Pitcairn

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Hori la Bounty kwenye Pitcairn; nyumba za Adamstown zaonekana upande wa kulia juu
Ramani ya visiwa

Pitcairn ni kisiwa katika Pasifiki na pia jina la funguvisiwa ambalo ni eneo la ng'ambo la Uingereza pekee katika Pasifiki.

Makao makuu ni kijiji pekee cha Adamstown.

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Pitcairn ni kisiwa chenye asili ya kivolkeno. Eneo lake ni km² 4.6 na idadi ya wakazi ni 46 tu, ambao wanazungumza Krioli maalumu ya Kiingereza na kuwa Waadventista Wasabato.

Visiwa vingine ni atolli za Oeno, Henderson na Ducie ambazo hazina wakazi. Watu walio karibu wako kwenye kisiwa cha Pasaka (km 2,000) na kwenye Polynesia ya Kifaransa (km 500).

Historia[hariri | hariri chanzo]

Hakuna uhakika kuhusu wakazi na wageni wa Pitcairn kabla ya kugunduliwa na kijana Pitcairn kwenye jahazi ya Kiingereza mwaka 1767. Inaaminiwa ya kwamba Wapolinesia walikalia visiwa tangu karne kadhaa, lakini hakuna uhakika kama walikuwepo bado wakati wa kufika kwa Wahispania waliopita sehemu hizi katika karne ya 17. Kwa vyovyote Waingereza hawakukuta tena watu.

Tangu mwaka 1790 kisiwa kilikaliwa na waasi wa Bounty iliyokuwa jahazi ya Kiingereza ambamo ulitokea uasi wa mabaharia dhidi ya nahodha. Waasi waliamua kujificha kwa sababu waliogopa adhabu ya kifo kulingana na sheria za Uingereza za wakati ule. Wakazunguka bahari pamoja na wanawake wa Tahiti wakakuta Pitcairn wakajenga makazi yao kisiwani.

Mwaka 1838 kisiwa kilitangazwa kuwa koloni la Uingereza.

Mwaka 1856 watu wa Pitcairn walihamishiwa kisiwa cha Norfolk kwa sababu walikuwa wengi mno kulingana na udogo wa kisiwa hata wakaona njaa. Lakini familia tano waliamua kurudi tena na ndio mababu wa wakazi wa leo.

Uchumi[hariri | hariri chanzo]

Uchumi unategemea hasa kilimo cha kijungujiko na misaada kutoka Uingereza. Mara chache kisiwa kinatembelewa na watalii.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]