Kitabu cha Mormoni

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Toleo la mwaka 1930.
Toleo la mwaka 1930.
Kitabu cha Mormoni kwa Kiswahili.
Kitabu cha Mormoni kwa Kiswahili.


Kitabu cha Mormoni ni mwandiko wa kidini wa jumuiya ya Wamormoni walioitwa hivyo kufuatana na jina la kitabu hicho. Wenyewe huamini ni kitabu kitakatifu chenye neno la Mungu.

Mormoni anatajwa kama nabii na kiongozi wa kidini anayetambulishwa mle kama mhariri wa kitabu. Kitabu cha Mormoni kilitolewa mwaka 1830 na Mmarekani Joseph Smith, Mdogo aliyedai kuwa alitafsiri kitabu kutoka kwa mabamba ya dhahabu aliyopewa na malaika wa Mungu.

Habari ndani ya Kitabu cha Mormoni

Kitabu cha Mormoni
Kitabu cha Mormoni

Kufuatana na taarifa za kitabu, watu walihama nchi za Biblia mara tatu kwenda bara la Amerika.

Kundi la kwanza walikuwa Wayaredi walioondoka Mesopotamia baada ya kukwama kwa ujenzi wa Mnara wa Babeli.

Mnamo mwaka 600 KK kundi la Wayahudi walioongozwa na nabii Lehi waliondoka Yerusalemu kabla ya mji kuangamizwa na Wababuloni, wakajenga jahazi kubwa na kufika katika nchi mpya. Baada ya kifo cha Lehi wafuasi wa wanawe Nefi na Lamani walianza kugombana na kuwa makabila mawili adui.

Wanefi walikutana baadaye na wafuasi wa Muleki aliyekuwa mwana wa mfalme Zedekia wa Yuda waliokimbia wakati wa anguko la Yerusalemu wa mwaka 587 KK.

Kitabu cha Mormoni chaendelea kueleza jinsi Yesu alivyowatembelea Wanefi baada ya ufufuko wake na kuwapa mafundisho ya hotuba ya mlimani pamoja na chakula cha Bwana.

Wanefi na Walamani waliungana baadaye kwa karne kadhaa na kuishi kwa amani, lakini amani hiyo ikavurugika na Wanefi waliangamizwa kabisa katika vita vikali. Kabla ya mwisho wa taifa, Mormoni mnamo mwaka 400 BK alipokea maagizo ya Mungu kukusanya habari zote na kuziandika katika mabamba ya dhahabu yaliyofichwa mahali alipoyakuta Joseph Smith.

Historia au riwaya?

Nje ya Wamormoni habari hizo hutazamwa kuwa si ya kihistoria. Wataalamu wasio Wamormoni huamini ya kwamba Joseph Smith alitunga mwenyewe taarifa hizo pamoja na hadithi ya mabamba ya dhahabu. Smith mwenyewe alieleza ya kwamba alirudisha mabamba ya maandiko kwa malaika baada ya kuyatafsiri.

Hadi leo Kitabu cha Mormoni kimetafsiriwa katika lugha 72 za sehemu mbalimbali za dunia.

Viungo vya Nje

Makala hii kuhusu kitabu fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kitabu cha Mormoni kama Mwandishi wake, hadithi au matoleo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.