Shirika la Utangazaji Tanzania

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru


Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC)
Nembo ya TBC
Nembo ya TBC
Kutoka mji Dar es salaam
Nchi Tanzania
Eneo la utangazaji Kote duniani
Kituo kilianzishwa mwaka 2000
Mwenye kituo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Tovuti tbc.go.tz

Shirika la Utangazaji Tanzania (zamani: Televisheni ya Taifa ya Tanzania) pia huitwa kwa Kiingereza: Tanzania Broadcasting Corporation ambapo mara nyingi huitwa kwa kifupi TBC, ni chombo cha habari kinachomilikiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Huwa inatangaza habari kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza.

Shirika hili lilianza tarehe 10 Machi mwaka 2000. Makao yake makuu yapo Kijitonyama jijini Dar es Salaam.

Zamani ilikuwa ikipatikana kwa Tanzania tu, lakini kwa sasa imepanua huduma yake ya urushaji wa matangazo na inapatikani karibuni Afrika nzima.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Kabla ya Uhuru[hariri | hariri chanzo]

Ikilinganishwa na maeneo mengine yaliyokuwa chini ya utawala wa Uingereza barani Afrika, kama vile Kenya, Zambia, na Nigeria, utangazaji wa redio na televisheni ulichelewa kufika Tanganyika.[1] Mwaka wa 1950, utawala wa Tanganyika ulimkabidhi W. H. Thorneycroft, mhandisi kutoka British Broadcasting Corporation (BBC) jukumu la kufanya uchunguzi juu ya uwezekano wa kuanzisha kituo cha redio kwa eneo hilo. Uchunguzi huo uliojulikana kama "Thorneycroft Plan". Juni 1950, Thorneycroft alipendekeza kuanzisha kituo cha majaribio ili kutoa uzoefu katika utayarishaji wa programu za ndani zinazolenga Waafrika. Serikali ya kikoloni iliweka dola 30,000 na kituo cha "Sauti ya Dar es Salaam" kikaanzishwa.[2] Matangazo ya redio yalianza rasmi tarehe 1 Julai 1951.[3] Wakati wa ziara yake mwishoni mwa mwaka wa 1951, Grenfell Williams aliona ilikuwa na wasikilizaji wachache na vifaa vya muda; na ukosefu wa Waafrika wenye elimu ilionyesha hitaji la msaada na mafunzo kutoka kwa BBC. BBC ilimtuma Mhandisi Mkuu, A. C. Rothney, ambaye alibadilishwa mnamo 1954 na A. B. Shone.[4] Mara ya kwanza ilitoa programu ya saa moja tu ya Kiswahili kila wiki, ambayo ilirudiwa mara mbili zaidi baadaye katika wiki na kwa sababu vifaa vyake havikuwa vya kisasa, ilikuwa vigumu kusikika nje ya Dar es Salaam.[5]

Wasanii wakiwa studio za Sauti ya Dar es Salaam miaka ya 1950.

Mnamo Februari 1952, transimita ya mawimbi ya kati ya Marconi 1¼ iliongezwa kwenye vifaa vinavyotumika, na baadaye, muda wa maongezi uliongezwa hadi saa moja kwa kila siku ambayo ilitangazwa jioni. [6]: 171 Mwaka wa 1953, programu iliongezwa hadi saa tatu kila siku, saa mbili kwa Kiswahili na moja kwa Kiingereza. Matangazo ya redio ya asubuhi kwa ajili ya shule yalianzishwa kwa hatua ya majaribio. Katika kukabali changamoto hizo mpya, afisa kutoka Idara ya Elimu alihamishiwa "Sauti ya Dar es Salaam". Zaidi ya hayo, Mwafrika mmoja na wazungu wawili wafanyakazi wa shirika hilo la utangazaji walirejea kutoka kozi za mafunzo zilizotolewa na BBC mjini London. Tatizo zaidi lilikuwa hali ya kifedha: hadi mwisho wa 1953, jumla ya ruzuku Pauni 66,000 zilikuwa zimetolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Kikoloni na Ustawi kwa ajili ya matumizi ya mradi huo.

Kuanzia Machi 1 hadi Aprili 30, 1954, matangazo ya kwanza ya vipindi vya kielimu yalianza kurushwa kusambaza elimu kwa shule za kati, shule za sekondari, na vituo vya mafunzo ya ualimu.[7] Jumla ya muda wa matangazo ya elimu ulikuwa saa tano kwa wiki, ambao ulitumiwa na programu ya matangazo ya shule (dakika 200), programu ya kufundisha Kiingereza "Sema Kiingereza" (dak. 60), na "Swahili by Radio" (dak. 40). Katika kipindi hicho, mapokeo tayari yalikuwa mazuri katika miji ya pwani, kama vile Tanga, Lindi, Mtwara, na Mombasa nchini Kenya, pamoja na Arusha, Kongwa, Nachingwea, na Mbeya.

Mwezi Machi 1955, Sauti ya Dar es Salaam ilibadilishwa hadhi na kuwa idara kamili ya serikali iliyopewa jina la Tanganyika Broadcasting Services (TBS). Kwa pesa za ufadhili utangazaji ulipanuliwa kufikia maeneo mengi ya nchi na makao makuu mapya yalianzishwa baadaye Pugu Road, Dar es Salaam (Sasa inajulikana kama Barabara ya Julius K. Nyerere).[8] TBS ilipatiwa ofisi chache, studio mbili, chumba cha uongozaji, maktaba ndogo ya rekodi, na kifaa cha kurekodi simu. Ilitumia transimita ya mawimbi mafupi ya Marconi kW 20, ambacho kilikuwa na nguvu zaidi katika Afrika ya Mashariki wakati huo, TBS ilisikika karibu eneo lote la nchi, pia ilisikika nchi mbali kama Japani, Ufini, na Nyuzilandi. [9] Matangazo ya TBS yalikuwa hewani kwa saa nane. Wakati wa mihula ya shule, vipindi vya elimu vilitangazwa kutoka saa mbili unusu hadi saa nne unusu asubuhi.

Ian Macleod alipotembelea Shirika la Utangazaji la Tanganyika, wakati wa ziara yake jijini Dar es Salaam, Desemba 1959.

Mnamo Februari 1956, mwanachama wa Huduma za Jamii aliwasilisha kwenye Baraza la Kutunga Sheria mswada wa shirika kuchukua madaraka ya huduma ya utangazaji. Alisisitiza kuwa itakuwa huru na haitaonekana kama chombo au mdomo wa Serikali. Katika mjadala uliofuata mjumbe mmoja aliuliza kama inaweza kuhamishiwa Dodoma katika ya nchi na mwingine alisisitiza haja ya kudhibiti uhariri sahihi na tahadhari juu ya kuanzishwa kwa utangazaji wa kibiashara.[10] Tarehe 1 Julai, 1956, TBS ilibadishwa na kuwa Tanganyika Broadcasting Corporation (TBC).[11] TBC ilikuwa shirika la umma kwa kufuata mtindo wa BBC. Hata hivyo uhuru wa kujiendesha na kujitawala ulibinywa kwa sababu ililazimika kufanya kazi na kufuatiliwa kwa karibu sana na serikali ya Kikiloni na kufanya kazi kama msemaji wa Serikali ya Kikoloni.[12]

Mnamo 1957, ruzuku ya Pauni 20,000 kutoka Mfuko wa Maendeleo na Ustawi wa Kikoloni na Ustawi (Colonial Development and Welfare Fund) ilipitishwa kwa ajili ya kupata transimita ya pili ya mawimbi mafupi (kw 10) na transimita nyingine ya mawimbi ya wastani (kw1¼). Kiasi cha Pauni 5,000 kinachohitajika kununua vifaa vipya kilitolewa na utawala. Jumla ya muda wa kurusha matangazo uliongezwa kutoka saa 27 hadi 37 kwa wiki. Takriban 70% ya vipindi vilitangazwa kwa Kiswahili. TBC ilitoa habari za ulimwengu kutoka Idhaa ya Kiswahili ya BBC yenye makao yake jijini London ambayo ilikuwa imezinduliwa tarehe 27 Juni 1957. Habari za kila siku za ndani kwa lugha ya Kiingereza zilipatikana kutoka gazeti la Tanganyika Standard.

Iain Macleod akiwa ameketi mbele ya kipaza sauti cha Shirika la Utangazaji la Tanganyika - Machi 1961.

Mnamo Mei 1958, Thomas W. Chalmers, afisa wa BBC, aliteuliwa kuwa mkurugenzi wa kwanza wa utangazaji. Chalmers, hapo awali alihusika kuendeleza Shirika la Utangazaji la Nigeria (NBC), akawa mtendaji mkuu wa bodi.[13]Tangu mwanzo, mkurugenzi alijitahidi kuhakikisha uhuru wa kisiasa wa TBC kwa kujaribu kuvutia matangazo ya biashara. Ingawa matangazo ya biashara yalianza kukubaliwa mwaka wa 1955, kituo bado kiliendeshwa kwa ruzuku ya serikali. Awali, shirika lilikuwa makini kufikia uwiano wa maoni wakati mada zenye utata zikijadiliwa. Lakini sera hii ilikuja kuwa chini ya shinikizo la serikali ili mijadala ya umma iendelee kwenye redio masuala fulani yakawa na ukomo zaidi.

Mwaka wa 1959, vifaa vya ziada, transimita ya mawimbi mafupi ya kW 10 na transimita ya mawimbi ya kati cha 1 ¼ kW, ziliongezwa. Kama matokeo ya uboreshaji huo, TBC iliweza kutangaza idhaa mbili kwa wakati mmoja - Idhaa cha Taifa kwa Kiswahili na idhaa ya pili kwa wasikilizaji wanaozungumza Kiingereza. Idhaa ya kwanza ilikuwa hewani asubuhi kutoka saa kumi na mbili na robo hadi saa mbili, mchana kutoka saa sita kamili hadi saa saba unusu, na jioni kutoka saa kumi unusu hadi saa nne na robo usiku. Idhaa ya pili, ambayo hasa ilitegemea kanda zilizorekodiwa na vyanzo vya nje kuhusu habari za Kitanzania, ilirusha matangazo yake kuanzia saa kumi na mbili kamili hadi saa mbili kamili asubuhi na kutoka saa moja jioni hadi saa nne na robo usiku. Zaidi ya hayo, kituo kilitangaza programu za kila siku kwa ajili ya wasikilizaji wa Kiasia kutoka saa kumi na mbili unusu mpaka saa moja jioni, matangazo hayo yalikuwa kwa lugha ya Hindustani na Gujerati.[14]

Tarehe 1 Julai 1960, TBC ilianzisha huduma yake ya habari, na Tanganyika Standard haikusambaza tena matangazo kwa kituo hicho ingawa TBC iliendelea kununua habari kutoka gazeti hilo kwa misingi ya uwakala. Kwa ripoti za kimataifa, TBC iliendelea kutegemea vipindi vya BBC katika lugha ya Kiingereza na Kiswahili. Hadi kufikia uhuru, matangazo ya redio katika nchi ya Tanganyika yalikuwa tayari yana matokeo ya kushangaza. Kwanza, visambaza sauti vitatu vya mawimbi mafupi ziliwezesha matangazo kupatikana karibu nchi nzima, na visambaza sauti viwili vya mawimbi ya kati zilihudumia Dar es Salaam na maeneo yake ya jirani. Pili, watu 94 kati ya 123 walioajiriwa na kituo walikuwa Waafrika waliofunzwa vyema na wenye uzoefu wa uendeshaji wa mfumo wa utangazaji.

Baada ya Uhuru[hariri | hariri chanzo]

Januari 1962, Mikidodi B. Mboe alimrithi Thomas Chalmers kama mkurugenzi wa utangazaji. Miongoni mwa matukio maarufu wakati wa Mboe ni kuanzishwa kwa Idhaa ya External Service na Idhaa ya tatu. Idhaa ya External Service iliyokuwa inarushwa na Radio Tanzania Dar es Salaam ilianzishwa mahususi kusaidia harakati za kupigania uhuru katika Rhodesia (sasa Zambia na Zimbabwe) na Nyasaland (sasa Malawi). Programu hii ilikuwa hewani kila siku kuanzia saa mbili kamili usiku hadi nne kamili usiku. Mwezi Machi 1964, matangazo ya Rhodesia na Nyasaland yalibadilishwa na programu ya ukombozi wa Afrika Kusini na Afrika Kusini Magharibi (sasa Namibia).[15] Ili kuongeza ufikiaji, iliongezwa transimita ya 100 kW kutoka China. Viongozi wa wapigania uhuru katika nchi hizo waliishi na kuratibu harakati za ukombozi katika nchi zao kutokea Tanzania ambapo walirusha matangazo ya redio ya kuhamasisha wananchi wao kushiriki katika mapambano hayo kupitia idhaa hiyo ya External Service. Mnamo Januari 1968, harakati nane za ukombozi, ikiwa ni pamoja na FRELIMO na SWAPO, walikuwa wakichangia urushaji wa matangazo ya redio katika lugha za Kiafrikaans, Kiingereza, Herero, Ndebele, Nyanja, Ovambo, Kireno, na Shona.[16] Baada ya nchi za Kusini mwa Afrika kupata uhuru, Idhaa ya External Service haikuendelea kurusha matangazo yake. Idhaa ya tatu pia ilianza shughuli zake mnamo 1962 na ililenga kuelimisha hadhira kwa kutangaza vipindi vya kielimu zaidi. Utangazaji wake ulikuwa hewani siku za wiki kutoka saa kumi na moja kamili hadi saa moja kamili jioni.

Orodha ya wakurugenzi wa shirika la utangazaji tangu mwaka 1958 hadi 1996.[17]
Jina Mwaka
Thomas W. Chalmers 1958 - 1962
Mikidodi B. Mboe 1962 - 1965
Yona Kazibure 1965 - 1967
Martin Kiama 1967 - 1972
Paul Sozigwa 1972 - 1979
David Wakati 1979 - 1991
Nkwabi Ng’wanakilala 1991 - 1994
Abdallah Ngororo 1994 - 1996
Abdul Ngarawa 1996

Mwaka 1965 Serikali ya kizalendo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipeleka Bungeni mswada wa kuvunjwa kwa Tanganyika Broadcasting Corporation (TBC) na Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) ilianzishwa kama idara ya Wizara ya Habari, Utangazaji na Utalii. Baada ya matangazo ya redio kuenea kulikuwa na shinikizo la kuongeza matangazo ya redio katika baadhi ya lugha za makabila, lakini Nyerere alikataa. Badala yake, RTD ilitumika kama njia ya kueneza Kiswahili kote nchini. Matangazo ya lugha ya Kiingereza yalifutwa mwaka 1970, Tanzania ikawa nchi pekee ya Kiafrika inayotumia lugha moja tu katika redio yake (Kiingereza bado kinatumika katika stesheni ya TBC International).[18] Muda wa matangazo ya kila siku uliongezeka hadi Saa 6 ¼ mnamo Septemba 26, 1970.

Bango la Radio Tanzania Dar es Salaam.

Serikali iliona redio kama njia yao bora ya kuunganisha vijiji na serikali na kuwahamasisha watu kujivunia nchi yao na kujaribu kuifanya kuwa bora zaidi. Uingizaji wa televisheni ulipigwa marufuku na sheria ya mwaka wa 1974, baraza la mawaziri la serikali ya Julius Kambarage Nyerere lilipinga kuanzishwa kwa televisheni, likisisitiza kuwa televisheni hiyo ilikuwa ghali sana na kwamba utangazaji wa redio Tanzania bado haujakamilika.

Hadi mwaka 1994, hapakuwa na matangazo yoyote ya televisheni yanayofanya kazi Tanzania Bara. Kituo pekee kilikuwa Televisheni ya Zanzibar (TVZ). TVZ ilianzishwa mwanzoni mwa miaka ya 1970 baada ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuingia mkataba na kampuni ya Uingereza kuanzisha kituo kisiwani humo.

Waandishi na wanahabari wa Redio Tanzania Dar es Salaam walipokwenda kumuaga Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Ikulu Dar es Salaam alipotangaza kustaafu mwaka 1985.

Mipango ya kuzindua kituo cha televisheni Tanzania bara ilifufuliwa mwaka wa 1985 wakati serikali ilipounda Kikosi Kazi cha Televisheni ambacho kilikuwa chini ya uenyekiti wa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Posta na Mawasiliano Tanzania (TPTC), F. C. Kasambala. Ripoti ya mwisho ya kikosi kazi iliyowasilishwa mnamo Oktoba 1989 ilisema mazingira yanaruhusu kuanzisha kituo cha televisheni na hivyo, ufungaji wa teknolojia hiyo unapaswa kuendelea haraka. Lakini kamati hiyo ilipoanza kuulizia gharama kutoka kwa taasisi za kimataifa ilionyesha ni ghali sana, kwa mfano, makadirio ya kwanza ya teknolojia ya upitishaji wa satelaiti yalifikia dola za Marekani bilioni moja. Tarehe 13 Oktoba 1989, gazeti la Business Times lilichapisha makala iliyodai: “Kwa Dola za Marekani milioni 7 tu ... Tanzania inaweza kuwa na TV.“ Siku chache tu baada ya makala ya Business Times kuchapishwa, mnamo Novemba 6, 1989, wakati huo Waziri wa Habari na Utangazaji, Hassan Diria, aliteua Kamati ya Ushauri ya Kiufundi ya Televisheni ambayo iliongozwa na Ambrose Ottaru. Baadaye, tarehe 12 Aprili 1990, kamati ilikabidhi ripoti yake kwa Diria. Ripoti hii ilipelekea kuwekwa kwa mikakati ya kukamilisha uanzishwaji wa kituo cha televisheni ifikapo mwaka 2000.[19]


Serikali ilianza kufanya majaribio ya huduma za matangazo ya Televisheni ya Taifa (TVT) tarehe 16 Oktoba 1999 na matangazo rasmi yakaanza terehe 15 Machi 2000. Tarehe 1 Julai, 2007 Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) na Televisheni ya Taifa (TVT) ziliunganishwa na kuwa Tanzania Broadcasting Corporation (TBC).

2010 - Sasa[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 2010, kampuni ya Star Media (T) Ltd yenye chapa ya StarTimes iliingia mkataba wa ushirikiano na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kurusha matangazo ya televisheni kidijitali.[20][21] StarTimes ni kampuni ya teknolojia ambayo ilianzishwa mwaka 1988, makao yake makuu yapo Beijing, China.[22]Baada ya kuibuka kwa hoja mbalimbali za kutilia mashaka mkataba huo,[23] wakati huo Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe aliunda Kamati ya kuchunguza ubia wa Kampuni ya StarTimes na TBC[24]. Aprili 13, 2018 mkataba mpya ulisainia ili kunufaisha kampuni zote mbili.[25]

Kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), serikali ilianzisha mpango wa kupanua usikivu maeneo yote nchini ambapo usikivu uliongezeka kutoka wilaya 87 mwaka 2017 sawa na asilimia 54 ambapo hadi Machi 2019 wilaya 102 zilifikiwa na matangazo ya redio ambayo ni sawa na asilimia 63.[26] Julai 26, 2021, UCSAF kwa kushirikiana na Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) ilizindua kituo cha kurushia matangazo ya TBC Taifa na TBC FM mkoani Dodoma,[27] kituo kama hicho kimejengwa pia katika mkoa wa Arusha na Morogoro kuboresha usikivu wa redio katika maeneo mbalimbali nchini.[28]

Agosti 3, 2021, Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) liliingia mkataba wa miaka 10 na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wa haki za kurusha matangazo ya redio ya mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara kuanzia msimu wa 2021/2022.[29]

Mkataba huo wenye thamani ya shilingi Bilioni 3.54 unaipa TBC haki ya kurusha matangazo kwa sauti[30] lakini hauvifungi vyombo vingine vya habari kurusha matangazo ya ligi kuu isipokuwa kwa makubaliano rasmi kati yao na TBC na TFF.[31]

Aprili 14, 2022, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa alizindua vituo vinne vya kuongeza usikivu wa redio za TBC Taifa na TBC FM vilivyopo Ruangwa (Lindi), Ludewa (Njombe), Mlimba (Morogoro) na Ngara (Kagera), tukio la uzinduzi limefanyika Ruangwa mkoani Lindi.[32]Vituo hivyo vilijengwa kwa ushirikiano na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF).

Programu[hariri | hariri chanzo]

TBC inarusha vipindi mbalimbali vinavyoakisi misimamo, mitazamo, maoni, mawazo, maadili, na ubunifu unaonyesha vipaji vya Kitanzania katika vipindi vya elimu na burudani, kutoa habari za aina mbalimbali, taarifa na uchambuzi kwa mtazamo wa Kitanzania na kuendeleza maslahi ya taifa na ya umma.[33]

Vituo[hariri | hariri chanzo]

TBC inaendesha matangazo ya redio na televisheni kwa umma. Matangazo ya televisheni yana chaneli tatu ambazo ni TBC1, TBC2 na chaneli mpya ya Tanzania Safari Chanel (Chaneli ya kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania)[34], hali ya kuwa matangazo ya redio yana chaneli tatu ambazo ni TBC Taifa, TBC FM na TBC International. TBC inapatikana pia kupitia satelaiti na mtandaoni.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Mytton, Graham (1983). Mass Communication in Africa (kwa Kiingereza). E. Arnold. uk. 78. ISBN 0713181400.  Check date values in: |year= (help)
  2. Katz, Elihu; Wedell, George (1978). Broadcasting in the Third World (kwa Kiingereza). Harvard University Press. ku. 247 – 250. ISBN 9780674494152. Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2022-07-05. Iliwekwa mnamo 2022-07-01.  Check date values in: |year= (help)
  3. Stephen Luscombe. "Advent of Radio & Broadcasting in Tanganyika: The African Archers". www.britishempire.co.uk. Iliwekwa mnamo 2022-06-27. 
  4. Armour, Charles (July, 1984). The BBC and the Development of Broadcasting in British Colonial Africa 1946-1956 (kwa Kiingereza). Oxford University Press on behalf of The Royal African Society. uk. 387.  Check date values in: |date= (help)
  5. Gunther, John (1955-1-1). Inside Africa (kwa Kiingereza). Harper & Brothers. ASIN B00005W6XZ.  Check date values in: |date=, |year= (help)
  6. Mytton, Graham (1976). The role of the mass media in nation-building in Tanzania. [Great Britain] : University of Manchester, 1976. uk. 171. OCLC 1065292903.  Check date values in: |accessdate= (help);
  7. Polomé, Edgar C.; Hill, C. P. (May 31, 2018). Routledge Revivals: Language in Tanzania (1980). Routledge. ISBN 9781138307582. Iliwekwa mnamo 29 June 2022.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  8. Armour, Charles (July, 1984). The BBC and the Development of Broadcasting in British Colonial Africa 1946-1956 (kwa Kiingereza). Oxford University Press on behalf of The Royal African Society. uk. 387.  Check date values in: |date= (help)
  9. Colonial (Great Britain. Colonial Office) (1957). Tanganyika Under United Kingdom Administration: Report by Her Majesty's Government in the United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland to the General Assembly of the United Nations for the Year. Colonial Office. uk. 43.  Check date values in: |accessdate= (help);
  10. Armour, Charles (July, 1984). The BBC and the Development of Broadcasting in British Colonial Africa 1946-1956 (kwa Kiingereza). Oxford University Press on behalf of The Royal African Society. uk. 388.  Check date values in: |date= (help)
  11. Bourgault, Louise M. (June 22, 1995). Mass Media in Sub-Saharan Africa. Indiana University Press. ku. 66 - 67. ISBN 978-0253209382. Iliwekwa mnamo 29 June 2022.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  12. "Tanzanian Broadcasting Corporation". tanzania.mom-gmr.org (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-06-26. 
  13. Colonial (Great Britain. Colonial Office) (1959). Tanganyika Under United Kingdom Administration: Report by Her Majesty's Government in the United Kingdom of Great Britain and Northern Ireland to the General Assembly of the United Nations for the Year. Colonial Office. uk. 96.  Check date values in: |accessdate= (help);
  14. Sturmer, Martin (1998). The Media History of Tanzania. Ndanda Mission Press, 1998. ku. 82 – 83. ISBN 9789976635928.  Check date values in: |accessdate= (help);
  15. Sturmer, Martin (1998). The Media History of Tanzania. Ndanda Mission Press, 1998. uk. 112. ISBN 9789976635928.  Check date values in: |accessdate= (help);
  16. MWAFFISI, M. S. (1985). Broadcasting in Tanzania: Case Study of a Broadcasting System. MA-Thesis, University of Washington. uk. 91.  Check date values in: |accessdate= (help);
  17. Sturmer, Martin (1998). The Media History of Tanzania. Ndanda Mission Press, 1998. ku. 82 – 83. ISBN 9789976635928.  Check date values in: |accessdate= (help);
  18. "Radio in Tanzania". www.pateplumaradio.com. Iliwekwa mnamo 2022-06-27. 
  19. Sturmer, Martin (1998). The Media History of Tanzania. Ndanda Mission Press, 1998. ku. 203 – 204. ISBN 9789976635928.  Check date values in: |accessdate= (help);
  20. "Star Africa Media in regional expansion drive". The New Times | Rwanda (kwa Kiingereza). 2009-07-24. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  21. "Chinese media company contributes to Tanzania's digital migration - China.org.cn". www.china.org.cn. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  22. "China-based StarTimes makes big march in Africa - CCTV News - CCTV.com English". english.cctv.com. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  23. "Magufuli Atilia Mashaka Mkataba wa TBC na Startimes". https://www.ippmedia.com. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  24. "Dkt Mwakyembe aunda kamati kufuatilia utekelezaji mkataba wa TBC na Star Times". Bongo5.com (kwa en-US). 2017-07-15. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  25. "Kampuni ya Star Media yaingia mkataba na TBC". Muungwana BLOG. Iliwekwa mnamo 2022-06-30. 
  26. Michuzi Blog. "External Service ya RTD ilisaidia nchi za kusini mwa Afrika kupata uhuru". MICHUZI BLOG. Iliwekwa mnamo 2022-07-03. 
  27. "TBC yazindua redio kwa mikoa kanda kati". dodomacc.go.tz (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-06-29. 
  28. "UCSAF | Serikali yadhamiria kumaliza tatizo la usikivu wa radio ifikapo 2025". www.ucsaf.go.tz. Iliwekwa mnamo 2022-06-29. 
  29. "TBC, TFF zaingia mkataba wa haki ya matangazo". Mwanaspoti (kwa Kiingereza). 2021-08-03. Iliwekwa mnamo 2022-06-29. 
  30. "TFF seals 3bn/- Premier League radio broadcasting rights". IPP Media (kwa Kiingereza). 2021-08-04. Iliwekwa mnamo 2022-06-29. 
  31. "TBC na TFF Waingia Mkataba Matangazo ya Redio – TFF" (kwa en-US). Iliwekwa mnamo 2022-06-29. 
  32. "WMTH | Habari". www.mawasiliano.go.tz. Iliwekwa mnamo 2022-07-02. 
  33. "Tanzanian Broadcasting Corporation". tanzania.mom-gmr.org (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2022-06-26. 
  34. "Premier launches Tanzania Safari Channel | Embassy of Tanzania in Tel Aviv, Israel". il.tzembassy.go.tz. Iliwekwa mnamo 2022-06-26. 

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]