Kisiwa cha Pasaka

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Ramani ya kisiwa.
Moai ni jina la vichwa hivi.

Kisiwa cha Pasaka (kwa Kirapanui: Rapa Nui; kwa Kihispania: Isla de Pascua) ni kisiwa cha Chile katika Pasifiki ya mashariki takriban 3,526 km kutoka mwambao wa Chile.

Anwani ya kijiografia ni 27°09′S 109°25′W.

Mji mkuu ni Hanga Roa.

Kuna wakazi 5,761 (2012).

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Kisiwa kiko peke yake baharini: kisiwa cha karibu ni Pitcairn km 2,000  upande wa magharibi.

Kina asili ya kivolkeno. Ni mlima ulioanza kukua chini ya bahari kwenye mgongo mashariki wa Pasifiki mita 3000 chini ya UB.

Umbo la kisiwa ni pembetatu lenye urefu mkubwa wa km 24  na upana mkubwa wa k, 13 . Eneo lote ni 162.5 km². Mlima mkubwa hufikia kimo cha 509 m juu ya UB.

Kando ya kisiwa kikuu kuna visiwa vidogo kadhaa bila watu.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Vichwa vya kisiwa cha Pasaka.

Inaaminika ya kwamba kisiwa kilikaliwa na watu kutoka Austronesia katika milenia ya 1 BK. Walileta nao ndizi, taro, viazi na miwa pamoja na kuku na panya.

Utamaduni wao ulistawi kwa karne kadhaa na alama zake ni sanamu kubwa za vichwa vya mawe kote kisiwani. Vichwa hivi huitwa "Moai" lakini hakuna uhakika kusudi lao lilikuwa nini.

Kuna pia mabaki ya mwandiko uliokuwa mwandiko wa pekee kati ya visiwa vyote vya Polynesia. Inaaminiwa ya kwamba wakati fulani idadi ya wakazi ilifikia 10,000 hadi 15,000.

Lakini utamaduni huo uliporomoka kabla ya kufika kwa Wazungu wa kwanza. Wataalamu huamini ya kwamba wenyeji walipata matatizo ya kiekolojia kwa sababu miti yote ilikatwa na rutuba ya ardhi ilipotea. Wengine huamini ya kwamba mabadiliko ya hali ya hewa yalikuwa na athira pia.

Wakati wa kufika kwa Waholanzi, waliokuwa Wazungu wa kwanza kukuta kisiwa kile baharini, walibaki watu 2,000 - 3,0000 pekee. Kufika huku kulitokea tarehe 5 Aprili 1722 ambayo ilikuwa siku ya Pasaka: hivyo hilo likawa jina la kisiwa.

Idadi ya wenyeji ikaendelea kushuka kutokana na magonjwa ya nje yaliyokuja na meli zilizopiga hodi kisiwani kila baada ya miaka kadhaa.

Katika karne ya 19 watu mamia walikamatwa na wafanyabiashara ya utumwa.

Chile ilitwaa kisiwa na kukitangaza sehemu ya eneo lake mwaka 1888. Wakati ule kilikuwa na watu 178 pekee. Idadi hii ilikua tena.

Leo hii takriban theluthi mbili ya wakazi ni Rapanui au wenyeji asilia ya kisiwa. Kwa jumla kuna Warapanui 4,647 (mwaka 2002): nusu yao wanaishi kisiwani na nusu nyingine Chile bara.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:



Makala hii kuhusu eneo fulani bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu eneo hilo kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Je, unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.


Usitaje majina ya madiwani na viongozi au maafisa wengine wa sasa maana wanabadilika haraka mno.