Uhuru Kenyatta

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Picha yake.

Uhuru Muigai Kenyatta (amezaliwa 26 Oktoba 1961) ni mwanasiasa nchini Kenya ambaye amekuwa rais wa nne wa Jamhuri ya Kenya kuanzia tarehe 9 Aprili 2013 mpaka tarehe 13 Septemba 2022.

Uhuru alihudumu kama mbunge wa Gatundu Kusini kuanzia mwaka wa 2002 hadi 2013. Pia alihudumu kama naibu waziri mkuu kuanzia 2007 hadi 2013.

Uhuru alihusika na chama cha Kenya Africa National Union (KANU) hapo awali kabla ya kubuni chama cha The National Alliance (TNA). Chama hicho kiliungana na kile cha United Republican Party (URP) kikiongozwa na William Samoei Ruto ili kubuni chama cha Jubilee, kilichompa Uhuru kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa 2013, naye William Ruto akichaguliwa kama naibu rais.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Maisha ya awali[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa kama mtoto wa pili wa Jomo Kenyatta aliyekuwa rais wa kwanza wa Kenya na mke wake Ngina Muhoho aliyeitwa Mama Ngina.

Uhuru ana dada wawili, Christine (aliyezaliwa 1953), Anna Nyokabi (aliyezaliwa 1963), na ndugu mmoja, Muhoho Kenyatta (aliyezaliwa 1965).

Familia yake inatoka kwenye kabila la Wakikuyu. Jina alilopewa, "Uhuru" ni la Kiswahili na alipewa jina hili nchi ya Kenya ilipokuwa inatarajia kupata uhuru kutoka kwa mkoloni.

Uhuru alisomea shule ya St Mary's mjini Nairobi. Kati ya mwaka 1979 na 1980, pia alifanya kazi kwa ufupi katika Benki ya Biashara ya Kenya.

Baada ya kuhitimu St. Mary's, Uhuru alisomea uchumi, sayansi ya siasa na mafunzo ya serikali katika chuo kikuu cha Amherst kule Marekani.

Baada ya kuhitimu, Uhuru alirejea nchini Kenya na kuanzisha kampuni iliyoitwa Wilham Kenya Limited ambayo iliuza nje ya nchi mazao ya kilimo.

Kuingia katika siasa[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1997 alijaribu kuingia mara ya kwanza katika siasa lakini alishindwa katika uchaguzi wa bunge.

Mwaka 1999 rais Daniel arap Moi alimpa cheo cha mwenyekiti wa bodi ya utalii. Moi aliendelea kumpandisha ngazi mwaka wa 2001 kwa kumpa nafasi ya mbunge wa kitaifa na waziri msaidizi. Baadaye akawa waziri wa serikali ya mtaa chini ya rais Daniel Arap Moi. Licha ya kutokuwa na uzoefu wa kisiasa, Uhuru alipendelewa na Moi kuwa mrithi wake.

Tangu Julai 2002 ilionekana wazi ya kwamba Moi alimtaka kama mgombea wa urais upande wa KANU atakayemfuata katika ikulu. Mwaka 2002 akawa makamu wa mwenyekiti wa KANU. Mkutano mkuu wa KANU katika mwezi Oktoba 2002 uliitikia mapenzi ya rais ukamtangaza Uhuru kama mgombea wa urais katika uchaguzi mkuu wa urais wa Disemba 2002.

Tendo hili lilisikitisha wanasiasa wengi wasiokuwa Wakikuyu na waliotegemea nafasi hiyo kwa ajili yao wenyewe. Waliondoka katika KANU na kuendelea katika ushirikiano wa upinzani wa NARC.

Uhuru ulishindwa na mgombea wa upinzani Mwai Kibaki katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2002 alipopata asilimia 31 tu za kura.

Kiongozi wa upinzani na wa chama[hariri | hariri chanzo]

Baada ya uchaguzi, akawa kiongozi wa upinzani kwenye bunge jipya. Kenyatta alimuunga mkono Mwai Kibaki ambaye alikuwa anawania kuchaguliwa tena kama rais na alichaguliwa kama waziri wa serikali ya mtaa kwa mara ya pili Januari 2008. Baadaye, aliteuliwa naibu waziri mkuu na waziri wa biashara Aprili 2008 akiwa kwenye serikali ya muungano.

Baadaye, Uhuru Kenyatta akawa waziri wa fedha kuanzia 2009 hadi 2012, wakati akiwa bado naibu waziri mkuu. Alituhumiwa na mahakama ya kimataifa ya jinai (ICC) kule The Hague, Uholanzi kwa makosa dhidi ya ubinadamu baada ya vurugu yaliyotokea baada ya uchaguzi mkuu wa 2007.

Kenyatta alijiuzulu kama waziri wa fedha 26 Januari 2012. Alichaguliwa kama rais wa nne wa jamhuri ya Kenya kwenye uchaguzi mkuu wa Machi 2013, akimshinda mpinzani wake Raila Odinga kwa kura chache sana.

Pingamizi dhidi yake ndani ya KANU[hariri | hariri chanzo]

Katika bunge alikuwa kiongozi wa upinzani, lakini aliona pia upinzani ndani ya chama hasa kutoka kwa pamoja na wanasiasa kutoka Bonde la Ufa. Kwenye mkutano wa chama cha Januari 2005 Uhuru alithibitishwa kwa kura nyingi na Biwott aliunda chama cha New Kanu.

Katika kura maalumu ya wananchi kuhusu katiba Uhuru alishikamana na viongozi wa LDP katika kambi ya Chungwa. Mipango yake ya kushiriki katika Orange Democratic Movement (ODM) yalipingwa vikali ndani ya chama kwa sababu wanaKANU pamoja na rais mstaafu Moi waliogopa kupotea kwa chama cha kwanza katika historia ya Kenya.

Katika Novemba 2006 Nicholas Biwott alirudia jaribio la kumpindua Uhuru kwa kuita mkutano wa Kanu mjini Mombasa bila idhini ya mwenyekiti wala kamati ya chama. Hapo alichaguliwa kuwa mweyekiti mpya. Kwa msaada wa serikali Biwott alifaulu kuandikisha kamati yake kama uongozi rasmi, na hivyo kumwondoa Uhuru katika nafasi ya kiongozi wa upinzani bungeni.

Uhuru alipinga uamuzi huo, na hatimaye mahakama kuu ikabatilisha kura ya Mombasa tarehe 29 Desemba 2006 ikathibitisha azimio hili mnamo Juni 2007.

Kuhamia upande wa Kibaki 2007[hariri | hariri chanzo]

Juni 2007 Uhuru alionyesha wazi ya kwamba alitaka kuacha ushirikiano na ODM kwa kutopeleka jina lake kati ya wagombea wa urais upande wa ODM. Badala yake alieleza ya kuwa atampigania rais Kibaki achaguliwe tena.

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 Uhuru alichaguliwa tena kama mbunge wa Garundu Kusini kwa tiketi ya KANU.

Urais[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kuongoza nchi kama rais kwa awamu moja (2013-2018), alishinda uchaguzi mkuu wa Agosti 2017 lakini mahakama kuu ikaamua na kuamuru urudiwe, marudio ambayo baada ya kujiondoa kwa mpinzani wake mkuu Raila Odinga, Kenyatta aliibuka mshindi kwa asilimia tisini na nane. Hatimaye alitangazwa rasmi kuwa mshindi na kuapishwa kwa kipindi chake cha pili kwa mujibu wa sheria.

Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Uhuru Kenyatta kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.