Dameski

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Damasko)
Dameski - دمشق
Damaskus bei Nacht, fotografiert vom Dschabal Qasiun aus; Die grünen Punkte sind Minarette
Habari za msingi
Mkoa Dameski
Anwani ya kijiografia 33°30'35" N; 36°18'33"E
Kimo 690 m juu ya UB
Eneo 105 km²
Wakazi 1.711.000 (2009)
Msongamano wa watu watu 15.056/km²
Simu 963 (nchi), 11 (mji)
Lage

Dameski (pia: Damasko, Damaskus, Damascus; kutoka Kiarabu: دمشق "dimashk") ni mji mkuu wa Syria, pia ni mji mkubwa wa nchi hiyo wenye wakazi milioni 2, wanaofikia 5 pamoja na miji jirani.

Dameski ni kati ya miji ya kale kabisa duniani iliyoendelea kukaliwa mahali palepale: inaaminiwa imekaliwa tangu miaka 8,000 au zaidi.


Mji wa Kale umo katika orodha ya urithi wa dunia ya UNESCO.

Jina[hariri | hariri chanzo]

Nchini mji huitwa mara nyingi الشام ("ash-shām"). Jina hilo latumiwa na Waarabu wengine kwa nchi yote ya Syria pia. Kihistoria "Shamu" ilikuwa jina la nchi yote upande wa mashariki wa bahari ya Mediteranea.

Haijulikani kutoka lugha gani jina la “Dameski” lilikuja. Dameski inaitwa na wenyeji wake kwa jina la “Sham” pia au wakati mwingine “al Fayhaa” au "Madinat al Yasamin", yaani “Mji wa Yasimini.”

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Dameski iko takriban kilometa 80 mashariki kwa pwani ya Mediteranea na kilometa 30 kutoka mpaka kati ya Syria na Lebanoni kando ya mto Barada. Iko kwenye kimo cha mita 680 juu ya UB.

Upande wa magharibi ni milima ya Lebanoni Ndogo inayozuia mawingu ya mvua kufika kutoka Mediteranea. Upande wa mashariki linaanza jangwa.

Kati ya mji, kuna mito midogo mingi, na mto mkuu ndio Barada. Zamani, palikuwa na bustani nyingi sehemu zote za nchi. Lakini kwa sababu ya uchafuzi wa mazingira na idadi ya watu ambayo imekuwa inapanda, siku hizi bustani ni chache na pia hakuna maji mengi mitoni kwa mji.

Mji wa kisasa una eneo la km2 105. Eneo la km2 77 limetumiwa kwa majengo, makazi na mashamba, na eneo lililobaki ni mlima wa Qassioun.

Hali ya hewa[hariri | hariri chanzo]

Kwa sababu ya milima ya Anti-Lebanon, kuna mvua chache mjini. Wakati wa baridi, kuna mvua na theluji mara kwa mara. Wakati wa joto, hali ya hewa ni kavu na joto.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Akiolojia imeonyesha makazi ya binadamu katika eneo la Dameski tangu milenia ya 5 KK.

Utawala wa Misri[hariri | hariri chanzo]

Mji ulitajwa mara ya kwanza kimaandishi kwa jina la "Tamasqu" (tmsq) katika taarifa za Misri ya Kale wakati wa Farao Thutmosis III (1479 KK - 1425 KK). Ilikuwa chini ya utawala wa Misri hadi mnamo mwaka 1100 KK.

Ufalme wa Aramu[hariri | hariri chanzo]

Tangu 1000 KK mji ukawa kitovu cha ufalme wa Aramu-Dameski unaotajwa mara nyingi katika Biblia pia. Baada ya kushindana mara nyingi na Israeli ulikwisha katika vita dhidi ya Assyria mwaka 732 KK.

Utawala wa Babeli, Uajemi, Wagiriki na Roma[hariri | hariri chanzo]

Assyria ilishindwa na Nebukadreza II wa Babeli na Dameski ikawa sehemu ya milki ya pili ya Babeli tangu 572 KK.

Mwaka 538 KK, Uajemi ilipochukua nafasi ya Babeli, Dameski ikawa mji mkuu wa jimbo la Syria.

Kufika kwa Aleksanda Mkuu tangu 333 KK kulibadilisha siasa ya Mashariki ya Kati na Dameski ikawa sehemu ya ulimwengu wa Kigiriki.

Wafuasi wa Aleksanda waliendelea kushindania mji huo baadaye: mara ukawa upande wa Waptolemayo (Misri) mara upande wa Waseleukido.

"Barabara iliyonyoka", Mtume Paulo alipobatizwa na Anania wa Damasko.

Tangu mwaka 64 KK Dola la Roma likaingia Shamu. Dameski ikawa mji mkuu wa jimbo la Kiroma likakua na kustawi. Mpangilio wa Waroma yanaonekana hadi leo katika mji wa kale wa Dameski, hata kama majengo ya nyakati zile yamefichwa mita 5 chini ya uwiano wa mji wa leo.

Barabara ya decumanus ya Kiroma, ambayo imetajwa katika Biblia ya Kikristo kama "barabara iliyonyoka" au "barabara iitwayo Nyofu" (Mdo 9:11), inaonekana hadi leo. Ndipo Mtume Paulo alipobatizwa baada ya kutokewa na Yesu mfufuka alipokuwa anakaribia mjini kwa lengo la kuwakamata Wakristo.

Kaisari Theodosio I alijenga kanisa kubwa la Mt. Yohane lililotunza kichwa cha Yohane Mbatizaji.

Waarabu na Waosmani[hariri | hariri chanzo]

Dameski ilivamiwa na jeshi la Waarabu Waislamu chini ya khalifa Umar I mwaka 636 B.K.. Kanisa la Mt. Yohane likabadilishwa kuwa msikiti mkuu.

Baada ya ushindi wa Muawiyya mwaka 661 juu ya Hussain ibn Ali alichukua cheo cha khalifa akikaa Dameski. Hivyo mji ukawa mji mkuu wa milki ya Wamuawiya iliyotawala kutoka Hispania hadi milango ya China.

Khalifa wa mwisho wa Wamuawiya Marwan II alihamisha makao yake kwenda Haran katika Mesopotamia ya kaskazini. Marwan alishindwa baadaye na Abu al-`Abbās `Abdu'llāh as-Saffāh aliyeanzisha utawala wa makhalifa Waabbasi na kupeleka mji mkuu Baghdad. Dameski haikurudishiwa tena umuhimu na heshima jinsi ilivyokuwa wakati wa Wamuawiya.

Iliendelea kuwa makao makuu ya kijimbo tu, isipokuwa kwa vipindi vifupi ilipokuwa mji huru tena, pasipo utawala wenye nguvu ya makhalifa.

Salah-ad-Din aliweka tena mji chini ya utawala wa Misri hadi 1516. Mnamo 1400 Dameski ilivamiwa na kuharibiwa kabisa na Timur.

Utawala wa Milki ya Waturuki Waosmani ulianza 1516 ukaendelea hadi 1918. Dameski ilijikuta tena mbali na mji mkuu wa milki huko Istanbul. Ilikuwa na umuhimu fulani kwa sababu misafara ya hija kwenda Maka ilianzia Dameski.

Ni kwamba mwaka 1516, kiongozi Mmisri wa Dameski alikimbia mji. Baada ya siku chache, Sultani Selim I alifika mjini akaweka mji juu ya Waosmani. Wakati ambapo Selim I alirudi Dameski, alijenga msikiti mpya, tekkiye (ni kama soko), na kaburi la Shaikh Muhi al Din ibn Arabi mtaani kwa Al Salhiyeh.

Waosmani walitawala Dameski kwa muda wa miaka 400, ila baina ya miaka 1832 na 1840 ilitawaliwa na Wamisri. Licha ya udogo wake, na kwa sababu ya mahali pake katika njia ya Hajj, Dameski ilikuwa mji muhimu kwa serikali ya Kiosmani. Mwaka 1560, Waosmani walijenga Tikkeyeh Suleymaniyeh ambapo wasafiri na wafanya Hajj waliweza kustarehe.

Wakati wa utawala wa Waosmani, Wayahudi na Wakristo wa Dameski waliweza kuendelea na dini zao wakiwa dhimmi (watu wasio Waislamu na waliolazimisha kulipa kodi kubwa kuliko ya Waislamu).

Mwanzo wa karne ya 20, wazo la utaifa wa Kiarabu lilianza Dameski kwa sababu ya sheria kutoka Istanbul ambazo zilitumiwa zibadilishe Dameski iwe “mji wa Kituruki” zaidi. Utekelezaji wa watu wenye elimu mwaka 1915 na mwaka 1916 ulikuza hilo wazo la utaifa wa Kiarabu. Lakini Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia ilivunja milki ya Waosmani ikaleta utawala wa Ufaransa katika Syria.

Mwaka 1918, mapinduzi ya Waarabu yalianza nchini Syria na baada ya muda mfupi, Waosmani waliondoka Syria na Waingereza walichukua nchi. Faisal ibn Hussein alikuwa mfalme mpya wa Syria. Mwaka 1920, serikali iliandika katiba mpya ya kidemokrasia. Lakini, mwaka huohuo Mkutano wa Versailles aliutolea Ufaransa nchi ya Syria kama nchi lindwa chini ya Shirikisho la Mataifa. Hivyo Ufaransa uliingia Syria mwaka 1920.

Mwaka 1925, mapinduzi mapya ambayo yalianzishwa na Hauran (eneo la mashamba kusini mwa nchi) yalifika Dameski. Wasyria walitaka uhuru wao. Lakini, Ufaransa ulitupa mabomu Dameski na waliacha mapinduzi.

Wakati wa Vita vikuu vya pili vya dunia jeshi la Ufaransa huru na jeshi la Uingereza, walichukua Dameski. Baada ya vita hivyo, Ufaransa ulitoa uhuru kwa Syria na Dameski ikawa mji mkuu wa nchi mpya.

Mji Mkuu wa Syria huru[hariri | hariri chanzo]

Uhuru wa Syria mwaka 1946 ulifanya Dameski mji mkuu wa nchi huru. Tangu hapo Dameski ikakua sana ikawa mji wa viwanda na biashara.

Uchumi[hariri | hariri chanzo]

Zamani, Dameski ulikuwa mji muhimu wa biashara. Mpaka sasa, biashara ni muhimu mjini. Kuna masoko na kampuni nyingi. Kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Syria, Dameski ni mji mkuu wa uchumi wa Syria.

Kuna viwanda vya serikali mjini. Lakini viwanda vya binafsi ni vichache, tena sasa ni vichache kuliko zamani kwa sababu ya vita. Lakini kwa sababu ya kutengwa kwa nchi kutokana na sababu mbalimbali na pia kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, hakuna uchumi wenye nguvu. Kuna ufukara mwingi na utovu wa ajira.

Taarifa za wakazi[hariri | hariri chanzo]

Mwaka wa 2011, idadi ya watu ilikuwa 1,711,000. Lakini, kuna miji midogo karibu sana na Dameski kama Duma, Harasta, Daraya, Jaramana, na Tal. Kwa jumla kuna watu zaidi ya milioni 5 wanaoishi katika kanda ya Dameski. Hasa baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, kuna watu wengi kuliko kila mahali pa Syria waliohamia Dameski. 

Dameski kuna mchanganyiko wa watu. Karibu watu wote ni Waarabu Waislamu, hasa Wasunni. Lakini, kuna watu walio Wakurdi, Waarmenia na Wakristo wengine wa madhehebu mbalimbali, Waalawi, na kadhalika.

Lugha nyingi zinazosemwa mjini ni pamoja na Kiarabu, Kifaransa, Kiarmenia na Kiaramu. Zamani, palikuwa na Wayahudi wengi mjini lakini waliondoka baada ya kuanzishwa kwa nchi ya Israel.

Mji wa Kale na Utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Mji wa Dameski wa Kale ni mji wa pekee duniani. Mji unajulikana kwa barabara ndogo zake, zinapopatikana na masoko, makasri, misikiti, makanisa yake. Mji wa kale ni mchanganyiko wa magofu ya Warumi, Waosmani, and Wafaransa. Maisha ndani ya mji wa Dameski yanafanana na maisha ya watu wa zamani.

Milango saba ya mji [hariri | hariri chanzo]

  • Bab al-Faradis
  • Bab al-Salam
  • Bab Tuma
  • Bab Sharqi
  • Bab Kisan
  • Bab al-Saghir
  • Bab al-Jabiyeh 

Makanisa maalum[hariri | hariri chanzo]

  • Kanisa la Mtakatifu Paulo
  • Nyumba ya Mtakatifu Anania
  • Kanisa la Kimarimia
  • Kanisa Katoliki la Kirumi
  • Kanisa la Mtakatifu Yohane
  • Kanisa la Kiorthodoksi la Mtakatifu George 

Misikiti maalum[hariri | hariri chanzo]

Maziara ya kichwa cha Yohane Mbatizaji ndani ya msikiti wa Muawiya inatembelewa na Waislamu na Wakristo vilevile.
  • Msitiki wa Waomaya (Mahali lilipo kaburi la Salaheddin, shujaa Mwislamu maalum sana)
  • Msitiki wa Sayyida Ruqaya
  • Msikiti wa Sinaniya
  • Msikiti wa Toba 

Khan (mahali ambapo wasafiri waliweza kustarehe)[hariri | hariri chanzo]

  • Khan Jaqmaq
  • Khan Asaad Pasha
  • Khan Suleyman Pasha 

Nyumba muhimu na makasri[hariri | hariri chanzo]

  • Kasri la Azem
  • Beit al-Aqqad
  • Maktab Anbar
  • Beit al-Mamlouka

Elimu[hariri | hariri chanzo]

Dameski ni pahali pa elimu Syria. Chuo Kikuu cha Dameski ni chuo kikuu kikubwa na cha zamani zaidi nchini. Baada ya sheria iliyoruhusu vyuo vikuu vya binafsi, kuna vyuo vikuu vipya kama: Syrian Virtual University, Chuo Kikuu cha Qalamoun, n.k.

Usafiri[hariri | hariri chanzo]

Uwanja wa ndege mkuu ni Uwanja wa Ndege wa Dameski ambao uko karibu na mji. Lakini sasa, kwa sababu ya vita, kuna ndege chache tu ambazo zinasafiri Dameski.

Hakuna huduma kubwa za usafirishaji. Kuna njia za basi ndogo. Wakazi wa mji wanategemea “microbus.” Microbus ni kama matatu ya Kenya au daladala za Tanzania. Huko Dameski, kuna njia zaidi ya mia moja ya microbus zinazokwenda kila mahali mjini.

Kuna pia shirika la “Chemin de Fer Syriens” ambalo ni shirika la treni. Lakini baada ya vita vya uraia, hakuna treni zozote nchini.

Makala hii kuhusu maeneo ya Asia bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Dameski kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.