Mpako wa wagonjwa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sehemu ya mchoro Sakramenti Saba (1445) wa Roger van der Weyden ikionyesha Mpako wa Wagonjwa.


Sakramenti za Wakatoliki na Waorthodoksi

Mpako wa wagonjwa ni ibada maalumu kwa ajili ya wagonjwa inayotumiwa na Wakristo wa madhehebu mbalimbali kufuatana na desturi ya Mitume wa Yesu na agizo la Barua ya Yakobo.

Kwa Kanisa Katoliki, Waorthodoksi na madhehebu mengine machache ni sakramenti iliyowekwa na Yesu Kristo, ingawa Injili haisemi.

Pamoja na Kitubio ni kati ya sakramenti mbili za uponyaji, zinazolenga kumrudishia Mkristo afya ya roho na mwili, iliyoathiriwa na dhambi na ugonjwa.

Kadiri ya imani hiyo, Mpako wa Wagonjwa ulianzishwa na Yesu, kama sakramenti zote. Maandiko yanasimulia huruma yake iliyomfanya awaponye wengi kwa namna mbalimbali na kuwapa Mitume uwezo wa kufanya vilevile kwa “kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina” (Math 10:1). Nao “wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza” (Mk 6:13). “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa, nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa” (Yak 5:14-15).

Mafuta ya wagonjwa yanamaanisha lengo la kuwaponya na kuwarudishia nguvu na uzuri. Kama kawaida, maneno yanaweka wazi zaidi kuwa lengo si kuponya mwili tu, bali hasa roho kwa kuitia msamaha na faraja katika mateso ambayo huenda yakaendelea. Kwa kuwa Mungu haponyi mwili kila mara, isipokuwa kwa faida na wokovu wa mgonjwa na wa wengine. Kama ndiyo mapenzi yake, kila mmoja ajifunze kufaidika vilevile na ugonjwa: “Makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke. Naye akaniambia, ‘Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu’. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu” (2Kor 12:7-9). “Sasa nayafurahia mateso niliyo nayo kwa ajili yenu, tena nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua ya mateso ya Kristo, kwa ajili ya mwili wake, yaani, kanisa lake” (Kol 1:24).

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Ukristo wa magharibi

Ukristo wa mashariki

Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mpako wa wagonjwa kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.