεκάτη, dekatē) inaagizwa na vitabu vingine vya Biblia ya Kiebrania, kama vile Mambo ya Walawi, Hesabu na Kumbukumbu la Sheria katika Torati.

Baadaye wajibu huo ulisisitizwa na Kitabu cha Malaki 3:8-12 [3]na Kitabu cha Tobiti 1:6–8 (humo zinatajwa aina tatu za zaka zilizozingatiwa baada ya uhamisho wa Babeli [4]).

Katika Agano Jipya, Yesu alilaumu Mafarisayo kwa kulipa zaka kamili hata kwa vitu vidogo kama mboga na viungo pamoja na kupuuzia mambo makubwa zaidi kama haki na huruma (Injili ya Mathayo 23:23 [5]).

Mtume Paulo alifundisha kuwa anayetumikia kwenye altare anastahili kupata riziki zake kwa njia hiyo (Waraka wa kwanza kwa Wakorintho 9:13 [6]). Pia alihimiza waamini kutoa kwa moyo mkunjufu (Waraka wa pili kwa Wakorintho 9:7 [7])

Katika Ukristo

Stoo ya zaka huko Kronenburg, Ujerumani.

Mwanzoni mwa Kanisa waamini walikuwa wanawajibika, lakini hakuna hata babu wa Kanisa mmoja aliyehimiza zaka.

Baadaye katika Ukristo wa Magharibi zilianza kutolewa sheria ili kuihimiza, kwa mfano huko Ufaransa katika mtaguso wa Tours (567) na ule wa Mâcon (585).

Hatimaye Papa Adrian I alipitisha maagizo hayo mwaka 787 na Mtaguso wa Trento uliyasisitiza[8].

Baadaye njia za kuwategemeza viongozi wa Kanisa zilitofautiana kadiri ya nchi na madhehebu.

Leo Wabaptisti na Wapentekoste ndio wanaoongoza kwa kusisitiza wajibu wa kutoa sehemu moja ya kumi ya mapato yote[9].

Kumbe Wakatoliki wanafundishwa kuwajibika ili kulipatia Kanisa mahitaji yake, kila mmoja kadiri ya uwezo wake, lakini kimataifa zaka haitajwi na Mkusanyo wa Sheria za Kanisa wala na Katekisimu ya Kanisa Katoliki [10].

Vilevile Waorthodoksi, wakiendeleza mapokeo yao ambamo zaka haikushurutishwa kamwe, wanahimizwa kutoa bila kulazimishwa kiasi fulani kilichokwishapangwa[11].

Katika Uislamu

Maana za zaka katika dini ya Uislamu ni nyingi. Kisheria ni kiwango maalumu cha mali kinachotolewa wakati maalumu kwa watu maalumu.

Umuhimu wa zaka katika Uislamu

Zaka [12] ni kati ya faradhi za dini ya Kiislamu, na ni ya tatu kati ya Nguzo Tano za Kiislamu. Kadiri ya Kurani, Mwenyezi Mungu anasema: "Na simamisheni swala na toeni zaka". [13]

Akasema Mtume Muhamad: "Umejengwa Uislamu kwa mambo matano: Kushuhudia ya kwamba hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu na kwamba Muhammad ni mja wake na ni Mtume wake, na kusimamisha Swala (tano za kila siku), na kutoa Zaka, na kuhiji nyumba tukufu (Al-ka’abah – ilioko Makkah), na kufunga Mwezi wa Ramadhani" [14].

Zaka ni mojawapo ya nguzo za Uislamu, ambayo inadai muumini atoe sehemu fulani ya mapato yake kwa maskini. Masharti ya mtu kulazimika kutoa zaka ni:

  • 1. Uislamu. Haikubaliwi zaka kwa kafiri, kwa sababu Mwenyezi Mungu hakubali matendo yake.
  • 2. Kuwa huru (muungwana). Haikubaliwi kwa mtumwa kutoa zaka, kwa sababu mali yake ni milki ya bwana wake.
  • 3. Kumiliki Nisabu (kiwango). Maana ya Nisabu ni kiwango maalumu cha mali ambacho kikifikiwa basi inalazimika mali hiyo kutolewa Zaka.

Masharti ya Nisabu

1. Iwe Nisabu ni ziada ya mahitaji ya dharura ambayo mtu hatosheki kwa kuyapata mahitaji hayo, kama chakula, mavazi na makazi, kwa sababu zaka ni wajibu kwa lengo la kuwaliwaza fukara. Hivyo basi inatakiwa mwenye kutoa hiyo mali asiwe mhitaji mwenyewe.

2. Iwe Nisabu inamilikiwa na mtu maalumu umiliki mkamilifu, basi haiwajibiki zaka kwa mali ambayo haimilikiwi na mtu maalumu, kwa mfano: mali iliyokusanywa kwa lengo la kujenga msikiti, au mali iliyowekwa wakfu kwa maslahi ya umma, au mali iliyoko kwenye hazina za jumuia za mambo ya kheri.

3. Mali kupitiwa na Mwaka: Ni mwaka wa Kiislamu uliokamilika. Hii ni kwamba ipite miezi kumi na miwili ya kalenda ya mtizamo wa mwezi hali ya kuwa Nisabu iko kwenye miliki ya mwenye mali. Na sharti hili ni peke yake kwa pesa (dhahabu na fedha), na mapato ya biashara, na wanyama wa mifugo. Ama mazao ya kilimo na matunda, na madini, hazina iliyozikwa ardhini si sharti kwa vitu hivi kupitiwa na mwaka.

Tendo hilo muhimu la kutoa msaada linatazamwa na Waislamu kama njia ya kujipatia utakaso wa uroho na ubinafsi na ya kubarikiwa katika riziki zao.

Hukumu ya anayekataa kutoa zaka

Anayekataa kutoa zaka, ama amekataa kwa kupinga kwamba si lazima kutoa [Juhuud: Ni kukataa kuwajibishwa kwake.], ama kwa ubahili.

Mwenye kukataa kutoa zaka kwa kupinga

Anayepinga wajibu wa zaka basi amekufuru kwa makubaliano ya umma wote – ikiwa mtu huyu anajua vizuri wajibu wa Zaka; kwa sababu atakuwa amemzulia uwongo Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Anayekataa kutoa zaka kwa ubahili

Atakayekataa kutoa zaka kwa ubahili wake basi huchukuliwa kutoka kwake zaka kwa nguvu wala hawi kafiri kwa kufanya hivyo kukataa kutoa zaka kwa ubahili.

Atakuwa ametenda dhambi kubwa miongoni mwa madhambi makubwa na ni uovu mkubwa sana.

Kwa kauli ya Mtume kuhusu wanaokataa kutoa zaka: “Mtu yeyote aliye na hazina ya dhahabu na fedha na wala haitolei zaka basi atachomwa nayo katika moto wa Jahannam na itajaaliwa kama vinoo ambavyo atapigwa navyo kwenye migongo na vipaji kila akipata ubaridi (yakipoa makali ya moto) anaregelewa tena (kupigwa navyo), mpaka Allaah amalize kuhukumu waja wake siku ambayo ni sawa na miaka elfu khamsini. Kisha ndio ataoneshwa njia yake ikiwa ni ya peponi au motoni” [15].

Lau atapigana na kukataa kutekeleza amri ya zaka basi mpigeni vita mpaka arudi katika kutekeleza amri ya Mwenyezi Mungu, na atoe zaka, kwa kauli ya Mwenyezi Mungu: "Lakini wakitubu na wakasimamisha swala na wakatoa zaka, basi iacheni njia yao (waacheni" [16]).

Kwa kauli ya Mtume: "Nimeamrishwa niwapige watu vita mpaka washuhudiye ya kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na wasimamishe swala, na watoe zaka, watakapofanya hivyo basi imeharamishwa kwangu damu yao na mali yao isipokuwa kwa haki ya Uislamu, na malipo yao yako kwa Mwenyezi Mungu" [17].

Abubakar pia alipiga vita mtu yeyote ambaye alipinga wajibu wa zaka, akasema: "Naapa kwa Mungu ya kwamba nitampiga vita yoyote aliyetenganisha kati ya swala na zaka, kwa hakika hiyo Zaka ni haki ya mali, Wallaahi kama wakinizuilia hata kwa (kamba ya) kutiwa shemere (anayofungwa mnyama kwenye pua zake) nitapambana nao maadamu walikuwa wakiitoa kwa Mtume" [18].

Katika Usingasinga

Katika dini ya Sikh muumini anadaiwa kutoa dasvand (ਦਸਵੰਦ) maana yake moja kwa kumi. Inaonekana sheria hiyo ilitokana na Uislamu.

Tanbihi

  1. 18 Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana. 19 Akambariki, akasema, Abramu na abarikiwe na Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi. 20 Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. Abramu akampa fungu la kumi la vitu vyote.
  2. 5 Na katika wana wa Lawi nao, wale waupatao ukuhani, wana amri kutwaa sehemu ya kumi kwa watu wao, yaani, ndugu zao, kwa agizo la sheria, ijapokuwa wametoka katika viuno vya Ibrahimu.
  3. 8 Je! Mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia zaka na dhabihu. 9 Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote. 10 Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la. 11 Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba, asema Bwana wa majeshi. 12 Na mataifa yote watawaiteni heri; maana mtakuwa nchi ya kupendeza sana, asema Bwana wa majeshi.
  4. 6 Katika jamaa yangu ni mimi peke yangu niliyekwenda kuabudu mara kwa mara huko Yerusalemu kutekeleza sheria inayowabana watu wote wa Israeli milele. Niliharakisha kwenda Yerusalemu na sehemu ya mazao ya kwanza ya mavuno na wanyama, zaka za mifugo na manyoya ya kwanza ya kondoo. 7 Vitu hivi niliwapa makuhani, wazawa wa Aroni, kwa ajili ya madhabahu. Niliwapa Walawi waliohudumu huko Yerusalemu zaka yangu ya divai, ngano, zeituni, makomamanga na matunda mengine. Kwa miaka sita mfululizo nilichukua fedha ya zaka na kuilipa huko Yerusalemu. 8 Sehemu ya tatu ya zaka niliwapa yatima, wajane na wageni walioishi miongoni mwa watu wa Israeli; niliwapelekea kama zawadi kila miaka mitatu. Tulipokula chakula tulifanya kulingana na Sheria ya Mose na mawaidha ya Debora mama wa babu yangu Ananieli. Baba yangu alikuwa amekufa akaniacha yatima.
  5. 23 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.
  6. 13 Hamjui ya kuwa wale wazifanyao kazi za hekaluni hula katika vitu vya hekalu, na wale waihudumiao madhabahu huwa na fungu lao katika vitu vya madhabahu?
  7. 7 Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.
  8. Croly, David O. (1834). An Essay Religious and Political on Ecclesiastical Finance, as regards the Roman Catholic Church in Ireland, etc. John Bolster. p. 72. The Council of Trent – the last general Council – declares that "tithes are due to God or to religion, and that it is sacrilegious to withold them." And one of the six precepts of the Church commands the faithful "to pay tithes to their pastors."
  9. Bob Smietana, Churchgoers Say They Tithe, But Not Always to the Church, lifewayresearch.com, USA, 10 May 2018
  10. CIC 222; KKK 2043
  11. Smith, Christian; Emerson, Michael O; Snell, Patricia (29 September 2008). Passing the Plate: Why American Christians Don't Give Away More Money. Oxford University Press. pp. 215–227. ISBN 9780199714117.
  12. [https://www.al-feqh.com/sw/zaaka-hukumu-yake-na-masharti-yake
  13. (Suratu An-Nur: 56)
  14. Imepokewa na Bukhari na Muslim
  15. Imepokewa na Bukhari
  16. Suratu At-tawbah: 5
  17. Imepokewa na Muslim
  18. Imepokewa na Bukhari

Marejeo

  • Albright, W. F. and Mann, C. S. Matthew, The Anchor Bible, Vol. 26. Garden City, New York, 1971.
  • The Assyrian Dictionary of the Oriental Institute of the University of Chicago, Vol. 4 "E." Chicago, 1958.
  • Fitzmyer, Joseph A. The Gospel According to Luke, X-XXIV, The Anchor Bible, Vol. 28A. New York, 1985.
  • Grena, G.M. (2004). LMLK—A Mystery Belonging to the King vol. 1. Redondo Beach, California: 4000 Years of Writing History. ISBN 0-9748786-0-X. 
  • Speiser, E. A. Genesis, The Anchor Bible, Vol.1. Garden City, New York, 1964.
  • Kelly, Russell Earl, "Should the Church Teach Tithing? A Theologian's Conclusions about a Taboo Doctrine," IUniverse, 2001.
  • Matthew E. Narramore, "Tithing: Low-Realm, Obsolete & Defunct" – April 2004 – ISBN|0-9745587-02
  • Croteau, David A. "You Mean I Don't Have to Tithe?: A Deconstruction of Tithing and a Reconstruction of Post-Tithe Giving" (McMaster Theological Studies)

Marejeo mengine

Viungo vya nje

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.