Sayyid Majid

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Seyyid Majid)
Picha yake.
Jumba la Sultani Zanzibar.

Sayyid Majid bin Said (kwa Kiarabu: ماجد بن سعيد البوسعيد‎‎; 18347 Oktoba 1870) alikuwa Sultani wa kwanza wa Zanzibar, akitawala tangu tarehe 19 Oktoba 1856 hadi kifo chake funguvisiwa la Zanzibar pamoja na pwani ya Afrika ya Mashariki kati ya Mogadishu (leo mji mkuu wa Somalia) na Rasi Delgado (leo Kaskazini mwa Msumbiji , karibu na mto Ruvuma).

Umuhimu wake kihistoria ni kwamba ndiye aliyeanzisha Usultani wa Zanzibar baada ya kifo cha baba yake, Sultani Sayyid Said, ambapo Usultani wa Omani uligawiwa mwaka 1856.

Athira ya nchi yake ilienea kupitia njia za misafara ya pembe za ndovu na watumwa hadi mto Kongo.

Wafanyabiashara kama Tippu Tip waliokuwa raia wa Usultani wakapita Tabora na Ujiji kwenda ziwa Tanganyika na kuingia ndani ya eneo la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ya leo. Wapagazi wao walibeba bidhaa kutoka Zanzibar zilizobadilishwa kwa pembe za ndovu hasa. Watumwa walikamatwa au kununuliwa wakabeba pembe hadi pwani.

Pamoja na hayo, sultani alipokea kwa moyo wamisionari Wakristo.

Mapadri Wakatoliki wa kwanza pamoja na masista walitokea Reunion wakakaa Unguja tangu tarehe 12 Desemba 1860 hadi mwaka 1863, walipokabidhi misheni kwa shirika la mapadri wa Roho Mtakatifu.

Waanglikana wa chama cha Misheni ya Vyuo Vikuu kwa Afrika ya Kati U.M.C.A. (Universities' Mission to Central Africa) ambacho kiliundwa ili kutekeleza wito kutoka David Livingstone kuhubiri Injili na kukomesha utumwa katika Afrika, waliingia Zanzibar mwaka 1864.

Baadaye wakajenga kanisa kuu mahali pa soko la watumwa lililofungwa, altari ikiwa imejengwa juu ya nafasi ya mti wa kuwafunga watumwa walioadhibiwa kwa viboko, na batizio kuwa mahali walipotupwa watoto watumwa ambao hawakuuzwa pamoja na mama zao.

Kwa kuwa Majid aliacha binti tu, alirithiwa na kaka yake, Sayyid Barghash.

Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Sayyid Majid kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.