Baraza la Mawaziri

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Baraza la mawaziri ni baraza linaloongoza tawi la utendaji la serikali. Wanachama wa baraza huitwa mawaziri ama makatibu, k.m. Kenya na Marekani.

Kazi ya baraza la mawaziri inatofautiana kulingana na nchi: katika baadhi ya nchi, ni kikundi kilicho na wajibu wa kufanya maamuzi kwa pamoja, kwingine, linaweza kuwa kikundi cha washauri au wasaidizi katika kufanya maamuzi kwa mkuu wa nchi au mkuu wa serikali. Baraza la mawaziri huwa na wajibu wa usimamizi wa kila siku wa shuguli za serikali.

Waziri huwa na jukumu la kutawala wizara, au idara Marekani. Pia, mawaziri huwa waanzilishi wazuri na muhimu wa miswada bungeni.

Uteuzi wa wanachama[hariri | hariri chanzo]

Katika mfumo wa serikali ya kiraisi kama Kenya, wanachama wa baraza la mawaziri huchaguliwa na rais, nao wanaweza kuchujwa na kupitishwa na bunge. Katika nchi nyingi, wanachama wa baraza la mawaziri hawawezi kuwa wabunge, na wabunge wanaoteuliwa lazima wajiuzulu ili wachukue wadhifa.

Katika demokrasia za serikali ya kibunge, sera kadhaa zipo. Kama vile, wajumbe wa baraza la mawaziri lazima wawe, hawawezi, au wanaweza kuwa wabunge, kulingana na nchi. Katika Uingereza, mawaziri lazima wateuliwe kutoka wabunge waliopo. Katika nchi zilizo na sera kali ya utengano baina ya matawi ya utendaji na bunge, kwa mfano, Lasembagi, Uswisi na Ubelgiji, wanachama wa baraza la mawaziri lazima wajiuzulu kutoka nafasi zao za bunge. Kuna nchi zilizo wastani ambapo mawaziri ni wabunge lakini hali haijalazimishwa iwe hivyo, kama kwa mfano katika Ufini. Waziri mkuu mgombea na/au rais mteule hupendekeza mawaziri katika bunge, ambalo linaweza kukubali au kukataa mapendekezo ya orodha ya mawaziri. Tofauti na mfumo wa kiraisi, baraza la mawaziri katika mfumo wa kibunge lazima lipitishwe na bunge, na waendelee kuwa na imani ya bunge: bunge linaweza kupitisha hoja ya kutokuwa na imani na kuondoa serikali nzima au waziri binafsi. 

Katika baadhi ya nchi (kwa mfano Tanzania na Kenya) mwanasheria mkuu pia ni mwanachama wa baraza la mawaziri, wakati katika baadhi ya nchi, ofisi ya mwanasheria mkuu huchukuliwa kuwa sehemu ya tawi la mahakama na kwa hiyo haruhusiwi kuwa katika baraza la mawaziri. Badala yake, kuna waziri wa sheria, tofauti na mwanasheria mkuu wa serikali. Aidha, katika Uswidi, Ufini na Estonia, baraza la mawaziri huwa na Kansela wa Sheria, mtumishi wa umma anayetenda kama mshauri wa kisheria wa baraza la mawaziri.

Katika demokrasia za vyama vingi, kuunda serikali kunahitaji msaada wa vyama mbalimbali. Kwa hivyo, serikali ya muungano hutungwa. Ushirika endelevu baina ya vyama shirika ni muhimu ili kudumisha imani ya bunge kwa baraza.

Asili ya baraza la mawaziri[hariri | hariri chanzo]

Malkia Victoria aliitisha Baraza Faragha siku yake ya kutawazwa mwaka 1837.

Katika Uingereza na makoloni yake, mabaraza ya mawaziri yalianza kama makundi madogomadogo ya Baraza Faragha la Uingereza.[1]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya sheria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Baraza la Mawaziri kama historia yake au uhusiano wake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.