Waraka wa kwanza kwa Wakorintho

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Agano Jipya

Mchoro wa Beatus de Facundus (1047) kuhusu 1Kor 15.

Barua ya kwanza kwa Wakorintho ni kati ya vitabu 27 vya Agano Jipya katika Biblia ya Kikristo

Kama vitabu vingine vyote vya Biblia, hiki pia kinatakiwa kisomwe katika mfululizo wa historia ya wokovu ili kukielewa kadiri ya maendeleo ya ufunuo wa Mungu kwa binadamu.

Mazingira[hariri | hariri chanzo]

Kutoka Korintho (mji wa Ugiriki) habari za kusikitisha zilimfikia Mtume Paulo akiwa Efeso (pengine mwaka 57): katika Kanisa hilo ambalo alilianzisha na kulipenda sana kulikuwa na shaka kuhusu imani, mafarakano, upinzani wa Wakristo wa Kiyahudi dhidi yake, na makwazo.

Kilichohatarisha zaidi jumuia hiyo ni karama mbalimbali ambazo hao Wakristo wachanga walizijali mno na hatimaye wakajivunia kuwa nazo.

Vilevile walivutiwa kumfuata mtu kama Apolo, mwenye ujuzi na ufasaha mkubwa, mambo yaliyopendwa sana na Wagiriki wa kale.

Ilimbidi Paulo arekebishe hali hiyo ili kuokoa hasa umoja wa Kanisa na heshima kwa viongozi wake halali.

Basi mwaka mzima akawa na mahangaiko kwa wafuasi wake wa Korintho akawaandikia walau barua nne au tano, ingawa sisi tunazo mbili tu; pengine sehemu za baadhi yake zimeshonwa ndani ya 2Kor.

Mpangilio[hariri | hariri chanzo]

Mpangilio wa barua ya kwanza una salamu na shukrani, halafu hukumu juu ya matatizo ya Wakristo hasa kufarakana (1Kor 1:10-16; 2:1-4:16), kuzini na kushtakiana mahakamani (1Kor 5-6).

Baada ya hapo akaanza kujibu maswali yao mbalimbali: kuhusu ndoa na useja (1Kor 7), nyama zilizotolewa sadaka kwa miungu (1Kor 8:1-11:1), mwenendo katika ibada na karama (1Kor 11:20-33; 12:4-13:13; 14:18-40), na hatimaye ufufuko wa wafu (1Kor 15:1-28,33-49).

Mwishoni kuna maagizo, taarifa na salamu mbalimbali (1Kor 16:1-4).

Ndiyo sababu barua ni ndefu na inagusa mambo mengi ambayo Paulo aliyatazama kwa hekima ya juu inayotokana na msalaba wa Kristo.

Madondoo muhimu[hariri | hariri chanzo]

Kati ya mambo mengi muhimu, barua hiyo inatunza simulizi la kwanza la karamu ya mwisho ya Bwana Yesu (11:23-25) na kanuni ya imani ya kwanza inayoorodhesha pia matokeo ya Yesu Kristo Mfufuka (15:3-8).

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Tafsiri ya Kiswahili[hariri | hariri chanzo]

  • [1] Agano Jipya kwa lugha ya Kiswahili

Vingine[hariri | hariri chanzo]

Wikiquote ina mkusanyiko wa dondoo kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya Agano Jipya bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Waraka wa kwanza kwa Wakorintho kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.