Korea Kaskazini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Korea Kaskazini


Korea ya Kaskazini (jina rasmi: Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Korea) ni nchi ya Asia ya Mashariki iliyoko kwenye nusu ya kaskazini ya rasi ya Korea.

Imepakana na Korea Kusini, China na Urusi.

Mji mkuu ni Pyongyang.

Historia

Korea Kaskazini kama nchi ya pekee ni tokeo la ugawaji wa Korea baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia.

Korea yote ilikuwa koloni la Japan kuanzia 1910 hadi mwaka 1945. Kwenye mwisho wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia jeshi la Urusi liliwafuata Wajapani kaskazini mwa rasi na Wamarekani waliingia kusini.

Mwanzoni kulikuwa na majadiliano ya kuunganisha Korea tena lakini Vita Baridi ilileta uadui kati ya pande hizo mbili. Kila moja ilianzisha serikali ya pekee katika kanda la utawala wake kufuatana na itikadi yake. Warusi walitaifisha tasnia na ardhi wakaacha serikali ya kikomunisti katika kaskazini na Wamarekani waliacha uchumi wa kibepari na serikali iliyochaguliwa katika kusini.

Katika vita ya Korea iliyofuata Korea ya Kaskazini iliweza kudumu kwa sababu ya msaada msaada wa kijeshi wa China iliyomwaga askari milioni moja nchini.

Kiongozi Mkomunisti Kim Il-Sung alishika mamlaka akatawala kama dikteta kwa msaada wa chama cha kikomunisti na jeshi.

Alipokufa mwaka 1994 mwana wake Kim Jong-il alichukua nafasi yake hadi alipofariki tarehe 17 Desemba 2011. Nafasi yake ilichukuliwa na mtoto wake Kim Jong-un.

Kim Il-Sung aliunda itikadi ya "Juche"; inaitwa falsafa ya kuendeleza Umaksi, lakini hali halisi ni itikadi inayotakiwa kutoa msingi kwa utawala wa kidikteta. Ingawa ilidai kutafuta maendeleo ya kujitegemea, Korea Kaskazini ilikuwa nchi iliyotegemea msaada kutoka Urusi kwa historia yake yote.

Baada ya mwisho wa Umoja wa Kisovyeti msaada huo ulikwisha na Korea Kaskazini iliingia katika kipindi kigumu sana kiuchumi.

Leo hii nchi haiwezi kulisha watu wakeː hutegemea usaidizi wa vyakula kutoka jumuiya ya kimataifa.

Udikteta katika Korea Kaskazini ni wa Kikomunisti kwa jina, lakini una tabia za kidini ndani yake. Kim Il-Sung alitangazwa kuwa "rais wa milele"; Kim Jong-Il hakutumia cheo rasmi isipokuwa "mwenyekiti wa kamati ya utetezi wa taifa" kinachomaanisha kitu kama "mkuu wa jeshi".

Katika mwaka 2006 Korea Kaskazini ililitekeleza mlipuko wa nyuklia.

Miji

Mji mkubwa ni Pyongyang ambao, pamoja na rundiko la jiji, una wakazi 3,702,757 (1 Januari 2005) na hivyo asilimia 16 za taifa huishi katika mji mkuu.

Miji mikubwa mingine haipitii nusu milioni ya wakazi. Watu wa Korea Kaskazini hawawezi kuhama kwa hiari yao kutoka mahali pamoja kwenda penginepo bila kibali.[1]

Watu

Wakazi karibu wote ni Wakorea asilia, isipokuwa Wachina na Wajapani wachache.

Lugha yao ni Kikorea, kinachotumika hata Korea Kusini na katika maeneo kadhaa ya China.

Upande wa dini, kuna dhuluma kubwa, ingawa katiba inatangaza uhuru. Kwa jumla kumbukumbu za nchi katika kuheshimu haki za binadamu si nzuri hata kidogo. Pamoja na hayo, 16% wanafuata dini za jadi, 13.5% Uchondo (mchanganyiko wa dini za jadi, Ubuddha, Utao na Ukatoliki), 4.5% ni Wabuddha na 1.7% Wakristo.

Uchumi

Maendeleo mwanzoni chini ya mfumo wa Ukomunisti

Picha ya Rasi ya Korea mnamo Machi 2017 kutoka angani wakati wa usiku inaonyesha upungufu wa umeme katika kaskazini; Korea Kusini inaonyesha nuru nyingi lakini Kaskazini iko gizani

Uchumi wa pande zote mbili za Korea ulikuwa duni sana baada ya Vita Kuu ya Pili. Mwanzoni nchi ilifuata mfano wa kutunga mipango ya miaka mitano kama Umoja wa Kisovyeti (Urusi). Viwanda, maduka na biashara yote vilitaifishwa na kuwekwa mkononi mwa dola. Siasa ililenga hali ya kujitegemea na biashara ya nje ilitekelezwa tu na nchi za kikomunisti. Pamoja na msaada kutoka Urusi na China kulikuwa na maendeleo ya haraka ya kiuchumi hadi mnamo 1960. Hapo tija ya mfumo wa uchumi unaopangwa ulianza kufikia misho wake na kuonyesha upungufu wa nguvukazi, ardhi ya kulima na vyombo vya usafiri na malengo ya mipango hayakufikiwa tena[2].

Kuanzia 1980 Korea Kusini ilianza kupita mafanikio ya uchumi wa kaskazini. [3]

Mwaka 1993 Korea Kaskazini iliacha kutangaza mipango ya uchumi.[4]

Kuporomoka kwa uchumi tangu 1990

Kuanzia mnamo 1991 kuporomoka kwa Umoja wa Kisovyeti na nchi nyingine za kikomunisti kulileta kupotea kwa masoko ya nje na mwisho wa misaada kutoka nje. Uzalishaji wa vyakula ulipungua sana kwa sababu matrekta na mashine nyingine ziliharibika bila vipuli kupatikana, Viwanda vya mbolea vilikwama kutokana na uhaba wa mafuta na kuharibika kwa mashine. Baada ya mafuriko na maafa ya asilia mengine uchumi uliporomoka kabisa. Wananchi walianza kuona njaa iliyoua angalau nusu milioni katika kipindi cha 1994 hadi 2000 [5]

Kuanzia mwaka 2000 msaada wa kimataifa ulileta msaada lakini uchumi ulibaki duni kwa sababu miundombinu iliyochakaa na uzalishaji mdogo wa umeme. Majaribio ya kulegeza uchumi wa kupangwa yalileta nafuu kwa sehemu za wananchi ilhali wanachama wa chama tawala, jeshi na wakazi wa miji mikubwa hasa Pyonyang walipewa kipaumbele lakini hali mbaya imeendelea hasa vijijini. Serikali bado inatwala karibu viwanda vyote na asilimia kubwa ya pato la taifa linatumiwa kwa jeshi ambalo ni jeshi kubwa duniani. [6]

Kuanzia mwaka 1998 masoko madogo ya wakulima yaliruhusiwa. Serikali ilijaribu kuyabana tena tangu mwaka 2009 lakini ililazimishwa kuyaruhusu tena[7].

Vyakula na makazi hutolewa kwa bei pungufu kwa misaada ya serikali, elimu na huduma za afya ni bure. [8] Kodi za mapato zilifutwa rasmi mwaka 1974.[9]

Kuna bidhaa katika maduka ya Pyongyang lakini hali ni tofauti katika sehemu kubwa za nchi.[10] ilhali wananchi wengi hutegemea masoko madogo.

Hata hivyo hadi mwaka 2017 Umoja wa Mataifa hutoa taarifa kuwa watu 2 kati ya 5 (40%) hawana chakula cha kutosha, hali inayoathiri hasa watoto. Zaidi ya asilimia 70 za wakazi wa Korea kaskazini hutegemea msaada wa chakula. Wakati wa mwaka 2016 ugawaji wa nafaka na viazi ulipungua kutoka lengo la gramu 380 kwa mtu na siku hadi gramu 300 pekee kwa miezi kadhaa.[11]

Jeshi

Jeshi la Wananchi wa Korea ni jeshi la Korea Kaskazini lenye askari 1,106,000, kwa hiyo nchi hii iko kati ya nchi tano duniani zilizo na jeshi la kudumu lenye askari zaidi ya milioni. Kulingana na idadi ya wakazi wanajeshi ni wengi kabisa; kuna mwanajeshi 1 kwa raia 20[12]. (kwa ulinganifu Uhindi uhusiano ni 1:865, Marekani 1:220). Pamoja na wanamgambo kuna watu milioni 4.7 waliotayarishwa kubeba silaha.

Jeshi huwa na matawi matano:

  • Jeshi la ardhi
  • Jeshi la maji
  • Jeshi la anga
  • Jeshi la makombora
  • Jeshi la shughuli mahsusi

Amri ya juu imo mikononi mwa kamati mbili: moja ni kamati ya ulinzi ya Chama cha Wafanyakazi wa Korea na nyingine ni Kamati ya Kisiasa ya Dola inayosimamia pia wizara ya ulinzi.

Wanaume wote wanakaguliwa na wanaweza kuandikishwa jeshini kwa miaka 10. Tangu mwaka 2015 pia wanawake wenye umri wa 17-20 waliomaliza shule ya sekondari wanaandikishwa kwa miaka 3. [13]

Jeshi huwa na idadi kubwa ya vifaa lakini kuna tatizo kubwa la kwamba vifaru, ndege za kijeshi na manowari ni za kale sana na teknolojia ni ya miaka ya 1950-1970. Hakuna uhakika kiasi gani zinafanya kazi kutokana na hali bovu ya tasnia na uhaba wa vipuli. Korea Kaskazini ilijitahidi kutengeneza makombora na vifaa vingine kwa kunakili sampuli kutoka Urusi na China lakini inaonekana idadi iliyoweza kutengenezwa ni ndogo. Imekadiriwa na watazamaji kuwa wanaanga wanakosa mafuta ya kufanya mazoezi ya kutosha. [14]

Jitihada za kutengeneza silaha za nyuklia zilileta mlipuko wa kwanza wa kinyuklia mwaka 2006. Hii imesababisha kuongezeka kwa hofu za majirani pamoja, na Korea Kaskazini iliahidi mara kadhaa kusimamisha mradi huo. Baada ya kurudia milikuko ya majaribio Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kura za wanachama wote lilitangaza adhabu dhidi ya nchi na kutakaza maendeleo ya programu hiyo lakini Korea Kaskazini imeendelea ikiaminiwa kuwa na akiba ndogo ya silaha hizi. Lakini hakuna uhakika kama kuna makombora yanayoweza kutegemewa kwa mashambulio.

Tazama pia

Tanbihi

  1. [www.unhcr.org/refworld/country,,,,PRK,4562d8cf2,487ca236c0,0.html United Nations High Commissioner for Refugees] (July 2, 2008) "UNHCR Freedom in the World 2008 - North Korea". Unhcr.org. Retrieved 2011-04-08
  2. 8http://cdn.loc.gov/master/frd/frdcstdy/no/northkoreacountr00word/northkoreacountr00word.pdf Country Study North Korea uk. 138]
  3. Country Study North Korea uk. 142
  4. Country Study North Korea uk. 140
  5. Noland, Marcus, Sherman Robinson and Tao Wang, Famine in North Korea: Causes and Cures, Institute for International Economics. Jalada kutoka ya awali juu ya 2017-08-08. Iliwekwa mnamo 2017-04-23.
  6. Economy North Korea, Encyclopædia Britannica Online, iliangaliwa 31 May 2014
  7. Kim Jong Eun's Long-lasting Pain in the Neck, TheDailyNK, 30 November 2010
  8. North Korea: a country study Federal Research Division, Library of Congress; edited by Robert L. Worden. 5th ed.p.cm. (Area handbook series) "Research completed October 2007." ISBN 978-0-8444-1188-0 1. Korea (North). Uk. 8
  9. DPRK—Only Tax-free Country Tovuti ya Globalsecurity, iliangaliwa 19 June 2009
  10. Pyongyang glitters but most of North Korea still dark Archived 7 Julai 2014 at the Wayback Machine. Taarifa ya AP / tovuti ya MSN News ya 28 Aprili 2013, iliangaliwa 15 Juni 2014
  11. North Korea hunger: Two in five undernourished, says UN (tovuti ya BBC 22 March 2017, iliangaliwa Aprili 2017
  12. North Korea Military Stats, tovuti ya Nation Master, iliangaliwa Aprili 2017
  13. North Korea introduces 'mandatory military service for women, The Guardian (UK), 31 January 2015, iliangaliwa Aprili 2017
  14. North Korea's military aging but sizable , taarifa ya CNN ya November 25, 2010 - iliangaliwa Aprili 2017

Viungo vya nje

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Serikali
Jeshi
Tovuti mbalimbali
Picha
Nchi na maeneo ya Asia

Afghanistan | Armenia2 | Azerbaijan | Bahrain | Bangladesh | Bhutan | Brunei | China | Falme za Kiarabu | Georgia2 | Hong Kong3 | Indonesia | Iraq | Israel | Jamhuri ya China (Taiwan) | Japani | Kamboja | Kazakhstan | Kirgizia | Korea Kaskazini | Korea Kusini | Kupro2 | Kuwait | Laos | Lebanoni | Macau3 | Malaysia | Maldivi | Mongolia | Myanmar | Nepal | Omani | Pakistan | Palestina | Qatar | Saudia | Singapuri | Sri Lanka | Syria | Tajikistan | Timor ya Mashariki | Turkmenistan | Uajemi | Ufilipino | Uhindi | Urusi1 | Uthai | Uturuki1 | Uzbekistan | Vietnam | Yemen | Yordani

1. Nchi ina maeneo katika Asia na Ulaya. 2. Nchi iko Asia lakini inahesabiwa pia kati ya nchi za Ulaya kwa sababu za historia au utamaduni. 3. Eneo la pekee la China.


Makala hii kuhusu maeneo ya Asia bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Korea Kaskazini kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.