Nenda kwa yaliyomo

Samia Suluhu Hassan

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Samia Hassan Suluhu)
Samia Suluhu Hassan


Aliingia ofisini 
17 Machi 2021
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa
Makamu wa Rais Philip Mpango
mtangulizi John Magufuli

tarehe ya kuzaliwa 27 Januari 1960 (1960-01-27) (umri 66)
Usultani wa Zanzibar
jina ya kuzaliwa Samia Suluhu Hassan
utaifa Mtanzania
chama Chama Cha Mapinduzi
ndoa Hafidh Ameir
watoto Mwanu Hafidh Ameir,Wanu Hafidh Ameir
mhitimu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe
Chuo Kikuu cha Manchester
Chuo Kikuu Huria cha Tanzania
SNHU
dini Uislamu

Samia Suluhu Hassan (alizaliwa 27 Januari 1960) ni Rais wa 6 wa Tanzania na mwanachama wa chama tawala cha Chama Cha Mapinduzi.[1] Kabla ya kuwa rais kutokana na kifo cha John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, Suluhu alikuwa makamu wa rais kwa sababu ya kuwa mgombea mwenza katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.[2]

Tarehe 5 Novemba 2015 aliapishwa kama makamu wa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akiwa mwanamke wa kwanza kufikia cheo hicho, akarudia baada ya uchaguzi mkuu wa tarehe 29 Oktoba 2020.

Sasa amekuwa rais wa kwanza mwanamke Tanzania na Afrika Mashariki na pia rais wa pili kutoka Zanzibar, wa kwanza akiwa Ally Hassan Mwinyi, Rais wa awamu ya pili.

Uchaguzi wa Oktoba 2025, uliomhakikishia Samia Suluhu Hassan ushindi wa asilimia 97.66 ya kura kadiri ya Tume ya Uchaguzi,[3] uligubikwa na tuhuma za wizi mkubwa wa kura na ukandamizaji mkali wa upinzani. Ujumbe wa waangalizi wa Umoja wa Afrika (AU) ulitangaza kuwa uchaguzi huo "haukuafiki" viwango vya kikanda na kimataifa, ikitaja kasoro nyingi na kukatwa kwa intaneti.[4]

Ofisi husika ya Umoja wa Mataifa na mashirika mengi ya haki za binadamu yalishutumu serikali yake kwa kuruhusu matumizi ya risasi za moto dhidi ya raia.[5] [6] Chama kikuu cha upinzani, Chadema, kilidai kuwa kimekusanya ushahidi wa vifo vya watu 1,000, kikiyaita matukio hayo kuwa ukiukwaji wa haki za binadamu.[3] Serikali ilikanusha madai hayo, huku Rais Hassan akikiri kutokea kwa vifo, alieleza kuwa idadi iliyotolewa na upinzani "imetiwa chumvi kupita kiasi".[7]

Tarehe 3 Novemba 2025 aliapishwa kwa awamu ya pili na kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Maisha ya awali

[hariri | hariri chanzo]

Suluhu alizaliwa katika Usultani wa Zanzibar.

Alisoma shule za msingi za Chwaka (Unguja), Ziwani (Pemba) na Mahonda (Unguja) katika miaka ya 1966 hadi 1972.

Aliendelea na masomo ya sekondari shule za Ngambo, Unguja (1973-1975) na Lumumba, Unguja (1976).[8]

Baada ya kumaliza masomo yake ya sekondari mnamo 1977, aliajiriwa na Wizara ya Mipango na Maendeleo kama karani. Alifuata kozi fupi kadhaa. Mnamo 1986, alihitimu kutoka Taasisi ya Usimamizi wa Maendeleo (Chuo Kikuu cha Mzumbe cha leo) na diploma ya hali ya juu katika utawala wa umma. [9]

Baada ya kuhitimu, aliajiriwa kwenye mradi uliofadhiliwa na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (World Food Programme). Kati ya miaka 1992 na 1994, alisoma kwenye Chuo Kikuu cha Manchester, Uingereza na kuhitimu stashahada ya uzamili katika uchumi. [10]

Mnamo mwaka 2015, alipata MSc yake katika Maendeleo ya Uchumi wa Jamii kupitia mpango wa pamoja kati ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Chuo Kikuu cha Kusini mwa New Hampshire. [11]

Kazi ya siasa

[hariri | hariri chanzo]

Mnamo mwaka 2000 aliamua kujiunga na siasa. Aliteuliwa na CCM kama mbunge wa viti maalumu katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar akateuliwa na rais Amani Karume kuwa waziri wa utalii na bishara. Alikuwa mwanamke pekee kwenye ngazi ya mawaziri akaona alidharauliwa na wenzake wa jinsia ya kiume kwa sababu ya jinsia yake. [12] Alichaguliwa tena mnamo 2005 kwenye viti maalum na aliteuliwa tena kama waziri katika wizara ya kazi, jinsia na watoto. [13]

Mwaka 2010 aligombea kwenye uchaguzi kwa Bunge la Kitaifa, akisimama katika jimbo la Makunduchi na kushinda kwa zaidi ya % 80. [14] Rais Jakaya Kikwete alimteua kuwa Waziri wa Nchi wa Mambo ya Muungano. [15] Mnamo 2014, alichaguliwa kama Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba iliyokuwa na jukumu la kuandaa katiba mpya ya nchi. [16] Mnamo tarehe 30 Aprili 2021 alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa CCM [17] akiwa mwenyekiti wa kwanza mwanamke.

Rais wa Tanzania

[hariri | hariri chanzo]

Samia Suluhu Hassan ni Rais wa sasa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). [18] Aliapishwa kushika madaraka tarehe 19 Machi 2021 kufuatia kifo cha Rais John Magufuli kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, na kuwa kiongozi wa kwanza mwanamke wa nchi hiyo. [19] Baadaye alikiongoza chama tawala katika uchaguzi mkuu wa 2025, ambapo CCM ilibaki madarakani na yeye kuchaguliwa tena kuwa rais kwa asilimia 97.66 ya kura, ikiendeleza utawala wa muda mrefu wa chama hicho katika siasa ya Tanzania. [20]

Urais wake umehusishwa na mabadiliko ya kisera pamoja na mijadala ya kisiasa. Ingawa mwanzo wa utawala wake ulionekana kuleta mazingira ya kisiasa yaliyo wazi zaidi, ikiwemo kupungua kwa baadhi ya vikwazo vya vyombo vya habari na ushiriki wa kisiasa, kumekuwa na wasiwasi kutoka kwa vyama vya upinzani na asasi za kiraia kuhusu kuendelea kuwepo kwa mipaka ya ushindani wa kisiasa, taarifa za kukamatwa au shinikizo la kisheria kwa wanasiasa wa upinzani, na vizuizi vya mikutano ya hadhara katika baadhi ya matukio. [21] Hali hizi zimeendelea kuwa sehemu ya mijadala ya kisiasa nchini. [22]

Kama mkuu wa nchi na serikali, anaongoza tawi la utendaji, mwelekeo wa sera za taifa, na mahusiano ya kimataifa. Serikali yake imejikita katika maendeleo ya kiuchumi, upanuzi wa miundombinu, na kuimarisha nafasi ya Tanzania katika mashirika ya kikanda kama Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika. [18] Vipaumbele vya kiuchumi vimejumuisha kuvutia uwekezaji wa kigeni na kuboresha miundombinu ya biashara na usafirishaji. [23]

Tanzania inaendelea kufanya kazi chini ya mfumo wa vyama vingi ambapo CCM bado ndiyo nguvu kuu ya kisiasa. Ingawa vyama vya upinzani hushiriki katika uchaguzi, vinakabiliwa na changamoto za kimuundo na kisiasa katika ushindani wa kitaifa, kama inavyoonekana katika matokeo ya 2025 ambapo CCM ilishinda viti 270 kati ya 272 vya wabunge vilivyochaguliwa moja kwa moja. [24] Maisha ya kisiasa nchini yanaathiriwa na mfumo huu wa muda mrefu wa chama tawala, pamoja na mijadala inayoendelea kuhusu utawala bora, uwajibikaji, na nafasi ya demokrasia. [25]

Samia Suluhu Hassan bado ni mhusika mkuu katika siasa za kisasa za Tanzania, akiwakilisha mwendelezo wa chama tawala huku pia akisimamia mabadiliko ya taratibu katika sera na utawala. Uongozi wake unaakisi muundo mpana wa siasa ya Tanzania, ambapo uthabiti wa taasisi na utawala wa chama kimoja kikuu huambatana na mijadala inayoendelea kuhusu mageuzi ya kisiasa na ushiriki wa wananchi. [23]

Makamu wa Rais

[hariri | hariri chanzo]

Mnamo Julai 2015, mteule wa urais wa CCM, John Magufuli alimchagua kuwa mgombea mwenza wa uchaguzi wa 2015 na kumfanya kuwa mgombea mwenza wa kwanza mwanamke katika historia ya chama hicho. [26] Baadaye alikuwa makamu wa rais wa kwanza mwanamke katika historia ya nchi kutokana na ushindi wa Magufuli katika uchaguzi. [27]

Maisha ya binafsi

[hariri | hariri chanzo]

Mnamo 1978 aliolewa na Hafidh Ameir aliye kwa sasa afisa kilimo mstaafu. Wana watoto wanne: binti mmoja na wavulana watatu. [28] Binti yake Wanu Hafidh Ameir (aliyezaliwa 9 Februari 1982), mtoto wa pili, ni mbunge wa viti maalum katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. [29]

  1. "Member of Parliament CV". Bunge la Tazania. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2015-07-13. Iliwekwa mnamo 19 Februari 2013.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  2. Mgombea mwenza Urais 2015 wa Mhe. John Pombe Magufuli ni..
  3. 1 2 (Kiingereza) Tanzania: Killings, Crackdown Follow Disputed Elections, Human Rights Watch, 4 Novemba 2025 (ilifikiwa 6 Novemba 2025)
  4. (Kiingereza) African Union observers slam Tanzania's violent election, African Business, 6 Novemba 2025 (ilifikiwa 6 Novemba 2025)
  5. https://www.ohchr.org/en/press-releases/2025/11/tanzania-election-related-killings-and-other-violations-must-be-investigated
  6. https://news.un.org/en/story/2025/11/1166334
  7. (Kiingereza) Tanzanian police warn against sharing images following deadly election protests, CNBC Africa (citant Reuters), 5 Novemba 2025 (ilifikiwa 6 Novemba 2025)
  8. [https://www.bbc.com/swahili/habari/2015/07/150712_profile_ccm_amina_salum_ali Wasifu wa makamu wa rais wa Tanzania Samia Hassan], tovuti ya BBC 13.07 / 05.11. 2015
  9. "Member of Parliament CV". Parliament of Tanzania. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 13 Julai 2015. Iliwekwa mnamo 19 Februari 2013.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  10. https://www.tanzania.go.tz/profiles/profiles/details/138 Ilihifadhiwa 22 Septemba 2020 kwenye Wayback Machine. Profile Details : Former VP of Tanzania, Tovuti ya serikali ya Tanzania, iliangaliwa Machi 2021
  11. "Member of Parliament CV". Parliament of Tanzania. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 13 Julai 2015. Iliwekwa mnamo 19 Februari 2013.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  12. Samia Suluhu Hassan, a tough journey, gazeti la Daily News, tarehe 18 Septemba 2014
  13. Tovuti ya Bunge 2010-2015
  14. Samia Suluhu Hassan, a tough journey, gazeti la Daily News, tarehe 18 Septemba 2014
  15. "Tanzania: History Made as Samia Picked Running Mate". AllAfrica. 13 Julai 2015.{{cite news}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  16. "Tanzania: Union 'Stalwart' Samia Is CA Vice-Chairperson". AllAfrica. 14 Machi 2014.{{cite news}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  17. https://www.bbc.com/swahili/live/habari-56939323
  18. 1 2 "Samia Suluhu Hassan". World Bank Live. World Bank. 2021. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  19. "Who is Samia Suluhu Hassan?". EdUKaid. EdUKaid. 2021. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  20. "Samia Suluhu Hassan wins Tanzania's presidential election". Xinhua. Xinhua News Agency. Novemba 1, 2025. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  21. "Missed Opportunity on Tanzania Election Violence". Human Rights Watch. HRW. Mei 5, 2026. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  22. "East African Autocrats Blame "Outsiders" for Popular Discontent". CFR.org. Council on Foreign Relations. Aprili 28, 2026. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  23. 1 2 "Tanzania Country Report 2026". bti-project.org. Bertelsmann Stiftung. Aprili 26, 2026. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  24. "United Republic of Tanzania National Assembly October 2025 Election". IPU Parline. Inter-Parliamentary Union. Novemba 2025. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  25. "President Samia Suluhu Hassan Wins Tanzania 2025 Election". TanzaniaInvest. TanzaniaInvest. Novemba 1, 2025. Iliwekwa mnamo Mei 7, 2026.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  26. Mohammed, Omar (12 Julai 2015). "Tanzania's ruling party nominates John Magufuli as presidential candidate". Quartz. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 11 Agosti 2015. Iliwekwa mnamo 12 Agosti 2015.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  27. "CCM's John Magufuli declared Tanzania fifth president". Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2015-10-31. Iliwekwa mnamo 2021-03-18.
  28. Samia Suluhu Hassan, a tough journey, gazeti la Daily News, tarehe 18 Septemba 2014
  29. "Hon. Wanu Hafidh Ameir". www.zanzibarassembly.go.tz. Ilihifadhiwa kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2021-03-18. Iliwekwa mnamo 2021-03-18.
Alitanguliwa na
John Magufuli
Rais wa Tanzania
2021-
Akafuatiwa na
[[]]